Kifo
Maana: Kukoma kwa utendaji wote wa uhai. Baada ya mtu kuacha kupumua, moyo wake kuacha kupiga, na ubongo wake kuacha kutenda, hatua kwa hatua nguvu za uhai huacha kutenda kazi katika chembe za mwili. Kifo ni kinyume cha uhai.
Je, mwanadamu aliumbwa na Mungu ili afe?
Sivyo, badala yake Yehova alimwonya Adamu juu ya kutotii, ambako kungetokeza kifo. (Mwa. 2:17) Baadaye, Mungu aliwaonya Waisraeli juu ya mwenendo ambao ungewafanya wafe mapema. (Eze. 18:31) Kisha akamtuma Mwana wake afe kwa ajili ya wanadamu ili wale ambao wangeamini uandalizi huo wapate uzima wa milele.—Yoh. 3:16, 36.
Andiko la Zaburi 90:10 husema kwamba muda wa kawaida wa maisha ya binadamu ni miaka 70 au 80. Ndivyo ilivyokuwa Musa alipoandika maneno hayo, lakini haikuwa hivyo tangu mwanzo. (Linganisha na Mwanzo 5:3-32.) Andiko la Waebrania 9:27 linasema, “Watu wamewekewa akiba kufa mara moja kwa wakati wote.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa maneno hayo yalipoandikwa. Lakini haikuwa hivyo kabla Mungu hajamhukumu Adamu mwenye dhambi.
Kwa nini tunazeeka na kufa?
Yehova aliwaumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu, wakiwa na tazamio la kuishi milele. Walipewa uhuru wa kuchagua. Je, wangemtii Muumba wao kwa sababu wanampenda na kuthamini yote aliyokuwa amewafanyia? Walikuwa na uwezo kamili wa kufanya hivyo. Mungu alimwambia Adamu hivi: “Kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” Shetani alimtumia nyoka kumshawishi Hawa avunje amri ya Yehova. Adamu hakumkaripia mke wake bali alijiunga naye katika kula lile tunda lililokatazwa. Kulingana na neno lake, Yehova alimhukumia Adamu kifo, lakini kabla ya kuwaangamiza hao watenda-dhambi wawili, kwa rehema Yehova aliwaruhusu wazae watoto.—Mwa. 2:17; 3:1-19; 5:3-5; linganisha na Kumbukumbu la Torati 32:4 na Ufunuo 12:9.
Rom. 5:12, 17, 19: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi—. . . . Kwa kosa la mtu mmoja kifo kilitawala kama mfalme . . . Kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa watenda-dhambi.”
1 Kor. 15:22: “Katika Adamu wote wanakufa.”
Ona pia kichwa, “Majaliwa.”
Kwa nini watoto hufa?
Zab. 51:5, BHN: “Mimi ni mkosefu tangu kuzaliwa kwangu, mdhambi tangu tumboni mwa mama yangu.” (Ona pia Ayubu 14:4; Mwanzo 8:21.)
Rom. 3:23; 6:23: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu . . . Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.”
Mungu “hawachukui” watoto kutoka kwa wazazi wao, kama vile ambavyo watu fulani wameambiwa. Ijapokuwa dunia inazaa chakula cha kutosha, mara nyingi wanasiasa na wafanyabiashara wenye ubinafsi huwazuia wale wenye uhitaji wasikipate, na hilo hutokeza kifo kwa sababu ya utapiamlo. Watoto fulani hufa katika msiba, sawa na watu wazima. Lakini sisi sote tumerithi dhambi; sisi sote si wakamilifu. Tulizaliwa katika ulimwengu ambao kila mtu—mwema na mbaya—mwishowe hufa. (Mhu. 9:5) Lakini Yehova ‘hutamani sana’ kuwaunganisha tena watoto pamoja na wazazi wao kupitia ufufuo, na kwa upendo amefanya uandalizi wa kutenda hivyo.—Yoh. 5:28, 29; Ayu. 14:14, 15; linganisha na Yeremia 31:15, 16; Marko 5:40-42.
Wafu wako wapi?
Mwa. 3:19: “Kwa jasho la uso wako utakula mkate mpaka utakaporudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.”
Mhu. 9:10: “Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote, kwa maana hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.”
Wafu wako katika hali gani?
Mhu. 9:5: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.”
Zab. 146:4: “Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo [“mawazo,” UV; “mafikili,” ZSB; “mipango,” BHN] yake hupotea.”
Yoh. 11:11-14: “‘Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.’ . . . Yesu akawaambia waziwazi: ‘Lazaro amekufa.’” (Pia Zaburi 13:3)
Je, kuna sehemu fulani ya mtu inayoendelea kuishi mwili unapokufa?
Eze. 18:4: “Nafsi [“nafsi,” ZSB] inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.”
Isa. 53:12: “Aliimwaga nafsi [“nafsi,” UV, ZSB] yake mpaka kufa.” (Linganisha na Mathayo 26:38.)
Ona pia vichwa, “Nafsi” na “Roho.”
Je, wafu wanaweza kuwasaidia au kuwadhuru walio hai kwa njia yoyote?
Mhu. 9:6: “Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua.”
Isa. 26:14: “Wao wamekufa; hawataishi. Wakiwa ni wasiojiweza katika kifo, hawataamka.”
Namna gani habari zinazotolewa na watu ambao wamerudiwa na fahamu baada ya kusemekana kwamba wamekufa na ambao walisema kuhusu maisha mengine?
Kwa kawaida, baada ya mtu kuacha kupumua na moyo kuacha kupiga, inachukua dakika kadhaa kabla ya nguvu za uhai kukoma hatua kwa hatua katika chembe za mwili. Jambo hilo linaweza kukawizwa kwa muda wa saa kadhaa mwili ukiwekwa katika baridi kali. Kwa sababu hiyo, mara nyingine inawezekana kumrudishia mtu fahamu kwa kuanzisha tena utendaji wa moyo na mapafu. Ingawa walionwa kana kwamba wamekufa, chembe zao za mwili zilikuwa bado zingali hai.
Watu wengi waliorudiwa na fahamu baada ya “kifo” cha aina hiyo, hawakumbuki lolote. Wengine husema walihisi ni kana kwamba walikuwa wakielea. Wengine husema waliona vitu vizuri; wengine waliogopeshwa na mambo yaliyowapata.
Je, kuna njia yoyote ya kitiba inayoweza kueleza kinachosababisha hali hizo?
Mhariri wa gazeti la kitiba la The Arizona Republic aliandika hivi: “Wakati nguvu za mwili zinapopungua sana, kama wakati ambapo mtu amepewa dawa ya kuondoa fahamu, au kwa sababu ya magonjwa au majeraha, uwezo wa mwili wa kuendeleza utendaji mbalimbali mwilini hupungua kabisa. Kwa hiyo, homoni za neva na umajimaji mwingine wa mfumo wa neva huenea kwa wingi mwilini. Baadhi ya matokeo yake ni kwamba mtu huyo anaweza kuona na kusikia mambo yasiyokuwako ambayo baada ya kurudiwa na fahamu humfanya afikiri kwamba alikuwa amekufa na sasa amefufuka.”—Mei 28, 1977, uku. C-1; pia jarida la kitiba la Ujerumani Fortschritte der Medizin, Na. 41, 1979; Psychology Today, Januari 1981.
Je, si kweli kwamba ushuhuda wa wale waliorudishiwa fahamu unathibitishwa na watu ambao wapendwa wao waliokufa wamewatokea na kusema nao?
Tafadhali, soma tena maandiko yaliyotangulia kunukuliwa kuhusu hali ya wafu. Neno la Mungu la kweli linatuambia nini kuhusu hali ya wafu?
Ni nani anayetaka wanadamu wasiamini maandiko hayo? Yehova alipowaonya wazazi wetu wa kwanza kwamba kutotii kungeleta kifo, ni nani aliyeyapinga maneno hayo? “Nyoka [aliyetumiwa na Shetani; ona Ufunuo 12:9.] akamwambia mwanamke: ‘Hakika hamtakufa.’” (Mwa. 3:4) Bila shaka, baadaye Adamu na Hawa walikufa. Kwa wazi, basi, ni nani aliyetunga lile wazo kwamba sehemu ya roho ya mwanadamu inabaki hai wakati mwili unapokufa? Kama vile tulivyokwisha kuona, Neno la Mungu halisemi hivyo. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli wa kale ilishutumu zoea la kuwasiliana na wafu kuwa ‘najisi’ na “chukizo.” (Law. 19:31; Kum. 18:10-12; Isa. 8:19) Je, Mungu mwenye upendo angeshutumu zoea hilo ikiwa walio hai wangekuwa wakiwasiliana tu na wapendwa wao ambao wamekufa? Kwa upande mwingine, ikiwa roho waovu wangekuwa wakichukua maumbo ya watu waliokufa na kuwapotosha wanadamu kwa kutia katika akili zao maoni ambayo yanaendeleza uwongo, je, halingekuwa jambo la upendo kwa Mungu kuwalinda watumishi wake dhidi ya udanganyifu huo?—Efe. 6:11, 12.
Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika desturi za kimapokeo za kuwaomboleza wafu?
Mpendwa wetu anapokufa, ni jambo la kawaida kuwa na huzuni, na si kosa kuonyesha huzuni
Baada ya kifo cha rafiki yake mkubwa Lazaro, ‘Yesu alitokwa na machozi.’ (Yoh. 11:35) Mara nyingine watumishi wa Mungu hupatwa na huzuni nyingi kwa sababu ya kifo.—2 Sam. 1:11, 12.
Lakini kwa sababu ya tumaini la ufufuo, Wakristo wanaambiwa hivi: “Hatutaki mkose kujua kuhusu wale walalao usingizi katika kifo; ili msiwe na huzuni kama wale watu wengine wasio na tumaini.”—1 The. 4:13.
Watumishi wa Yehova hawakatai desturi zote zinazohusiana na kifo
Mwa. 50:2, 3: “Yosefu akawaamuru watumishi wake, matabibu, wampake baba yake dawa ya kumfanya asioze . . . nao wakatumia siku 40 kamili kwa ajili yake, kwa maana hiyo ndiyo hesabu ya siku ambazo kwa desturi wao hutumia kupaka dawa ya kumfanya mtu asioze.”
Yoh. 19:40: “Wakauchukua mwili wa Yesu na kuufunga kwa vitambaa pamoja na manukato, sawa na jinsi Wayahudi walivyo na desturi ya kutayarisha kwa ajili ya maziko.”
Watu wanaotaka kumpendeza Mungu huepuka desturi ambazo hazipatani na Neno lake
Desturi fulani huonyesha waziwazi huzuni ya mtu. Lakini Yesu alisema: “Wakati mnapofunga [kwa sababu ya huzuni], msiwe na nyuso zenye huzuni kama wanafiki, kwa maana wao hukunja nyuso zao ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Kwa kweli ninawaambia ninyi, Wanapata thawabu yao kwa ukamili. Lakini wewe, unapofunga, paka kichwa chako mafuta na unawe uso wako, ili uonekane kuwa unafunga, si na wanadamu, bali na Baba yako aliye mahali pa siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.”—Mt. 6:16-18.
Desturi fulani zinatokana na imani ya kwamba mtu ana nafsi isiyoweza kufa ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa na, kwa hiyo, inajua yale ambayo walio hai wanafanya. Lakini Biblia inasema hivi: “Wafu . . . hawajui lolote kamwe.” (Mhu. 9:5) Pia, “Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.”—Eze. 18:4.
Desturi nyingi hutokana na imani ya kwamba wafu wanahitaji msaada wa walio hai au hutokana na kuogopa kwamba huenda wafu wakawadhuru walio hai ikiwa hawatatulizwa. Lakini Neno la Mungu linaonyesha kwamba wafu hawahisi maumivu wala raha. “Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Zab. 146:4; ona pia 2 Sam. 12:22, 23.) “Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua.”—Mhu. 9:6.
Mtu Akisema—
‘Ni mapenzi ya Mungu’
Unaweza kujibu: ‘Watu wengi huamini hivyo. Lakini nimeona ni muhimu kuchunguza yale ambayo Mungu anasema kuhusu jambo hilo.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘(Soma Mwanzo 2:17.) Baba akimwonya mwanawe kwamba kufanya jambo fulani kutahatarisha uhai wake, je, ungesema kwamba baba huyo anataka mwanawe afanye jambo hilo?’ (2) ‘Basi mapenzi ya Mungu kuwahusu wanadamu ni nini? Yesu alisema hivi: “Haya ndiyo mapenzi ya Baba yangu, kwamba kila mtu ambaye humtazama Mwana [yaani, anatambua na kukiri kwamba Yesu kwa kweli ndiye Mwana wa Mungu] na kumwamini awe na uzima wa milele, nami nitamfufua katika siku ya mwisho.” (Yoh. 6:40)’
‘Watu wataendelea kufa sikuzote’
Unaweza kujibu: ‘Wanadamu wamekuwa wakifa mpaka leo hii, sivyo?’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Lakini ona ahadi hii nzuri ajabu ambayo Mungu anatoa katika Ufunuo 21:3, 4 (au Isaya 25:8).’
‘Mtu hufa wakati wake unapofika’
Unaweza kujibu: ‘Watu wengi wana maoni kama yako. Je, unajua kwamba Wagiriki wengi wa kale walikuwa na maoni hayohayo? Waliamini kwamba kulikuwa na miungu mitatu ya kike iliyoamua muda ambao kila mwanadamu angeishi. Lakini Biblia ina maoni tofauti kabisa kuhusu maisha.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘(Soma Mhubiri 9:11.) Mfano: Jiwe linaweza kuvunjika kutoka kwenye nyumba na kumwangukia mpita-njia. Je, Mungu ndiye aliyesababisha jambo hilo? Ikiwa hivyo ndivyo ilivyo, je, ni haki kumshtaki mwenye nyumba kwa sababu ya uzembe? . . . Kama Biblia inavyosema, kwa mpita-njia huyo, tukio hilo halikuwa limepangwa mapema wala halikuwa limetarajiwa, bali alikuwa papo hapo wakati jiwe hilo lilipoanguka.’ (2) ‘Biblia inatuambia kwamba tukiepuka mwenendo mbaya, tutaulinda uhai wetu. (Met. 16:17) Ikiwa wewe ni mzazi, nina hakika kwamba unatumia kanuni hiyohiyo unapowafundisha watoto wako. Unawaonya juu ya mambo ambayo yanaweza kusababisha kifo. Yehova anawafanyia wanadamu wote jambo hilohilo leo.’ (3) ‘Yehova anajua yatakayotokea wakati ujao. Kupitia Biblia yeye anatuambia jinsi tunavyoweza kufurahia maisha marefu zaidi kuliko yale ya watu wanaopuuza maneno yake. (Yoh. 17:3; Met. 12:28)’ (Ona pia kichwa, “Majaliwa.”)