‘Mkono wa Yehova’ Maishani Mwangu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA LAWRENCE THOMPSON
USIKU mmoja katika 1946, baba yangu nami tuliketi katika gari tukivitazama vimulikaji vya kizio cha kaskazini vikimeta-meta angani. Tuliongea juu ya ukuu wa Yehova na udogo wetu. Tulirudia matukio ya miaka ambayo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku katika Kanada. Baba alikazia kwangu jinsi Yehova alikuwa ametegemeza na kuwaongoza watu Wake muda wa miaka hiyo.
INGAWA nilikuwa na miaka 13 tu, niliweza kuthamini ukweli wa yale ambayo baba alikuwa akisema. Pia alikazia kwangu hisi ya uharaka na ya ukubwa wa kazi ya kuhubiri ambayo bado ingefanywa. Baba alinukuu Hesabu 11:23 akatia mkazo kwangu kwamba, kwa kweli, mkono wa Yehova haupungui urefu kamwe. Ni kukosa kwetu tu kutia imani katika yeye na kumtumaini kunakozuia yale atakayotufanyia. Hayo yalikuwa mazungumzo mazuri sana kati ya baba na mwana, ambayo sitasahau kamwe.
Kujifunza vichapo vya Watch Tower, hasa kile kitabu Salvation, kilichotangazwa katika 1939, kilikuwa pia na uvutano mkubwa sana juu ya maisha yangu ya mapema. Sitasahau kamwe kielezi cha kutazamisha kwenye utangulizi wacho: “Lile gari-moshi la abiria la mwendo wa kasi, lililokuwa limejaa abiria, lilikuwa likienda mbio mwendo wa [kilometa 160] kwa saa. Ni lazima livuke mto kwenye daraja lililofanya mchirizo wa [digrii 180], hivi kwamba watu katika behewa la mwisho la gari-moshi hilo wangeweza kuona injini . . . Wanaume wawili waliokuwa katika behewa la mwisho la gari-moshi hilo . . . waliona kwamba sehemu ya mwisho ya daraja hilo ilikuwa ikiwaka moto ikiwa inaanguka mtoni. Waling’amua kwamba walikuwa wakikabili hatari kubwa. Hiyo kwa kweli ilikuwa hali ya dharura. Je! gari-moshi hilo lingeweza kusimamishwa kwa wakati ufaao ili kuokoa maisha za wale abiria wengi waliokuwa ndani yalo?”
Kikifanya utumizi wa kielezi hicho, kitabu kilimalizia hivi: “Leo vilevile, mataifa yote na watu wote wa dunia wanakabili hali ya dharura iliyo kubwa zaidi. Wanaonywa kama vile Mungu aamuruvyo, kwamba msiba wa Har–Magedoni uko huko mbele tu. . . . Wakiwa wameonywa hivyo, ni lazima sasa kila mtu ambaye ameonywa hivyo achague mwendo atakaochukua.”
Gari-moshi hilo la mwendo wa kasi, daraja hilo lenye kuwaka moto, na uharaka wa kazi ya kuhubiri zilikaziwa kikiki akilini mwangu.
Utendaji wa Kuhubiri wa Mapema
Nilianza kushiriki katika kazi ya kuhubiri katika 1938, nilipokuwa na miaka mitano. Henry na Alice Tweed, mapainia (wahudumu wa wakati wote), wawili walikuwa wakienda nami, na tulikuwa tukitumia muda wa saa 10 hadi 12 tukiongea na watu. Nilifurahia sana siku hizo nzima-nzima katika utumishi wa Yehova. Kwa hiyo nilisisimuka mwaka uliofuata wakati baba na mama waliponiruhusu niwe mhubiri na kuripoti utendaji wangu kikweli.
Katika siku hizo za mapema, tulishiriki katika maandamano ya kuarifu, tukitembea kwenye barabara kuu za miji tukiwa tumevaa mabango yenye shime zilizofunua dini bandia na kutangaza Ufalme wa Mungu. Tulitumia pia vinanda vya kuchukulika, tukacheza rekodi za ujumbe mbalimbali wenye msingi wa Biblia mlangoni penyewe pa wenye nyumba. Tulikuwa tukicheza rekodi zenye hotuba za J. F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Society, ambazo nilikuwa nimekariri baadhi yazo. Ningali naweza kukumbuka kwa wazi akisema: “Imesemwa mara nyingi, Dini ni mtego na hila!”
Kazi Yetu Yapigwa Marufuku Katika Kanada
Wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku katika Kanada, kama vile ilivyokuwa imepigwa marufuku katika Ujerumani ya Nazi na nchi nyinginezo. Kwa hiyo tulitumia Biblia tu lakini tukaendelea na kazi tuliyoamriwa na Mungu kwa kutii maagizo ya Biblia. (Mathayo 28:19, 20; Matendo 5:29) Tulijifunza namna ya kukabiliana na mashambulio ya polisi kwenye mikutano yetu na katika nyumba zetu. Pia tulikuja kupata maarifa ya kushuhudia mbele ya mahakimu na kuwajibu mawakili wenye kuhoji-hoji.
Kaka yangu Jim na mimi tulikuja kuwa wastadi wa kutupa vijitabu kutoka kwenye magari yaliyo mwendoni hadi kwenye milango na veranda. Kwa kuongezea tulitenda tukiwa matarishi na, nyakati fulani, tukiwa walinzi kwa wale waliokuwa wakivuka mpaka ili kuhudhuria mikusanyiko katika United States.
Nyumba yetu ilikuwa sehemu za nje-nje za Port Arthur (sasa Thunder Bay), Ontario, kwenye uwanja wa hektari moja hivi uliozingirwa na miti na vichaka. Tulikuwa na ng’ombe mmoja, ndama mmoja, nguruwe, na kuku—vyote hivyo vilitumika kuwa kisingizio kizuri kwa ajili ya kazi yetu ya kuwasaidia Wakristo wenzetu wachanga waliokuwa wakisakwa ili kufungwa gerezani kwa ajili ya kuhubiri Ufalme wa Mungu.
Usiku, magari, malori, na matrela yaliyokuwa yakibeba Wakristo wachanga yalikuwa yakiingia na kutoka uwanja wetu uliokuwa umefichwa. Tulikuwa tukiwapa vijana hao makao, kuwaficha, kuwageuza sura na kuwapa chakula kisha kuwaacha waende zao. Baba na mama yangu, pamoja na wafanyakazi hao wengine wa mapema, walikuwa watumishi wenye moyo wote waliofinyanga moyo wangu mchanga umtumikie na kumpenda Yehova Mungu.
Katika Agosti 1941, niliweka maisha yangu wakfu kwa Yehova, nikabatizwa katika ziwa dogo lililokuwa ndani kabisa msituni. Baadhi yetu tulikuwa tumekusanyika usiku sana kwa ajili ya tukio hilo katika kibanda kilichonurishwa kwa taa ya mkono. Wakionekana wakitutilia shaka, polisi walipitapita, wakati wote wakichunguza lile ziwa kwa taa za mkono za kutafuta-tafuta, lakini hawakutupata.
Sehemu Nyingi za Utumishi wa Wakati Wote
Katika 1951, nilihitimu shule ya upili, nikasafiri karibu kilometa 1,600 ili kufanya mgawo wa upainia katika Cobourg, Ontario. Kutaniko hilo lilikuwa dogo, na sikuwa na painia mwenzangu. Lakini nikikumbuka kwamba mkono wa Yehova haupungui urefu, nilikodi chumba kimoja, nikajipikia chakula, na kuwa na furaha kumtumikia Yehova. Mwaka uliofuata nilialikwa kutumikia kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Toronto. Nikiwa huko nilijifunza masomo mengi yenye thamani yaliyonifanya niwe bora zaidi kwa ajili ya utumishi wa Ufalme wa wakati ujao.
Baada ya mimi kutumikia katika Toronto kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja, Lucy Trudeau nami tulioana, na katika kipupwe cha 1954, tulipokea mgawo wa upainia katika Levis, Quebec. Hali ya hewa ilikuwa baridi sana, ghasia za watu na uchokozi wa polisi ulikuwa wenye kutia hofu; na kujifunza Kifaransa kulikuwa jambo gumu. Kupitia hayo yote mkono wa Yehova haukupungua urefu kamwe, kwa hiyo ingawa kulikuwa nyakati ngumu, tulikuwa na baraka nyingi pia.
Kwa kielelezo, tuliombwa tukague meli (Arosa Star na Arosa Kulm) ambazo Sosaiti ilipanga kutumia ili kuwasafirisha wajumbe kwenye ile mikusanyiko mikubwa ya kimataifa ya Ulaya katika 1955. Wakitamani sana kufanya biashara na Sosaiti, wasimamizi wa kampuni za usafirishaji wa meli walituonyesha ukaribishaji-wageni pindi kwa pindi, jambo lililokuwa pumziko lenye kupendeza kutoka katika ile huduma yenye mkazo wa akili katika Quebec wakati huo.
Katika vuli ya 1955, nilialikwa kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye, na tulitumia kipupwe hicho tukitembelea makutaniko ya mbali katika kaskazini mwa Ontario kwenye baridi kali sana. Mwaka uliofuata tulihudhuria Watchtower Bible School of Gilead katika United States, na baadaye tukapewa mgawo kwenda Brazili, Amerika Kusini, tukiwa wamishonari.
Tulitumikia katika mgawo wetu mpya kwa moyo na nafsi yetu yote na upesi tukaweza kuhubiri na kufundisha katika lugha ya Kireno. Mwanzo-mwanzo wa 1957, nilipewa mgawo tena wa kufanya kazi nikiwa mwangalizi asafiriye. Sasa, badala ya kutumikia Kaskazini penye baridi kali sana, tulilazimika kuvumilia hali yenye joto jingi sana. Nyakati nyingi tulilazimika kutua na kuondoa mchanga wenye joto jingi kutoka katika viatu vyetu au kukata kipande cha muwa cha kutafuna-tafuna ili kurudisha nguvu zetu. Lakini tulibarikiwa.
Katika mji wa Regente Feijo, nilisema na polisi mkuu, naye akaamuru maduka yote yafungwe na kuambia kila mtu aende kwenye uwanja wa mji. Chini ya kivuli cha mti wa maua wenye majani mapana, nilitoa hotuba ya Biblia kwa watu wote wa mji huo. Leo kuna kutaniko la Mashahidi huko.
Kuwalea Watoto Wetu Brazili
Lucy alipopata mimba katika 1958, tulikaa katika Juiz de Fora na kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Katika miaka miwili iliyofuata, binti zetu, Susan na Kim, walizaliwa. Walithibitika kuwa baraka ya kweli katika huduma, wakavutia watu katika mji huo. Tuliposukuma viti vyao vidogo vyenye magurudumu kwenye barabara zenye mawe ya bapa, watu walikuwa wakitoka ili kuwaona. Kwa kuwa uhitaji wa wahubiri wa Ufalme ulikuwa mkubwa katika Recife, kusini tu mwa ikweta, tulihamia mahali hapo penye joto jingi sana.
Katika 1961, niliweza kupanga usafirishaji kwa ndege kwa ajili ya Mashahidi waliokuwa wakienda kwenye mkusanyiko katika São Paulo lakini mimi mwenyewe pia nikaweza kuhudhuria mkusanyiko huo wenye kukumbukika. Lakini, baada ya dakika 20 hivi tukiwa hewani, ndege ilianza kuelekea nchini kwa ghafula, ikiwarusha abiria kotekote katika ndege. Sehemu ya ndani ya ndege iliharibika; viti viling’olewa kutoka mahali pavyo, na abiria wakajeruhiwa na kuvuja damu. Kwa furaha, rubani aliweza kuzuia ndege isianguke, tukatua salama. Hakuna yeyote kati yetu aliyejeruhiwa vibaya sana asiweze kuendelea hadi São Paulo katika ndege nyingine. Tulifurahia mkusanyiko mzuri ajabu, lakini nilisema sitakwenda kwa ndege kamwe tena!
Hata hivyo, nilipowasili nyumbani kutoka kwenye mkusanyiko, mgawo mwingine ulikuwa ukiningojea. Nilipaswa nishughulikie mkusanyiko mmoja uliokuwa ndani sana msituni katika Teresina, Jimbo la Piauí. Ningepaswa niende huko kwa ndege. Ingawa niliogopa sana, nilikubali mgawo huo, nikitegemea mkono wa Yehova.
Katika 1962 mwana wetu, Greg, alizaliwa katika Recife. Ingawa sikuweza kupainia tena, kwa sababu sasa nilikuwa na familia, niliweza kuwa na uvutano unaofaa juu ya lile kutaniko dogo. Sikuzote watoto walikuwa na hamu ya kuungana nasi katika huduma, kwa kuwa tuliifanya iwe yenye kupendeza kwao. Kila mmoja wao, tangu umri wa miaka mitatu, aliweza kufanya utoaji milangoni. Tulizoea kutokosa kamwe kuhudhuria mikutano au kushiriki katika utumishi wa shambani. Hata mmoja katika familia alipokuwa mgonjwa na mwingine akaweza kubaki nyumbani naye, wengine walikuwa wakihudhuria mkutano au kushiriki katika huduma ya shambani.
Kwa muda wa miaka iliyopita, tukiwa familia tulizungumzia kwa ukawaida mitaala ya shule ya watoto na miradi yao maishani, tukiwatayarisha kwa ajili ya kazi-maisha pamoja na tengenezo la Yehova. Tulikuwa waangalifu tusije tukawaacha waingiwe na uvutano mbalimbali wenye kudhoofisha, kama televisheni. Hatukuwa na televisheni nyumbani mwetu mpaka watoto walipofikia miaka yao ya utineja. Na ingawa tulikuwa na uwezo, hatukuwaharibu kwa vitu vya kimwili. Kwa kielelezo, tulinunua baiskeli moja tu, ambayo watoto wote watatu walipaswa kuishiriki.
Tulifanya mambo pamoja kwa kadiri tulivyoweza, kucheza mpira wa vikapu, kuogelea, na kufanya safari za kifamilia. Safari zetu zilihusiana na kuhudhuria mikusanyiko ya Kikristo au kuzuru makao ya Betheli katika nchi mbalimbali. Safari hizo zilitupa sisi wakati wa kuongea pamoja kwa uhuru hivi kwamba Lucy na mimi tungeweza kujua yale yaliyokuwa ndani ya mioyo ya watoto wetu. Tunamshukuru Yehova sana kwa ajili ya miaka hiyo yenye furaha!
Hatimaye, miaka yetu kumi katika Tropiki karibu na ikweta ikaathiri afya ya Lucy. Kwa hiyo tulifurahia badiliko la mgawo kwenda kusini kwenye halijoto ya kiasi zaidi, katika Kuritiba, Jimbo la Paraná.
Kurudi Kanada
Katika 1977, baada ya miaka 20 hivi katika Brazili, Lucy na mimi tulirudi Kanada pamoja na watoto wetu ili kusaidia kumtunza baba yangu aliyekuwa mgonjwa. Mazingira ya kitamaduni yalikuwa tofauti kama nini kwa familia yetu! Lakini hayakuwa tofauti kiroho, kwa kuwa tulidumisha utaratibu wetu uleule pamoja na udugu wetu wa Kikristo wenye upendo.
Katika Kanada, huduma ya wakati wote ilikuja kuwa jambo lililohusisha familia yote wakati binti zetu, mmoja baada ya mwingine, walipoingia huduma ya upainia ya wakati wote. Sisi sote tulichangia mradi wa familia yetu. Machumo yoyote kutoka kwa kazi ya muda-muda yaliwekwa katika hazina ya gharama ya kudumisha nyumba yetu na magari matatu yaliyohitajiwa ili kupitia eneo letu lililotapakaa. Kila juma, baada ya funzo letu la Biblia la familia, tulizungumzia mipango yetu ya familia. Mazungumzo hayo yalisaidia kuonyesha kila mtu tulikokuwa tukielekea na yale tuliyokuwa tukifanya na maisha zetu.
Mwana wetu Greg, kama vile dada zake wenye umri mkubwa zaidi, alikuwa pia na mradi wa huduma ya wakati wote. Tangu alipokuwa na miaka mitano, alionyesha tamaa ya kufanya kazi kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti, inayoitwa Betheli. Hakuacha kamwe kuwa na mradi huo, na baada ya kuhitimu shule ya upili, aliuliza mama yake na mimi hivi: “Mwafikirije, nitoe ombi la kutumikia Betheli?”
Ingawa hisia zetu za moyoni ziliathiriwa kumruhusu mwana wetu aondoke, tulijibu hivi bila kusita: “Hutauhisi kamwe mkono wa Yehova kadiri utakavyouhisi ukiwa Betheli—kiini chenyewe cha tengenezo la Yehova.” Katika miezi miwili alienda Betheli ya Kanada. Hiyo ilikuwa katika 1980, naye ametumikia huko tangu wakati huo.
Miaka ya 1980 ilituletea Lucy na mimi magumu mapya. Tulirudia hali ya kwanza—tukiwa sisi wawili tu. Kufikia wakati huo Susan alikuwa ameolewa na alikuwa akipainia pamoja na mume wake, na Kim na Greg wote wawili walikuwa wakitumikia katika Betheli. Tungefanya nini? Swali hilo lilijibiwa upesi katika 1981 tulipoalikwa kutumikia mzunguko wa Kireno, ulioenea kilometa 2,000 hivi za Kanada. Tungali twafurahia kazi ya kusafiri.
Tangu wakati huo Kim ameolewa na kuhudhuria Gileadi, na sasa atumikia pamoja na mume wake katika kazi ya mzunguko katika Brazili. Susan na mume wake wangali Kanada, wakiwalea watoto wao wawili, na mume wa Susan anapainia. Hata ingawa katika miaka ya karibuni familia yetu imetenganishwa kimwili kwa sababu ya migawo yetu katika utumishi wa wakati wote, tunaendelea kuwa karibu kiroho na kihisiamoyo.
Lucy na mimi tunatazamia wakati ujao mwangavu pamoja na familia yetu katika dunia iliyosafishwa. (2 Petro 3:13) Kama vile Musa wa zamani, tumejionea wenyewe ukweli wa jibu la lile swali lisilotazamia jibu kwenye Hesabu 11:23: “Je! mkono wa BWANA [Yehova, NW] umepungua urefu wake? Sasa utaona kwamba neno langu litatimizwa kwako, au sivyo.” Kwa kweli, hakuna kiwezacho kumzuia Yehova asiwabariki watumishi wake kwa ajili ya utumishi wao wa moyo wote.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Pamoja na mke wangu, Lucy