Msifu Yehova Sikuzote
1 Kuna utendaji mchache ulio muhimu sana ambao sikuzote hustahili uangalifu wetu. Miongoni mwao twatia ndani kula, kupumua, na kulala. Mambo haya ni ya lazima ikiwa tutajitegemeza kimwili. Mtume Paulo aliweka kuhubiri habari njema katika mpangilio sawa na huo aliposihi hivi: “Sikuzote na tumtolee Mungu dhabihu ya sifa.” (Ebr. 13:15, NW) Kwa hiyo, kumsifu Yehova pia kwastahili uangalifu wetu wa daima. Ni jambo ambalo twapaswa kujaribu kufanya kila siku, sikuzote kumsifu Baba yetu wa kimbingu.
2 Wakati wengine walijaribu kugeuza uangalifu wake mahali kwingine, Yesu aliitikia hivi: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 4:43) Wakati wa huduma yake ya miaka mitatu na nusu, kila kitu alichofanya kila siku kilihusiana moja kwa moja katika njia fulani na kumtukuza Mungu. Twajua kwamba Paulo alihisi hivyo, kulingana na wazo aliloeleza kwenye 1 Wakorintho 9:16 (HNWW): “Ole wangu kama sitaihubiri Habari Njema!” Wakristo wengine waaminifu walitiwa moyo kuwa tayari sikuzote kutetea tumaini lao kwa wengine. (1 Pet. 3:15) Leo mamia ya maelfu ya mapainia wenye bidii na mamilioni ya wahubiri wa kutaniko hujitahidi kuiga vielelezo hivyo vyema.
3 Tunapofikiria juu ya bidii ya moyo wote iliyoonyeshwa na Yesu Kristo, Kigezo chetu, tunasukumwa kufuata hatua zake kwa ukaribu. (1 Pet. 2:21, NW) Nyakati fulani twaweza kuvunjika moyo tunapolazimika kukabili matatizo ya maisha ya kila siku. Twaweza kutumiaje fursa za kumsifu Yehova kwa faida kila siku tunapokuwa na kazi ya kimwili ya wakati wote? Wala hatuwezi kuacha wajibu wa familia ambao huhitaji wakati wetu mwingi. Vijana wengi wamejawa na shughuli za lazima za kwenda shuleni kila siku. Huenda wengine wahisi kwamba haiwezekani kumsifu Yehova hadharani kila siku. Nyakati fulani, wengine wanaweza kumaliza mwezi mzima bila kushiriki habari njema katika njia fulani.
4 Yeremia alikuwa mtu ambaye hangeweza kujizuia kutoa habari njema. Alipokosa kwa muda mfupi kusema katika jina la Yehova, alihisi moto usiovumilika ukiwaka ndani yake. (Yer. 20:9) Akikabili kile kilichoonekana kuwa matatizo yenye kulemea, Yeremia sikuzote alipata njia fulani ya kuzungumza ujumbe wa Yehova kwa wengine. Je, twaweza kuiga kielelezo chake cha moyo mkuu na kuendelea bila kukoma katika kutafuta fursa za kumsifu Muumba wetu kila siku?
5 Kuzungumza kwetu kuhusu Yehova hakupasi kuwa katika pindi rasmi tu, nyakati zilizopangwa kimbele kwa ajili ya kutoa ushahidi pamoja na wahubiri wengine katika eneo la kutaniko. Tunachohitaji tu ni sikio linalosikiza. Tunakutana na watu kwa kuendelea kila siku—wanakuja nyumbani kwetu, tunafanya kazi pamoja nao, tunapiga foleni pamoja nao kwenye maduka makubwa, au twasafiri nao katika basi. Kinachohitajika tu ni salamu ya kirafiki na swali lenye kuamsha fikira au elezo ambalo litaanzisha mazungumzo. Wengi wamepata hiyo ikiwa njia yenye matokeo zaidi ya kutoa ushahidi. Tunapokuwa na fursa nyingi za kuzungumza na wengine kuhusu habari njema, lingekuwa jambo lisilowazika kwa upande wetu kumaliza mwezi mzima bila kutoa ushahidi wa Ufalme.
6 Pendeleo la kumsifu Yehova halitakoma kamwe. Kama mtunga-zaburi alivyoonyesha, kila kitu kinachopumua chapasa kuwa kinamsifu Yehova, na kwa hakika twataka kutiwa ndani. (Zab. 150:6) Ikiwa moyo wetu watusukuma kufanya hivyo sikuzote, tutatumia fursa za kuzungumza kuhusu Yehova na Neno lake kwa faida kila siku.