Yakobo Anahimiza Ibada Safi na Yenye Matendo Ifuatwe
WEWE una maoni gani juu ya kushauriwa na mwanamume mzee? Namna gani ikiwa mashauri unayopewa yana mafaa ya kiroho na yanasemwa wazi bila kuficha jambo? Je! utayafuata?
Barua ya Yakobo, iliyoandikwa kabla ya mwaka wa 62 W.K., ina mashauri ya namna hiyo yenye kusema mambo wazi. Mwandikaji alikuwa mwanamume mzee—mwenye ujuzi wa miaka karibu 30 hivi katika kushughulika na matatizo ya waabudu wenzake. Ndiyo, Yakobo yule mzee Mkristo, aliyekuwa ndugu-mzazi-mmoja wa Yesu Kristo, angeweza kuandika kwa kutoboa mambo wazi kwa sababu ya mambo aliyokuwa amejionea mwenyewe, bila kuambiwa na mtu mwingine. (Marko 6:3) Mifano yenye kueleza mambo bila kuyaficha na maulizo yenye kupenya mioyo aliyotumia yaliipa nguvu njia yake ya kuandika kwa uthabiti mwingi, nayo ilionyesha wazi kwamba dini chafu ya kufuatwa kijuujuu tu haimpendezi Yehova.
Yakobo alitoa maagizo yenye mafaa kama alivyoongozwa na Mungu, na maagizo hayo yanafaa kwa matumizi leo sawasawa na yalivyokuwa katika karne ya kwanza. Kwa kuwaza juu ya mashauri yake yaliyoongozwa na Mungu, tunaweza kupata majibu ya maulizo fulani ya maana. Na maneno yake yanapasa kutuchochea tusonge mbele katika ibada safi na yenye matendo.
Inatupasa Tuoneje Majaribu?
Yakobo aliandikia “kabila kumi na mbili” za Israeli wa kiroho zilizotawanyika katika sehemu zote za ulimwengu uliojulikana siku hizo. Lakini mashauri aliyotoa yanatumika pia kwa “mkutano mkubwa.” (Ufunuo 7:4-9; Wagalatia 6:16) Yeye alihimiza waabudu wenzake wayaone majaribu kwa furaha kwa sababu furaha yenye kudumu itatokana nayo ikiwa tutayavumilia tukiwa na imani. Imetupasa tumwombe Mungu hekima tukiwa na uhakika ili tuishi kwa njia itakayompendeza, hasa wakati tunapoelekewa na majaribu. Wafuasi wapakwa mafuta wa Yesu ambao wanavumilia jaribu kwa uaminifu wataipokea “taji ya uzima,” yaani, hali ya kutokuweza kufa wakiwa mbinguni. Uvumilivu wenye uaminifu wa “mkutano mkubwa” utafanya wapate uzima wa milele katika dunia-Paradiso.—Yakobo 1:1-12; Luka 23:43, NW.
Wakati tunapopatwa na jaribu, haitupasi kukata shauri kwamba Mungu anajaribu kutushawishi tutende dhambi, kwa maana yeye hafanyi hivyo. Bali, tamaa mbaya ndani yetu inatumika kuwa kishawishi cha kutenda dhambi. Yehova siye chanzo cha uovu bali ni chanzo cha kila kilicho chema, kutia ndani ile zawadi bora ya uzaliwa wa kiroho.—Yakobo 1:13-18; Waefeso 1:13, 14.
Dini ya Kweli Ni Nini?
Ili tuwe wazoeaji wa dini ya kweli, ni lazima tuwe wepesi wa kuitikia neno la Mungu kwa utii. Ni lazima pia tuwe wakawivu wa kuonyesha hasira na ni lazima tujiondolee kabisa mambo yote ambayo Mungu anayahesabu kuwa machafu. Kuondoa ubaya moyoni na akilini kunaruhusu neno la kweli lisitawi humo, na ni lazima sisi tuwe watendaji wa lile neno wala si wasikiaji tu, tuyaache Maandiko yawe kiongozi chetu kweli kweli. Fikiria jambo hili: Baada ya mtu kujitazama uso katika kioo, anaenda zake na kusahau yeye ni mtu wa namna gani. Lakini, ili sisi tumwabudu Yehova kwa njia inayokubalika hatuwezi kuwa wasikiaji wasahaulifu. Bali, ni lazima tuchungulie ile “sheria kamilifu,” kukubali kila jambo linalotakwa kwa Wakristo, na ni lazima tutende kupatana nalo.—Yakobo 1:19-25.
Ikiwa Mungu atatuona sisi kuwa waabudu wa kweli, ni lazima pia tuzuie ulimi kwa hatamu, tuuzuie usiseme mambo ya uchongezi, kusengenya watu na mambo kama hayo. Zaidi ya hilo, kulingana na maoni ya Yehova, ibada iliyo “safi” (takatifu, inayong’aa kwa usafi) na “isiyo na taka” (isiyotiwa doa la ubaya) inatia ndani kuwahangaikia wenye uhitaji kwa matendo. Pia tunatakwa ‘tujilinde na dunia [ulimwengu, NW ] pasipo mawaa,’ ulimwengu wa wanadamu wasiomtumikia Mungu. Hatuwezi kumpendeza Yehova na huku tunafanya mambo ya udhalimu yanayofanywa na ulimwengu. Bila shaka, Yakobo hakutaja matakwa yote ya ibada ya kweli. Lakini alionyesha kwamba utumishi wa kweli anaopewa Yehova ni safi na ni wenye matendo. —Yakobo 1:26, 27.
Je! Kuna Ubaya Wo Wote wa Kujigawa Katika Jamii za Watu wa Vyeo Mbalimbali?
Yakobo alionyesha kwamba ibada safi inahitaji pia kutokuonyesha upendeleo katika kushughulika na matajiri na maskini pia. Watu fulani wenye kujiita Wakristo walikuwa wakitoa maamuzi maovu kwa kuwaonyesha matajiri upendeleo na hivyo wakawa wakigawa watu katika jamii zenye vyeo mbalimbali. Sisi na tusiwe kamwe na hatia ya upendeleo huo usio wa kimungu!—Yakobo 2:1-4.
Kwa uhakika, ni lazima Wakristo wakubali kwamba, wakiwa jamii kwa ujumla, matajiri wamelikufuru jina la Kristo kwa kutesa wafuasi wake. Basi, badala ya kutenda dhambi kwa kuwa na migawanyiko ya jamii za watu wenye vyeo mbalimbali na kuwapendelea matajiri, inatupasa kuifuata ile “sheria ya kifalme” kwa kuwaonyesha upendo ndugu zetu wote. Tunawezaje kutazamia kufurahia rehema ya Mungu ikiwa sisi hatuwaonyeshi maskini rehema na upendo? Kwa kweli, katika kundi kukiwa na migawanyiko ya jamii za watu wenye vyeo mbalimbali hilo lingekuwa jambo lisilopatana na ibada safi.—Yakobo 2:5-13; Mathayo 22:39; Matendo 10:34, 35.
Tunaweza Kuthibitishaje kwamba Tuna Imani?
Mtume Paulo alionyesha kwamba watu wanatangazwa na Yehova Mungu kuwa wenye haki (waadilifu, NW ) kwa sababu ya imani yao katika Yesu Kristo wala si kupitia matendo ya Torati ya Musa. (Warumi 3:19-28) Yakobo alikubaliana na jambo hilo, lakini akaonyesha wazi kwamba ni lazima imani yetu ithibitishwe kuwa iko hai kwa matendo ya kimungu ambayo imani hiyo inatuchochea kuyafanya. Imani isiyotuchochea tufanye matendo mema si halisi nayo haitatuletea wokovu. Kwa mfano: Ikiwa mwamini mwenzetu hana nguo za kumfunika vya kutosha wala hana chakula, kumwambia maneno matupu hakutamsaidia; ni lazima apewe msaada wa vitu hivyo. Hata mashetani wanaamini kuna Mungu mmoja, lakini hawafanyi rnatendo mema. Kwa hiyo imani inayosemwa kuwa ipo bila matendo mema ya kuiunga mkono haina utendaji, haina matokeo kwa habari ya kupata wokovu. Abrahamu, “baba” ya wote walio na imani ya kweli, alionyesha imani yake kwa matendo wakati alipomtoa Isaka. Rahabu pia alikuwa na imani yenye matendo, kwa maana ‘alihesabiwa kuwa ana haki kwa matendo’ ya kulinda wale wapelelezi Waisraeli. Kwa hiyo, ijapokuwa imani tupu ambayo mtu anajidai kuwa nayo imekufa kama mzoga, kwa kujitia katika matendo ya Kikristo yanayoongozwa na makusudi mema tunathibitisha kwamba sisi tuna imani halisi iliyo hai.—Yakobo 2:11-26.
Sababu Gani Tuzuie Ulimi?
Ibada safi na yenye matendo inahitaji pia mtu achukue hatua thabiti ya kuzuia ulimi. Kwanza, Wakristo wote—na hasa walimu katika kundi—ni lazima waepuke kutoa maoni yenye makosa. Yakobo alionyesha kwamba kama vile farasi wanavyoweza kuongozwa kwa hatamu, sisi tunaweza kuongoza sehemu zile nyingine zote za miili yetu yenye maelekeo ya kutenda dhambi tukiuzuia ulimi kwa hatamu. Hata meli kubwa inaweza kuongozwa kwa usukani mdogo! Lakini tukishindwa kuzuia ulimi, unaweza kuleta uharibifu wenye kuenea sana, kama vile unavyofanya moto wenye kuwaka sana. Kupitia uchongezi, ushuhuda wa uongo, kusingizia mtu na mambo kama hayo, ulimi usiozuiwa kwa hatamu ‘unautia unajisi’ mwili wote, kuichafua nafsi yote ya mwenye kunena. Zaidi ya hilo ulimi usiozuiwa unaweza kuuwasha moto mwendo mzima wa maisha na unaweza kuleta uharibifu mkubwa kama Gehena.—Yakobo 3:1-6.
Bila shaka, jitihada kubwa inahitajiwa ili kuzuia ulimi. Ingawa mwanadamu mwenye dhambi amezoeza namna zote za wanyama, hakuweza kuuzuia ulimi kwa ukamilifu. Lakini ni lazima tujitahidi kuuzuia ulimi. Kwa sababu ulimi usiozuiwa unaweza kutoa matusi, maneno ya uchongezi, na unaweza kupoteza watu kupitia fundisho la uongo, na hivyo hivyo, huo ni kitu chenye madhara kilichojawa na sumu yenye kufisha. Na ebu fikiri namna lingekuwa jambo lisilofaa kutumia ulimi vibaya—kifaa kilichoumbwa kwa kusudi hasa la kumsifu Mungu -—kuutumia ili kuwatakia maovu wanadamu ambao yeye amewaumba! Hilo lingekuwa jambo lisilo na upatani kama lilivyo jambo lisilo na upatani kupata maji matamu na machungu kutokana na chemchemi ile ile moja au kupata zeituni kutokana na mitini.-—Yakobo 3:7-12.
Ni Nani Mwenye Hekima Kweli Kweli?
Hekima ya kweli inahitajiwa na Wakristo wote na hasa na walimu wenye kufundisha watu wale wengine walio katika ibada safi. Mtu aliye na hekima kweli kweli anaonyesha woga unaofaa juu ya Mungu na ni mpole. Kwa kweli, ili mwanamume atumikie kwa njia inayokubalika akiwa mwalimu ni lazima awe mpole, si mkali-mkali, wala mwenye majivuno wala mwenye kushikilia maoni yake mwenyewe tu. Zaidi ya hilo, wivu na mashindano kwa uhakika hayampasi mwalimu Mkristo wala mfuasi mwingine yeyote wa Kristo. Bali, hekima ya wale walio na vitabia hivyo ni ya kinyama, hata ya kishetani.-—Yakobo 3:13-16.
Hekima ya kimbingu ni safi katika tabia, ni yenye kuamanika, ni yenye kujadilika (yenye kiasi) na ni “tayari kutii.” Kwa mfano, mwalimu Mkristo aliye mwenye kujadilika hatokezi maneno matupu ya kudai kwa mkazo kwamba mambo yako hivi au vile. Na kati ya mambo mengine, hekima ya kimbingu imejawa na “matunda mema,” ambayo yanatia ndani matendo yote yanayopatana na wema, uadilifu na kweli. Kama ilivyo, ili uadilifu usitawi, ni lazima amani iwepo. Walimu na wengine kundini wanaoendeleza amani wanaonyesha kwamba wao ni wenye hekima kweli kweli.—Yakobo 3:17, 18, NW.
Tunaweza Kuzuiaje Ugomvi?
Amani ya waabudu wenzi wa Yakobo ilikuwa ikichafuliwa kwa sababu wengine kati yao walikuwa na hatia ya mambo kama upendeleo, kuhukumu wengine isivyofaa na kujiachilia wawe na wivu. Mambo hayo yalileta ugomvi katika kundi. Nacho chanzo cha mapigano hayo kilikuwa nini? Kilikuwa tamaa zisizotoshelezwa za mwili! Tamaa mbaya hizo ziliwafanya wawe watamanifu wa kutaka vyeo na zilileta roho ya chuki na uuaji.—Yakobo 4:1-3.
Ili kuzuia ugomvi katika kundi ni lazima tuepuke urafiki na ulimwengu, ambao ni uzinzi wa kiroho. Kufanya hivyo kunahitaji tuepuke maoni, miradi, njia na matendo ya ulimwengu wa watu waliotengwa mbali na Mungu. Ingawa maelekeo ya kuona kijicho yanaendeleza ugomvi na kuwakaza sana wanadamu wenye dhambi, yanaweza kupingwa kupitia roho ya Mungu, ambayo kwa uhakika ni wonyesho wa fadhili zisizostahilika kutoka kwake. Msaada huo unaweza kupatikana na watumishi wanyenyekevu wa Yehova wanaosali bila kuacha wapewe naye usaidizi na kumtii. Wanaweza kumpinga Ibilisi na wafanikiwe kufanya hivyo. Bila shaka, watu wo wote wenye kujiita Wakristo ambao wamedhihirisha maoni mabaya wanapaswa kumkaribia Mungu katika sala, wajinyenyekeze mbele zake na kuacha kunenea ndugu zao au kuwahukumu isivyo haki. Ni jambo lisilofaa kabisa wanadamu wenye dhambi kuhukumu jirani zao na hali Yehova ndiye Mpaji Mkuu wa sheria na ndiye Hakimu!—Yakobo 4:4-12.
Kuepuka kujitegemea kwa majisifu kutasaidia pia kuleta amani katika kundi. Kwa kuwa maisha katika mfumo huu ni kama mvuke unaotoweka, tungekuwa wapumbavu tukikaza fikira zetu juu ya mfumo huu na kujigamba-gamba juu ya mambo tunayopanga kufanya. Badala ya hivyo, angalau katika mioyo yetu inatupasa tuseme, “Yehova akipenda.” Ingawaje, sisi hatuwezi kutimiza jambo lo lote lenye kudumu bila upendeleo na msaada wake, naye anataka aonyeshwe unyenyekevu na hali ya kumkiri yeye kuwa chanzo cha uhai na vitu vyote vizuri. Inatupasa sisi tutende kulingana na maarifa ya kujua hivyo, kwa maana kufanya vingine ni kutenda dhambi.—Yakobo 4:13-17.
Kwa Sababu Gani Tuonyeshe Subira?
Kati ya mambo mengine, Yakobo anakazia uhitaji wa kuonyesha subira halafu. Inaelekea kuwa ndani ya makundi walikuwamo matajiri wachache waliotambua kama yeye alivyotambua kwamba utajiri wa kimwili si kitu unapolinganishwa na mali za kiroho ambazo Wakristo wanazo. Lakini, wakiwa jamii kwa ujumla, matajiri waliwaonea maskini na wakawapinga wenye haki (waadilifu). Yakobo alionyesha kwamba ni lazima sisi tuvumilie mambo hayo na magumu mengine kwa subira mpaka hukumu itakapowajilia waonezi wakati wa “kuwapo kwa Bwana” Yesu Kristo. Tunahitaji kuwa kama yule mkulima anayeyangoja mavuno kwa subira. Tukiwa wenye harara na kukosa kuvumilia kwa uaminifu, tungeipoteza faraja na baraka zinazokuja wakati wa kuwapo kwa Bwana.—Yakobo 5:1-8, NW.
Ni lazima pia sisi waabudu wa kweli tuwe wenye subira kwa waamini wenzetu, tusiwaonee uchungu, kuguna au kuvuta pumzi kwa roho ya kuchukizwa sana nao. Halafu Yakobo akaonyesha kwamba manabii wa Yehova ni mfano mwema wa kuvumilia maovu na kuonyesha subira. Kama Ayubu wa kale, sisi tunaweza kufarijiwa na jambo la kwamba tutapata huruma na rehema kuu za Yehova tukivumilia kwa subira tukiwa na mioyo safi iliyokazwa kikiki juu ya Mungu.—Yakobo 5:9-11.
Sala Ina Matokeo ya Kadiri Gani?
Baada ya kuwaonya Wakristo wenzake kwa upole wasiwe wakila viapo kwa njia ovyoovyo tu na bila sababu nzito, Yakobo aliwahimiza wawe watu wenye kusali. Sala ni ya maana hasa kama mtu ana udhaifu au ugonjwa wa kiroho. Inapokuwa hivyo, ingefaa kuwaita wanaume wazee wa kundi, ambao wanaweza kuonyesha vikumbusho vya Kimaandiko vinavyofariji kama mafuta yanayotia burudisho. Wazee hao watatoa sala kwa ajili ya yule anayehitaji msaada, na “kule kuomba kwa imani” kutakuwa na matokeo. Yehova atasamehe dhambi ambazo huenda ikawa mtu mwenye kutubu alitenda kisha atamrudishia afya yake ya kiroho. Kwamba “kuomba kwake mwenye haki kwafaa sana” inathibitishwa na uhakika wa kwamba sala za Eliya zilijibiwa na Yehova.—Yakobo 5:12-18.
Namna gani Mkristo akitanga-tanga kwa kuiacha ile njia ya kweli? Watu mmoja mmoja wenye sifa za kuwastahilisha kiroho wanapaswa wajaribu kumsaidia kupitia sala yenye juhudi na kupitia matumizi ya bidii ya Neno la Mungu. Ikiwa kwa njia hiyo mwenye kukosa ‘anarejezwa atoke katika njia ya upotevu,’ nafsi yake, yaani, mtenda dhambi mwenyewe, ataokolewa asipatwe na laana na kifo cha milele. Mtu yule aliyemkaripia ameshiriki kufunika au kusamehe dhambi za mkosaji.—Yakobo 5:19, 20.
Endelea Kusonga Mbele Katika Ibada Safi
Barua ya Yakobo inajibu maulizo ya maana kabisa kwa kutoboa majibu waziwazi, kama tulivyoona. Lakini sisi binafsi tutakuwa na maoni gani juu ya mashauri hayo yaliyoongozwa na Mungu tuliyopewa na mwanamume mzee mwenye ujuzi? Ni mashauri yenye kutoboa waziwazi nayo yanafaa kwa njia ya kiroho. Kwa hiyo je! tutayafuata?
Tukiyatumia mashauri ya Yakobo kwa juhudi, yatatusaidia kuvumilia majaribu, kuizoea dini ya kweli, kuepuka kuonyesha upendeleo na yatatusaidia tuthibitishe kwa matendo mema kwamba tuna imani halisi, iliyo hai. Zaidi ya hilo, yatatusaidia tuzuie ulimi, tutende kwa hekima ya kimbingu, tuzuie ugomvi katika kundi na kuonyesha subira tukiwa mashahidi wa Yehova walio wanyenyekevu na wenye kawaida ya kusali. Kwa sababu ya kufuata mashauri ya Yakobo, matokeo ni kwamba sisi tutaweza zaidi kumtukuza Baba yetu wa kimbingu kwa kusonga mbele katika ibada safi na yenye matendo.