Roho ya Ulimwengu
Maana: Nguvu zinazowachochea wanadamu ambao si watumishi wa Yehova Mungu, zikiwafanya watu hao waseme na kutenda mambo kulingana na tabia fulani ya kawaida. Ijapokuwa watu hutenda kulingana na mapendezi yao binafsi, wale walio na roho ya ulimwengu wana maelekeo fulani ya msingi, njia za kutenda mambo, na miradi maishani ambayo ni kawaida ya mfumo wa mambo uliopo ambao mungu na mtawala wake ni Shetani.
Kwa nini mtu anapaswa kuhangaikia kwa uzito asitiwe uchafu na roho ya ulimwengu?
1 Yoh. 5:19: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Shetani amesitawisha roho inayotawala fikira na shughuli za wanadamu ambao si watumishi waliokubaliwa wa Yehova. Ni roho ya ubinafsi na kiburi ambayo imeenea sana hivi kwamba ni kama hewa ambayo wanadamu wanapumua. Tunahitaji kuwa waangalifu sana ili tusijiweke chini ya mamlaka ya Shetani kwa kuruhusu roho hiyo iongoze maisha yetu.)
Ufu. 12:9: “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.” (Tangu jambo hilo litukie, baada ya kuzaliwa kwa Ufalme mwaka wa 1914, uvutano wa Shetani na roho wake waovu umeongezeka sana kati ya wanadamu. Roho yake imewachochea watu wawe na ubinafsi na jeuri zaidi. Hasa wale wanaojaribu kumtumikia Yehova husongwa sana ili wawe sehemu ya ulimwengu, watende kama wengine wanavyotenda, na kuacha ibada ya kweli.)
Baadhi ya tabia za roho ya ulimwengu tunazopaswa kuziepuka ni gani?
1 Kor. 2:12: “Basi sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.” (Roho ya ulimwengu ikitia mizizi katika fikira na tamaa za mtu, upesi matunda yake huonekana katika matendo yanayoonyesha roho hiyo. Kwa hiyo, kuachana na roho ya ulimwengu hutaka, si kuepuka tu matendo yasiyo ya Kikristo na mambo yanayopita kiasi, bali pia kufikia msingi wa jambo lenyewe kwa kusitawisha mitazamo inayoonyesha roho ya Mungu na kuzipenda kikweli njia zake. Unapaswa kukumbuka jambo hilo unapofikiria mambo yanayofuata ambayo huonyesha roho ya ulimwengu.)
Mtu kufanya mambo anayotaka, bila kujali mapenzi ya Mungu
Shetani alimhimiza Hawa ajiamulie mwenyewe yaliyokuwa mema na yaliyokuwa mabaya. (Mwa. 3:3-5; kwa kutofautisha ona Methali 3:5, 6.) Wengi wanaofuata mwendo wa Hawa hawajui mapenzi ya Mungu kwa wanadamu, wala hawataki kuyajua. Wao hufanya wapendavyo tu. Wale wanaojua matakwa ya Mungu na kujaribu kuyafuata wanahitaji kuwa waangalifu ili roho ya ulimwengu isiwafanye wapuuze kimakusudi shauri la Neno la Mungu kuhusu yale ambayo huenda wakayaona kuwa ‘mambo madogo.’—Luka 16:10; ona pia kichwa “Uhuru.”
Kutenda mambo kwa kiburi
Shetani ndiye aliyeanza kuruhusu hali ya kujiona kupita kiasi iharibu moyo wake. (Linganisha na Ezekieli 28:17; Methali 16:5.) Kiburi ni nguvu zinazoleta migawanyiko katika ulimwengu ambao Shetani anautawala, kikiwafanya watu wajione kuwa bora kuliko wale wa makabila mengine, mataifa mengine, lugha nyingine, na hadhi za kiuchumi. Hata wale wanaomtumikia Mungu huenda wakahitaji kuondoa kabisa maoni hayo. Wanahitaji pia kujilinda ili kiburi kisije kikasababisha wayafanye mambo madogo kuwa makubwa, au kiwazuie kukubali makosa yao wenyewe na kupokea shauri na hivyo wafaidike na msaada mwingi wa upendo ambao Yehova huandaa kupitia tengenezo lake.—Rom. 12:3; 1 Pet. 5:5.
Kuonyesha mtazamo wa kuasi mamlaka
Shetani, ambaye jina lake linamaanisha “Mpinzani,” ndiye aliyeanzisha uasi. Kwa kumkaidi Yehova, Nimrodi, ambaye jina lake huenda likamaanisha “Acheni Sisi Tuasi,” alionyesha kwamba yeye alikuwa mtoto wa Shetani. Kuiepuka roho hiyo kutawazuia watu wanaomwogopa Mungu wasiwakaidi watawala wa kilimwengu (Rom. 13:1); kutawasaidia watoto watii mamlaka ya wazazi wao inayotoka kwa Mungu (Kol. 3:20); kutakuwa ulinzi dhidi ya kuunga mkono waasi-imani, ambao hawawaheshimu wale ambao Yehova amewakabidhi madaraka katika tengenezo lake linaloonekana.—Yuda 11; Ebr. 13:17.
Kufuatilia tamaa za mwili wenye dhambi
Uvutano huo unaweza kuonwa na kusikiwa kila mahali. Kuna uhitaji wa kujilinda daima tusiwe na tamaa hizo. (1 Yoh. 2:16; Efe. 4:17, 19; Gal. 5:19-21) Fikira na tamaa ambazo huenda zikathibitisha kwa uzito jambo hilo huenda zikaonekana katika maneno ya mtu, mizaha anayosimulia, muziki anaosikiliza, dansi anazocheza, au kutazama sinema zinazoonyesha ngono zisizo za adili. Sehemu hii ya roho ya ulimwengu inajionyesha katika kutumia vibaya dawa za kulevya, ulevi, uzinzi, uasherati, na kufanya ngono na watu wa jinsia moja. Jambo hilo huonekana pia wakati mtu anapomtaliki mwenzake na kumchukua mwingine, labda kisheria, lakini kinyume cha Maandiko.—Mal. 2:16.
Mtu kuruhusu maisha yake yatawaliwe na tamaa ya kupata vitu anavyoona
Shetani alisitawisha tamaa hiyo ndani ya Hawa, akamshawishi afanye jambo lililoharibu uhusiano wake na Mungu. (Mwa. 3:6; 1 Yoh. 2:16) Yesu alikataa kwa uthabiti kishawishi cha namna hiyo. (Mt. 4:8-10) Wale wanaotaka kumpendeza Yehova wanahitaji kujilinda wasije wakaruhusu ulimwengu wa kibiashara usitawishe roho kama hiyo ndani yao. Watu wanaonaswa na mtego huo hupata huzuni nyingi na kuangamia kiroho.—Mt. 13:22; 1 Tim. 6:7-10.
Mtu kujionyesha mali zake na mambo yanayodhaniwa kuwa mafanikio
Zoea hilo, pia, “hutokana na ulimwengu” na wale wanaokuwa watumishi wa Mungu wanahitaji kuliacha kabisa. (1 Yoh. 2:16) Linatokana na kiburi, na badala ya kujenga wengine kiroho, huwawekea vishawishi vya vitu vya kimwili na miradi ya kupata mafanikio ya kilimwengu.—Rom. 15:2.
Mtu kuonyesha hisia zake kwa kutumia matukano na matendo ya jeuri
Hayo ni “matendo ya mwili” ambayo watu wengi wanapaswa kupigana sana nayo. Wakiwa na imani ya kweli na msaada wa roho ya Mungu, wanaweza kuushinda ulimwengu badala ya kuacha roho yake iwatawale.—Gal. 5:19, 20, 22, 23; Efe. 4:31; 1 Kor. 13:4-8; 1 Yoh. 5:4.
Mtu kuutumaini na kuutegemea uwezo wa wanadamu kutatua mahangaiko yake
Mtu wa kimwili huona kwamba yale anayoweza kuona na kugusa ndiyo mambo muhimu kikweli. Matumaini na mahangaiko yake hutegemea ahadi na vitisho vya wanadamu wengine. Yeye huwategemea wanadamu wanaotawala wamsaidie, naye hukata tamaa wanaposhindwa. (Zab. 146:3, 4; Isa. 8:12, 13) Kwa maoni yake, hakuna uzima mwingine. Hatari ya kifo humfanya kuwa mtumwa kwa urahisi. (Kwa kutofautisha, ona Mathayo 10:28; Waebrania 2:14, 15.) Lakini nguvu mpya huendesha akili za watu wanaopata kumjua Yehova, wale wanaojaza ahadi zake katika akili na mioyo yao, na wanaojifunza kumwomba msaada kila wakati wanapokuwa na uhitaji.—Efe. 4:23, 24; Zab. 46:1; 68:19.
Kuwapa wanadamu na vitu heshima ya ibada ambayo ni haki ya Mungu
“Mungu wa mfumo huu wa mambo,” Shetani Ibilisi, huchochea matendo yote mbalimbali ambayo hupotosha mwelekeo wa ibada ambao Mungu alimpa mwanadamu. (2 Kor. 4:4) Watawala fulani wametendewa kama miungu. (Mdo. 12:21-23) Mamilioni ya watu husujudia sanamu. Mamilioni zaidi huwatukuza waigizaji na wanamichezo mashuhuri. Mara nyingi sherehe huwapa wanadamu fulani heshima wasiyostahili. Roho hii imeenea sana hivi kwamba wale wanaompenda Yehova kikweli na wanaotaka kumtolea ibada ya pekee wanahitaji kukaa macho kila siku ili wajiepushe na uvutano wa roho hiyo.