Mafunzo Juu ya Maandiko Yenye Pumzi ya Mungu na Habari ya Msingi Yayo
Funzo Namba 8—Faida za “New World Translation”
Mazungumzo juu ya lugha yalo ya ki-siku-hizi, upatano wayo, kutafsiri kwayo vitenzi, na lugha yenye kitendo ya Neno la Mungu alilopulizia.
1. (a) New World Translation inasahihisha maelekeo gani, na kwa jinsi gani? (b) Katika Kiingereza, ni kwa nini Yehova hutumiwa badala ya Yahweh au namna nyingine ya jina hilo?
KATIKA miaka ya karibuni hesabu fulani ya tafsiri za Biblia za ki-siku-hizi zimetangazwa zikasaidia sana wapendao Neno la Mungu waelewe maana ya miandiko ya awali kwa upesi. Hata hivyo, tafsiri nyingi zimeondoa matumizi ya jina la kimungu kutoka maandishi matakatifu. Kwa upande ule mwingine, New World Translation huadhimisha na kustahi jina linalostahili la Mungu Aliye Juu Zaidi kwa kulirudisha mahali palo panapofaa katika maandishi-awali. Jina hilo sasa laonekana mahali 6,973 katika kisehemu cha Andiko la Kiebrania, na pia katika mahali 237 katika sehemu ya Andiko la Kigiriki, jumla ya mahali 7,210. Namna ya Yahweh hurejezewa kwa ujumla na wasomi wa Kiebrania, lakini uhakika wa matamshi haujulikani sasa. Kwa hiyo, namna ya Kilatini Yehova yaendelea kutumiwa kwa sababu imekuwa ikitumiwa kwa karne nyingi na ndiyo tafsiri ya Kiingereza inayokubalika zaidi ya Tetragrammatoni, au jina la Kiebrania lenye herufi nne יהוה. Msomi wa Kiebrania R. H. Pfeiffer alionelea hivi: “Hata isemweje juu ya asili yenye kutilika shaka, ‘Yehova’ ndiyo tafsiri inayofaa ya Kiingereza ya Yahweh na yapasa kubaki hivyo.”a
2. (a) Je! kuna vielelezo vya kurudisha jina la kimungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? (b) Ni shaka gani linaloondolewa kwa njia hiyo?
2 New World Translation siyo tafsiri ya kwanza kurudisha jina la kimungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kutoka angalau karne ya 14 na kuendelea, watafsiri wengi walihisi wamelazimika kurudisha jina la Mungu kwenye maandishi-awali, hasa katika sehemu ambazo waandishi wa Andiko la Kigiriki la Kikristo wananukuu kutoka maandishi-awali ya Andiko la Kiebrania yenye jina la kimungu. Tafsiri nyingi za wamisionari za lugha ya ki-siku-hizi, kutia ndani za Kiafrika, Kiesia, Kiamerika, na tafsiri za visiwa vya Pasifiki za Maandiko ya Kigiriki, hutumia jina Yehova kwa wingi, sawa na vile baadhi ya tafsiri za lugha za Kiulaya. Popote ambapo jina la kimungu limetafsiriwa, hakuna shaka tena juu ya ni “bwana” gani anayetajwa. Ni Bwana wa mbingu na dunia, Yehova, ambaye jina lake linatakaswa kwa kufanywa maalumu na tofauti katika New World Translation of the Holy Scriptures.b
3. Ni kwa njia gani New World Translation husaidia kuwasilisha kani, upendezi, na maana ya maandishi ya awali?
3 New World Translation huongezea utakaso wa jina la Yehova kwa kuyaweka Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu katika lugha iliyo wazi, yenye kueleweka inayotokeza maana inayokusudiwa kwa uwazi kwenye akili ya msomaji. Hutumia lugha yenye kueleweka vyepesi, ya ki-siku-hizi, ni yenye upatano kwa kadiri iwezekanayo katika tafsiri zayo za maneno, hueleza kitendo au hali inayosimuliwa katika vitenzi vya Kiebrania na Kigiriki kwa usahihi, na hutofautisha kati ya wingi na umoja katika kutafsiri kiwakilishi-nafsi huru “you” (Kiingereza) na namna ya kuamuru ya kitenzi mahali ambapo muktadha hauonyeshi wazi. Katika njia hizo na nyingine nyingi, New World Translation hutokeza katika uneni wa ki-siku-hizi, kwa kadiri kubwa iwezekanayo, kani, upendezi, na maana ya yale maandishi ya awali.
MATUMIZI YA MANENO KATIKA LUGHA YA KI-SIKU-HIZI
4. (a) Mtafsiri mmoja wa mapema wa Biblia alieleza juu ya kusudi gani bora? (b) Ni jambo gani limekuwa la lazima kwa kadiri wakati umepita?
4 Tafsiri za kale zaidi za Biblia zina maneno mengi yasiyotumika ya karne ya 16 na ya 17. Ingawa hayaeleweki sasa, yalieweka upesi wakati huo. Kwa kielelezo, mwanamume mmoja aliyehusika sana katika kuyatia ndani ya Biblia ya Kiingereza alikuwa ni William Tyndale, ambaye yaripotiwa alimwambia mmoja wa wapinzani wake wa kidini: ‘Mungu akihifadhi uhai wangu, kabla ya miaka mingi nitafanya mvulana anayeshika jembe ajue mengi juu ya Maandiko zaidi yako wewe.’ Tafsiri ya Tyndale ya Maandiko ya Kigiriki ilikuwa nyepesi vya kutosha kueleweka na mvulana-mshika-jembe wa wakati wake. Hata hivyo, mengi ya maneno aliyotumia sasa yamekuwa ya kikale, hivi kwamba ‘mvulana anayeshika jembe’ hawezi tena kuelewa kwa uwazi maana ya maneno mengi katika Tafsiri ya Biblia ya King James. Kwa hiyo, imekuwa lazima kuondoa kifuniko cha lugha ya kikale na kurudisha Biblia kwenye lugha ya kawaida ya makabwela.
5. Biblia yapasa itokee katika lugha gani, na kwa nini?
5 Lugha ya kabwela ndiyo iliyotumiwa katika kuandika Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu. Mitume na Wakristo wengine wa mapema hawakutumia Kigiriki cha maandishi yaliyo bora sana cha wanafalsafa kama vile Plato. Walitumia Kigiriki cha kila siku, yaani, Koine, au Kigiriki cha kawaida. Kwa hiyo, Maandiko ya Kigiriki, kama vile Maandiko ya Kiebrania yaliyotangulia, yaliandikwa katika lugha ya akina yahe. Basi, ni jambo lenye maana sana kwamba tafsiri za Maandiko ya awali ziwe pia katika lugha ya akina yahe, ili zieleweke upesi. Ni kwa sababu hiyo kwamba New World Translation hutumia, si lugha ya kikale ya karne tatu au nne zilizopita, bali uneni ulio wazi, wenye uhai wa ki-siku-hizi ili wasomaji wapate kujua kikweli inayosema Biblia.
6. Toa kielezi cha mafaa ya kutumia semi za wakati huu badala ya maneno yasiyotumiwa tena.
6 Ili kutoa wazo fulani juu ya ukubwa wa badiliko katika lugha ya Kiingereza tangu karne ya 17 mpaka karne ya 20, angalia ulinganishi ufuatao kutoka King James Version na New World Translation. “Suffered” katika King James Version huwa “allowed” katika New World Translation (Mwa. 31:7), “was bolled” huwa “had flower buds” (Kut. 9:31), “spoilers” huwa “pillagers” (Amu. 2:14), “ear his ground” huwa “do his plowing” (1 Sam. 8:12), “when thou prayest” huwa “when you pray” (Mt. 6:6), “sick of the palsy” huwa “paralytic” (Mk. 2:3), “quickeneth” huwa “makes . . . alive” (Rum. 4:17), “shambles” huwa “meat market” (1 Kor. 10:25), “letteth” huwa “acting as a restraint” (2 The. 2:7), na kadhalika. Kutokana na hayo thamani ya New Wolrd Translation katika kutumia maneno ya kisasa badala ya maneno yasiyotumika tena yaweza kuthaminiwa.
ULINGANISHI WA TAFSIRI ZA MANENO
7. Ni jinsi gani New World Translation ni yenye upatano katika tafsiri zayo za maneno?
7 New World Translation hufanya kila jitihada kuwa na upatano katika tafsiri zayo za maneno. Kwa neno lolote lile la Kiebrania au Kigiriki, kuna neno moja la Kiingereza, nalo limetumiwa kwa ulinganishi kwa kadiri ambayo nahau au muktadha waruhusu katika kutoa maana kamili ya Kiingereza. Kwa kielelezo, neno la Kiebrania neʹphesh kwa upatano latafsiriwa “soul” (nafsi). Neno linalolingana na hilo la Kigiriki, psy·kheʹ, hutafsiriwa “soul” kila linapotokea.
8. (a) Toa vielelezo vya homografu. (b) Hilo limeshugulikiwaje katika tafsiri hiyo?
8 Katika mahali fulani-fulani tatizo limetokea la tafsiri ya homografu. Hayo ni maneno katika lugha ya awali ambayo huendelezwa kwa njia ile ile lakini yenye maana za msingi tofauti. Kwa hiyo, tatizo ni kutia neno lenye maana sahihi wakati wa kutafsiri. Katika Kiingereza kuna homografu kama vile “Polish” (mtu wa Poland) na “polish” (kupiga sulu) na “lead” (kuongoza kondoo) na “lead” (mtaimbo) au katika Kiswahili ni kama vile “kaa” (la moto) na “kaa” (la kinywa) na “paka” (hayawani) na “paka” (rangi), ambayo huendelezwa sawasawa lakini ni maneno yaliyo tofauti kabisa. Kielelezo kimoja cha Biblia ni rav ya Kiebrania, linalowakilisha maneno yenye mashina tofauti kabisa, na kwa hiyo hayo hutafsiriwa tofauti-tofauti katika New World Translation. Rav kwa kawaida zaidi lina maana ya “wengi,” kama vile katika Kutoka 5:5. Hata hivyo, neno rav linalotumiwa katika vyeo, kama katika “Rabshake” (Kiebr., Rav-sha·qehʹ) katika 2 Wafalme 18:17, humaanisha “chief” (mkuu) kama wakati linapotafsiriwa “his chief court official” katika Danieli 1:3. (Ona pia Yeremia 39:3, NW, kielezi-chini.) Neno rav, linalofanana katika umbo, humaanisha “archer” (mpiga-upinde), hilo likieleza sababu ya ile tafsiri katika Yeremia 50:29. Wataalamu wa maneno, kama vile L. Koehler na W. Baumgartner, wamekubaliwa na watafsiri kuwa ni wenye amri katika kutenganisha maneno hayo yanayoendelezwa kwa kufanana.
9. Mwelezaji mmoja wa Kiebrania na Kigiriki alikadiriaje New World Translation?
9 Kwa habari ya sehemu hiyo ya ulinganishi, angalia jinsi mwelezaji wa Kiebrania na Kigiriki Alexander Thomson alivyosema katika pitio lake juu ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures: “Kwa wazi tafsiri hiyo ni kazi ya wasomi stadi na werevu, ambao wamejaribu kutokeza maana ya kweli ya maandishi-awali ya Kigiriki kwa kadiri ambayo lugha ya Kiingereza yaweza kueleza. Tafsiri hiyo ina lengo la kutumia maana moja ya Kiingereza kwa kila neno kuu la Kigiriki, na kuwa yenye uhalisi kwa kadiri iwezekanayo. . . . Neno ambalo kwa kawaida hutafsiriwa ‘stahiki’ kwa ujumla hutafsiriwa kwa usahihi sana kuwa ‘julisha rasmi kuwa mwadilifu.’ . . . Neno kwa ajili ya Msalaba hutafsiriwa ‘mti wa mateso’ hayo yakiwa ni maendeleo mengine. . . . Luka 23:43 limetafsiriwa vizuri, ‘Kwa kweli nakuambia wewe leo, Wewe utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.’ Hayo ni maendeleo makubwa yanayopita tafsiri zilizo nyingi.” Juu ya tafsiri ya Maandiko ya Kiebrania, mpitiaji uyo huyo alitoa elezo hili: “Tafsiri ya New World yastahili mtu ajipatie. Ni yenye kitendo na ina uhai, na hufanya msomaji afikiri na kujifunza. Hiyo si kazi ya Wachambuzi wa Biblia, bali ya wasomi wanaostahi Mungu na Neno Lake.”—The Differentiator, Aprili 1952, kurasa 52-7, na Juni 1954, ukurasa 136.
10. Toa kielezi juu ya jinsi ufanani wa New World Translation hutegemeza kweli ya Biblia.
10 Upatano wa New World Translation umeshinda mazungumzo mengi ya istilahi (maneno) za Biblia katika shamba. Kwa kielelezo, miaka kadhaa iliyopita, sosaiti moja ya watu wenye kushika mawazo yao katika New York iliuliza Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ipeleke wanenaji wawili wahutubie kikundi chao juu ya mambo ya Kibiblia, ombi ambalo lilikubaliwa. Wanaume hao wenye elimu walishikilia methali ya Kilatini, falsum in uno falsum in toto, inayomaanisha kwamba hoja ikithibitishwa ni bandia katika jambo moja basi hiyo ni bandia katika yote. Wakati wa mazungumzo hayo, mtu mmoja alitokezea Mashahidi wa Yehova tatizo juu ya utegemeko wa Biblia. Akauliza Mwanzo 1:3 lisomewe wasikilizaji, na hilo likafanywa, katika New World Translation: “Na Mungu akachukua hatua ya kusema: ‘Acha nuru ije kuwapo.’ Kisha nuru ikaja.” Ndipo akiwa na uhakika, akauliza Mwanzo 1:14, nalo likasomwa pia katika New World Translation: “Na Mungu akaendelea kusema: ‘Acha vimulikaji vije kuwapo katika upana wa mbingu.’” “Ngoja,” akasema, “unasoma nini? Biblia yangu yasema Mungu alifanya nuru mnamo siku ya kwanza, na tena mnamo siku ya nne, na huo ni ukosefu wa upatano.” Ingawa alidai ajua Kiebrania, ilipasa atajiwe kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “nuru” katika mstari 3 lilikuwa ’ohr, hali neno katika mstari 14 lilikuwa tofauti, likiwa ni ma·’ohrʹ, ambalo hurejezea kimulikaji, au chanzo cha nuru. Mwanamume huyo mwenye elimu akaketi chini hali ameshindwa.c Upatano wenye uaminifu wa New World Translation ulikuwa umejishindia jambo, ukategemeza Biblia kuwa yenye kutegemeka na yenye mafaa.
KUTAFSIRIWA KWA UANGALIFU KWA VITENZI
11. Ni sehemu gani yenye nguvu ya Maandiko ya awali imehifadhiwa katika New World Translation? Jinsi gani?
11 New World Translation hutoa uangalifu wa pekee katika kuwasilisha maana ya kitendo cha vitenzi vya Kigiriki na Kiebrania. Katika kufanya hivyo, New World Translation hujaribu sana kuhifadhi haiba ya pekee, wepesi wa kueleweka, kani, na namna ya kueleza maandishi ya lugha ya awali. Kwa hiyo imekuwa lazima kutumia vitenzi vishirikishi katika Kiingereza ili kuwasilisha kwa uangalifu hali barabara ya vitendo. Kwa sababu ya uwezo wa vitenzi vyayo, Maandiko ya awali ni yenye nguvu sana na yenye ushawishi wa kitendo.
12. (a) Ni nini njia moja ambayo Kiebrania hutofautiana na lugha za Magharibi? (b) Eleza hali mbili za kitenzi cha Kiebrania.
12 Kitenzi cha Kiebrania hakina “viambishi vya wakati” kwa maana ambayo maneno “viambishi vya wakati” hutumiwa katika lugha zilizo nyingi. Katika Kiingereza, vitenzi huonwa hasa kwa maoni ya kiambishi cha wakati: uliopita, wa sasa, na wakati ujao. Kitenzi cha Kiebrania, kwa upande ule mwingine, kwa msingi huieleza hali ya kitendo, yaani, kitendo huonwa ama kikiwa kamili (hali kamilifu) au si kamili (hali isiyokamilika.) Hali hizo za kitenzi cha Kiebrania zaweza kutumiwa kuonyesha vitendo katika wakati uliopita au katika wakati ujao, muktadha ukiwa unaamua wakati. Kwa kielelezo, hali kamili, au iliyokamilishwa, ya kitenzi kwa asili huwakilisha vitendo katika wakati uliopita, lakini pia hutumiwa kunena juu ya tukio la wakati ujao kama kwamba limekwisha tukia na kupita, hilo likionyesha uhakika walo wa wakati ujao au daraka lalo la kutukia.
13. Ni kwa nini maoni yanayofaa kwa hali ya kitenzi cha Kiebrania ni ya maana ili kupata kuelewa kwa usahihi Mwanzo 2:2, 3?
13 Kuwasilisha kwa usahihi hali ya kitenzi cha Kiebrania katika Kiingereza ni jambo la maana sana; ama sivyo, maana yaweza kupotoshwa na wazo lililo tofauti kabisa kutolewa. Kwa kielelezo, fikiria semi za kitenzi katika Mwanzo 2:2, 3. Katika tafsiri nyingi, zikinena juu ya Mungu akipumzika siku ya saba, semi kama vile “yeye alipumzika,” “yeye aliacha,” “alikuwa ameacha,” “kisha yeye akapumzika,” “Mungu alipumzika,” na “yeye alikuwa amepumzika” hutumiwa. Kutokana na hayo yanavyosomeka mtu angeweza kukata kauli kwamba kupumzika kwa Mungu siku ya saba kulikamilishwa wakati uliopita. Lakini angalia jinsi New World Translation inavyotokeza maana ya vitenzi vinavyotumiwa katika kifungu kwenye Mwanzo 2:2, 3: “Na kufikia siku ya saba Mungu akaja kukamilisha kazi yake aliyokuwa amefanya, na yeye akachukua hatua ya kupumzika mnamo siku ya saba kutokana na kazi yake yote ambayo alikuwa amefanya. Na Mungu akachukua hatua ya kubariki siku ya saba na kuifanya takatifu, kwa sababu katika hiyo yeye amekuwa akipumzika kutokana na kazi yake yote ambayo Mungu ameumba kwa kusudi la kufanyiza.” Usemi katika mstari 2 “yeye akachukua hatua ya kupumzika” ni kitenzi katika hali ya kutokamilika katika Kiebrania na kwa hiyo huonyesha wazo la kitendo kisicho kamili au chenye kuendelea. Tafsiri “yeye akachukua hatua ya kupumzika” yapatana na yanayosemwa kwenye Waebrania 4:4-7. Kwa upande ule mwingine, kitenzi katika Mwanzo 2:3 ki katika hali ya kukamilika, lakini kwa kusudi la kupatanisha na mstari 2 na Waebrania 4:4-7, chatafsiriwa “yeye amekuwa akipumzika.”
14. Ikiepuka maoni yenye kosa ya kiendelezi waw, New World Translation inajaribu sana kufanya nini kwa vitenzi vya Kiebrania?
14 Moja ya sababu za ukosefu wa usahihi katika kutafsiri namna za vitenzi vya Kiebrania ni nadharia ya kisarufi iitwayo kiendelezi waw. Waw (ו) ndicho kitenzi cha Kiebrania ambacho kwa msingi humaanisha “na.” Huwa kamwe hakisimami peke yacho bali sikuzote huunganishwa na neno jingine, mara nyingi pamoja na kitenzi cha Kiebrania, ili kufanyiza neno moja pamoja nalo. Imedaiwa, na bado hudaiwa, na wengine kwamba uhusiano huo una uwezo wa kubadili kitenzi kutoka hali moja mpaka nyingine, yaani, kutoka kutokamilika mpaka kukamilika (kama ambavyo imefanywa katika tafsiri nyingi, kutia ndani za ki-siku-hizi, kwenye Mwanzo 2:2, 3) au kutoka ya kukamilika mpaka ya kutokamilika. Tafsiri hiyo isiyo sahihi ya namna ya kitenzi imeongoza kwenye vurugu nyingi na kwenye tafsiri mbaya ya maandishi-awali ya Kiebrania. New World Translation haitambui kwamba herufi waw ina mamlaka yoyote ya kubadili hali ya kitenzi. Badala yake, jaribio limefanywa kutokeza kani inayofaa na ya kutofautisha kitenzi cha Kiebrania, hivyo kuhifadhi kwa usahihi maana ya awali.d
15. (a) Vitenzi vya Kigiriki vimetafsiriwa kwa uangalifu gani? (b) Toa kielezi juu ya mafaa ya kutokeza kwa usahihi lile wazo lenye kuendelea.
15 Uangalifu kama huo umefanywa katika kutafsiri vitenzi vya Kigiriki. Katika Kigiriki viambishi vya wakati vya vitenzi havionyesha tu wakati wa kitendo au hali, bali pia aina ya kitendo, kiwe ni cha muda mfupi, kinaanza, kinaendelea, chenye kurudiwa-rudiwa, au kukamilishwa. Uangalifu kwa maana hizo katika miundo ya vitenzi vya Kigiriki huongoza kwenye tafsiri ya moja kwa moja yenye kani kamili ya kitendo kinachoelezwa. Kwa kielelezo, si kwamba tu kutia maana ya wazo la kiendelezi mahali ambapo hilo hutokea katika kitenzi cha Kigiriki hutokeza ladha yenyewe ya hali bali pia hufanya onyo na shauri lenye nguvu zaidi. Mathalani, kutokuamini kwenye kuendelea kwa Mafarisayo na Masadukayo kwatobolewa waziwazi na maneno haya ya Yesu: “Kizazi kiovu na chenye uzinzi chafuliza kutafuta ishara.” Na uhitaji wa kitendo chenye kuendelea katika mambo yanayofaa waonyeshwa vizuri na maneno ya Yesu: “Endeleeni kupenda maadui wenu.” “Fulizeni, basi, kuendelea kutafuta ufalme kwanza.” “Fulizeni kuuliza, na itapewa kwenu nyinyi; fulizeni kuendelea kutafuta, na nyinyi mtapata; fulizeni kuendelea kubisha, na itafunguliwa kwenu nyinyi.”—Mt. 16:4; 5:44; 6:33; 7:7, NW.
16. (a) Kwa kufikiria kiambishi cha wakati aorist cha Kigiriki, maelezo ya Yohana juu ya “dhambi” kwenye 1 Yohana 2:1 yasomekaje?
16 Kigiriki kina kiambishi cha wakati kisicho cha kawaida kinachoitwa aorist, ambacho hurejezea kitendo cha muda mfupi. Vitenzi vya sifa katika aorist vyaweza kutafsiriwa katika njia mbalimbali, kulingana na muktadha wavyo. Njia moja ambayo hicho hutumiwa ni kuonyesha kitendo kimoja cha aina fulani, ingawa hakihusiani na wakati wowote hasa. Kielelezo kama hicho chapatikana kwenye 1 Yohana 2:1, ambapo tafsiri nyingi hutafsiri kitenzi cha “dhambi” kwa kuruhusu mwendo wenye kuendelea wa dhambi, ambapo New World Translation husomeka, “kufanya kitendo cha dhambi,” yaani, kitendo kimoja cha dhambi. Hilo huwasilisha maana sahihi ya kwamba endapo Mkristo anafanya kitendo cha dhambi, ana Yesu Kristo, ambaye hutenda kama mtetezi, au msaidiaji, kwa Baba wa kimbingu. Kwa hiyo, 1 Yohana 2:1 halipingi kwa vyovyote bali linafanya tu kutofautisha laana ya ‘zoea la dhambi’ inayopatikana kwenye 1 Yohana 3:6-8 na 5:18, NW.e
17. Licha ya kuonyesha kitendo chenye kuendelea, kiambishi cha wakati kisichotimilika cha Kigiriki chaweza kuonyesha jambo gani jingine? Toa kielezi.
17 Kiambishi cha wakati kisichotimilika katika Kigiriki chaweza kueleza si kitendo tu kinachoendelea bali pia kitendo kinachojaribiwa lakini kisitimizwe. Angalia jinsi Waebrania 11:17 katika King James Version (Union Version) husomeka: “Kwa imani Ibrahamu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee.” Kitenzi “akamtoa” chatofautiana katika umbo katika mionekano hiyo miwili katika Kigiriki. Mwonekano wa kwanza ni katika kiambishi cha wakati timilifu (kilichokamilishwa), na hali cha pili kiko katika umbo la kutotimilika (lililopita na linaloendelea). New World Translation, kwa kufikiria viambishi hivyo vya wakati vilivyo tofauti, hutafsiri hivi mstari huo: “Abrahamu, alipojaribiwa, ni kama kwamba alimtoa Isaka, na mwanamume huyo . . . alijaribu kutoa mwana wake mzaliwa-pekee.” Maana iliyokamilika ya kitenzi cha kwanza yahifadhiwa kwa njia hiyo, na hali kiambishi cha wakati kisichotimilika cha kitenzi cha pili chaonyesha kwamba kitendo hicho kilikusudiwa au kilifanyiwa jaribio lakini hakikutekelezwa kikatimilika.—Mwa. 22:9-14.
18. Ni nini limekuwa tokeo la uangalifu mkubwa wa kazi ya sehemu nyinginezo za uneni? Toa kielelezo kimoja.
18 Uangalifu mkubwa kwa utendaji wa sehemu nyingine za uneni, kama vile kisa cha nomino, umeongoza kwenye kuondoa kunakoelekea kuwa kupingana-pingana. Kwa kielelezo, kwenye Matendo 9:7, katika kusimulia ono la kutokeza la Sauli akiwa njiani kwenda Dameski, tafsiri kadhaa husema kwamba waandamani wake wa safari ‘walisikia sauti’ lakini hawakuona yeyote. Kisha, kwenye Matendo 22:9, ambapo Paulo anasimulia kisa hicho, tafsiri izo hizo husomeka kwamba ingawa waliona ile nuru, ‘hawakusikia sauti ile.’ Hata hivyo, katika mrejezo wa kwanza, neno la Kigiriki kwa “sauti” liko kwa umbo la kiwakilishi kimilikishi, lakini katika kisa cha pili, liko kwa umbo la kiwakilikishi kibainishi, kama lilivyo kwenye Matendo 9:4. Kwa nini tofauti hiyo? Hakuna lolote la hayo linalowasilishwa katika tafsiri zilizo juu katika Kiingereza (pia Kiswahili), hata hivyo Kigiriki, kwa kubadili umbo, huonyesha kitu tofauti. Wanaume hao walisikia kihalisi “sauti” lakini hawakuisikia kwa njia aliyoisikia Paulo, yaani, kusikia maneno na kuyaelewa. Kwa hiyo, New World Translation, ikitambua matumizi ya kiwakilishi kimilikishi kwenye Matendo 9:7, husomeka kwamba wanaume waliokuwa naye walikuwa ‘wakisikia, kwa hakika, kelele ya sauti, lakini hawakumwona mtu yeyote.”
“YOU” (NYINYI) YA WINGI YAONYESHWA
19, 20. (a) New World Translation imefanya nini kwa namna za kuzungumza za kidini zilizotumika, na kwa nini? (b) Toa kielezi juu ya jinsi “you” ya Kiingereza ya umoja yaweza kutofautishwa na ile ya wingi.
19 Maumbo ya Kiingereza ya zamani zaidi ya umoja wa nafsi ya pili, “thee,” “thou,” na “thy,” yamehifadhiwa katika tafsiri fulani za ki-siku-hizi katika visa ambavyo Mungu anazungumzwa. Hata hivyo, katika lugha zile ambazo Biblia iliandikwa, hakukuwako umbo la pekee la kiwakilishi cha kibinafsi kwa matumizi ya kumzungumza Mungu, lakini umbo lilo hilo lilitumiwa wakati wa kuzungumza kwa binadamu mwenzi. Kwa hiyo New World Translation imeondoa matumizi hayo ya kidini ambayo sasa ni ya kikale na hutumia “you” (“wewe” na “nyinyi” katika Kiingereza hazitofautishwi. Zote ni “you”) Ili kutofautisha wingi “you” wa nafsi ya pili (Kiswahili “nyinyi”) na vitenzi ambavyo hesabu yavyo ya wingi haitambuliki mara moja katika Kiingereza, maneno hayo huchapwa herufi zote zikiwa kubwa kidogo. Mara nyingi husaidia msomaji kujua kama maandishi fulani ya Andiko yaliyopewa yanarejezea “you” kwa mtu mmmoja, au “YOU” kwa kikundi cha watu, kundi.
20 Kwa kielelezo, kwenye Warumi 11:13, NW, (Kiingereza) Paulo ananena na wengi: “now I speak to YOU who are people of the nations.” Lakini kwenye mstari 17 Kigiriki chabadilika kuwa “you” ya mmoja, na matumizi yanaelekezwa kwa mtu mmoja mmoja hasa: “However, if some of the branches were broken off but you . . . were grafted in . . . ”
NEW WORLD TRANSLATION KATIKA LUGHA NYINGINEZO
21. (a) Imewezekanaje kwa wengi zaidi na zaidi ya watu wa dunia kufurahia mafaa za New World Translation? (b) Jumla ya hesabu ya nakala za New World Translation zilizochapwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi kufikia 1989 ni ngapi?
21 Katika 1961 ilitangazwa kwamba Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi ilikuwa ikichukua hatua ya kutafsiri New World Translation katika lugha sita zaidi zinazotumiwa sana, yaani, Kiholanzi, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kireno, na Kihispania. Kazi hiyo ya kutafsiri ilikabidhiwa watafsiri stadi na waliojiweka wakfu, wote wakifanya kazi pamoja katika makao makuu ya Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi katika Brooklyn, New York. Walitumika wakiwa halmashauri kubwa ya kimataifa wakifanya kazi chini ya mwekelezo wenye ustadi. Ilikuwa katika Julai 1963, kwenye “Habari Njema za Milele” Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova kule Milwaukee, Wisconsin, U.S.A., kwamba malimbuko ya kazi hiyo ya tafsiri yalipatikana wakati New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilipotolewa kwa mara ya kwanza wakati ule ule mmoja katika lugha sita zilizo juu. Sasa wakaaji wa dunia wenye kunena lugha nyingine tofauti na Kiingereza wangeweza kuanza kufurahia faida za tafsiri hiyo ya kisasa. Tangu wakati huo, kazi ya kutafsiri imeendelea, hivi kwamba kufikia 1989 New World Translation of the Holy Scriptures ilikuwa imetokea katika lugha 11, kukiwa nakala zaidi ya 56,000,000 zilizochapwa.f
SHUKRANI KWA CHOMBO CHENYE NGUVU NYINGI
22, 23. Tafsiri hii ya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu inafaidi Mkristo katika njia zipi zenye kutokeza?
22 Kwa kweli New World Translation ni chombo chenye nguvu nyingi cha kuonyesha kwamba “kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa.” Kwa mawazo yaliyozungumzwa katika funzo hili, twaweza kuthamini kwamba hiyo ni sahihi na yenye kutegemeka na kwamba yaweza kutoa shangwe halisi kwa wale wanaotamani kusikia Mungu akinena na binadamu kwa mchocheo katika lugha ya ki-siku-hizi, iliyo hai. Lugha ya New World Translation ni yenye kuamsha kiroho, na humwelewesha msomaji upesi usemi wenye kitendo wa Maandiko ya awali yaliyopuliziwa na Mungu. Hatuhitaji tena kusoma na kusoma tena mistari ili tuelewe vifungu visivyokuwa wazi. Hiyo hunena kwa nguvu na uwazi tangu usomaji wa kwanza wenyewe.
23 New World Translation of the Holy Scriptures ni tafsiri ya uaminifu ya Neno la Mungu, “upanga wa roho.” Ikiwa hivyo, kwa kweli hiyo ni silaha yenye kufanikiwa katika vita ya kiroho ya Mkristo, ni msaada katika ‘kupindua mafundisho na mawazo bandia yaliyoimarishwa kwa nguvu yaliyoinuliwa juu ya maarifa ya Mungu.’ Jinsi inavyotuwezesha vizuri kujulisha rasmi kwa kueleweka vizuri zaidi mambo yanayohusiana na Ufalme wa Mungu wa uadilifu—ndiyo, “matendo makuu ya Mungu”!—Efe. 6:17; 2 Kor. 10:4, 5, NW; Mdo. 2:11.
[Maelezo ya Chini]
a Introduction to the Old Testament, Robert H. Pfeiffer, 1952, ukurasa 94.
b Kingdom Interlinear Translation, chapa ya 1985, kurasa 1133-8.
c Insight on the Scriptures, Buku 1, ukurasa 528.
d Reference Bible, nyongeza 3C, “Vitenzi vya Kiebrania Vinavyoonyesha Kitendo Kiendelevu.”
e Insight on the Scriptures, Buku 1, ukurasa 1008.
f Chapa kamili zimechapwa katika Kidenmark, Kiholanzi, Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kijapan, Kireno, na Kihispania (pia sehemu katika Kifinland na Kisweden).