Utafuteni Ufalme wa Mungu Kwanza —Kwa Kumtolea Dhabihu za Sifa Sikuzote
1 Wale wanaotafuta Ufalme kwanza hujali sikuzote kusema juu ya Yehova na kuongea juu ya Ufalme wake. (Zab. 145:11-13) Kila siku kuna fursa za kubariki jina lake na kusema juu ya habari njema. (Zab. 96:2) Kumsifu Yehova kulikuwa furaha ya mtunga-zaburi aliyetangaza hivi: “Tumejisifia Mungu mchana kutwa.” (Zab. 44:8) Ikiwa twahisi vivyo hivyo, tutakuwa na nia ya kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya Ufalme.
2 Yehova hajaweka matakwa hususa ya kiwango cha wakati tunachopaswa kutumia katika huduma, bali yeye hututia moyo tuwe tukimsifu “sikuzote.” (Ebr. 13:15, NW) Hali zetu zikiruhusu, twapaswa kuweka uwe mradi wetu kutumia wakati fulani tukimsifu Yehova kila juma. Wale ambao tayari wanafanya hivyo huenda wakaweza kupanga mambo yao ili watumikie wakiwa mapainia-wasaidizi pindi kwa pindi au kwa kuendelea. Watu fulani ambao wamekuwa wakifurahia utumishi wa upainia msaidizi wanaweza kujiandikisha wawe mapainia wa kawaida.
3 Hata hali zetu ziwe zipi, je, inawezekana tuongeze dhabihu yetu ya sifa? Bidii yachochewa na uthamini. Funzo la kibinafsi la Neno la Mungu husitawisha uthamini. Mikutano ya kutaniko hutusukuma tuonyeshe uthamini huo kwa njia zitumikazo. Ushirika wa karibu pamoja na wasifaji wengine wenye bidii waweza ‘kutuhimiza katika kazi nzuri.’ (Ebr. 10:24) Kwa kutumia kikamili kwa manufaa maandalizi yanayotolewa na kutaniko, huenda tukaweza kuongeza dhabihu yetu ya sifa.
4 Nabii wa kike Ana aliweka kielelezo chema katika utumishi wa Yehova. Ajapokuwa mwenye umri wa miaka 84, yeye “alikuwa hakosi kamwe hekaluni, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana.” (Lk. 2:37, NW) Kujihusisha kwake kwa nafsi yote katika utendaji wa kutaniko kulimletea utoshelezo mkubwa wa kibinafsi. Simulizi la Biblia kuhusu uaminifu wake ni kitia-moyo kwetu leo.
5 Paulo alipendekeza kwamba ‘wale walio na nguvu wapaswa kuuchukua udhaifu wao wasio na nguvu.’ (Rum. 15:1) Yamkini kuna watu fulani katika kutaniko lenu ambao watanufaika na usaidizi na kitia-moyo chako chenye fadhili. Mwaliko wa kuandamana nawe kwenye huduma ya shambani huenda tu uwe ndio unaohitajiwa. Mhubiri huenda akahitaji usafiri au mtu wa kuhubiri naye. Kivunja-moyo huenda kikawa tatizo la mwingine, na huenda ikawa wewe ndiwe unayeweza kutoa tegemezo lenye kujenga linalohitajika ili kuhuisha bidii ya mtu kwa utumishi wa Ufalme. (1 The. 5:14) Utayari wako wa ‘kushiriki pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao’ huonyesha tamaa yako ya kuhisiwa moyoni ya kuongeza sifa kwa jina la Yehova.—Rum. 12:13.
6 Haiwezekani kuhesabu mambo yote ambayo tayari Yehova ametufanyia na bado atakayotufanyia. Hakuna vile tunavyoweza kumlipa kwa baraka hizi. Kuna sababu zenye nguvu zaidi zilizoje kwa ‘kila kitu kipumuacho kimsifu Yehova’!—Zab. 150:6, NW.