Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • T-16 kur. 2-6
  • Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?
  • Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kifo, na Lile Linalotukia Wakati Sisi Tunapokufa
  • Jinsi Wanadamu Wanavyoweza Kuishi Tena
  • Wakati Mpendwa Anapokufa
  • Inakuwaje kwa Wapendwa Wetu Waliokufa?
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Inakuwaje Wakati wa Kufa?
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Faraja kwa Waombolezao
    Amkeni!—2002
  • Swali la 2: Ni Nini Kitakachonipata Nitakapokufa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?
T-16 kur. 2-6

Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa?

“Mtu akifa, je! atakuwa hai tena?” mwanamume Ayubu akauliza hivyo zamani za kale. (Ayubu 14:14) Labda wewe, pia, umetaka kujua jambo hilo. Wewe ungehisi jinsi gani kama ungejua kwamba inawezekana kuungana tena pamoja na wapendwa wako papa hapa duniani chini ya hali zilizo bora kabisa?

Basi, Biblia inatoa ahadi hii: “Wafu wako wataishi. . . . Watainuka.” Na Biblia inasema hivi pia: “Wenye haki watairithi [dunia, NW], nao watakaa humo milele.”—Isaya 26:19; Zaburi 37:29.

Ili kuwe na uhakika wa kweli kweli katika ahadi hizo, sisi tunahitaji kujiuliza maulizo fulani ya msingi: Kwa sababu gani watu wanakufa? Wafu wako wapi? Na tunaweza kuwaje na uhakika kwamba wanaweza kuishi tena?

Kifo, na Lile Linalotukia Wakati Sisi Tunapokufa

Biblia inaeleza wazi kwamba Mungu hakukusudia hapo kwanza wanadamu wafe. Yeye aliumba watu wawili wa kwanza Adamu na Hawa, akawaweka katika paradiso ya kidunia iliyoitwa Edeni, na kuwaagiza wawe na watoto na kupanua kao lao la Paradiso lifike duniani pote. Wao wangekufa ikiwa tu wangekosa kutii maagizo yake.—Mwanzo 1:28; 2:15-17.

Wakiwa na ukosefu wa uthamini kwa fadhili za Mungu, Adamu na Hawa walikosa kutii na wakatozwa adhabu waliokuwa wameambiwa. ‘Utairudia ardhi,’ Mungu akamwambia Adamu, ‘ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’ (Mwanzo 3:19) Kabla ya kuumbwa kwake Adamu hakuwako; yeye alikuwa mavumbi. Na kwa kutokutii, au dhambi yake, Adamu alihukumiwa kurudi kwenye mavumbi, kwenye hali ya kutokuwako.

Hivyo kifo ni kutokuwapo kwa uzima. Biblia inaweka utofautiano kati ya mambo hayo mawili: “Mshahara wa dhambi ni kifo; lakini zawadi anayotoa Mungu ni uzima wa milele.” (Warumi 6:23, Habari Njema kwa Watu Wote) Ikionyesha kwamba kifo ni hali ya kutokuwa na fahamu kabisa, Biblia inasema: “Kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5) Wakati mtu anapokufa, Biblia inaeleza hivi: “Pumzi yake hutoka, hurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:3, 4.

Hata hivyo, kwa kuwa ni Adamu na Hawa peke yao waliokosa kutii amri hiyo katika Edeni, kwa sababu gani sisi sote tunakufa? Ni kwa sababu sisi sote tulizaliwa baada ya kutokutii kwa Adamu, na kwa hiyo sisi sote tulirithi dhambi na kifo kutoka kwake. Ni kama vile Biblia inavyoeleza: “Kwa mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote.”—Warumi 5:12; Ayubu 14:4.

Hata hivyo huenda mtu fulani akauliza: ‘Je! wanadamu hawana nafsi isiyoweza kufa ambayo inaendelea kuwa hai baada ya kifo?’ Wengi wamefundisha hivyo, hata wakasema kwamba kifo ni mlango wa kuingia katika uzima mwingine. Lakini wazo hilo halitokani na Biblia. Bali, Neno la Mungu linafundisha kwamba wewe ni nafsi, kwamba nafsi yako ni wewe tu, ukiwa pamoja na sifa zako zote za kimwili na kiakili. (Mwanzo 2:7; Yeremia 2:34; Mithali 2:10) Pia, Biblia inasema: “Nafsi inayofanya dhambi—hiyo yenyewe ndiyo itakayokufa.” (Ezekieli 18:4, NW) Hakuna mahali ambako Biblia inafundisha kwamba mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa inayoendelea kuwa hai baada ya kufa kwa mwili.

Jinsi Wanadamu Wanavyoweza Kuishi Tena

Baada ya dhambi na kifo kuingia ulimwenguni, Mungu alifunua kwamba lilikuwa kusudi lake kwamba wafu warudishwe kwenye uzima kwa njia ya ufufuo. Hivyo Biblia inaeleza: “Abrahamu . . . alihesabu kwamba Mungu alikuwa na uwezo wa kumwinua [Isaka mwanaye] hata kutoka kwa wafu.” (Waebrania 11:17-19, NW) Uhakika wa Abrahamu haukuwekwa mahali pasipofaa, kwa maana Biblia inasema hivi juu ya Mwenye Nguvu Zote: “Naye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai; kwa kuwa wote huishi kwake.”—Luka 20:37, 38.

Ndiyo, Mungu Mwenye Nguvu Zote hana uwezo tu bali pia ana tamaa ya kufufua wafu ambao yeye anachagua. Yesu Kristo mwenyewe alisema: “Msione hili kuwa ajabu, kwa sababu ile saa inakuja ambayo katika hiyo wale wote walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake watoke.”—Yohana 5:28, 29, NW; Matendo 24:15.

Si muda mrefu baada ya yeye kusema hilo, Yesu alikutana na andamano la maziko likitoka katika mji wa Kiisraeli wa Naini. Mwanamume yule mfu kijana alikuwa ndiye mtoto wa pekee wa mjane mmoja. Alipoona kihoro kingi sana sana cha mwanamke yule, Yesu aliguswa moyo kuona huruma. Kwa hiyo, akiiambia ile maiti, yeye akaamuru: “Kijana, nakuambia, Inuka”! Na mwanamume huyo akaketi, naye Yesu akampa kwa mamaye.—Luka 7:11-17.

Kama ilivyokuwa katika kisa cha mjane huyo, kulikuwa pia na furaha kuu wakati Yesu alipotembelea kao la Yairo, afisa-msimamizi wa sinagogi la Kiyahudi. Binti yake mwenye umri wa miaka 12 alikuwa amekufa. Lakini Yesu alipofika kwenye kao la Yairo, alienda alikokuwa mtoto yule mfu na kusema: “Msichana, amka!” Naye akafanya hivyo!—Luka 8:40-56, NW.

Baadaye, Lazaro rafiki wa Yesu alikufa. Wakati Yesu alipofika kwenye kao lake, Lazaro alikuwa amekuwa mfu kwa siku nne. Ingawa alikuwa na kihoro kingi sana sana, Martha dada yake alijieleza kuwa mwenye tumaini, akisema: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” Lakini Yesu alienda kwenye kaburi lile, akaagiza jiwe liondolewe, na kuita hivi: “Lazaro, njoo huku nje”! Naye akafanya hivyo!—Yohana 11:11-44.

Sasa fikiria jambo hili: Hali ya Lazaro ilikuwa nini wakati wa siku nne hizo alipokuwa mfu? Lazaro hakusema lo lote juu ya kuwa katika mbingu ya raha nyingi sana au moto wa mateso, jambo ambalo kwa uhakika angalifanya kama angalikuwa amekuwa kule. Hapana, Lazaro alikuwa hana fahamu kabisa katika kifo na angalibaki akiwa hivyo mpaka “ufufuo siku ya mwisho” kama Yesu hangalimrudishia uhai.

Ni kweli kwamba miujiza hiyo ya Yesu ilikuwa yenye manufaa ya muda tu, kwa kuwa wale ambao yeye alifufua walikufa tena. Hata hivyo, yeye alitoa uthibitisho miaka 1,900 iliyopita kwamba, kwa uwezo wa Mungu, wafu wanaweza kuishi tena kweli kweli! Kwa hiyo kwa miujiza yake Yesu alionyesha kwa kadiri ndogo mambo yatakayotukia duniani chini ya Ufalme wa Mungu.

Wakati Mpendwa Anapokufa

Wakati adui kifo anapopiga, kihoro chako kinaweza kuwa kikuu, hata ingawa huenda wewe ukawa una tumaini katika ufufuo. Abrahamu alikuwa na imani kwamba mke wake angeishi tena, na bado tunasoma kwamba “Abrahamu akafika kuomboleza Sara na kumulilia.” (Mwanzo 23:2, Zaire Swahili Bible) Na namna gani juu ya Yesu? Wakati Lazaro alipokufa, yeye “aliugua rohoni, akafadhaika roho yake,” na muda mfupi baada ya hapo “akalia machozi.” (Yohana 11:33, 35) Kwa hiyo, wakati mtu fulani unayependa anapokufa, kulia hakuonyeshi udhaifu.

Wakati mtoto anapokufa, inakuwa vigumu hasa kwa mama yake. Hivyo Biblia inakiri kwamba mama anaweza kuhisi kihoro kichungu. (2 Wafalme 4:27) Bila shaka, ni vigumu kwa baba aliyefiwa pia. “O laiti mimi ningalikufa, mimi mwenyewe, badala ya wewe,” akaomboleza Mfalme Daudi wakati Absalomu mwanaye alipokufa.—2 Samweli 18:33, NW.

Hata hivyo, kwa sababu wewe una uhakika katika ufufuo, huzuni yako haitakuwa isiyopungua. Kama vile Biblia inavyosema, wewe ‘hutahuzunika kama wengine wasio na tumaini.’ (1 Wathesalonike 4:13) Bali, utamkaribia Mungu katika sala, na Biblia inaahidi kwamba ‘yeye atakutegemeza.’—Zaburi 55:22.

Isipokuwa imeonyeshwa vingine, mitajo yote ya Biblia imetolewa katika Biblia ya Union Version na New World Translation of the Holy Scriptures (NW) ya Kiingereza.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki