Sasa Ndio Wakati Wa Kumtafuta Yehova
“Toka mbinguni BWANA [Yehova, NW] aliwachungulia wanadamu, aone kama yuko mtu mwenye akili, amtafutaye Mungu [Yehova, NW].”—ZABURI 14:2.
1, 2. (a) Wengi huwa na maoni gani juu ya Mungu wa kweli, Yehova? (b) Twajuaje kwamba Yehova ana habari juu ya ubaridi wa ainabinadamu?
LEO, Mungu wa kweli, Yehova, hukataliwa na wasioamini kuna Mungu, wanaoamini kwamba ya Mungu hayajulikani, waabudu wa miungu bandia, na mamilioni ambao hudai kuamini katika Mungu lakini humkana kwa kazi zao. (Tito 1:16) Wengi huamini kama mwanafalsafa Mjerumani wa karne ya 19 Nietzsche kwamba “Mungu ni mfu.” Je! ni kwamba Yehova hana habari juu ya ubaridi huu wa kupindukia? Sivyo, kwa maana alimpulizia Daudi roho yake kuandika hivi: “Mpumbavu amesema moyoni, Hakuna Mungu [Yehova, NW]; wameharibu matendo yao na kuyafanya chukizo, hakuna atendaye mema.”—Zaburi 14:1.
2 Daudi aliendelea hivi: “Toka mbinguni BWANA [Yehova, NW] aliwachungulia wanadamu, aone kama yuko mtu mwenye akili, amtafutaye Mungu [Yehova, NW].” Ndiyo, Bwana Mwenye Enzi Kuu ana habari juu ya wale ambao hutafuta kumjua na kumtumikia. Hivyo, ni jambo muhimu tumtafute kwa bidii ya moyoni sasa. Hiyo itamaanisha tofauti kati ya uhai wa milele na utokomeo wa milele.—Zaburi 14:2; Mathayo 25:41, 46; Waebrania 11:6.
3. Kuna uwezekano gani kwa wakati ujao?
3 Kwa hiyo, twaweza kuona ni kwa nini ni jambo la maana sana tusaidie wengine wamtafute Yehova sasa. Kungali kuna mamilioni ya watu ambao hawajapata kamwe kukutana na mmoja wa Mashahidi wa Yehova wala kusikia ‘habari njema za ufalme.’ Na kadiri ambavyo ukubwa wa idadi ya “umati mkubwa” utaongezeka kabla ya “dhiki kubwa,” sisi hatujui. Lakini hakika kuna uwezekano wa wengi zaidi kumtafuta na kumpata Yehova Mungu katika wakati ujao ulio karibu kabla haijawa kuchelewa mno. Sasa swali ni, Sisi twaweza kufanya nini tusaidie maelfu kwa maelfu wampate Mungu?—Mathayo 24:14; Ufunuo 7:9, 14.
4, 5. Katika kutafuta-tafuta mungu, wengi hupendelea nini zaidi?
4 Watu wengi ulimwenguni leo wanatafuta-tafuta, lakini kutafuta-tafuta nini? Ni wachache sana wanaomtafuta kikweli Mungu wa kweli mmoja, Yehova. Wengi hupendelea mungu mwenye kupatana na tamaa na maoni yao wenyewe ya kuegemea upande. Kama vile George Gallup, Jr., mchunguza maoni ya watu alivyosema: “Kwa kweli huoni tofauti sana kati ya wanakanisa na wasio wanakanisa katika mambo ya kupunja, kuepa kodi, na kuiba-iba, sana-sana kwa sababu kuna wingi wa dini yenye kufurahisha jamii ya watu.” Yeye aongezea kwamba “wengi wanajifanyizia tu dini inayowapa starehe na kuwasisimua . . . Mtu fulani aliiita dini ya kibandiko tu.”
5 Wengine watasema, “Dini yangu ni nzuri kiasi cha kunifaa mimi.” Bila shaka, kwa kweli swali lapasa kuwa, “Je! dini yangu ni nzuri kiasi cha kumfaa Mungu?” Ni kweli, walio wengi katika Jumuiya ya Wakristo na Uhindu huridhika kuheshimu mno mifano na sanamu zao. Walio wengi wa wale waitwao eti Wakristo hupata kwamba mungu fulani wa Kiutatu asiye na jina awatosha wao. Na Waislamu zaidi ya milioni 900 huamini katika Allah. Kwa upande mwingine, mamilioni ya wasioamini katika Mungu husema hakuna Mungu.
Wale Ambao Wahitaji Msaada
6. Wasomaji wengi wa Mnara wa Mlinzi wamegundua nini?
6 Lakini namna gani wale kati yetu ambao husoma kwa ukawaida gazeti hili? Sisi tumemtafuta-tafuta Mungu wa kweli tukampata. Tumeyathibitisha kuwa kweli maneno ya Yakobo 4:8: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” Kwa ushirika wenye utendaji pamoja na kundi la Kikristo, sisi tumemkaribia Mungu zaidi, na tumejionea wenyewe jinsi Yehova hutukaribia sisi zaidi.—Yohana 6:44, 65.
7. Twajuaje kwamba kuna watu wengi ambao wangali wapendezwa na kuwa watendaji katika ukweli?
7 Hata hivyo, twajua kwamba kungali kuna watu wengi wafurahio kushirikiana pindi kwa pindi pamoja na watu wa Yehova lakini bado hawajachukua kitendo chanya kumkaribia Yehova kwa wakfu na ubatizo. Twajuaje hilo? Katika 1990 karibu watu milioni kumi walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Lakini ni wangapi wanaohubiri habari njema za Ufalme kwa utendaji? Ni kidogo tu zaidi ya milioni nne. Hiyo yamaanisha sisi tuna watu karibu milioni sita wenye urafiki kuelekea ukweli na ambao nyakati fulani huona shangwe ya kushirikiana na sisi lakini ambao bado hawajaanza kuipendekeza lugha iliyo safi ya ukweli kwa kuhubiri habari njema za Ufalme. Bila shaka lolote, katika pindi za mara kwa mara wengi hufanya ujasiri kuongea ili kutetea Yehova na utawala wa Ufalme wake. Hata hivyo, hawajajitambulisha waziwazi kuwa Mashahidi wa Yehova. Hawa pia twataka kuwasaidia.—Sefania 3:9; Marko 13:10.
8, 9. (a) Yehova atutia moyo tufanye nini? (b) Kwa nini si jambo la hekima kupuuza shauri la Yehova?
8 Twataka kuwatia moyo hawa wawe Mashahidi wa Yehova walio na furaha na watendaji katika awamu ya mwisho ya ile kazi kubwa ambayo sasa yatimizwa ulimwenguni pote. Tafadhali angalia mwaliko wa Yehova wenye upendo kwenye Mithali 1:23: “Geukeni kwa ajili ya maonyo yangu; tazama, nitawamwagia roho yangu, na kuwajulisheni maneno yangu.” (Linganisha Yohana 4:14.) Inatia moyo kama nini kujua kwamba Yehova ataitikia hatua zetu chanya za kujitambulisha pamoja na jina na ibada yake! Hakika, sisi hatutaki kutiwa miongoni mwa wale ambao huelezwa kwenye Mithali 1:24, 25: “Nimeita, nanyi mkakataa; nimeunyosha mkono wangu, asiangalie mtu; bali mmebatilisha shauri langu, wala hamkutaka maonyo yangu.”
9 Wale ambao huliachilia mbali shauri la Yehova kwamba wamtafute-tafute maadamu aweza kupatikana na ambao huahirisha uamuzi wao mpaka wakati ambapo kwa kweli wataona dhiki kubwa ikianza watapata kwamba wamengoja muda mrefu mno. Mwendo wa jinsi hiyo ungeonyesha ukosefu wa imani na hekima na ungekuwa ni kudharau fadhili zisizostahiliwa za Yehova.—2 Wakorintho 6:1, 2.
10. Kwa nini kutojali na ubaridi ni hatari?
10 Kutoa kielezi cha uhitaji wa hatua ya haraka hii, je! wewe ungefuata ushauri mwema wa daktari wakati ambapo tu ugonjwa wako wa kichomi umeongezeka mara mbili? Au, badala yake, ungefanya hivyo uonapo dalili za kwanza za ugonjwa? Basi mbona ungoje muda mrefu zaidi ndipo ujitenge na ulimwengu mgonjwa wa Shetani na kujipanga upande wa Yehova na Mashahidi wake? Matokeo ya kutojali, ubaridi, na kuachilia mambo yaonyeshwa wazi kwenye Mithali 1:26-29: “Mimi nami nitacheka siku ya msiba wenu, nitadhihaki hofu yenu ifikapo . . . Ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; watanitafuta kwa bidii, wasinione. Kwa kuwa walichukia maarifa, wala hawakuchagua kumcha BWANA [Yehova, NW].” Acheni tusipatikane ‘tukimtafuta Yehova’ ikiwa kuchelewa mno!
11. Ni msaada gani upatikanao kwa wale wanaotafuta-tafuta kumtumikia Mungu?
11 Watu fulani wasomao gazeti hili huenda bado wako katika mwendo wa kumtafuta-tafuta Mungu wa kweli. Sisi twafurahi kwamba wewe unadumu katika kutafuta-tafuta kwako. Twasali kwamba maarifa yako ya Biblia yakusukume kuchukua kitendo chanya zaidi usimame imara upande wa ukweli. Uhakikishiwe kwamba kila kundi la Mashahidi wa Yehova lasimama tayari kukusaidia katika kutafuta-tafuta kwako.—Wafilipi 2:1-4.
Wakati wa Bidii na Kitendo
12, 13. Kwa nini twahitaji kuchukua kitendo kuhusu ibada ya kweli?
12 Kwa nini yahitajiwa sana sisi sote tuchukue kitendo cha kujitambulisha pamoja na Yehova Mungu na ibada yake ya kweli? Kwa sababu matukio ya ulimwengu yanaelekea kwenye upeo. Kurasa za historia zinafunguka upesi kuliko vile binadamu awezavyo kuzisoma. Sasa sio wakati wa kukaa kando wala wa kuwa vuguvugu. Yesu alisema wazi sana: “Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya.” Alisema pia: “Mtu akinionea aibu mimi na maneno yangu, wakati Mwana wa Mtu atakapokuja katika utukufu wake na wa Baba na wa malaika watakatifu, atamwonea aibu mtu huyo.”—Mathayo 12:30, UV; Luka 9:26, HNWW.
13 Sasa ndio wakati wa bidii na kitendo! Sisi twajua ni wapi yanakoelekea matukio ya ulimwengu, na Har–Magedoni yajikusanya-kusanya kule mbele kwenye upeo wa macho. Kwa hiyo, mwito ni kumtafuta Yehova sasa kabla ya ‘siku ya hasira yake,’ maadamu apatikana bado. Kwenye dhiki kubwa, itakuwa kuchelewa mno.—Sefania 2:2, 3; Warumi 13:11, 12; Ufunuo 16:14, 16.
14. Tuna sababu gani za kumtafuta-tafuta Mungu?
14 Kwa kweli, ainabinadamu wote wapaswa kutafuta upendo wa Mungu sasa. Mtume Paulo alieleza hilo kwa kufaa kwenye Matendo 17:26-28: “[Mungu] alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu. Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu.” Maneno ya mwisho hayo, “kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu,” yatupa sisi sababu ya kutosha kumtafuta-tafuta Mungu. Kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, sisi tumo katika kile kizio chembamba chenye uhai cha dunia hii iliyo ndogo sana. Je! hatupaswi kumshukuru Bwana Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote mzima? Na je! hatupaswi kuonyesha shukrani zetu kwake kwa njia ya matendo?—Matendo 4:24.
15. (a) Mwanahistoria Arnold Toynbee alihisi ni nini kusudi la dini ya hali ya juu zaidi? (b) Ni lazima sisi tufanye nini tuweze kutukuza Mungu?
15 Mwanahistoria Arnold Toynbee aliandika hivi wakati mmoja: “Kusudi la kweli la dini ya hali ya juu zaidi ni kuangaza mashauri na kweli za kiroho zilizo kiini chayo ili ziingie ndani ya nafsi nyingi kadiri ziwezavyo kufikiwa, ili kwamba kila moja ya nafsi hizo iwezeshwe kwa njia hiyo kutimiza lengo la kweli la Binadamu. Lengo la kweli la binadamu ni kumtukuza Mungu na kumwonea Yeye shangwe milele.” (An Historian’s Approach to Religion, kurasa 268-9) Ili kumtukuza Mungu, ni lazima kwanza tumtafute-tafute na kupata maarifa sahihi juu yake na makusudi yake. Hivyo, mwito wa Isaya wafaa sana: “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu; mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA [Yehova, NW], naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:6, 7.
Ni Msaada Gani Wenye Kutumika Tuwezao Kutoa?
16. (a) Ni mwito gani wa ushindani wenye kukabili kundi la Kikristo? (b) Ni kwa njia gani yenye kutumika twaweza kusaidia wengine kumtumikia Yehova?
16 Yale mamilioni haya ya watu wenye kupendezwa ambao hawajawa bado wahubiri watendaji yatutokezea sisi sote mwito wa ushindani. Tunafanya nini kwa njia yenye kutumika tukiwa wazee, watumishi wa huduma, mapainia, na wahubiri ili kusaidia wale wenye urafiki kuelekea ukweli ili wawe washiriki watendaji katika ibada ya kweli pamoja nasi? Njia moja ya kutoa msaada wenye kutumika mahali ambapo wahitajiwa ni kwenda kwenye nyumba zao na kuwapeleka mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme ili wao pia waweze kuona shangwe ya manufaa za roho ya Yehova kwa ukawaida. Shauri la Paulo kwa Waebrania, katika sura ya 10, mistari 24 na 25, ni lenye uharaka sana leo kama lilivyokuwa wakati huo: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.” Sisi twawatia moyo wote watakao kupata nia njema ya Yehova washirikiane pamoja na Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme la kwao.
17. Ikiwa tutasaidia wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo katika kumtafuta-tafuta Yehova, ni maswali gani yanayohitaji kujibiwa?
17 Ikiwa sisi hujifunza Biblia pamoja na mtu fulani ahudhuriaye mikutano kwa ukawaida, je! twaweza kumsaidia astahili kuwa mhubiri wa habari njema? (Ona Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu, kurasa 97-9.) Na mara yeye akiisha kuwa mhubiri asiyebatizwa, je! sisi twamtolea mwaliko wa kwenda pamoja nasi kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri peupe na kwenye mengine ya mafunzo yetu na ziara za kurudia? (Ona toleo la Desemba 1, 1989 la Mnara wa Mlinzi, ukurasa wa 31.) Ndiyo kusema, wapya hao wakiisha kustahili, je! sisi huwatia moyo kwa kuwaacha wajionee wenyewe kiasi fulani cha matokeo mazuri ya utendaji wetu wa kuhubiri?—Mathayo 28:19, 20.
Yehova Astahili Kutafutwa-tafutwa
18. Yehova ameonyeshaje rehema yake kuelekea ainabinadamu?
18 Kwa sababu ya dhabihu ya ukombozi ya Kristo Yesu, Yehova hatuhesabii dhambi zetu na kutojali kwetu kwa zamani ikiwa twatubu na kujizoeza imani. Angalia maneno ya Daudi: “Hakututenda sawasawa na hatia zetu, wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu. Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, kadiri ile ile rehema zake ni kuu kwa wamchao. Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi. Kama vile baba awahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA [Yehova, NW] anavyowahurumia wamchao. Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.”—Zaburi 103:10-14; Waebrania 10:10, 12-14.
19. Kuna kitia-moyo gani kwa wale ambao wamepeperuka mbali kutoka kwenye ukweli?
19 Yehova ndiye Mungu mfadhili na mwenye rehema kweli kweli. Sisi tukimjia kwa unyenyekevu na toba, yeye hutusamehe na kusahau. Haweki kinyongo cha milele chenye tokeo la mateso ya milele katika moto wa helo. Sivyo, ni kama vile Yehova alivyosema: “Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako.” Hicho chapasa kuwa kitia-moyo kilichoje kwa wowote ambao huenda wakawa walipeperuka kutoka kwenye ukweli wakaachilia uhusiano wao pamoja na Yehova! Wao pia watiwa moyo kumtafuta-tafuta Yehova sasa na kurudi ndani ya ushirika wenye utendaji pamoja na watu wa jina lake.—Isaya 43:25.
20, 21. (a) Ni kielelezo gani cha kutia moyo tulicho nacho katika Yuda ya kale? (b) Wakaaji wa Yuda walipaswa kufanya nini ili wapate baraka ya Yehova?
20 Katika habari hii tuna kielelezo cha kutia moyo katika Mfalme Asa katika Yuda ya kale. Yeye aling’oa ibada bandia kutoka ufalme wake, lakini masalio ya ibada ya kipagani bado yakabaki. Usimulizi kwenye 2 Nyakati 15, mistari 2 hadi 4, watuambia yale ambayo nabii Azaria alimwambia Asa kuwa kikumbusha: “BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; nanyi mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi. Basi tangu siku nyingi Israeli wamekuwa hawana Mungu wa kweli . . . lakini walipomgeukia BWANA [Yehova, NW], Mungu wa Israeli, katika msiba wao, na kumtafuta, akaonekana kwao [ndipo alipojiacha apatikane nao, NW].”
21 Yehova hakucheza na Mfalme Asa mchezo wa jifiche-nikutafute bali ‘alijiacha apatikane.’ Mfalme aliitikiaje ujumbe huu? Katika sura ile ile, mistari 8 na 12 yajibu hivi: “Naye Asa alipoyasikia maneno hayo, . . . akatiwa nguvu, akayaondolea mbali machukizo yote katika nchi . . . akaifanyiza tena madhabahu ya BWANA [Yehova, NW], iliyokuwako mbele ya ukumbi wa BWANA [Yehova, NW]. [Yuda] wakafanya agano, ya kuwa watamtafuta BWANA [Yehova, NW], Mungu wa baba zao, kwa mioyo yao yote, na kwa roho [nafsi] zao zote.” Ndiyo, walimtafuta Yehova kwa bidii ‘kwa mioyo yao yote, na kwa nafsi zao zote.’ Tokeo lilikuwa nini kwa taifa? Mstari wa 15 watuambia: “Na Yuda wote wakakifurahia kile kiapo; kwani wameapa kwa moyo wao wote, na kumtafuta kwa mapenzi yao pia; naye ameonekana kwao [ndipo alipojiacha apatikane nao, NW]; naye BWANA [Yehova, NW] akawastarehesha pande zote.”
22. Ni nini chatutia moyo tuwe watendaji sasa katika utumishi wa Yehova?
22 Sasa, je! hicho si kitia-moyo kwa sisi sote tuchukue kitendo chanya kuhusu ibada safi ya Yehova? Twajua kwamba kuna uwezekano kwa mamilioni zaidi wamfurahishe Yehova. Bila shaka wengi wa hawa wanafanya mabadiliko katika maisha zao ili kutimiza matakwa ya Kimaandiko kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Wengine wanakua katika muono-ndani na imani, wanamtafuta Yehova, na karibuni watasukumwa na moyo kushiriki lugha iliyo safi pamoja na wengine kwa kuwapelekea uelewevu wa kina cha ndani juu ya ukweli kuhusu Yehova na Ufalme wake. Na kwa nini ni muhimu sana kwamba sisi sote tumtafute-tafute Yehova sasa wakati apatikanapo? Kwa sababu ulimwengu mpya wake ulioahidiwa u karibu!—Isaya 65:17-25; Luka 21:29-33; Warumi 10:13-15.
Je! Wakumbuka?
◻ Ni nani waonyeshao ubaridi kuelekea Mungu wa kweli, Yehova?
◻ Ni kwa kadiri gani dini mara nyingi huathiri mwenendo?
◻ Kuna uwezekano gani wa ongezeko katika Mashahidi watendaji?
◻ Kwa nini sasa ndio wakati wa bidii na kitendo?
◻ Kwa nini Yehova astahili kutafutwa-tafutwa?
[Picha katika ukurasa wa 10]
Rafiki wengi wa Mashahidi wa Yehova wahudhuriao Ukumbusho ni watu wawezao kuwa watumishi wa Mungu
Hudhurio la Ukumbusho 1990: 9,950,058
Kilele cha wahubiri 1990: 4,017,213
[Picha katika ukurasa wa 12]
Katika siku ya Mfalme Asa, taifa lilimgeukia Yehova