Baraka Zitokanazo na Kuhubiri Pamoja na Wengine
1 Je, wewe huhisi manufaa za kufurahiwa katika kufanya kazi pamoja na wengine katika huduma? Yesu alihisi hivyo. Ingawa mavuno yalikuwa mengi na wafanyakazi wachache, aliwatuma wanafunzi 70 shambani wakiwa “wawili wawili.” Wote walikuwa na kipindi chenye kuthawabisha kama nini wakihubiri katika “kila mji na kila mahali alipokusudia kwenda mwenyewe”!—Luka 10:1, 17; Mt. 9:37.
2 Inasisimua kufanya kazi pamoja na wengine. Wengine wetu ni wenye haya na huona ikiwa vigumu kuwafikia watu tusiowajua. Kuwa na mtu mwingine kando yetu kwaweza kutupa uhakika wa kusema Neno la Mungu kwa ujasiri. Tukiwa pamoja na mtu mwingine, inaweza kuwa rahisi kwetu kufanya kazi hiyo kwa njia ambayo tumezoezwa. (Mit. 27:17) Mwanamume mwenye hekima alisema: “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja.”—Mhu. 4:9.
3 Ni vizuri kuhubiri pamoja na wahubiri na mapainia mbalimbali. Waandamani wa mtume Paulo katika utumishi walitia ndani Barnaba, Sila, Timotheo, na Yohana Marko, nao walifurahia baraka nyingi walipokuwa wakihubiri pamoja. Ndivyo inavyoweza kuwa leo. Je, umepata kuhubiri pamoja na mtu ambaye amekuwa katika kweli kwa muda mrefu? Baada ya kutazama ustadi wake katika kutoa ushahidi, yamkini umepata mawazo fulani mazuri ambayo yamekusaidia ufanye maendeleo. Je, umeandamana na wahubiri ambao ni wapya kwa kadiri? Basi huenda umeweza kushiriki baadhi ya uliyojifunza na hivyo ukaweza kuwasaidia wawe wenye matokeo zaidi na kupata shangwe nyingi katika huduma.
4 Je, kwa sasa wewe unaongoza funzo la Biblia? Ikiwa ndivyo, kwa nini usimkaribishe mmoja wa wazee au mwangalizi wa mzunguko aandamane nawe? Inanufaisha kwa wanafunzi wetu wa Biblia kufahamu vizuri waangalizi. Ikiwa unasitasita kuongoza funzo mzee akiwepo, labda atakuwa tayari kuliongoza na akuache utazame. Baadaye, jihisi huru kumwomba madokezo ya jinsi unavyoweza kumsaidia mwanafunzi afanye maendeleo upesi zaidi.
5 Uwe mwandamani mwenye kutia moyo unapohubiri pamoja na wengine. Uwe na maelezo chanya kuhusu eneo. Usipige porojo kuhusu wengine au kulalamika juu ya mipango ya kutaniko. Kaza akili yako kwenye huduma na baraka zitokazo kwa Yehova. Ukifanya hivyo, wewe pamoja na waandamani wako mtarudi nyumbani mkiwa mmeburudishwa kiroho.
6 Hali zako huenda zikafanya iwe vigumu kwako kuhubiri kwa ukawaida pamoja na ndugu na dada wengine. Hata hivyo, ikiwezekana, kwa nini usipange kuwa na nyakati fulani za kuhubiri pamoja na mhubiri mwingine? Nyote wawili mtabarikiwa!—Rum. 1:11, 12.