Mwige Yehova kwa Kujali Wengine Kikweli
1 Yehova ni kielelezo kikubwa kupita vyote cha kuonyesha kujali wengine. Akiwa Mwenye Enzi Kuu, yeye ajua sana mahitaji ya viumbe vyake vya kibinadamu. (1 Pet. 5:7) Yesu alitia moyo wafuasi wake kuonyesha tabia za Baba yake, ambaye hufanya jua liangaze na mvua inyeshe kwa watu waadilifu na wasio waadilifu. (Mt. 5:45) Wewe waweza kumwiga Yehova kwa kuonyesha wengine hangaiko la kweli—ukiwa tayari kushiriki ujumbe wa Ufalme na kila mtu unayemkuta. Kwa kuzifahamu kikamili broshua zitakazotumiwa kwenye huduma wakati wa Julai, utakuwa katika hali nzuri ya kutolea wengine usaidizi wa kiroho. Madokezo yafuatayo yatoa mawazo fulani ya jinsi unavyoweza kutayarisha kwa ajili ya ziara ya kwanza kisha kufuatia kupendezwa kwa ziara za kurudia za wakati ufaao.
2 Unapotoa broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?” waweza kusema:
◼ “Je, umepata kujiuliza ni kwa nini Mungu ameruhusu binadamu wateseke ikiwa anawajali kikweli? [Ruhusu itikio.] Broshua hii haiandai tu jibu lenye kuridhisha kwa swali hilo bali pia huonyesha kwamba Mungu ameahidi kuondoa uharibifu wote ambao mwanadamu amejiletea mwenyewe na makao yake, dunia.” Soma fungu la 23 kwenye ukurasa 27. Onyesha picha iliyo chini, na usome Zaburi 145:16 kutoka fungu la 22. Toa broshua hiyo. Ikikubaliwa, uliza swali linaloweza kujibiwa kwenye ziara ifuatayo, kama vile: “Je, ungependa kujua jinsi Mungu atakavyotimiza kusudi lake kwa kuletea wanadamu baraka na kubadili dunia kuwa paradiso?”
3 Unapowarudia wale ulioangushia broshua “Je! Kweli Mungu Anatujali?” unaweza kuanzisha mazungumzo mengine kwa njia hii:
◼ “Nilipokutembelea wakati uliopita, tuliona kwamba kwa kweli Mungu anatujali na kwamba ni kusudi lake kuondoa uharibifu wote ambao mwanadamu amejiletea mwenyewe na makao yake ya kidunia.” Fungua broshua kwenye picha iliyo kwenye kurasa 2-3 na useme: “Tulimaliza mazungumzo yetu kwa swali, Mungu atatimizaje kusudi lake la kuletea mwanadamu baraka na kubadili dunia iwe paradiso? Unafikirije?” Ruhusu itikio. Fungua ukurasa 17, na usome fungu la 2 na Danieli 2:44. Baada ya hapo, soma fungu la 12 kwenye ukurasa 18. Muulize mwenye nyumba kama angependa kuchunguza nawe sehemu ya 9 ya broshua hiyo. Akipenda, jifunze naye sehemu hiyo.
4 Huu ni mfikio unaoweza kutumiwa katika kutoa broshua “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa.” Onyesha jalada layo na useme:
◼ “Leo tunagawa broshua hii ambayo imeleta faraja na tumaini kwa mamilioni ya watu ambao wamepoteza wapendwa wao katika kifo. Je, umepata kujiuliza kuna tumaini gani kwa wafu? [Ruhusu itikio.] Biblia huonyesha waziwazi ahadi ya Mungu ya ufufuo.” Soma Yohana 5:28, 29. Fungua broshua na utoe maelezo kuhusu mambo yaliyo kwenye fungu la mwisho katika ukurasa 28 na fungu la kwanza kwenye ukurasa 31. Onyesha picha zinazoandamana nazo. Toa broshua. Unaweza kutayarisha njia ya ziara ya kurudia kwa kuuliza, “Twaweza kuwaje na uhakika kwamba hatimaye kifo kitaondolewa kabisa?”
5 Mahali ulipoangusha broshua “Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa,” huenda ukataka kutumia utoaji huu kwenye ziara ya kurudia:
◼ “Tulipoongea mbeleni, tulizungumzia tumaini zuri ajabu la ufufuo. Broshua niliyokuachia yaeleza kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatimaye kifo kitaondolewa kabisa. Je, hukuona ahadi za Mungu kuwa zenye kufariji sana na zenye kutoa uhakikisho?” Ruhusu itikio. Kisha fungua ukurasa 31 katika broshua, na usome fungu la pili na la tatu, pamoja na Ufunuo 21:1-4. Kazia tarajio tulilo nalo la kufurahia uhai bila kufa kamwe. Ikitegemea kupendezwa kulikoonyeshwa na hali ya wakati huu, unaweza kutoa funzo la Biblia katika kitabu Ujuzi au uulize swali jingine ili kufungua njia ya ziara itakayofuata.
6 Unaweza kusema yafuatayo unapotoa broshua “Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai—Wewe Waweza Kulipataje?”:
◼ “Watu wengi wameshangaa kusudi la uhai ni nini. Wamejiuliza wenyewe: ‘Kwa nini nipo hapa? Naenda wapi? Wakati ujao una nini kwangu?’ Unafikiri twaweza kupata majibu wapi? [Ruhusu itikio.] Angalia vile Biblia husema. [Soma Zaburi 36:9.] Je, si jambo la kiakili kukata kauli kwamba ni Muumba wa mwanadamu awezaye kabisa kueleza ni kwa nini tupo hapa? [Ruhusu itikio.] Broshua hii yaonyesha kusudi tukufu ambalo Mungu analo kwetu sisi.” Fungua kurasa 20-21, soma maelezo ya picha, na utoe maelezo kuhusu picha; kisha toa broshua. Ikikubaliwa, uliza: “Twaweza kuwaje na uhakika kwamba ni kusudi la Mungu kwa wanadamu kuishi milele katika Paradiso duniani?” Panga wakati wa kurudi.
7 Ikiwa broshua “Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai—Wewe Waweza Kulipataje?” iliangushwa, unaweza kusema jambo kama hili urudipo:
◼ “Katika ziara yangu iliyopita, kwa kweli nilifurahia kuzungumza pamoja nawe maoni ya Biblia kwamba maisha ya wanadamu kwa kweli yana kusudi.” Onyesha picha iliyo kwenye ukurasa 31 na uulize, “Twaweza kuwaje na uhakika kwamba bado ni kusudi la Mungu kwamba wanadamu waishi milele katika Paradiso duniani?” Soma fungu la 3 kwenye ukurasa 20. Zungumza mambo yaliyo chini ya kichwa kidogo, “Bado ni Kusudi la Mungu,” kwenye ukurasa 21. Angalia jalada upande wa mwisho wa broshua, na usome kuhusu toleo la funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Onyesha kitabu Ujuzi, na uonyeshe jinsi ya kukitumia kikiwa msaada wa funzo la Biblia.
8 Huduma yetu yapaswa kuonyesha upendezi wenye unyoofu tulio nao katika kusaidia watu wenye mioyo ya haki ‘waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4, NW) Kwa hiyo, weka wakati katika ratiba yako ya utumishi kurudia kila mtu ambaye ulimwangushia broshua. Kuonyesha hangaiko kwao huenda kukatokeza kusaidia watambuliwe kwa ajili ya wokovu wale wanaopiga kite na kuugua kuhusu mambo yenye kuchukiza yanayofanywa katika dini za uwongo. (Eze. 9:4, 6) Pia utapata shangwe na uradhi unaotokana na kujua kwamba unamwiga Yehova kwa kujali wengine kikweli.—Linganisha Wafilipi 2:20.