Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w89 6/15 kur. 15-20
  • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Adabu Hutukuza Yehova
  • Kwenye Jumba la Ufalme
  • Katika Huduma Yetu ya Peupe
  • Adabu Huanzia Nyumbani
  • Kikundi cha Watu Wenye Adabu
  • Kusitawisha Adabu za Kikristo Katika Ulimwengu Usio na Adabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuwa na Adabu Nzuri Ni Sifa ya Watu wa Mungu
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Kuonyesha Adabu Tukiwa Wahudumu wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Je, Ni Muhimu Kuwatendea Wengine kwa Adabu?
    Vijana Huuliza
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
w89 6/15 kur. 15-20

“Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”

“Ila tu jiendesheni kwa namna inayozistahili habari njema juu ya Kristo.”​—WAFILIPI 1:27, NW.

1. Tukio moja hivi majuzi katika Jiji la New York lilifanya meya atoe sifa gani? (Warumi 13:3)

“Zaidi ya Mashahidi 1,000” walikuja kwenye Jumba la Jiji katika Manhattan siku ya Septemba 29, 1988, ikaripoti The New York Times. Walikuja kuunga mkono pendekezo la ujenzi lililokuwa likisikizwa mbele ya Baraza la Makadirio la jiji hilo. Ingawa pendekezo la kuruhusu kujengwa kwa kao jipya kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova lilikataliwa, meya “alisifu Mashahidi kuwa ‘watu wanyofu kabisa’ na akasema walikuwa ‘wa kusifika kweli kweli.’”

2. Adabu za Mashahidi ni tofauti jinsi gani, na kwa nini?

2 Kwa kawaida, watu zaidi ya elfu moja wanapokuja pamoja kuonyesha wanaunga mkono kusudi fulani lisilopendwa na wengi, ni jambo gani linaloweza kutazamiwa? Kwa kawaida kunakuwako kusukumana, kupiga makelele, hata kutumia nguvu na jeuri halisi. Kwa nini Mashahidi ni tofauti? Ni kwa sababu wanatambua kwamba nyakati zote mwenendo wao unaonyesha jinsi imani yao ilivyo. Wao wanalikumbuka vema shauri la Kimaandiko: “Mwe na mwenendo mzuri kati ya Mataifa, ili, iwapo huwasingizia kuwa watenda mabaya, wayatazamapo matendo yenu mazuri, wamtukuze Mungu siku ya kujiliwa.”​—1 Petro 2:12.

Adabu Hutukuza Yehova

3. Adabu zetu zinatimiza fungu gani katika kuheshimu Yehova?

3 Ni wazi kwamba kutukuza Yehova Mungu kwa mwenendo mwema ni sehemu ya daraka letu la Kikristo. (Mathayo 5:16) Bila shaka, mwenendo mwema ni kutia ndani mambo mengi​—kwa kielelezo, ufuataji haki, bidii nyendelevu, na maadili mema. Hata hivyo, sifa hizi kwa kawaida huthaminiwa na wale tu wanaotujua vema au wale tunaoshughulika nao kwa ukawaida, kama rafiki zetu, watu wa ukoo, waajiri, wafanya kazi wenzetu, na walimu. Namna gani watu walio wengi zaidi tunaoonana nao hivi hivi tu? Hapa hasa ndipo adabu zetu zinapohitajiwa. Kwa maana kama vile karatasi ya kuvutia iliyofungiliwa kwenye zawadi ya thamani inavyoipa upendezi mwingi, adabu zinafanya kile tunachotolea watu kiwe na upendezi mwingi. Hata tuwe tuna sifa gani nyingine za Kikristo au tuwe tuna makusudio ya kusifika kama nini, hayatakuwa na matokeo mengi ikiwa hatuna adabu. Kwa hiyo adabu zetu zinaweza kumleteaje Yehova utukufu?

4. Inatupasa tuangalie adabu zetu katika maeneo gani ya maisha?

4 “Ila tu jiendesheni kwa namna inayozistahili habari njema,” anasema Paulo. (Wafilipi 1:27, NW) Bila shaka, hii inatia ndani huduma yetu ya peupe. Lakini mwenendo na adabu zetu kwenye mahali petu pa ibada, katika ujirani wetu, kazini, shuleni, ndiyo, katika kila upande wa maisha zetu, zinahusika moja kwa moja pia katika matokeo ya huduma yetu. “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe,” anaandika Paulo. (2 Wakorintho 6:3) Sisi tunaweza kuhakikishaje kwamba tunatumia shauri hilo? Tunaweza kufanya nini tusaidiane sisi kwa sisi, hasa kuwasaidia wachanga walio miongoni mwetu, waonyeshe adabu za Kikristo nyakati zote?

Kwenye Jumba la Ufalme

5. Inatupasa tutambue nini tunapokuwa kwenye Jumba la Ufalme?

5 Jumba la Ufalme ni mahali petu pa ibada. Tunakuwa hapo kwa kualikwa na Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Katika maana hiyo, sisi ni wageni kwenye nyumba ya Yehova. (Zaburi 15:1; Mathayo 18:20) Je! wewe ni mgeni mwema unapokuja kwenye Jumba la Ufalme? Ili tuwe hivyo, ni lazima tuonyeshe ufikirio na staha inayofaa si kwa mkaribishaji tu bali pia kwa wageni wale wengine. Hiyo inahusisha nini ndani?

6. (a) Kuchelewa mikutano nyakati zote kunaonyesha ukosefu wa nini? (b) Ni jambo gani linaweza kufanywa ili kushinda tatizo hili?

6 Kwanza, kuna lile jambo la kufika katika wakati unaofaa. Inakubaliwa kwamba si rahisi sikuzote kufanya hivyo. Watu fulani huishi mbali; wengine wana jamaa na watoto wa kutayarisha. Jitihada wanayofanya kuja kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida inastahili pongezi kweli kweli. Hata hivyo, imeonwa kwamba watu fulani wameangukia tabia ya kufika mikutanoni wakiwa wamechelewa. Wanaweza kufanya nini warekebishe jambo hili? Kwanza ni lazima mtu atambue kwamba si sikuzote ambapo tabia ya kuchelewa kwenye mikutano ya Kikristo huonyesha kutothamini ubora wa mikutano. Watu fulani wanaochelewa-chelewa huonekana wakiionea​—shangwe mikutano sawasawa na mtu mwingine yeyote​—mara wakiisha kufika pale. Lakini ilivyo ni kwamba, huenda tatizo likatokana na mipango mibaya na kutofikiria Wakristo wenzao. Moja ya sababu tunazoshauriwa ‘tusiache kukusanyika pamoja’ ni ili tupate ‘kuangaliana na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.’ (Waebrania 10:24, 25) Ni vigumu kufanya hivyo ikiwa sisi hufika tumechelewa, muda baada ya muda, na hivyo kuvuta kando fikira za wengine au kuwasumbua. Walio wastadi wanapendekeza kwamba, ili tusichelewe, inatupasa tufike mapema vya kutosha badala ya kufika pale wakati ule ule uliowekwa. Je! wewe unahitaji kujizoeza jambo hili?

7. Eleza usikizi kwenye mikutano unahusianaje na adabu.

7 Adabu zinataka kwamba tuelekezee watu usikizi wetu wanaponena nasi. (Mithali 4:1, 20) Hii inatumika pia kwa mikutano ya Kikristo, ambapo wahudumu wa Mungu wananena ili kutupa sisi zawadi fulani ya kiroho ili kutujenga. Ungekuwa wonyesho wa ukosefu mkubwa sana wa adabu kwa upande wetu kama tungesinzia-sinzia, tumnong’oneze-nong’oneze aliyeketi karibu nasi, tutafune-tafune gamu au vitu vya aina ya peremende, tusome mambo mengine, au tushughulikie mambo mengine wakati wa mkutano. Kijana Elihu hakuketi kwa saburi tu muda wote wa zile hotuba ndefu zilizotolewa na Ayubu na wale waandamani watatu, bali pia ‘aliendelea kutega sikio’ kwa waliyosema na ‘akaendelea kuwageuzia usikizi wake.’ (Ayubu 32:11, 12, NW) Adabu za Kikristo zitatusukuma tuonyeshe staha inayofaa kwa mnenaji na ujumbe wake wenye msingi wa Biblia kwa kumpa usikizi na kumuunga mkono kwa njia isiyogawanyika.

8. Tunaonyeshaje kwamba sisi ni wanafunzi wenzi wa Yesu Kristo?

8 Kabla na baada ya mikutano, adabu za Kikristo zinatia ndani kupendezwa kwa bidii na wengine waliopo penye Jumba la Ufalme. Paulo aliona kwamba washiriki wapakwa mafuta wa kundi la Kikristo ‘sasa si wageni wala wapitaji, bali ni watu [washiriki, AW] wa nyumbani mwake Mungu.’ (Waefeso 2:19) Je! wewe unatendea Mashahidi wenzako kama watu usiowajua na kama wageni, au kama washiriki wa nyumba ile ile moja? Salamu ya kirafiki, kuwatikisa mkono kwa uchangamfu, tabasamu yenye fadhili​—labda yote hayo ni mambo madogo, lakini ni sehemu ya ushuhuda wa kwamba sisi ni wanafunzi wenzi wa Yesu Kristo. Ikiwa sisi hufanya fadhili hizo tunapokuta watu tusiowajua, je! hatupaswi kufanya hivyo “hasa kuelekea wale wanaohusiana nasi katika imani”?​—Wagalatia 6:10, NW.

9. Watoto wanaweza kufundishwaje kuonyesha upendezi katika watu wengine zaidi ya wale wa umri wao wenyewe?

9 Je! watoto wanaweza kufundishwa kuonyesha upendezi wa aina hii katika watu wasio wa umri wao wenyewe? Huenda watu wazima fulani wakahisi kwamba watoto wanahitaji kwenda wakacheze na rafiki zao wadogo baada ya kuketi muda wa saa moja au mbili wakisikiliza kwenye mikutano. Lakini Jumba la Ufalme sipo mahali pa mchezo. (Mhubiri 3:1, 17) Wakati mvulana wa miaka minne na nusu alipoulizwa na mwalimu wake ana ndugu na dada wangapi, yeye alijibu: “Ni wengi sana hata siwezi kuhesabu wote.” Baadaye, wazazi wake walipomuuliza juu ya jambo hili, mvulana huyo alieleza hivi: “Mimi sijui nina ndugu na dada wangapi. Ninapoenda kwenye Jumba la Ufalme, ni wengi sana.” Kwake yeye, wote wanaohudhuria ni ndugu na dada zake.

Katika Huduma Yetu ya Peupe

10. Ni agizo gani kutoka kwa Yesu linaloweza kutusaidia ‘tujiendeshe kwa namna inayozistahili habari njema’ tunapokuwa katika huduma yetu?

10 Bila shaka ‘kujiendesha kwa namna inayozistahili habari njema’ kunahusisha ndani huduma yetu ya peupe. Ni lazima tuzingatie akilini kwamba tuna ujumbe wa amani, na adabu zetu zinapasa kuonyesha kwamba ndivyo ulivyo. (Waefeso 6:15) Agizo kutoka kwa Yesu ni kwamba: “Nanyi mkiingia katika nyumba isalimuni. Na nyumba ile ikistahili, amani yenu na iifikilie.” Kwa kuwa wachangamfu, wenye urafiki, na wenye staha, tunajulisha mwenye nyumba kwamba tunapendezwa naye kikweli moyoni. Ingawa hivyo, nyakati fulani, huenda mtu tunayekuta mlangoni akawa hana urafiki, hata mtaka ugomvi. Je! sisi tutafadhaika na kuanza kujiendesha kwa namna yake? Angalia vile Yesu alivyoendelea kusema: “La, kwamba [nyumba ile ] haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi.” (Mathayo 10:12, 13) Adabu zetu mlangoni zinapasa sikuzote kuistahili “huduma ya upatanisho.”​—2 Wakorintho 5:18, NW.

11. Kuvalia kwetu na sura ya kibinafsi kunaathirije fungu letu la kuwa wahudumu wa Mungu?

11 Adabu zetu zinanena juu yetu kwa njia nyinginezo pia. Kwa kielelezo, je! sura yetu ya kibinafsi inalistahili fungu letu tukiwa mhudumu wa Neno la Mungu? Namna gani vifaa tunavyotumia​—mkoba wa vitabu, Biblia, na vitabu vya Kibiblia? Mchangia habari katika gazeti moja anawapa wanakazi ushauri huu: “Valia kikazi, si kwa mtindo wa kuhudhuria karamu, kwa mtindo wa kikusanyiko cha starehe au mchezo fulani.” Kwa nini? Kwa sababu mavazi yako na sura ya kibinafsi “ni njia ya mkato ya kuwaeleza watu wanaokuzunguka wewe ni nani na wewe ni nini na ni mahali gani panapokufaa katika utaratibu wa mambo.” Kwa hiyo tunapoendesha “shughuli” yetu ya kihuduma, mavazi na sura yetu hayapasi kuvaliwa ovyoovyo tu wala kuwa machafu-machafu, wala hayapasi kuwa na uzuri unaochoma macho ya watu wala yenye madoido ya kupita kiasi, bali sikuzote yawe ‘yanazistahili habari njema.’​—Linganisha 1 Timotheo 2:9, 10.

12. Adabu zinaweza kuonyeshwaje kuhusiana na haki na mali za mwenye nyumba?

12 Ingawa inatupasa ‘tuwe tayari sikuzote kuzitetea’ habari njema, adabu za Kikristo zinataka kwamba tufanye hivyo “kwa tabia pole ya moyoni na staha yenye kina kirefu.” (1 Petro 3:15, NW) Hiyo inatia ndani kustahi haki na mali za mwenye nyumba. Je! sisi hupanga utendaji wetu ili tuzuru wakati unaomfaa mtu tunayemzuru? Je! tuko chonjo kuangalia kama tunakatiza shughuli au kazi fulani muhimu? Je! sisi ni wakarimu katika kutumia maneno kama “Je! naweza?” “Tafadhali,” na “Asante”? Je! tunajitahidi kuhusisha mwenye nyumba katika maongezi, au sisi tunayatawala kwa kuhofu kwamba huenda tusimalize mambo tuliyojitayarisha kusema?

13. Toa kielezi juu ya jinsi adabu katika huduma huleta matokeo mema mara nyingi.

13 Adabu, zikiwa pamoja na hangaikio la kibinafsi lenye moyo mweupe, mara nyingi zinafungua njia ya ushuhuda mwema. Hii ndiyo sababu mara nyingi watoto wenye adabu hupata usikizi na upendezi wa wenye nyumba mahali ambapo huenda watu wazima wakashindwa kufanya hivyo. Shahidi wa miaka 13 katika Meksiko alikuta msichana mchanga aliyetaka kujifunza. Hata hivyo, msichana huyo alisema angelazimika kufanya hivyo bila kujulikana na baba yake. Lakini mhubiri yule mchanga akahisi kwamba, ikiwa ndivyo, yeye mwenyewe anapaswa kumwomba ruhusa baba huyo kwa sababu ya kumstahi. Kwa hiyo akajitolea kunena na baba huyo na kumwambia kwamba mambo ambayo wangejifunza yalikuwa ya maana sana. Kwa kuona jinsi dada huyo mchanga alivyokuwa akichukua mambo kwa uzito na kwa kuthamini kwamba alikuwa amemjia yeye moja kwa moja, baba huyo alisema: “Ikiwa mambo mtakayojifunza ni ya maana hivyo, basi jamaa yangu yote inapaswa kujifunza.” Tokeo likawa kwamba kijana huyu wa miaka 13 alianzisha funzo la Biblia pamoja na jamaa nzima, kutia na mwana mmoja aliyefunga ndoa, pamoja na mke wake na watoto wengine waliokwisha kukua.

Adabu Huanzia Nyumbani

14. Adabu huanzia wapi, na ni jambo gani lililo la maana?

14 Mara nyingi adabu za Mashahidi wachanga ni ushuhuda mzuri unaoonyesha wazi mazoezi wanayopokea nyumbani. Kweli kweli, adabu zetu ni wonyesho wa njia yetu ya maisha. Kwa sababu hii, kinyume cha vile huenda watu fulani wakafikiri, adabu zinapasa kupewa umaana mkubwa nyumbani. Katika jambo hili, kama ilivyo katika pande nyingine za maisha ya jamaa, kielelezo cha wazazi ndicho cha maana zaidi. (2 Timotheo 1:5) Kuambia watoto, “Fanya kama nisemavyo, si kama nitendavyo” kwa uhakika si njia ya kuwafundisha adabu. Mtu hujifunza mambo mengi sana yanayohusiana na adabu, si kwa maagizo ya maneno tu, bali kwa kuona na kuiga. “Wazazi hawawi wamefanya yote kabisa kwa kuwa walimu tu; wao pia ni violezo, kwa maana watoto wetu wanajifunza kwa kuiga njia zetu,” anasema Beverley Feldman, mtungaji wa Kids Who Succeed. Watoto wako wanaona wewe ukiwa na adabu za aina gani?

15. Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao wasitawishe tabia za kuwa na adabu muda wa maisha yote?

15 “Akina baba, msiwe mkiwachokoza watoto wenu” ndilo shauri la Biblia. (Waefeso 6:4, NW) Watoto huchokozeka na kuvurugika mawazo wanapoambiwa kwamba wanapaswa kuwa wenye fadhili na ufikirio, na bado wanaona wazazi wao wakibishana, wakisengenya watu, wakitenda kwa ufidhuli, au wakiudhika kwa urahisi. Je! wao wanaweza kulaumiwa wakitenda kwa namna iyo hiyo? Kwa upande ule mwingine, andiko linaendelea kusema hivi: “Bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” Na hiyo inatia ndani mambo yale ya msingi yanayohusu adabu, kama kusema, “Habari,” “Tafadhali,” “Asante,” na “Pole,” kuonyesha staha kwa wenye umri mkubwa, na kushirikiana vitu na wengine. (Walawi 19:32; Warumi 16:3-7) Sifa hizi ambazo wanajifunza nyumbani wakati wa utoto zitakuwa zenye thamani muda wa maisha yote.​—Mithali 22:6.

16. Ni jitihada gani zinazohitajiwa, matokeo yakiwa nini?

16 Kwa hiyo wazazi na watoto pia wanapaswa kuzoea adabu zikiwa sehemu ya kawaida yao ya kila siku badala ya kungoja mpaka pindi fulani ya pekee. Katika kufanya hivyo, wazazi wanapaswa kuwa wenye saburi na wavumilivu kuhusu makosa ambayo pasipo shaka watoto watafanya. Wajulisheni kwamba mnathamini sana wakiwa na mwenendo mwema, na mwe wepesi kuwapongeza wakati maendeleo yanapofanywa. Bila shaka, hii inataka jitihada nyingi kwa upande wenu. Lakini je! Maandiko hayakusema kwamba kanuni za kimungu zinapasa kukazwa kikiki katika watoto wakati “uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo [uamkapo, NW]”? (Kumbukumbu 6:7) Kufanya hivyo hufanyiza hali ya kirafiki na ya starehe nzuri nyumbani, ambayo inasaidia sana kuwakuza watoto wako wakawe watu wazima wenye msaada kwa watu, wenye kujali, na wenye adabu. Halafu watakuwa chanzo cha sifa na heshima kwako na kwa Muumba wao, Yehova Mungu.

Kikundi cha Watu Wenye Adabu

17. Ni nini huonwa kwenye Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova?

17 Wale “Mashahidi zaidi ya 1,000” waliokusanyika nje ya Jumba la Jiji katika Jiji la New York alasiri hiyo ya Septemba walionyesha kwa kadiri ndogo tu jinsi Mashahidi wa Yehova hujiendesha kwa ukawaida. Mahali pengine, mwanamume mmoja alikuja kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza na baadaye akasema: “Kwa siku moja nilikuta watu, ambao hatujuani kabisa, walio na upendo wa kweli kuliko wale niliopata kuwakuta wakati wowote katika kanisa ambamo nililelewa.” Tokeo likawa nini? “Ilionekana wazi kwamba nilikuwa nimeupata ukweli,” yeye akasema. Mwanamume huyu alibadili mwendo wake wa maisha, na miezi saba baadaye akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova na kubatizwa.​—Linganisha 1 Wakorintho 14:25.

18. Kiwango cha adabu za Mashahidi wa Yehova kimeathirije watu wa nje?

18 Kiwango cha adabu na mwenendo bora wa Mashahidi kwenye mikusanyiko yao ya kitaifa na kimataifa kimesifiwa sana. Katika pindi moja ya jinsi hiyo hivi majuzi katika Japani, mwongozi wa safari katika basi ya utalii alisema hivi: “Nyinyi watu mlipokuwa mkishuka basi, kila mmoja wenu, kutia na walio wachanga, hamkukosa kuniambia, ‘Asante sana.’ Hiyo ilinifurahisha sana!” Kwenye mkusanyiko mwingine, mtumikia watu kwenye kituo cha gari-moshi cha hapo karibu aliambia Shahidi hivi: “Kulikuwako vurugu kubwa sana wakati kusanyiko lililotangulia la watu 12,000 lilipofanywa kwenye Osaka Castle Hall.” Lakini akaendelea kusema hivi: “Nyinyi watu mna utaratibu kweli kweli, na mzigo umetuondokea. Tafadhali tupelekeeni shukrani zetu kwa yeyote yule anayesimamia kazi.”

19. Kila mmoja wetu anapaswa aazimie kufanya nini kuhusu adabu?

19 Maelezo hayo yanaonyesha nini? Kwamba Mashahidi wa Yehova kwa ujumla ‘wanajiendesha kwa namna inayozistahili habari njema.’ Namna gani sisi mmoja mmoja? Kama watoto wanaotegemea baba mwenye upendo, sisi sote, wachanga kwa wazee, na tutegemee Baba yetu wa kimbingu, Yehova, ili tupate kufundishwa kuwa watu wenye adabu, hata katika ulimwengu usio na adabu.​—Kumbukumbu 8:5; Mithali 3:11, 12.

Wewe Unakumbuka?

◻ Kwa nini adabu zinahitajiwa kuwa sehemu ya mwenendo mwema?

◻ Ni adabu gani zinazofaa mahali petu pa ibada?

◻ Adabu zinaweza kuonyeshwaje katika huduma ya shambani?

◻ Wazazi wanaweza kusaidiaje watoto wao wasitawishe adabu?

◻ Ni kiwango gani cha juu tunachopaswa kujitahidi kuunga mkono kuhusu adabu?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki