SURA YA NANE
Ilinde Familia Yako Dhidi ya Mavutano Yaletayo Uharibifu
1-3. (a) Mavutano yaletayo uharibifu yanayotisha familia hutokana na vyanzo vipi? (b) Wazazi wahitaji usawaziko gani katika kuilinda familia yao?
SASA uko karibu kumruhusu mvulana wako mdogo aende shuleni, na mvua inakunya sana. Utashughulikiaje hiyo hali? Je, utamwacha aende akirukaruka nje bila kabuti? Au utamvisha mavazi mengi mno ya kumkinga hivi kwamba hawezi kusonga kwa urahisi? Bila shaka, hufanyi yoyote ya hayo. Utampa tu kile kinachohitajiwa ili asilowe.
2 Kwa njia iyo hiyo, ni lazima wazazi wapate njia yenye usawaziko ya kuilinda familia yao dhidi ya mavutano yaletayo uharibifu ambayo huvurumishwa juu yao kutokana na vyanzo vingi—shughuli ya vitumbuizo, vyombo vya habari, marika, na nyakati nyingine hata mashule. Wazazi fulani hufanya kidogo au hawafanyi lolote ili wakinge familia zao. Wengine, wakiona karibu mavutano yote ya nje kuwa yenye madhara, ni wazuifu sana hivi kwamba watoto huhisi kana kwamba wanasongwa pumzi. Je, usawaziko wawezekana?
3 Ndiyo wawezekana. Kuwa mwenye kupita kiasi hakufai na kwaweza kusababisha msiba. (Mhubiri 7:16, 17) Lakini wazazi Wakristo hupataje usawaziko ufaao katika kuilinda familia yao? Fikiria sehemu tatu: elimu, mashirika, na tafrija.
NI NANI ATAKAYEWAFUNDISHA WATOTO WENU?
4. Wazazi Wakristo waoneje elimu?
4 Wazazi Wakristo huthamini sana elimu. Wao wajua kwamba masomo husaidia watoto kusoma, waandike, na kuwasiliana, na pia kusuluhisha matatizo. Yapaswa pia kuwafundisha jinsi ya kujifunza. Stadi ambazo watoto hupata shuleni zaweza kuwasaidia wafanikiwe yajapokuwa magumu ya ulimwengu wa leo. Kwa kuongezea, elimu nzuri huenda ikawasaidia wafanye kazi iliyo bora zaidi.—Mithali 22:29.
5, 6. Huenda watoto shuleni wakafanywaje wapate habari iliyopotoka juu ya mambo ya kingono?
5 Hata hivyo, shule pia huwaleta watoto pamoja na watoto wengine—wengi wao wana maoni yaliyopotoka. Kwa kielelezo, fikiria maoni yao juu ya ngono na maadili. Katika shule moja ya upili Nigeria, msichana mwenye kufanya ngono za ovyo-ovyo alikuwa akiwatolea shauri wanafunzi wenzake juu ya ngono. Wao walimsikiliza kwa hamu, hata ingawa mawazo yake yalijaa upuuzi aliokuwa amepata katika fasihi za ponografia. Baadhi ya wasichana walijaribu shauri lake. Likiwa tokeo, msichana mmoja alipata mimba nje ya ndoa akafa kutokana na kujitoa-mimba.
6 Kwa huzuni, baadhi ya habari isiyofaa ya kingono shuleni hutoka kwa walimu, si kwa watoto. Wazazi wengi wanafadhaika mashule yanapofundisha watoto kuhusu ngono bila kutoa habari juu ya viwango vya kiadili na madaraka. Mama mmoja wa msichana wa miaka 12 alisema hivi: “Twaishi katika eneo lenye kufuata dini, lishikalo mapokeo sana, na bado katika shule ya kwetu yenyewe, wanawapa watoto kondomu!” Yeye na mume wake walihangaika walipopata kujua kwamba binti yao alikuwa akitongozwa na wavulana wa umri wake mwenyewe wafanye ngono naye. Wazazi waweza kuilindaje familia yao dhidi ya mavutano hayo mabaya?
7. Habari isiyofaa ya kingono yaweza kupingwaje kwa njia bora zaidi?
7 Je, yafaa kuwakinga watoto wasisikie lolote juu ya mambo ya kingono? La. Ni bora nyinyi wenyewe kuwafundisha watoto wenu kuhusu ngono. (Mithali 5:1) Ni kweli, katika sehemu za Ulaya na Amerika Kaskazini, wazazi wengi huepa habari hii. Vivyo hivyo, katika nchi fulani za Afrika, wazazi hawazungumzi sana na watoto wao kuhusu ngono. “Si sehemu ya utamaduni wa Afrika kufanya hivyo,” asema baba katika Sierra Leone. Wazazi fulani huhisi kwamba kuwafundisha watoto wao kuhusu ngono ni kuwapa mawazo yatakayowaongoza kwenye kufanya ukosefu wa adili! Lakini maoni ya Mungu ni nini?
MAONI YA MUNGU JUU YA NGONO
8, 9. Ni habari gani iliyo bora juu ya mambo ya kingono inayopatikana katika Biblia?
8 Biblia huelewesha wazi kwamba hakuna jambo la aibu kuhusu kuzungumzia ngono katika hali inayofaa. Katika Israeli, watu wa Mungu waliambiwa wakusanyike pamoja, kutia na “watoto” wao, ili kusikiliza usomaji kwa sauti kubwa wa Sheria ya Kimusa. (Kumbukumbu la Torati 31:10-12; Yoshua 8:35) Sheria ilitaja kwa uwazi mambo kadhaa ya kingono, kutia na hedhi, mitoko ya shahawa, uasherati, uzinzi, ugoni-jinsia-moja, ngono kati ya watu wa ukoo, na ngono pamoja na mnyama. (Mambo ya Walawi 15:16, 19; 18:6, 22, 23; Kumbukumbu la Torati 22:22) Baada ya usomaji wa jinsi hiyo bila shaka wazazi walikuwa na mengi ya kuwaelezea wachanga wao wenye udadisi.
9 Kuna mistari katika sura ya tano, ya sita, na ya saba ya Mithali inayotoa shauri la mzazi lenye upendo juu ya hatari za ukosefu wa adili katika ngono. Mistari hiyo huonyesha kwamba huenda nyakati nyingine ukosefu wa adili ukawa wenye kushawishi. (Mithali 5:3; 6:24, 25; 7:14-21) Lakini inafundisha kwamba huo ni mbaya nao una matokeo yaletayo msiba, nayo inatoa mwongozo ili kusaidia vijana waepuke njia zenye ukosefu wa adili. (Mithali 5:1-14, 21-23; 6:27-35; 7:22-27) Zaidi ya hayo, ukosefu wa adili unatofautishwa na uradhi wa raha ya kingono katika hali yayo inayofaa, katika ndoa. (Mithali 5:15-20) Hicho ni kigezo chema kama nini cha kufundisha kwa wazazi kufuata!
10. Kwa nini kuwapa watoto ujuzi wa kimungu kuhusu ngono kusiwaongoze kufanya ukosefu wa adili?
10 Je, kufundisha huko huongoza watoto wafanye ukosefu wa adili? La hasha, Biblia hufundisha: “Waadilifu wanaokolewa kwa ujuzi.” (Mithali 11:9, NW) Je, mwataka kuwaokoa watoto wenu na mavutano ya ulimwengu huu? Baba mmoja alisema hivi: “Tangu watoto walipokuwa wachanga sana, sisi tumejaribu kuwa wenye uwazi kabisa nao kwa habari ya ngono. Kwa njia hiyo, wanaposikia watoto wengine wakiongea kuhusu ngono, wao hawawi wenye udadisi. Hakuna fumbo kubwa.”
11. Watoto waweza kufundishwaje hatua kwa hatua kuhusu mambo ya kindani ya maisha?
11 Kama ilivyoonyeshwa katika sura za mapema, elimu ya ngono yapaswa kuanza mapema. Mnapowafundisha watoto wadogo kutaja majina ya sehemu za mwili, msiruke sehemu zao za siri kana kwamba hizo ni zenye aibu kwa kadiri fulani. Wafundisheni majina yanayofaa ya sehemu hizo. Wakati upitapo, masomo kuhusu kuwa na faragha na mipaka ni ya muhimu. Kwa kufaa wazazi wote wawili wapaswa kuwafundisha watoto kwamba sehemu hizi za mwili ni za pekee, ambazo kwa kawaida hazipasi kuguswa na wengine au kufunuliwa kwao, na hazipasi kamwe kuzungumziwa kwa njia mbaya. Watoto wakuapo hata kufikia umri mkubwa zaidi, wanapaswa kujulishwa kuhusu jinsi mwanamume na mwanamke wanavyokuja pamoja ili kupata mimba ya mtoto. Kufikia wakati miili yao wenyewe ianzapo kuingia ubalehe, wanapaswa tayari wawe wamejua vizuri sana mabadiliko yapasayo kutazamiwa. Kama ilivyozungumziwa katika Sura ya 5, elimu hiyo yaweza pia kusaidia kuwalinda watoto dhidi ya kutendwa vibaya kingono.—Mithali 2:10-14.
MGAWO WA WAZAZI WA MASOMO YA NYUMBANI
12. Ni maoni gani yaliyopotoka ambayo mara nyingi hufundishwa mashuleni?
12 Wazazi wahitaji wawe tayari kupinga mawazo mengine yasiyo ya kweli ambayo huenda yakafundishwa shuleni—falsafa za kilimwengu kama vile mageuzi, utukuzo wa taifa, au wazo la kwamba hakuna kweli zozote zilizo kamilifu. (1 Wakorintho 3:19; linganisha Mwanzo 1:27; Mambo ya Walawi 26:1; Yohana 4:24; 17:17.) Maofisa wengi wa shule wenye moyo mweupe hutia umaana usiofaa kwenye elimu ya ziada. Ingawa jambo la elimu ya ziada ni chaguo la kibinafsi, walimu fulani husisitiza kwamba hiyo ndiyo njia pekee ya kupata mafanikio yoyote ya kibinafsi.a—Zaburi 146:3-6.
13. Watoto wanaohudhuria shule waweza kulindwaje dhidi ya mawazo mabaya?
13 Ikiwa wazazi watapinga mafundisho mabaya au yaliyopotoka, ni lazima wajue ni mafunzo gani hasa watoto wao wanapokea. Kwa hiyo wazazi, kumbukeni kwamba nyinyi pia mna mgawo wa masomo ya nyumbani! Onyesheni kupendezwa kikweli na elimu ya watoto wenu. Ongeeni nao baada ya shule. Waulizeni yale wanayojifunza, lile wanalopenda zaidi, na lile wanaloona kuwa gumu zaidi. Pitieni migawo ya masomo ya nyumbani, maandishi, na matokeo ya mitihani. Jaribuni kupata kuwajua walimu wao. Julisheni walimu kwamba mnathamini kazi yao na kwamba mnataka kuwa wenye kusaidia kwa njia yoyote mwezavyo.
MARAFIKI WA WATOTO WENU
14. Kwa nini ni muhimu kwamba watoto wamwogopao Mungu wachague marafiki wema?
14 “Ala, ulijifunza wapi hilo?” Ni wazazi wangapi wameuliza swali hilo, wakishtushwa na jambo fulani ambalo mtoto wao amesema au kufanya na ambalo halionekani kuwa tabia yake? Na ni mara ngapi jibu huhusiana na rafiki fulani mpya shuleni au katika ujirani? Ndiyo, waandamani hutuathiri sana, tuwe ni vijana au wazee. Mtume Paulo alionya hivi: “Msiongozwe vibaya. Mashirika mabaya huharibu mazoea yenye mafaa.” (1 Wakorintho 15:33; Mithali 13:20) Vijana hasa wanasongwa kwa urahisi na marika. Wanaelekea kutokuwa na uhakika juu yao wenyewe na huenda nyakati nyingine wakahisi kulemewa na tamaa ya kupendeza na kuvutia washiriki wao. Ni muhimu kama nini basi, kwamba wachague marafiki wema!
15. Wazazi waweza kuwaongozaje watoto wao katika kuchagua marafiki?
15 Kama vile kila mzazi ajuavyo, watoto hawatachagua vizuri sikuzote; wao wahitaji mwongozo fulani. Si jambo la kuwachagulia marafiki wao. Bali, kadiri wakuavyo, wafundisheni ufahamu na wasaidieni waone ni sifa zipi wanazopaswa kuthamini katika marafiki. Sifa kuu ni kumpenda Yehova na kupenda lililo sawa machoni pake. (Marko 12:28-30) Wafundisheni kupenda na kustahi wale walio na sifa ya ufuatiaji wa haki, fadhili, ukarimu, bidii yenye kuendelea. Wakati wa funzo la familia, wasaidieni watoto wafahamu sifa hizo katika watu wanaotajwa katika Biblia kisha wazione sifa hizohizo katika wengine kutanikoni. Wekeni kielelezo kwa kutumia viwango hivyohivyo katika kuchagua marafiki wenu wenyewe.
16. Wazazi waweza kuchunguzaje uteuzi wa marafiki wa watoto wao?
16 Je, mwajua ni nani walio marafiki wa watoto wenu? Kwa nini msiwaombe watoto wenu wawalete nyumbani ili mweze kuwajua? Mwaweza pia kuwauliza watoto wenu maoni ya watoto wengine kuhusu marafiki hao. Je, wanajulikana kwa ajili ya kuonyesha uaminifu-maadili wa kibinafsi au kwa kuishi maisha maradufu? Ikiwa la pili ni kweli, wasaidieni watoto wenu wasababu juu ya kwa nini mashirika hayo yangeweza kuwaumiza. (Zaburi 26:4, 5, 9-12) Ukiona mabadiliko yasiyofaa katika mwenendo, mavazi, mtazamo, au usemi wa mtoto wako, huenda ukahitaji kuongea kuhusu marafiki wake. Huenda mtoto wako akawa anashinda na rafiki anayetokeza uvutano hasi.—Linganisha Mwanzo 34:1, 2.
17, 18. Zaidi ya kuonya dhidi ya washiriki wabaya, huenda wazazi wakatoa msaada gani wenye kutumika?
17 Hata hivyo haitoshi tu kuwafundisha watoto wenu kuepuka washiriki wabaya. Wasaidieni wapate walio wema. Baba mmoja asema: “Tulikuwa sikuzote tukijaribu kutoa badala. Kwa hiyo shule ilipotaka mwana wetu ajiunge na timu ya mpira, mke wangu nami tuliketi naye na kuzungumzia ni kwa nini hilo lisingekuwa wazo zuri—kwa sababu ya waandamani wapya ambao wangehusika. Lakini tukadokeza kukusanya baadhi ya wale watoto wengine kutanikoni na kuwapeleka wote kwenye bustani ili wacheze mpira. Na hilo lilisuluhisha tatizo.”
18 Wazazi wenye hekima husaidia watoto wao wapate marafiki wema kisha wafurahie tafrija inayofaa pamoja nao. Lakini, kwa wazazi wengi, jambo hili la tafrija hutokeza magumu yalo lenyewe.
NI AINA GANI YA TAFRIJA?
19. Ni vielelezo gani vya Biblia vionyeshavyo kwamba si dhambi kwa familia kuwa na raha?
19 Je, Biblia hulaumu kuwa na raha? La hasha! Biblia husema kwamba kuna “wakati wa kucheka . . . na wakati wa kucheza.”b (Mhubiri 3:4) Watu wa Mungu katika Israeli la kale walifurahia muziki na kucheza dansi, michezo, na vitendawili. Yesu Kristo alihudhuria karamu kubwa ya arusi na “karamu [kubwa] ya makaribisho” ambayo Mathayo Lawi alimfanyia. (Luka 5:29; Yohana 2:1, 2) Kwa wazi, Yesu hakuwa mtu asiyetaka shangwe. Kucheka na raha kusionwe kamwe kuwa dhambi nyumbani mwako!
Tafrija iliyochaguliwa vizuri, kama vile safari hii ya kupiga kambi ya familia, yaweza kusaidia watoto wajifunze na kukua kiroho
20. Wazazi wakumbuke nini katika kuandalia familia tafrija?
20 Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Kwa hiyo ibada ya Yehova yapaswa iwe chanzo cha upendezi, si jambo lisababishalo ukosefu wa shangwe maishani. (Linganisha Kumbukumbu la Torati 16:15.) Kiasili watoto ni wachangamfu na wenye kujaa nishati iwezayo kutokezwa katika michezo na tafrija. Tafrija iliyochaguliwa vizuri ni zaidi ya raha tu. Ni njia ya mtoto kujifunza na kuwa mkomavu. Kichwa cha familia kina daraka la kuandaa mahitaji ya nyumba yacho katika kila jambo kutia na tafrija. Hata hivyo, usawaziko unatakwa.
21. Ni mitego gani iliyomo katika tafrija leo?
21 Katika “siku [hizi] za mwisho” zenye taabu, jamii ya kibinadamu imejaa watu walio “wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu,” kama vile ilivyotolewa unabii katika Biblia. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa wengi, tafrija ndilo jambo kuu maishani. Kuna vitumbuizo vingi sana vinavyopatikana hivi kwamba vinaweza kwa urahisi kuchukua mahali pa mambo yaliyo ya maana zaidi. Isitoshe, vitumbuizo vingi vya kisasa hukazia ukosefu wa adili katika ngono, ujeuri, utumizi mbaya wa madawa, na mazoea mengine yaliyo yenye madhara sana. (Mithali 3:31) Ni nini liwezalo kufanywa ili kuwalinda vijana salama na vitumbuizo vyenye madhara?
22. Wazazi waweza kuwazoezaje watoto wao wafanye maamuzi yenye hekima kwa habari ya tafrija?
22 Wazazi wahitaji kuweka mipaka na vizuizi. Lakini zaidi ya hayo, wao wahitaji kuwafundisha watoto wao jinsi ya kuamua ni tafrija gani iliyo yenye madhara na kujua ni kiasi gani kilicho kingi mno. Mazoezi hayo huchukua wakati na jitihada. Fikiria kielelezi. Baba wa wavulana wawili aliona kwamba mwana wake mwenye umri mkubwa zaidi alikuwa akisikiliza stesheni mpya ya redio mara nyingi sana. Kwa hiyo siku moja alipokuwa akiendesha lori lake kwenda kazini, huyo baba alifungua stesheni iyo hiyo. Mara kwa mara alitua na kuandika maneno ya nyimbo fulani. Baadaye aliketi pamoja na wana wake na kuzungumzia yale aliyokuwa amesikia. Aliuliza maswali ya kupata maoni, akianzia na “Mwafikirije?” naye akasikiliza majibu yao kwa subira. Baada ya kusababu juu ya jambo hilo kwa kutumia Biblia, hao wavulana walikubali kutosikiliza stesheni hiyo.
23. Wazazi waweza kuwalindaje watoto wao dhidi ya vitumbuizo visivyofaa?
23 Wazazi Wakristo wenye hekima huchunguza muziki, programu za televisheni, kanda za video, vitabu vya katuni, michezo ya video, na sinema zinazowapendeza watoto wao. Wao huangalia michoro kwenye jalada, maneno ya nyimbo, na makasha, nao husoma maoni ya watu katika magazeti ya habari na hutazama madondoo. Wengi hushtuka kuona baadhi ya “vitumbuizo” vinavyotolewa kwa watoto leo. Wale wanaotaka kuwalinda watoto wao dhidi ya mavutano yasiyo safi huketi pamoja wakiwa familia na kuzungumzia hatari, wakitumia Biblia na vichapo vyenye msingi wa Biblia, kama vile kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na makala katika magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni!c Wazazi wanapoweka mipaka imara, wakiwa bila ugeugeu na kuwa wenye kiasi, wao kwa kawaida huona matokeo mazuri.—Mathayo 5:37; Wafilipi 4:5.
24, 25. Ni nini baadhi ya namna za tafrija zifaazo ambazo familia zaweza kufurahia pamoja?
24 Bila shaka, kuzuia namna za tafrija zenye madhara ni sehemu tu ya pigano. Ni lazima mabaya yapingwe na mema, ama sivyo huenda watoto wakapeperuka kuingia mwendo mbaya. Familia nyingi za Kikristo zina makumbukumbu mengi sana machangamfu na yenye furaha ya kufurahia tafrija pamoja—kufanya mandari, kutalii kwa miguu, kupiga kambi, kucheza michezo, kusafiri ili kutembelea watu wa ukoo au marafiki. Watu fulani wameona kwamba kusoma pamoja tu kwa sauti ili kustarehe ni chanzo kikubwa cha raha na faraja. Wengine hufurahia kusimulia hadithi za kuchekesha au zenye kupendeza. Wengine bado wamesitawisha pamoja utendaji mbalimbali wa kufurahisha, kwa kielelezo, kuunda vitu vya mbao na ufundi mwingineo, na pia kucheza ala za muziki, kufanya sanaa, au kujifunza juu ya uumbaji wa Mungu. Watoto wanaojifunza kufurahia mambo hayo yenye kustarehesha wanalindwa dhidi ya vitumbuizo vingi visivyo safi, na wanajifunza kwamba kuna mengi zaidi kwa habari ya tafrija kuliko kuketi tu bila kufanya lolote na kutumbuizwa. Mara nyingi kushiriki hufurahisha zaidi kuliko kutazama tu.
25 Huenda pia vikusanyiko vya kirafiki vikawa namna ya tafrija yenye kuthawabu. Vinaposimamiwa vizuri na kutokuwa vikubwa mno au vyenye kuchukua wakati mwingi sana, vyaweza kuwapa watoto wako mengi zaidi kuliko raha tu. Vyaweza kusaidia kuongeza kina cha mahusiano ya upendo kutanikoni.—Linganisha Luka 14:13, 14; Yuda 12.
FAMILIA YENU YAWEZA KUUSHINDA ULIMWENGU
26. Kwa habari ya kuilinda familia dhidi ya mavutano yasiyofaa, ni sifa gani iliyo ya maana zaidi?
26 Bila shaka, kuilinda familia yenu dhidi ya mavutano ya ulimwengu yaletayo uharibifu hutaka jitihada nyingi. Lakini kuna jambo moja litakaloleta mafanikio zaidi ya mengine yote. Hilo ni upendo! Mahusiano ya familia yaliyo ya karibu, yenye upendo yatafanya nyumba yenu iwe mahali salama nayo yatachochea uwasiliano, ambao ni ulinzi mkubwa dhidi ya mavutano mabaya. Isitoshe, kusitawisha upendo wa aina nyingine ni jambo lililo la maana hata zaidi—kumpenda Yehova. Kupenda huko kunapoipenya familia, watoto huelekea zaidi kukua wakichukia wazo lenyewe la kutompendeza Mungu kwa kushindwa na mavutano ya kilimwengu. Na wazazi wampendao Yehova kutoka moyoni watajaribu kuiga utu wake wenye upendo, kiasi, ulio na usawaziko. (Waefeso 5:1; Yakobo 3:17) Wazazi wakifanya hivyo, watoto wao hawatakuwa na sababu ya kuiona ibada ya Yehova kuwa tu orodha ya mambo wasiyoruhusiwa kufanya au kuwa njia ya maisha isiyo na raha au ucheshi, ambayo wanataka kuikimbia upesi iwezekanavyo. Bali, wao wataona kwamba kumwabudu Mungu ndiyo njia ya maisha yenye furaha, iliyo kamili zaidi ya zote iwezekanavyo.
27. Familia yaweza kuushindaje ulimwengu?
27 Familia zinazoendelea kuwa zenye muungano katika utumishi wa Mungu wenye furaha, ulio na usawaziko, zinazojitahidi kwa moyo wote kudumu zikiwa “bila doa na bila waa” mbali na mavutano yenye kufisidi ya ulimwengu huu, ni chanzo cha shangwe kwa Yehova. (2 Petro 3:14; Mithali 27:11) Familia hizo hufuata katika hatua za miguu za Yesu Kristo, aliyekinza kila jitihada ya ulimwengu wa Shetani ya kumtia unajisi. Karibu na mwisho wa uhai wake wa kibinadamu, Yesu aliweza kusema: “Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Familia yako pia na iushinde ulimwengu na kufurahia maisha milele!
a Ili kupata mazungumzo juu ya elimu ya ziada, ona broshua Mashahidi wa Yehova na Elimu, iliyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc., kurasa 4-7.
b Neno la Kiebrania linalofasiriwa hapa “kucheka” laweza, katika namna nyinginezo, kufasiriwa “kucheza,” “kuandaa kitumbuizo fulani,” “kusherehekea,” au hata “kuwa na raha.”
c Vilivyotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 99]
Tafrija iliyochaguliwa vizuri, kama vile safari hii ya kupiga kambi ya familia, yaweza kusaidia watoto wajifunze na kukua kiroho