Yehova
Maana: Jina la Mungu wa pekee wa kweli. Jina alilojipatia yeye mwenyewe. Yehova ndiye Muumba na, kwa haki, ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu mzima. “Yehova” hutafsiriwa kutoka Herufi Nne za Kiebrania, יהוה, ambazo humaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Katika lugha nyingi, herufi hizo nne za Kiebrania huwakilishwa na herufi JHVH au YHWH.
Jina la Mungu hupatikana wapi katika Bibia zinazotumiwa na watu wengi leo?
The New English Bible: Jina Yehova hupatikana katika Kutoka 3:15; 6:3. Ona pia Mwanzo 22:14; Kutoka 17:15; Waamuzi 6:24; Ezekieli 48:35. (Lakini ikiwa tafsiri hii na nyinginezo hutumia “Yehova” mahali kadhaa, kwa nini lisitumiwe kila mahali ambapo zile Herufi Nne hupatikana katika maandishi ya Kiebrania?)
Revised Standard Version: Kielezi-chini katika Kutoka 3:15 husema: “Neno hili BWANA linapoandikwa kwa herufi kubwa, huwakilisha jina la Mungu, YHWH.”
Today’s English Version: Kielezi-chini katika Kutoka 6:3 husema hivi: “BWANA: . . . Mahali ambapo maandishi ya Kiebrania yana jina Yahweh, ambalo mara nyingi hutoholewa kuwa Yehova, tafsiri hii hutumia jina BWANA kwa herufi kubwa, kama ilivyo katika tafsiri nyingi za Kiingereza.”
King James Version: Jina Yehova linapatikana katika Kutoka 6:3; Zaburi 83:18; Isaya 12:2; 26:4. Ona pia Mwanzo 22:14; Kutoka 17:15; Waamuzi 6:24.
American Standard Version: Katika tafsiri hii, jina Yehova linatumiwa kotekote katika Maandiko ya Kiebrania, kuanzia Mwanzo 2:4.
Douay Version: Kielezi-chini katika Kutoka 6:3 husema: “Jina langu Adonai. Jina, lililo katika maandishi ya Kiebrania, ndilo jina la Mungu linalofaa zaidi, linaloonyesha kuwako kwake kwa milele, (Kut. 3, 14,) ambalo Wayahudi kwa sababu ya heshima nyingi hawalitamki kamwe; bali, badala yake, popote linapopatikana katika Biblia, wao husoma Adonai, linalomaanisha Bwana; na kwa hiyo, wao huweka nukta au irabu, ambazo ni za jina Adonai, kwenye herufi nne za lile jina lingine lisiloweza kutamkwa, Jod, He, Vau, He. Kwa sababu hiyo watu fulani wa kisasa wametunga jina Yehova, lisilojulikana kwa watu wote wa kale, wawe Wayahudi au Wakristo; kwa sababu ya kutotumiwa kwa muda mrefu, matamshi yenyewe ya jina hilo, lililo katika maandishi ya Kiebrania, sasa yamesahaulika kabisa.” (Inapendeza kwamba The Catholic Encyclopedia [1913, Buku la 8, uku. 329] husema hivi: “Yehova, jina la Mungu katika Agano la Kale; kwa hiyo Wayahudi waliliita lile jina tukufu, lile jina kuu, lile jina la pekee.”)
The Holy Bible iliyotafsiriwa na Ronald A. Knox: Jina Yahweh linapatikana kwenye vielezi-chini katika Kutoka 3:14 na 6:3.
The New American Bible: Kielezi-chini katika Kutoka 3:14 hupendelea jina “Yahweh,” lakini jina hilo halionekani katika maandiko yenyewe ya tafsiri hiyo. Ona pia nyongeza inayoitwa Bible Dictionary chini ya “Lord” na “Yahweh,” katika Saint Joseph Edition.
The Jerusalem Bible: Zile Herufi Nne za Kiebrania zimetafsiriwa kuwa Yahweh, kuanzia mahali ambapo zinapatikana kwanza, katika Mwanzo 2:4.
Tafsiri ya Ulimwengu Mpya: Katika tafsiri hii, jina Yehova linatumiwa katika Maandiko ya Kiebrania na pia katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Linapatikana mara 7,210.
An American Translation: Katika Kutoka 3:15 na 6:3 jina Yahweh limetumiwa, likifuatwa na “BWANA” katika mabano.
The Bible in Living English, S. T. Byington: Jina Yehova limetumiwa katika Maandiko yote ya Kiebrania.
The ‘Holy Scriptures’ iliyotafsiriwa na J. N. Darby: Jina Yehova linapatikana katika Maandiko yote ya Kiebrania, pia katika vielezi-chini vingi katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kuanzia Mathayo 1:20.
The Emphatic Diaglott, Benjamin Wilson: Jina Yehova linapatikana katika Mathayo 21:9 na mahali penginepo 17 katika tafsiri hii ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
The Holy Scriptures According to the Masoretic Text—A New Translation, Jewish Publication Society of America, Max Margolis mhariri mkuu: Kwenye Kutoka 6:3 zile Herufi Nne za Kiebrania hupatikana katika Kiingereza.
The Holy Bible iliyotafsiriwa na Robert Young: Jina Yehova linapatikana katika Maandiko yote ya Kiebrania katika tafsiri hii sisisi.
Union Version: Jina Yehova linapatikana katika Kutoka 6:2, 3, 6-8; Zaburi 68:20; 83:18; Isaya 12:2; 26:4; 49:14. Ona pia Mwanzo 22:14; Kutoka 17:15; Waamuzi 6:24, Yeremia 16:21; Habakuki 3:19.
Biblia Habari Njema: Kielezi-chini katika tafsiri hii husema hivi: “Katika makala ya Kiebrania ni Yahweh, jina takatifu la Mungu ambalo katika utamaduni wa Wayahudi halikutamkwa.”
Zaire Swahili Bible: Jina Yehova linapatikana katika Kutoka 6:2, 3; Zaburi 83:18; Isaya 12:2; 26:4. Ona pia Mwanzo 22:14; Kutoka 17:15; Yeremia 16:21; Habakuki 3:19.
Verbum Bible: Kielezi-chini katika Kutoka 3:14 husema hivi: “Mungu anajifumbua kwa jina la Yahwe, maana yake ‘Ndimi.’”
Kwa nini tafsiri nyingi za Biblia hazitumii jina la Mungu au hulitumia mara chache tu?
Dibaji ya Revised Standard Version husema hivi: “Halmashauri imerudia matumizi ya King James Version kwa sababu mbili: (1) neno ‘Yehova’ haliwakilishi kwa usahihi namna yoyote ya Jina lililotumiwa katika Kiebrania; na (2) matumizi ya jina lolote la Mungu mmoja na wa pekee, kana kwamba kulikuwako miungu mingine ambayo alipaswa kujitofautisha nayo, yalikoma katika dini ya Kiyahudi kabla ya wakati wa Kikristo na haifai kabisa kulitumia katika imani ya Kanisa zima la Kikristo.” (Kwa hiyo, maoni yao wenyewe kuhusu jambo linalofaa yametumiwa kuwa msingi wa kuondoa katika Biblia Takatifu jina la Mtungaji wake, Mungu, ambaye jina lake linapatikana katika lugha ya kwanza ya Kiebrania mara nyingi kuliko jina lingine lolote au cheo chochote. Wanakubali kwamba wanafuata kielelezo cha wafuasi wa dini ya Kiyahudi, ambao Yesu alisema hivi kuwahusu: “Mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.”—Mt. 15:6.)
Watafsiri ambao wamehisi kwamba wana wajibu wa kulitia jina la Mungu angalau mara moja au labda mara kadhaa katika maandiko yenyewe, ijapokuwa hawakufanya hivyo kila mara linapopatikana katika Kiebrania, kwa wazi wamefuata kielelezo cha William Tyndale, aliyetia jina la Mungu katika tafsiri yake ya Pentateuki iliyochapishwa mwaka wa 1530, hivyo akibadili lile zoea la kuliacha kabisa jina hilo.
Je, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walioongozwa na roho ya Mungu walilitumia jina Yehova?
Jerome, katika karne ya nne, aliandika hivi: “Mathayo, ambaye pia ni Lawi, ambaye aliacha kazi ya kukusanya kodi akawa mtume, kwanza kabisa alitunga Injili ya Kristo huko Yudea katika lugha na herufi za Kiebrania kwa faida ya waamini waliokuwa wakitahiriwa.” (De viris inlustribus, sura ya 3) Injili hiyo inatia ndani manukuu 11 ya moja kwa moja ya sehemu za Maandiko ya Kiebrania ambamo zile Herufi Nne zinapatikana. Hakuna sababu yoyote ya kuamini kwamba Mathayo hakunukuu mistari hiyo jinsi ilivyokuwa imeandikwa katika maandishi ya Kiebrania aliyoyanukuu.
Waandikaji wengine walioongozwa na roho ya Mungu ambao walichangia yaliyomo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walinukuu mamia ya mistari kutoka katika Septuajinti, tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania katika Kigiriki. Mistari mingi ilikuwa na zile Herufi Nne za Kiebrania katika nakala za Kigiriki za Septuajinti za kwanza. Kupatana na maoni ya Yesu mwenyewe kuhusu jina la Baba yake, wanafunzi wa Yesu wangeendelea kutumia jina hilo katika manukuu yao.—Linganisha na Yohana 17:6, 26.
Katika Journal of Biblical Literature, George Howard wa Chuo Kikuu cha Georgia aliandika hivi: “Sisi tunajua hakika kwamba Wayahudi wanaosema Kigiriki waliendelea kuandika יהוה katika Maandiko yao ya Kigiriki. Isitoshe, haielekei kwamba Wakristo wa kwanza Wayahudi wasemao Kigiriki wasiopenda mabadiliko walikuwa tofauti. Ijapokuwa huenda walimrejelea Mungu kwa kutumia maneno [Mungu] na [Bwana], lingalikuwa jambo lisilo la kawaida kabisa kwao kuondoa zile Herufi Nne kutoka katika maandishi ya Biblia yenyewe. . . . Kwa kuwa Herufi Nne hizo bado zilikuwa zimeandikwa katika nakala za Biblia ya Kigiriki ambayo ndiyo iliyokuwa Maandiko ya kanisa la kwanza, tunaweza kuamini kwamba waandikaji wa A[gano] J[ipya], walipokuwa wakinukuu kutoka katika Maandiko, walizitumia zile Herufi Nne katika maandishi ya Biblia. . . . Lakini zilipoondolewa katika A[gano] la K[ale] la Kigiriki, ziliondolewa pia katika manukuu ya A[gano] la K[ale] katika A[gano] J[ipya]. Kwa hiyo, karibu na mwanzo wa karne ya pili, zile Herufi Nne ziliacha kutumiwa hatua kwa hatua katika Maagano yote mawili kwa sababu ya majina ya badala yaliyokuwa yakitumiwa.”—Buku la 96, Na. 1, Machi 1977, uku. 76, 77.
Kati ya jina Yehova na Yahweh, ni lipi lililo sahihi?
Leo hakuna mwanadamu anayeweza kujua hakika jinsi lilivyotamkwa hapo kwanza katika Kiebrania. Kwa nini? Hapo kwanza Kiebrania cha Biblia kiliandikwa kwa konsonanti tu, bila irabu. Wakati lugha hiyo ilipokuwa ikitumiwa kila siku, ilikuwa rahisi kwa wasomaji kutamka maneno kwa kutumia irabu zinazofaa. Hata hivyo, baadaye Wayahudi wakaja kuwa na mawazo ya kishirikina ya kwamba ni kosa kulitamka jina la Mungu kwa sauti, kwa hiyo wakawa wakitumia majina ya badala. Karne nyingi baadaye, wasomi wa Kiyahudi walisitawisha mfumo wa nukta za kuonyesha irabu zinazotumiwa kusoma Kiebrania cha kale, lakini wao waliweka irabu za majina ya badala pamoja na zile konsonanti nne zinazowakilisha jina la Mungu. Kwa hiyo matamshi ya kwanza ya jina la Mungu yakasahaulika.
Wasomi wengi wanapendelea “Yahweh,” lakini hawana hakika wala hawakubaliani. Kwa upande mwingine, “Yehova” ndilo jina linalotambuliwa kwa urahisi kwa sababu limetumiwa kwa muda mrefu katika Kiswahili.
J. B. Rotherham, katika The Emphasised Bible, alitumia jina Yahweh katika Maandiko yote ya Kiebrania. Hata hivyo, baadaye katika kitabu chake Studies in the Psalms, alitumia jina “Jehovah.” Alieleza hivi: “JEHOVAH—matumizi ya jina hilo la Ukumbusho la Kiingereza . . . katika tafsiri ya sasa ya Zaburi halitokani na shaka yoyote kuhusu matamshi yaliyo sahihi zaidi, kuwa ni Yahwéh; bali ni kutokana na ushahidi tu unaofaa uliochaguliwa ili kufurahisha macho na masikio ya watu, ambapo jambo muhimu ni kutambuliwa kwa urahisi kwa lile jina la Mungu linalokusudiwa.”—(London, 1911), uku. 29.
Baada ya kuzungumzia matamshi mbalimbali, profesa Mjerumani Gustav Friedrich Oehler alifikia mkataa huu: “Kuanzia sasa na kuendelea mimi nalitumia jina Yehova, kwa sababu, kwa hakika, jina hili limezoelewa katika msamiati wetu na haliwezi kuondolewa.”—Theologie des Alten Testaments, chapa ya pili (Stuttgart, 1882), uku. 143.
Msomi Mjesuti Paul Joüon asema hivi: “Katika tafsiri zetu, badala ya jina (la kukisiwa) Yahweh, tumetumia jina Jéhovah . . . ambalo ndilo jina la kawaida linalotumiwa katika Kifaransa.”—Grammaire de l’hébreu biblique (Roma, 1923), kielezi-chini katika uku. 49.
Majina mengi hubadilika kwa kadiri fulani yanapotamkwa katika lugha nyingine. Yesu alizaliwa akiwa Myahudi, na katika Kiebrania labda jina lake lilitamkwa Ye·shuʹa‛, lakini waandikaji wa Maandiko ya Kikristo walioongozwa na roho ya Mungu hawakusita kutumia jina la Kigiriki, I·e·sousʹ. Katika lugha nyingine nyingi matamshi hutofautiana kidogo, lakini sisi hutumia jina la kawaida katika lugha yetu. Hivyo ndivyo ilivyo kuhusu majina mengine ya Biblia. Basi, tunaweza kumwonyeshaje heshima inayofaa Yule mwenye jina muhimu kuliko majina yote? Je, tungefanya hivyo kwa kutotaja kamwe wala kuandika jina lake kwa sababu hatujui vizuri jinsi lilivyokuwa likitamkwa hapo kwanza? Au, badala yake, je, hatungetumia matamshi na herufi za kawaida katika lugha yetu, huku tukisema mambo mazuri kumhusu Mwenye jina hilo na kujiendesha kwa njia inayomletea heshima tukiwa waabudu wake?
Kwa nini ni muhimu kujua na kutumia jina la Mungu?
Je, una uhusiano wa karibu na mtu yeyote ambaye hujui jina lake? Kwa watu wanaoona kwamba Mungu hana jina mara nyingi yeye ni nguvu tu zisizo na utu, si mtu halisi, si mtu wanayemjua na kumpenda na ambaye wanaweza kusema naye kutoka moyoni katika sala. Wanaposali, sala zao huwa desturi tu, kurudia-rudia kidesturi maneno yaliyokaririwa.
Yesu Kristo amewapa Wakristo wa kweli utume wa kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote. Wanapowafundisha watu hao, wanawezaje kumtofautisha Mungu wa kweli na miungu ya uwongo ya mataifa? Ni kwa kutumia tu jina Lake, kama Biblia yenyewe inavyolitumia.—Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 8:5, 6.
Kut. 3:15: “Mungu akamwambia Musa . . . : ‘Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, “Yehova Mungu wa mababu zenu . . . amenituma kwenu.” Hilo ndilo jina langu mpaka wakati usio na kipimo, na huo ndio ukumbusho wangu kwa kizazi baada ya kizazi.’”
Isa. 12:4: “Mpeni Yehova shukrani! Liitieni jina lake. Tangazeni matendo yake kati ya vikundi vya watu. Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”
Eze. 38:17, 23: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema hivi, ‘ . . . Nami hakika nitajitukuza mwenyewe na kujitakasa mwenyewe na kujijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.’”
Mal. 3:16: “Wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana, kila mmoja na mwenzake, na Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza. Na kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake kwa ajili ya wale wenye kumwogopa Yehova na kwa ajili ya wale wanaolifikiria jina lake.”
Yoh. 17:26: “[Yesu alimwomba Baba yake:] Nami nimewajulisha [wafuasi wake] jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”
Mdo. 15:14: “Simioni ameeleza kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.”
Je, Yehova katika “Agano la Kale” ndiye Yesu Kristo katika “Agano Jipya”?
Mt. 4:10: “Yesu akamwambia: ‘Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, “Yehova [“Bwana,” UV na nyinginezo] Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”’” (Ni wazi Yesu hakuwa akisema kwamba yeye mwenyewe alipaswa kuabudiwa.)
Yoh. 8:54: “Yesu akajibu [Wayahudi]: ‘Ikiwa mimi ninajitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu. Baba yangu ndiye ambaye hunitukuza, yule ambaye ninyi mnasema kwamba ni Mungu wenu.’” (Maandiko ya Kiebrania yanamtambulisha waziwazi Yehova kuwa Mungu ambaye Wayahudi walidai kuabudu. Yesu hakusema kwamba yeye mwenyewe ni Yehova, bali kwamba Yehova ni Baba yake. Hapa Yesu alionyesha wazi kabisa kwamba yeye na Baba yake walikuwa watu wawili tofauti.)
Zab. 110:1: “Neno la Yehova kwa Bwana wangu [Daudi] ni: ‘Keti kwenye mkono wangu wa kuume Mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.’” (Kwenye Mathayo 22:41-45, Yesu alieleza kwamba yeye mwenyewe ndiye “Bwana” wa Daudi, ambaye alitajwa katika Zaburi hiyo. Kwa hiyo, Yesu si Yehova bali ndiye aliyekuwa akiambiwa na Yehova maneno hayo.)
Flp. 2:9-11: “Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha [Yesu Kristo] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.” (Ona kwamba Yesu Kristo hapa anatofautishwa na Mungu Baba na kwamba anamtii Yeye.)
Mtu anawezaje kumpenda Yehova ikiwa anapaswa kumwogopa pia?
Biblia hutuambia kwamba tunapaswa kumpenda Yehova (Luka 10:27) na pia kumwogopa. (1 Pet. 2:17; Met. 1:7; 2:1-5; 16:6) Kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa kutatufanya tuwe waangalifu sana tusimkasirishe. Kumpenda Yehova kutatusukuma tutake kufanya mambo yanayompendeza, kumshukuru kwa kutuonyesha upendo na fadhili zisizostahiliwa kwa njia nyingi.
Mfano: Mwana huogopa kumkasirisha baba yake, lakini kuthamini yote ambayo baba yake humfanyia kunapaswa pia kumsukuma mwana huyo kumpenda baba yake kikweli. Huenda mwogeleaji akasema kwamba yeye anaipenda bahari, lakini kuiogopa bahari humfanya afahamu kwamba kuna mambo anayopaswa kuepuka kufanya. Vivyo hivyo, kumpenda Mungu kunapaswa kuambatana na kuogopa kufanya lolote litakalomkasirisha.