Iweni Watendaji—Si Wasikiaji Tu
1 Wakristo wa kweli leo huzingatia moyoni onyo pole la Biblia la kuwa watendaji wa neno, si wasikiaji tu. (Yak. 1:22) Kufanya hivyo huwafanya wawe tofauti kabisa na wale ambao, ijapokuwa wanadai kuwa Wakristo, hutoa utumishi wa mdomo tu kwa Mungu. (Isa. 29:13) Yesu alisema waziwazi kwamba ni wale tu wafanyao mapenzi ya Mungu watakaookolewa.—Mt. 7:21.
2 Ibada bila matendo ya kimungu haina maana. (Yak. 2:26) Kwa hiyo sisi twapaswa kujiuliza, ‘Matendo yangu yanaonyeshaje kuwa imani yangu ni ya kweli? Ni nini kinachoonyesha kwamba kwa kweli naishi kupatana na yale ninayoamini? Naweza kumwigaje Yesu kikamili?’ Majibu ya moyo mweupe kwa maswali haya yatatusaidia tuone ni maendeleo gani tumefanya au bado twahitaji kufanya katika kufanya mapenzi ya Mungu.
3 Tukiwa wafuasi wa Yesu, lazima tuwe na mradi mkuu uleule maishani kama ule ulioonyeshwa na mtunga-zaburi: “Tumejisifia Mungu mchana kutwa, na jina lako tutalishukuru milele.” (Zab. 44:8) Ukristo ni njia ya maisha inayojionyesha yenyewe kila siku na katika kila kitu tufanyacho. Sisi hupata uradhi ulioje tunapoonyesha katika utendaji wetu wote tamaa yetu ya moyoni ya kumsifu Yehova!—Flp. 1:11.
4 Kumtolea Yehova Sifa Hutia Ndani Mengi Zaidi ya Kuishi Maisha Manyoofu: Ikiwa Mungu angekuwa anataka mwenendo mzuri tu, tungejishughulisha tu na kutakasa utu wetu. Hata hivyo, ibada yetu hutia ndani pia kutangaza kotekote sifa bora zaidi za Yehova na kufanya tangazo la hadharani kwa jina lake!—Ebr. 13:15; 1 Pet. 2:9.
5 Kuhubiriwa hadharani kwa habari njema ni mojapo kazi muhimu zaidi tufanyazo. Yesu alijitoa mwenyewe kwa kazi hii kwa sababu alijua ilimaanisha uhai udumuo milele kwa wale ambao wangesikiliza. (Yn. 17:3) Leo ‘huduma ya lile neno’ ni ya maana pia; ndiyo njia pekee ambayo kwayo watu wanaweza kuokolewa. (Mdo. 6:4; Rum. 10:13) Tukitambua manufaa zilizo nyingi, twaweza kujua ni kwa nini Paulo alituonya kwa upole ‘tulihubiri neno’ na ‘tulifanye kwa hima.’—2 Tim. 4:2, NW.
6 Kumsifu Yehova kwapaswa kujaza nafasi maisha yetu kadiri gani? Mtunga-zaburi alisema kwamba kulikuwa akilini mwake mchana kutwa. Je, sisi hatuhisi hivyo? Naam, na tutaona kila tukutanapo na mtu mwingine kuwa pindi iwezayo kutumiwa kusema juu ya jina la Yehova. Tutatafuta fursa zinazofaa za kuelekeza mazungumzo yetu kwenye mambo ya kiroho. Pia tutajitahidi kushiriki kwa ukawaida katika utendaji wa utumishi wa shambani uliopangwa na kutaniko. Wale walio na hali nzuri wanaweza kufikiria kwa uzito utumishi wa painia, kwa kuwa hili hutusaidia kuweka kazi ya kuhubiri ikiwa mbele zaidi katika maisha yetu ya kila siku. Neno la Mungu hutuhakikishia kwamba kwa kuwa watendaji wenye kuendelea wa mapenzi ya Mungu, tutakuwa wenye furaha.—Yak. 1:25.