“Hizo Pesa Hutoka Wapi?”
WATAZAMAJI wa vidio ya Watch Tower Society iitwayo “Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name” wavutiwa. Wao huona wanaume na wanawake wenye sura za kupendeza watokao katika jamii na malezi mbalimbali, wakitabasamu na kufanya kazi pamoja kwa muungano. Hawavutiwi tu na maelfu ya wafanyakazi wenye furaha bali pia wanavutiwa na majengo makubwa yaliyo kwenye makao makuu ya Sosaiti ya Brooklyn na katika mashamba yao katika Wallkill, New York. Hiyo vidio huonyesha kwamba ndani ya hayo majengo mna tekinolojia ya kisasa—vifaa vya kasi sana vya uchapaji na ujalidi vitokezavyo mamilioni mengi ya vichapo kila mwezi, vifaa vingi mbalimbali vya kompyuta na idara nyingi za kutegemeza uchapishaji wa vichapo.
Jambo hili laonyesha matumizi makubwa sana ya mali. Hivyo wengine huuliza, “Hizo pesa hutoka wapi?”
Wenye kuzuru makao makuu ya ulimwengu ya Sosaiti huvutiwa vilevile. Wao huinua shingo zao ili waone jengo la makao la orofa 30, moja la majengo mengine mengi yatumiwayo yakiwa makao kwa wahudumu zaidi ya 3,000 wenye kujitolea. Kutembelea Kitovu cha Kielimu cha Watchtower kilicho kipya karibu kilometa 110 kaskazini mwa Brooklyn pia huvutia sana wengi wenye kuzuru. Kikiwa bado kinaendelea kujengwa, kina wafanyakazi wapatao 1,200. Kila mwaka madarasa mawili ya kuzoeza wamishonari na kutumwa ng’ambo kwenye migawo yao yatafanywa huko. Pia ni kutoka mahali hapo mwongozo unatolewa kwa zaidi ya makutaniko ya Mashahidi wa Yehova 10,000 katika Marekani. Matawi mengi pia ulimwenguni pote hivi majuzi yamepanua majengo yao au yamo katika hatua ya kufanya hivyo. Kufanya kazi yote hiyo huhitaji kiasi kikubwa sana cha pesa. Watu huuliza, “Hizo pesa hutoka wapi?”
Jibu ni kwamba hizo hutoka kwa watu wa kawaida kama yeyote kati yetu. Wao ni watu, ulimwenguni pote, watamanio kufanya yote wawezayo kuendeleza kazi muhimu ya Kikristo ya kuhubiri na kufundisha. Mioyo kama hiyo ya kutoa kwa hiari si ya kwanza kuonekana.
Kielelezo Kilichowekwa na Israeli la Kale
Zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, uhitaji wa michango ya ukarimu ulitokea. Yehova alikuwa amemwagiza Musa ajenge tabenakulo, au “hema ya kukutania,” ili itumiwe katika ibada Yake. Muundo uliotolewa kimungu ulihitaji vifaa vya thamani vya aina mbalimbali. Yehova aliamuru hivi: “Kutoka miongoni mwenu twaeni mchango kwa Yehova. Acha kila mwenye moyo wa kupenda aulete ukiwa mchango wa Yehova.” (Kutoka 35:4-9, NW) Watu waliitikiaje? Simulizi hilo hutuambia kwamba “Wakaja, kila mmoja ambaye moyo wake ulimsukuma, nao wakaleta, kila mmoja ambaye moyo wake ulimchochea, mchango wa Yehova kwa ajili ya kazi ya hema la kukutania na kwa ajili ya utumishi walo wote na kwa ajili ya mavazi matakatifu.” Polepole, hilo “toleo la hiari” likawa kubwa hivi kwamba likawa ‘kubwa sana kuliko yale yaliyohitajiwa kwa ajili ya kazi ambayo Yehova aliamuru ifanywe.’ (Kutoka 35:21-29; 36:3-5, NW) Watu walionyesha roho ya kutoa na ya ukarimu kama nini!
Chini ya miaka 500 baadaye, mbiu ilipigwa tena kwa ajili ya mchango wa ukarimu kutoka kwa Waisraeli. Tamaa ya Mfalme Daudi ya kumjengea Yehova nyumba ya kudumu katika Yerusalemu ilikuwa karibu itimizwe kupitia mwanaye Sulemani. Daudi mwenyewe alikusanya na kuchanga sehemu iliyo kubwa ya kile ambacho kingehitajiwa. Wengine walijiunga na Daudi alipopiga mbiu ya kuleta “zawadi kwa Yehova.” (NW) Tokeo likawa nini? “Hao watu wakafurahi, kwa sababu wametoa kwa hiari yao wenyewe, kwa sababu kwa ukamilifu wa moyo, kwa hiari yao wenyewe, wamemtolea BWANA; mfalme Daudi naye akafurahi kwa furaha kuu.” (1 Mambo ya Nyakati 22:14; 29:3-9) Fedha na dhahabu pekee zingekuwa na thamani ya karibu dola bilioni 50 kulingana na thamani ya sasa ya pesa!—2 Mambo ya Nyakati 5:1.
Twaona katika vielelezo hivyo kwamba hakuna aliyelazimishwa kutoa. Ilikuwa kwa “hiari” kabisa na kutolewa “kwa moyo wa ukunjufu.” Yehova angependezwa tu na mchango uliotolewa kwa moyo wote. Vilevile, fursa ilipotokea ya kuchanga pesa ili kusaidia Wakristo wenye uhitaji, mtume Paulo aliandika kwamba hazikupaswa ziwe kitu kitolewacho ‘kwa unyimivu.’ Yeye aliongeza hivi: “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.”—2 Wakorintho 9:5, 7.
Uhitaji Leo
Je, kuna uhitaji wa michango leo? Kwa kweli upo, na utaongezeka hata zaidi kadiri wakati upitavyo. Kwa nini?
Wakristo wamepewa maagizo hususa kwa ajili ya wakati huu wa mwisho. Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.”—Mathayo 28:19, 20, NW.
Ili kutimiza kazi hii kubwa ya kufundisha na kuhubiri huku tukikaribia zaidi na zaidi sehemu ya mwisho wa “umalizio wa mfumo wa mambo” huchukua wakati mwingi na mali nyingi. Kwa nini? Kwa sababu ya yote yanayohusika katika kutoa ujumbe wa Ufalme wa Mungu “mpaka sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8, NW) Watu wengi hawajui Maandiko vizuri kama walivyojua Wayahudi wa karne ya kwanza. Kwa kweli, idadi kubwa ya wakaaji wa dunia hata hawaijui Biblia na hawaioni kuwa Neno la Mungu. Ni lazima wahubiri wazoezwe na kutumwa nchi za mbali. (Warumi 10:13-15) Na fikiria idadi ya lugha zinazohusika! Wenye kuhubiriwa wanahitaji kuwa na Biblia na vichapo vyenye kutegemea Biblia ili wavisome na kujifunza katika lugha zao wenyewe. Ili kuwafikia wote kwa utaratibu na kuwasaidia polepole wafikie ukomavu wa kiroho ili waweze kusaidia wengine pia huhitaji tengenezo kubwa sana.—2 Timotheo 2:2.
Yesu alisema kwamba “habari njema ya ufalme” ni lazima kwanza ‘ihubiriwe katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.’ (Mathayo 24:14) Kwa hiyo, sasa ndiyo wakati wa kutoa yote tuwezayo ili kutimiza kazi hiyo muhimu. Mali zetu zitatumika kwa njia bora zaidi kabla mali za kimwili hazijakosa thamani yoyote ile yenye kutumika.—Ezekieli 7:19; Luka 16:9.
Hizo Pesa Huenda Wapi?
Watch Tower Society huchapisha fasihi ya Biblia kwa zaidi ya lugha 230, vilevile maandishi ya Braille kwa vipofu na vidio katika lugha ya ishara kwa ajili ya viziwi. Kazi hiyo huhitaji timu za watafsiri na wasomaji wenye kuhakikisha usahihi kwa kila lugha. Kuwazia tu kufanya kazi hiyo yote, hasa kwa gazeti la Mnara wa Mlinzi, ambalo huchapishwa kwa lugha 121 kila mwezi na sawia kwa lugha 101 kati ya lugha hizo, ni jambo la kushangaza. Na bado lafaa ili watu duniani pote waweze kupata na kusoma habari ileile. Kila mwaka kuna maongezeko katika gharama ya karatasi na vifaa vingine vitumiwavyo katika kutoa ujumbe wa Ufalme kwa njia iliyochapishwa au ya kaseti za kusikiliza au ya vidio. Gharama kama hizo zahitaji kugharimiwa kwa upaji kutoka kwa akina ndugu.
Kazi ya kuhubiri na kufundisha inaendeshwa katika maeneo yenye makutaniko zaidi ya 75,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Ili kuwaunganisha na kuwatia moyo, waangalizi wasafirio waliozoezwa hutembelea kila kutaniko karibu mara mbili kila mwaka. Makusanyiko pia huwa na sehemu muhimu katika kutoa maagizo. Majengo makubwa ni lazima yakodiwe kwa ajili ya mikusanyiko yenye kuimarisha imani. Michango yenu hutumiwa pia kwa makusudi haya.
Kwa kuwa makusanyiko kwa ujumla hufanywa mara tatu tu kila mwaka, makutaniko ya mahali-mahali hukutanika kwa ajili ya mikutano mitano ya kila juma. (Linganisha Kutoka 34:23, 24.) Kuongezeka kwa wapya wanaoitikia habari njema kumemaanisha kuongezeka kwa maelfu ya makutaniko mapya kila mwaka. Kwa msaada wa mamilioni ya dola katika mkopo utolewao na Sosaiti, mamia ya Majumba ya Ufalme mapya hujengwa kila mwaka, na mengine mengi yanajengwa upya na kupanuliwa. Ingawa hizo ni pesa zinazokopwa, kurudishwa na kukopwa tena, uhitaji huendelea kuongezeka.
Sehemu moja ambayo imekuwa na ongezeko kubwa sana ni katika mataifa ya Ulaya Mashariki yaliyokuwa chini ya ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. Ilikuwa shangwe kama nini kusikia habari nzuri kwamba kazi ilikuwa imefunguliwa katika sehemu hizo! Sasa wamishonari wanatumwa katika nchi nyingi kati ya hizo. Matawi mapya yamefunguliwa katika baadhi ya nchi, ikiongeza idadi ya wahudumu wajitoleaji ambao ni wafanyakazi wa familia ya Betheli ya ulimwenguni pote hadi zaidi ya 15,000. Bila shaka, ni lazima majengo ya tawi yanunuliwe au yajengwe ili kuwapa mahali pa kuishi. Michango yenu husaidia kujaza uhitaji huo.
Kazi hii yote haijakosa kutambuliwa na Shetani na roho waovu wake. Wao hufanya yote wawezayo ili kukomesha jitihada za watumishi waaminifu wa Yehova au kuwasababishia matatizo. (Ufunuo 12:17) Hilo lamaanisha ongezeko la mzigo wa kesi za kisheria ili kulinda haki za watu wa Mungu za kuhubiri na kuishi kulingana na sheria zake za uadilifu. Kuongezea hayo, vita vinavyoongezeka katika mfumo wa mambo wa Shetani, na vilevile misiba ya asili, humaanisha kwamba ugavi wa msaada mara nyingi huhitajiwa kwa ajili ya ndugu na dada zetu na wengine pamoja nao wenye kupatwa na msiba. Michango yenu husaidia kuandaa msaada huu muhimu.
Yehova Atakuthawabisha
Kutumia wakati na mali zetu kwa ukarimu ili kuendeleza kazi ya Bwana huleta baraka nyingi hata zaidi. Jinsi gani? Kwa sababu, Mungu, ambaye kwa kweli vitu vyote ni mali yake, atatuthawabisha. Mithali 11:25 husema: “Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa; anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.” Yehova hupendezwa kwelikweli tufanyapo sehemu yetu ili kuendeleza ibada yake. (Waebrania 13:15, 16) Yeye aliwaahidi hivi Waisraeli wa kale ambao wangeleta michango iliyohitajiwa chini ya agano la Sheria: ‘Nijaribuni kwa njia hiyo, asema BWANA wa majeshi; mjue kama sitawafungulia madirisha ya mbinguni, na kuwamwagieni baraka, hata isiwepo nafasi ya kutosha, au la.’ (Malaki 3:10) Ufanisi wa kiroho ambao watumishi wa Yehova huonea shangwe leo ni uthibitisho wa kwamba Mungu hutimiza ahadi yake.
Kazi hii tukufu ya kutangazia watu wote siku ya wokovu na kusaidia wanyoofu wa moyo kuingia katika barabara ya uzima haitaendelea milele. (Mathayo 7:14; 2 Wakorintho 6:2) Lakini wote walio wa “kondoo wengine” wa Bwana ni lazima wakusanywe. (Yohana 10:16) Ni muhimu kama nini kukubali mwito huo leo! Na kila mmoja wetu atakuwa mwenye furaha kama nini, akikumbuka akiwa katika huo ulimwengu mpya wenye uadilifu, na kusema, ‘nilishiriki kikamili katika kazi hiyo ya mkusanyo wa mwisho’!—2 Petro 3:13.
[Sandukupage 30, 31]
JINSI AMBAVYO WENGINE HUTOA UPAJI KWA AJILI YA KAZI YA KUHUBIRI UFALME
MICHANGO KWA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE: Wengi huweka kando au hupangia kiasi cha fedha ambazo wao hutia katika masanduku ya michango yaliyo na kibandiko hiki: “Michango kwa Kazi ya Sosaiti ya Ulimwenguni Pote—Mathayo 24:14.” Kila mwezi, makutaniko hupeleka kiasi hicho ama kwenye makao makuu ya ulimwengu katika Brooklyn, New York, ama kwenye ofisi ya tawi ya mahali hapo.
ZAWADI: Upaji wa hiari wa fedha waweza kupelekwa moja kwa moja kwenye Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya Sosaiti inayotumikia nchi yako. Vito au mali nyingine zenye thamani zaweza kutolewa pia. Barua fupi yenye kutaarifu kwamba hiyo ni zawadi ya moja kwa moja yapasa iambatane na michango hiyo.
MPANGO WA UPAJI WENYE MASHARTI: Fedha zaweza kupewa Watch Tower Society kuwa amana hadi kifo cha mpaji, kukiwa na uandalizi wa kwamba kukiwa na uhitaji wa kibinafsi, zitarudishwa kwa mpaji.
BIMA: Watch Tower Society yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mpango wa bima ya maisha au katika mpango wa kustaafu kazi au malipo ya uzeeni. Sosaiti yapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
AKIBA ZA BENKI: Akiba za benki, hati za amana, au akiba za fedha za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zaweza kuwekwa zikiwa amana kwa ajili ya au kuweza kulipwa wakati wa kifo kwa Watch Tower Society, kulingana na matakwa ya benki ya hapo. Sosaiti yapasa kujulishwa juu ya mipango yoyote kama hiyo.
HISA NA DHAMANA: Hisa na dhamana zaweza kupewa Watch Tower Society ama zikiwa zawadi ya moja kwa moja ama zikiwa chini ya mpango ambao mapato yaendelea kulipwa kwa mpaji.
MASHAMBA NA NYUMBA: Mashamba na nyumba ziwezazo kuuzwa zaweza kupewa Watch Tower Society ama kwa kutoa zawadi ya moja kwa moja ama kwa kuweka shamba au nyumba ya maisha kwa ajili ya mpaji, ambaye aweza kuendelea kuishi humo muda wa maisha yake. Mtu apaswa kuarifu Sosaiti kabla ya kuipa Sosaiti hati yoyote ya mashamba na nyumba.
WASIA NA AMANA: Mali au fedha zaweza kupangwa kuwa urithi wa Watch Tower Society kwa njia ya wasia wenye kutekelezwa kisheria, au Sosaiti yaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Amana inayofaidi tengenezo la kidini yaweza kuandaa faida fulani za kodi. Nakala ya wasia au mkataba wa amana yapasa kupelekwa kwa Sosaiti.
UTOAJI ULIOFANYIWA MPANGO: Sosaiti imetayarisha broshua ya lugha ya Kiingereza yenye kichwa “Utoaji Uliofanyiwa Mpango.” Wale walio katika Marekani wanaopanga kufanya zawadi ya kipekee kwa Sosaiti sasa au kuacha wasia wafapo waweza kupata habari hii kuwa yenye maana. Hiyo ni kweli hasa wakati wanapotaka kutimiza mradi fulani wa familia au mpango wa kupata mali huku wakitumia mapunguzo ya kodi ili kupunguza gharama ya hiyo zawadi au wasia. Habari hii yaweza kupatikana kwa kuandikia Sosaiti kwa kutumia anwani ionyeshwayo hapa chini.
Kwa habari zaidi kuhusu mambo kama hayo, andikia International Bible Students Association, P. O. Box 47788, Nairobi, Kenya.