Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Mkono wa Yehova’ Maishani Mwangu
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Machi 1
    • wa huduma ya wakati wote. Tangu alipokuwa na miaka mitano, alionyesha tamaa ya kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti, inayoitwa Betheli. Hakuacha kamwe kuwa na mradi huo, na baada ya kuhitimu shule ya upili, aliuliza mama yake na mimi hivi: “Mwafikirije, nitoe ombi la kutumikia Betheli?”

      Ingawa hisia zetu za moyoni ziliathiriwa kumruhusu mwana wetu aondoke, tulijibu hivi bila kusita: “Hutauhisi kamwe mkono wa Yehova kadiri utakavyouhisi ukiwa Betheli—kiini chenyewe cha tengenezo la Yehova.” Katika miezi miwili alienda Betheli ya Kanada. Hiyo ilikuwa katika 1980, naye ametumikia huko tangu wakati huo.

      Miaka ya 1980 ilituletea Lucy na mimi magumu mapya. Tulirudia hali ya kwanza—tukiwa sisi wawili tu. Kufikia wakati huo Susan alikuwa ameolewa na alikuwa akipainia pamoja na mume wake, na Kim na Greg wote wawili walikuwa wakitumikia katika Betheli. Tungefanya nini? Swali hilo lilijibiwa upesi katika 1981 tulipoalikwa kutumikia mzunguko wa Kireno, ulioenea kilometa 2,000 hivi za Kanada. Tungali twafurahia kazi ya kusafiri.

      Tangu wakati huo Kim ameolewa na kuhudhuria Gileadi, na sasa atumikia pamoja na mume wake katika kazi ya mzunguko katika Brazili. Susan na mume wake wangali Kanada, wakiwalea watoto wao wawili, na mume wa Susan anapainia. Hata ingawa katika miaka ya karibuni familia yetu imetenganishwa kimwili kwa sababu ya migawo yetu katika utumishi wa wakati wote, tunaendelea kuwa karibu kiroho na kihisiamoyo.

      Lucy na mimi tunatazamia wakati ujao mwangavu pamoja na familia yetu katika dunia iliyosafishwa. (2 Petro 3:13) Kama vile Musa wa zamani, tumejionea wenyewe ukweli wa jibu la lile swali lisilotazamia jibu kwenye Hesabu 11:23: “Je! mkono wa BWANA [Yehova, NW] umepungua urefu wake? Sasa utaona kwamba neno langu litatimizwa kwako, au sivyo.” Kwa kweli, hakuna kiwezacho kumzuia Yehova asiwabariki watumishi wake kwa ajili ya utumishi wao wa moyo wote.

  • Je! Wewe Unafanya Mapenzi ya Mungu?
    Mnara wa Mlinzi—1994 | Machi 1
    • Je! Wewe Unafanya Mapenzi ya Mungu?

      KATIKA huduma yao ya nyumba kwa nyumba, Mashahidi wa Yehova wawili walikutana na kasisi wa Kanisa la Episkopali. Alionekana kuwa mtu mwenye kupendeza, mwenye ndevu, wa karibu miaka 60, aliyekuwa amevalia T-shati iliyokuwa imeandikwa jina la kanisa lake. Bila kutua alisema hivi: “Ningetamani washiriki wa kanisa letu wawe wenye bidii kama ninyi katika kulieneza Neno, lakini ni lazima niwaombe msitembelee nyumba yangu tena.”

      Ndiyo, kuna watu wengi wanaosifu kazi ya Mashahidi wa Yehova na kuwapongeza kwa ajili ya bidii na idili yao. Lakini, hawapendezwi hata kidogo na yale ambayo Mashahidi wanafanya, wala hawangefikiria kufanya kazi hiyo wao wenyewe. Hata hivyo, hali hiyo ionekanayo kuwa yenye kupingana, si jambo jipya hata kidogo. Ilionwa na Yesu katika siku zake, naye alikazia jambo hilo kikiki kupitia kielezi chenye kuchochea fikira.

      “Mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende. Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki; baadaye akatubu, akaenda. Je! katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya babaye?”—Mathayo 21:28-31.

      Jibu ni wazi. Kama vile ule umati uliomsikia Yesu, sisi tungeitikia, “Ni yule wa pili.” Lakini zaidi ya jambo hilo la wazi, kupitia kielezi hicho, Yesu alikuwa akituonyesha kwamba kufanya yale ambayo baba alitaka ndilo lililokuwa jambo la maana. Ingawa mwana wa pili alisema kwamba hakutaka kwenda, alienda hata hivyo akapongezwa kwa kufanya hivyo. Kufanya kazi ya aina ifaayo ni jambo la maana vilevile. Mwana wa pili alitenda kwa kufanya kazi katika shamba la mizabibu la babake; naye hakwenda kufanya kazi katika shamba la mizabibu lake mwenyewe.

      Hayo yote yanamaanisha nini hasa kwetu? Mungu ataka nini kutoka kwa waabudu leo? Twaweza kujifunza nini kutoka kwa maisha ya Yesu yatakayotusaidia kufanya mapenzi ya babake? Hayo ni maswali ya maana, na kupata kwetu majibu yafaayo kutamaanisha hali njema yetu ya milele, kwa kuwa “yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu milele.”—1 Yohana 2:17; Waefeso 5:17.

      “Mapenzi ya Mungu” Ni Nini?

      Nomino “mapenzi” imeorodheshwa zaidi ya mara 80 katika Comprehensive Concordance of the New World Translation of the Holy Scriptures. Katika mara 60 hivi kati ya hizo (au karibu asilimia 75 kati ya mara hizo) inarejezea mapenzi ya Mungu. Semi kama vile “mapenzi ya Mungu,” na “mapenzi ya Baba yangu,” yanatukia zaidi ya mara 20. Kutokana na hayo twaweza kuona kwamba mapenzi ya kimungu yapaswa yawe yenye maana kuu kwetu. Kufanya mapenzi ya Mungu kwapaswa kuwe jambo kuu maishani mwetu.

      Katika Kiingereza nomino “mapenzi” yamaanisha ‘tamaa, kutaka, azimio, kitu kinachotamaniwa, hasa chaguo au azimio la mtu mwenye mamlaka au nguvu.’ Kwa hiyo basi, Yehova, aliye Mamlaka Kuu Zaidi, ana mapenzi, tamaa au azimio. Hilo ni nini? Maandiko hutuambia kwamba kwa sehemu “mapenzi ya [Mungu] ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4, NW) Yesu Kristo na Wakristo wa mapema walifanya kazi kwa moyo wote ili kuletea wengine huo ujuzi sahihi.—Mathayo 9:35; Matendo 5:42; Wafilipi 2:19, 22.

      Ni nani wafanyao mapenzi ya Mungu leo? Miongoni mwa wale watu wapatao bilioni mbili wanaodai kuwa wafuasi wa Yesu Kristo, ni wangapi walio kama yule mwana mchanga zaidi katika kielezi cha Yesu, aliyekwenda na kufanya mapenzi ya babake? Si ngumu kupata jibu. Wafuasi wa kweli wa nyayo za Yesu Kristo wangekuwa wakifanya kazi aliyosema wangefanya: “Na sharti Injili [habari njema, NW] ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Mashahidi wa Yehova, ambao ni zaidi ya milioni nne na nusu ulimwenguni pote, wanahubiri kwa bidii habari njema za Ufalme wa Mungu na kufundisha wengine, wakielekezea Ufalme kuwa tumaini pekee la ainabinadamu la kupata amani na usalama. Je! wewe unashiriki kikamili katika kufanya mapenzi ya Mungu? Je! wewe unahubiri juu ya habari njema za Ufalme kama vile Yesu alivyofanya?—Matendo 10:42; Waebrania 10:7.

      Kupata Shangwe Katika Kufanya Mapenzi ya Mungu

      Ingawa kuna shangwe katika kujifunza mapenzi ya Baba, kuna shangwe nyingi zaidi katika kuwafundisha wengine mapenzi ya Mungu. Yesu alipata shangwe katika kufundisha watu juu ya Babake. Hilo lilikuwa kama chakula kwake. (Yohana 4:34) Sisi pia tutaonea shangwe furaha ya kweli tukifanya kama vile Yesu alivyofanya, kuhubiri na kufundisha mambo aliyofundisha, mambo aliyopokea kutoka kwa Babake. (Mathayo 28:19, 20) Kama vile Yesu alivyoahidi, “mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda.”—Yohana 13:17.

      Kutoa kielezi: Mama mmoja ambaye hivi karibuni alianza tena huduma ya painia ya wakati wote alisema hivi: “Kuona uso wa mwanafunzi wa Biblia ukichangamka wakati kweli mbalimbali za Biblia zigusapo moyo kunasisimua sana! Ni shangwe nyingi sana kwangu kuona mwanafunzi mmoja hasa akiandika kwa urefu maandiko yote kabla ya funzo na kuandika mambo machache wakati wa funzo ili aweze kujibu maswali yoyote ya kupitia baadaye.” Mwingine kati ya wanafunzi wake wa Biblia alikuwa amepata kusikia kidogo juu ya kweli katika miaka ya mapema ya utineja wake. Sasa akiwa ameolewa na kuwa na mahangaiko juu ya matatizo fulani ya kibinafsi, alikuwa akitamani kuwapata Mashahidi. Alifurahi kama nini wakati yule dada painia alipompata! Mwanamke huyo mchanga alifurahi sana kuanza funzo lake la Biblia tena.

      Kudumisha Shangwe ya Kufanya Mapenzi ya Mungu

      Mfalme Daudi wa Israeli ya kale ni mmoja aliyejaribu kufanya mapenzi ya Mungu muda wote wa maisha yake. Yajapokuwa magumu na mibano mingi iliyoletwa dhidi yake, alipuliziwa kusema hivi: “Kufanya mapenzi yako, Ee Mungu wangu, ndiyo furaha yangu; naam, sheria yako imo moyoni mwangu.” (Zaburi 40:8) Kufanya mapenzi ya Yehova kulikuwa ndani kabisa ya nafsi ya Daudi, katika kiumbe chake mwenyewe. Hiyo ilikuwa ndiyo siri ya shangwe yake isiyofifia katika kumtumikia Yehova. Kufanya mapenzi ya Mungu hakukuwa jambo gumu kwa Daudi. Badala ya hivyo, lilikuwa jambo lenye kupendeza, jambo lililotoka moyoni mwake. Muda wote wa maisha yake, aling’ang’ana kufanya vizuri awezavyo kumtumikia Mungu wake, Yehova, hata ingawa nyakati nyingine alifanya dhambi na kupungukiwa.

      Pindi kwa pindi, huenda shangwe yetu ikapunguka. Huenda tukachoka au kushuka moyo. Labda yale yaliyotukia zamani yaendelea kutuletea matatizo, dhamiri yetu ikitusumbua juu ya tendo fulani baya lililofanywa zamani sana. Mara nyingi, twaweza kushinda hisia hizo kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukamili zaidi. Twaweza kuwa na lengo la kuandika sheria ya Mungu ‘moyoni mwetu,’ kama vile Daudi alivyofanya. Tukijaribu kufanya mapenzi ya Mungu kwa moyo wote, yaani, vizuri tuwezavyo, yeye atatuthawabisha kulingana na hayo kwa sababu yeye ni mwaminifu.—Waefeso 6:6; Waebrania 6:10-12; 1 Petro 4:19.

      Kwa kupendeza, kwenye Waebrania 10:5-7, mtume Paulo alinukuu maneno ya Daudi kwenye Zaburi 40:6-8 akayatumia kuhusu Yesu Kristo. Kwa kufanya hivyo, Paulo alionyesha jinsi Yesu alivyokuwa karibu na Babake. Neno la Kiebrania “mapenzi” huwa na mawazo ya ‘jambo la kupendeza, tamaa, upendeleo, au upendezi.’ Kwa hiyo, Zaburi 40:8 laweza kusomwa hivi kuhusu Kristo: “Nimependezwa, Ee Mungu wangu, kufanya upendezi wako.”a Yesu alitaka kufanya yale ambayo yalimpendeza Babake. Yesu alifanya zaidi ya yale aliyotakiwa afanye. Alifanya yale yaliyokuwa karibu na moyo wa Babake, na alionea shangwe kuyafanya.

      Maisha yote ya Yesu yalikazia kufundisha wengine mapenzi ya Mungu na yale waliyopaswa wafanye ili kupata baraka ya Mungu. Yeye alikuwa mhubiri na mwalimu wa wakati wote na alipata shangwe kuu katika kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo yafuatana kwamba kadiri tufanyavyo kazi ya Yehova kwa wingi zaidi, ndivyo tutakavyopokea shangwe nyingi zaidi. Je! wewe pia waweza kutumikia wakati wote katika kazi ya kuhubiri ili shangwe yako iongezeke pia?

      Msaada mwingine katika kudumisha shangwe katika kufanya mapenzi ya Mungu ni kuendelea kukazia macho wakati ujao. Ndivyo Yesu alivyofanya. “Kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba [mti wa mateso, NW] na kuidharau aibu.” Kwake, shangwe ilikuwa kuthibitika kuwa mwaminifu kwa Mungu hadi mwisho na kupata thawabu ya umaliki kwenye mkono wa kulia wa Babake.—Waebrania 12:2.

      Ebu wazia ile shangwe itakayokuja wakati ujao kwa wale wanaoendelea kufanya mapenzi ya Mungu. Wao wataona uharibifu wa wale wanaosisitiza kufanya mapenzi yao wenyewe yenye ubinafsi hata ingawa hayo husababisha kuteseka kwa wale wanaojitahidi kufanya mapenzi ya Mungu. (2 Wathesalonike 1:7, 8) Fikiria ile shangwe ya wapendwa watakaofufuliwa ya kupata fursa ya kujifunza mapenzi ya Mungu. Au fikiria kusudi la Mungu la kurudisha dunia kuwa Paradiso. Na mwishowe, wazia ule uhuru utakaotokana na kuharibiwa kabisa kwa Shetani, yule mpinzani wa mapenzi ya Yehova.

      Ndiyo, kufanya mapenzi ya Mungu leo kwaweza kuleta shangwe nyingi sasa na furaha isiyokoma katika wakati ujao. Lijapokuwa itikio tupatalo katika kazi ya kuhubiri, acheni tuige kielelezo cha Yesu cha kupata upendezi katika kufanya mapenzi ya Babake.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona kielezi-chini cha Zaburi 40:8, NW.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki