Kutia Alama Kunakoleta Ukombozi
1 Kabla ya kutekeleza hukumu zake za uadilifu, Yehova sikuzote hutoa onyo na kuandalia wanyenyekevu njia ya kuokokea. Katika siku ya Ezekieli, kulikuwa wale waliokuwa wakitweta na kupiga kite kuhusu mambo ya kuchukiza yaliyokuwa yakifanywa. Yehova alisababisha wenye ustahili hao watiwe alama kwa ajili ya ukombozi wao. (Eze. 9:4-6) Kazi yetu ya kuhubiri leo hutimiza kusudi lilo hilo. Twaweza kutimiza sehemu muhimu.
2 Kupata watu wanyoofu ni hatua ya kwanza tu. Twapanga ziara ya kurudia. Utayarishaji kwa ajili ya ziara ya kurudia wafanywa kwa mara ya kwanza kwa kuandika angusho na habari iliyozungumzwa. Mafanikio yetu ya kurudi tena yatategemea zaidi tulilojitayarisha kusema na kufanya tunaporudi.
3 Kwa kufuatia angusho la “Mnara wa Mlinzi,” ungeweza kukazia kichwa chalo kikuu:
◼ “Angalia kwamba kwenye jalada la mbele la Mnara wa Mlinzi kuna maelezo ‘Unaotangaza Ufalme wa Yehova.’ Kinachofanya gazeti hili kuwa lisilo na kifani ni kwamba hilo hutetea Ufalme wa Mungu kuwa suluhisho pekee la matatizo ya ulimwengu. Huelezea utakalotimiza Ufalme wa Mungu mapenzi ya Mungu yatakapotimizwa duniani. Hii ndiyo habari njema ambayo Yesu alisema ingehubiriwa katika dunia yote.” Soma Mathayo 24:14, na ueleze jinsi Mnara wa Mlinzi liwezavyo kupatikana kwa kawaida na kutumiwa katika funzo la kibinafsi la Biblia.
4 Huenda ukapendelea kukazia tu Biblia yenyewe na kutilia mkazo uhitaji wa kuisoma kwa kawaida. Ungeweza kusema:
◼ “Yaonekana kwamba karibu kila mtu tujuaye angethamini ushauri wenye kutumika wa jinsi ya kukabili matatizo ya kila siku ya maisha. Unafikiri ni wapi tunapoweza kupata ushauri tunaoweza kutumaini? [Ruhusu itikio.] Wengi ambao wameweka tumaini lao katika ushauri wa marafiki au ambao wamelipa kwa ajili ya ushauri wa wastadi wametamaushwa sana. Kwa upande mwingine, mamilioni ya watu wameona Biblia kuwa chanzo pekee cha ushauri wawezao kutumaini. Biblia huandaa mafundisho juu ya jinsi ya kushinda matatizo tunayokabili leo. [Soma 2 Timotheo 3:16, 17.] Ijapokuwa huenda ukaona Biblia kuwa ngumu kuielewa, acha nikuonyeshe jinsi unavyoweza kuitumia ili ufungue hazina ya shauri lenye hekima.” Endelea kwa kufungua kwenye “Upendo” katika sehemu “Bible Words Indexed” nyuma ya New World Translation, na uonyeshe baadhi ya marejezo ambayo huonyesha jinsi upendo unavyoweza kutusaidia tutatue tofauti zetu na wengine.
5 Ukiwa na mradi wa kuanzisha funzo la Biblia, huenda ukachagua kutumia kitabu “Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani,” ukitumia utangulizi huu:
◼ “Twapenda familia zetu na twazitakia mema. Familia yako ingenufaikaje kwa kuishi katika ulimwengu kama huu?” Onyesha vielezi kwenye kurasa 156-157. Soma andiko moja au mawili yaliyonukuliwa kwenye kurasa hizo, na ueleze kwamba hizi ndizo ahadi zilizofanywa na Yehova Mungu, asiyeweza kusema uwongo. Rejezea orodha ya sura zilizo kwenye kurasa 5-6, na umwulize mwenye nyumba ni habari gani impendezayo zaidi; fungua sura achaguayo, na mzungumze fungu moja au mawili.
6 Ungependa kusaidia mtu mwingine atiwe alama ya kukombolewa? Mafanikio hutokana na ‘kutimiliza huduma yako kikamili’ kwa kujitayarisha vizuri na kufuatia mara hiyo kupendezwa kote unakopata.—2 Tim. 4:5.