-
Kugeuza Utu wa Watu Katika Paradiso ya KenyaMnara wa Mlinzi—1978 | Juni 1
-
-
siku tatu. Wakati alipokuwa akijifunza Biblia alipingwa sana na wazazi wake, rafiki zake wa zamani na jirani, lakini baadaye aliweza kusaidia wengine wa wapinzani hao wakaanza kujifunza Biblia. Leo yeye ni “painia” mwenye kuzihubiri “habari njema,” naye anaonyesha wengine ile kweli, ambayo hata yule rafiki yake mwenye duka amekwisha ikubali pia.
Tukisonga mbele magharibi, tunazifikia pwani na Ziwa Victoria lenye kupendeza, na huko ndiko wanakokaa Wanailo wa pekee wapatikanao Kenya, yaani, Waluo. Waluo, ambao ni watu waliohama kutoka Bonde la upande wa juu wa Mto Nailo, wana mfufulizo wa sherehe za kutia vijana wao jandoni, na wakati wa sherehe hizo vijana fulani wanakubali kung’olewa meno mawili au zaidi katika taya la chini ili kuhakikisha wao ni mashujaa. Desturi zao za kufanya maziko na matanga (maombolezo) ya muda mrefu zinaonyesha wanaamini sana kwamba wanaweza kupashana habari na mababu waliokufa. Katika Kisumu, ambayo ndiyo makao makuu ya eneo hilo, na ambao ndio mji wa tatu kwa ukubwa katika Kenya, mkuu mmoja wa serikali alielezwa kweli ya Biblia kwa mara ya kwanza mwaka 1965 na mfanya kazi mwenzake. Ingawa hakuanza kujifunza Biblia kwa makini, nyakati zote aliwasalimu kirafiki Mashahidi waliopita karibu na afisi yake. Miaka kumi ilipita, lakini lo! alifurahi namna gani kuonyesha wakf wake kwa kubatizwa majini mwaka juzi! Kwa sababu ya furaha aliyopata aliomba apewe pendeleo la kulipa gharama ya jumba ambamo kusanyiko la mzunguko lilifanywa wakati wa juma ya kubatizwa kwake. Baada ya muda mfupi amesaidia wengine walio karibu yake, kutia na mkewe, wakaiona kweli na kugeuza nia zao.
Wanaokaa katika mwinuko ulioko mashariki ya kaskazini ya Ziwa Victoria mpaka kwenye eneo la chini la Mlima Elgon, wenye urefu wa mita 4,322 (futi 14,178), ni watu wanaoitwa Abaluhya, nalo hilo ni jina la mwungano wa jamii kubwa ya Wabantu. Watu hao wanazikubali habari njema kwa kuzithamini mioyoni mwao. Mwaka juzi, katika kijiji kimoja kilicho karibu sana na ikweta katika eneo hilo la magharibi, kijana wa miaka kumi na mitano alivumilia upinzani mwingi na kuweka maisha yake wakf kwa Yehova. Ndipo alipopata habari kwamba miezi mitatu baadaye kungekuwa na kusanyiko “Utumishi Mtakatifu” Nairobi, kilomita 340 (maili 210) kutoka hapo, kisha akatafuta kazi apate fedha za safari hiyo. Mwangalizi-msimamizi ndiye akawa ‘banki’ yake ya kumwekea fedha. Ajabu ni kwamba, alipopata pesa za kumwezesha kusafiri, alianza kutafuta nyingine pia, Ziwe za nani? Ziwe za rafiki mwenye kupendezwa wa umri wake, maana alimtaka yeye awe na nafasi iyo hiyo ya kufurahia kipindi cha Kusanyiko la wilaya!
GUMU LA TABIA
Kati ya makabila yote ya Kenya, labda Wamasai ndio wanaojulikana zaidi ulimwenguni pote. Wao ni wenye sifa ya kuwa na uhodari mwingi sana na kukaa peke yao wakijisimamia wenyewe. Desturi zao nyingi za zamani zingali hazijageuzwa na desturi za Kizungu. Wao wanavaa vazi lenye rangi kama ya udongo mwekundu na kujipamba kwa kuvaa shanga, huku chakula chao kikiwa ni maziwa hasa yenye damu nyingi ya ng’ombe. Wangali wanashikilia mpango wa “moran,” ambapo vijana wanaume wanatengwa peke yao na kuwekewa sheria ngumu za kujinyima vitu mpaka watakapostahili kuwa wazee, ijapokuwa wanaruhusiwa kulala na wanawake. Jambo la ajabu linalofanywa na Waelgeyo/Marakwet ni kukubali kuoana baada ya mke kuchukua mimba, lakini si kabla ya hapo. Maisha ya makabila hayo mawili yanaonyesha mengine ya matatizo ya tabia yanayowapata pamoja na wengine wanaotaka kugeuza utu wao upatane na kanuni njema za Biblia.
Desturi imeenea sana ya wanaume na wanawake kuishi pamoja na kuzaa watoto bila ya kuoana kisheria maisha yao yote. Watu wengi wanatosheka wanapooana kwa muda tu, kwa kufuata mipango ya kabila lao. Mara nyingi watu wanakawia kuoana kisheria kwa sababu ya mahari nyingi sana kudaiwa. Lakini, baada ya kujifunza kanuni bora za Mungu, wengi wamefanya bidii kwa moyo mweupe wakaandikisha ndoa zao. Wazee wa Mashahidi wa Yehova, waliowekwa rasmi na serikali na kupewa cheti, wamewasaidia sana watu hao kwa sababu wanatoa utumishi wao bila malipo, si kama wachungaji wa Jumuiya ya Wakristo ambao kwa kawaida wanaomba malipo mengi. Hivyo, waume na wake karibu 600 wamesaidiwa kuoana kupatana na kanuni njema za Mungu. Huu ni mfano wa mume na mke waliooana:
Mwanamume mmoja alijaribu kumzuia mama ya watoto wake asijifunze Biblia na Mashahidi. Lakini, mwanamke huyo alivumilia na kuzidi kufanya maendeleo, akitaka kumpendeza mungu. Mwanamume huyo alipokataa kuandikisha mwungano wao kisheria, mwanamke huyo alimwacha akavumilia kuishi maisha yasiyo na gharama nyingi. Aliona ukweli wa maneno yaliyo katika Zaburi 37:25, yanayoonyesha kwamba Mungu atasaidia wapendao haki, basi akaweza kuwapa riziki watoto alioachiwa. Jambo hilo lilimshangaza mwanamume huyo, lakini aliendelea kufanya upinzani kiasi cha kuwaomba wanasiasa waipige marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova nchini. Lakini kwa njia ya ajabu akaanza ‘kugeuza nia yake.’ Alipokuwa akipeleka watoto wake katika matembezi mafupi, mwana wake wa miaka mitatu alimwambia maneno fulani yakamsumbua moyo. Mtoto huyo alikuwa akimwambia mambo kama haya: “Baba, utakapoacha kuvuta sigara na kunywa pombe kisha ununue kitabu cha nyimbo na Biblia, tutakwenda kwenye Jumba la Ufalme wala hutaharibiwa.” Mwishowe, mtu huyo alikubali kujifunza Biblia, akafanya maendeleo, akaandikisha ndoa yake kisheria, na kuanza kumtumikia Mungu pamoja na jamaa yake ambayo sasa ina umoja.
MAENDELEO YA MIAKA YA KARIBUNI
Tangu mwaka 1973 mwendo wa mpanuko umeongezwa. Hali zilionyesha wazi sana mwaka huo kwamba ingewapasa Mashahidi wenyeji wachukue madaraka makuu ya kupelekea wengine “habari njema.” Kwa kusaidiwa na Yehova wameweza kutimiza madaraka hayo na kupeleka ujumbe kwenye maeneo ya mbali zaidi ya nchi. Wakati uo huo, kulikuwa na mfululizo wa matukio katika nchi jirani yakaonyesha kwamba hali ya mambo inazidi kuharibika nyakati zote. Ukavu mwingi ulitokea ukafanya watu wengi wafikirie jinsi wanavyomtegemea Mpaji wetu wa mbinguni. Bei za vitu zinazopanda na hatari mbalimbali za nchi jirani zimesaidia wengine kuona kwamba unabii wa Biblia unasema kweli. Matatizo yanayopatikana ulimwenguni pote ya ulevi, uvunjaji sheria, matumizi mabaya ya dawa za kulevya na kuvunjika kwa jamaa yameenea sana, yakafanya wengine, sana sana vijana, wajue kwamba viongozi wao wa kidini wameshindwa kuwapa uongozi na kwa hiyo lazima wategemee uongozi mzuri mahali pengine. Katika maeneo yote ya nchi, na kati ya watu wa namna zote, Mashahidi wa Yehova wanawaendea na kuwasaidia watu wanaotaka kwa moyo mweupe kuuvaa utu mpya na kugeuza maisha yao.
Miaka ya karibuni wahubiri na waalimu wa “habari njema” wanaoitwa “mapainia” wamehamia maeneo mengi mapya, na mengine kati ya hayo yakawa na maendeleo yenye kutia sana moyo. Limuru, ambao ni mji wenye viwanda karibu na ukingo wa mashariki wa lile Bonde Kuu, umekuwa hauna wahubiri wa Ufalme, lakini baada ya muda unaopungua miaka mitatu sasa una wahubiri kumi na sita wanaohubiri kweli ya Biblia kwa bidii. Katika kipindi icho hicho eneo lenye rutuba la Wakikuyu, ambao ni watu wenye bidii, pamoja na eneo la Wameru na Waembu katika mitelemko ya Mlima Kenya wenye theluji, limekuwa na ongezeko la kutoka Mashahidi 30 wenye bidii likawa na zaidi ya 140. Kati yao kuna mzee Mkikuyu aliyezaliwa miaka karibu 80 iliyopita, wakati ambao watu walikuwa wakitobolewa matundu masikioni kisha yanarefushwa na kukunjiliwa upande wa juu wa sikio. Kwa kawaida yeye anatembea kilomita karibu 20 (maili 12), akipanda vilima na kutelemka, ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hata pawe ni mahali gani, kando-kando ya Mlima Kenya, katika mitelemko yenye misitu inayopendeza ya Bonde la Mau magharibi ya Nakuru, au katika eneo lenye mashamba mengi sana kando-kando ya Kisii katika magharibi ya kusini ya Kenya, ukuzi umekuwa mkubwa sana.
Katika pwani ya Bahari Kuu ya Bara Hindi, karibu na Mombasa, mume na mke mmoja wanaongoza jumla ya mafunzo ya Biblia kumi na tisa katika nyumba za wenye kupendezwa. Wanaufurahia sana utumishi wao kiasi cha kwamba walimwita mtoto wao wa kwanza “Painia.” Katika Kenya nzima, watu zaidi ya 1,045 walibatizwa kuonyesha wakf wao miaka mitatu na nusu iliyopita. Wengine zaidi wanataka kuvaa utu mpya, kama inavyoonekana kutokana na hesabu ya wanaohudhuria mikutano, ambayo ni mara mbili ya Mashahidi waliopo. Hesabu ya waliohudhuria mwadhimisho wa Chakula cha Bwana cha Jioni Aprili 3 (mwaka jana) walizidi 5,000 kwa mara ya kwanza, wakiwa ni watu 5,582.
Ndiyo, utu unageuzwa kati ya makabila yote ya Kenya, na humu tumetaja machache tu. Kutoka mito yenye barafu ya Mlima Kenya, iliyo juu kuliko mito yo yote katika milima ya Amerika au ya Ulaya, mpaka kwenye kando za pwani zinazopendeza sana na zenye joto jingi, na kutoka maeneo makavu ya kaskazini yenye jangwa, kuja kwenye misitu iliyo milimani na katika mashamba yaliyoinuka yenye rutuba mpaka kwenye nyanda zenye manyasi za Masai Mara, katika ukingo wa nyanda za Serengeti, watu wanausikia ujumbe wa Biblia na kubadili nia zao. Kwa hiyo, uifikiriapo Kenya pamoja na wanyama wake walio katika makao ya asili, na vilevile umfikiriapo simba hodari akimwendea swala polepole ili ajipatie chakula, ufikirie pia utu na tabia zinazogeuzwa kwa uwezo wa Neno la Mungu. Uzifikiriapo desturi mbalimbali, mazoea na lugha mbalimbali, fikiria pia jinsi watu hao wanavyounganishwa kuwa jamaa moja yenye furaha ya wanaume na wanawake Wakristo wanaomtumikia Muumba kwa sababu ya kugeuza utu wao. Hakika, utu wa watu unageuzwa sana katika paradiso ya kiroho ya Kenya.
-
-
Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya YehovaMnara wa Mlinzi—1978 | Juni 1
-
-
Katiwa Nguvu Kunena Maneno ya Yehova
“[Yehova] asema hivi, . . . sema . . . maneno yote ninayokuamuru kuwaambia, usizuie hata neno moja.”—Yer. 26:2.
1. Yeremia alikuwa nabii wa namna gani, naye Yehova alimtiaje nguvu?
YEREMIA alikuwa nabii mwaminifu. Kwa sababu alikuwa mwenye bidii akiyatangaza “maneno” ya Yehova, taifa zima lilimtakia mabaya. Lakini alipomlilia Yehova amsaidie, Mungu wake alimfariji, akisema: “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya.” Usemi huo wa Yehova ulimpa nguvu za kuvumilia.—Yer. 15:10, 15, 20.
2. Yeremia alionyesha sifa gani za kupendeza? (Ebr. 13:6)
2 Yeremia alitii kwa kuyatangaza “maneno yote” ya ujumbe mkali wa hukumu ambao Yehova alimpa aunene. ‘Hakuzuia hata neno moja.’ (Yer. 26:2) Hakupunguza maneno yo yote alipokuwa akiufunua wazi uovu wa taifa la Kiyahudi, wa watawala wake na watu wake. Yeremia alihitaji uhodari ili aweze kufanya hivyo, tena alihitaji kuamini kabisa kwamba Yehova angeweza kumsaidia maana alikuwa nabii Wake.
3. Ni nani wanaotumikia kama “Yeremia” wa kisasa,nao wameingizwa katika agano gani?
3 Vivyo hivyo, katika nyakati za kisasa, Yehova ameyainua mabaki machache ya mashahidi wake waliotiwa mafuta watumikie wakiwa jamii ya Yeremia, hasa katika makao ya Jumuiya ya Wakristo yenye unafiki (udanganyifu). Wao pia ‘wanapaswa kusema maneno yote ambayo Yehova anaamuru.’ Maneno hayo ni yenye ujumbe wa kulipa moyo na tumaini kundi la kweli la Kikristo, wala si wa kuonyesha maangamizi tu ya Jumuiya ya Wakristo na mataifa mengine yote. Waisraeli hao wa kiroho wameingizwa katika “agano jipya” lililoelezwa na nabii kwa maneno yenye shauku (bidii) yaliyo katika Yeremia 31:33, 34:
“Bali agano hili ndilo nitakalofanya na nyumba ya Israeli, baada ya siku zile, asema [Yehova]; Nitatia sheria yangu ndani yao, na katika mioyo yao nitaiandika; nami nitakuwa Mungu wao, nao watakuwa watu wangu. Wala hawatamfundisha kila mtu jirani yake, na kila mtu ndugu yake, wakisema, Mjue [Yehova]; kwa maana watanijua wote, tangu mtu aliye mdogo miongoni mwao hata aliye mkubwa miongoni mwao, asema [Yehova]; maana nitausamehe uovu wao, wala dhambi yao sitaikumbuka tena.”
4. Watu wa Mungu wanatazamia tumaini gani kama Ibrahimu? (Ebr. 13:12-15)
4 Yehova anajengea hao “wazao wa Israeli” mji wa mbinguni ambao hautang’olewa, wala hautabomolewa tena mpaka umilele. (Linganisha Waebrania 9:13-15.) Tumaini hilo linatukumbusha jinsi Yehova alivyomtia nguvu Ibrahimu mwaminifu kwa kumpa tumaini la kupata “mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Ebr. 11:10) Na sasa tunaishi katika siku ambazo bibi-arusi wa Kristo, yaani, “mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya,” unakaribia kukamilika mbinguni, wakati, ambao ‘utashuka’ kwa njia ya mfano uletee wanadamu baraka za milele.—Ufu. 21:2-5, 9.
5. Inatupasa tujulishe wengine “maneno” gani kwa shauku? (b) Ni ujumbe gani wenye sehemu mbili ambao lazima jamii ya Yeremia iuhubiri? (Linganisha Isaya 61:1, 2.)
5 Mji huo ndio ufalme wa mbinguni ambako Yehova anayaelekeza mabaki ya kondoo zake akiyachunga kwa kumtumia Yesu Kristo. Kwa sasa wazee walio kati ya kondoo hao wanatumikia kama wachungaji wadogo wenye kuchunga makundi ya watu wake waliopo duniani kwa uaminifu. (Yer. 23:3, 4) Wao ni mabalozi wa ufalme wa “Chipukizi la haki,” yaani, Daudi Mkubwa, Yesu Kristo, ambaye unabii unasema hivi juu yake:
“Naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi. . . . Na jina lake atakaloitwa ni hili, [Yehova] ni haki yetu.” (Yer. 23:5, 6; linganisha Isaya 32:1, 2; 2 Wakorintho 5:20.)
Inatupasa tuwe wenye shauku (bidii) nyingi ya kutaka kujulisha wengine “maneno” ya Yehova juu ya ufalme huo wenye haki. Lakini Yehova anaiagiza jamii ya kisasa ya Yeremia itangaze pia ujumbe wa maangamizi!
JUMUIYA YA WAKRISTO ITAANGAMIA
6. “Maneno” ya Yeremia yanawafaaje viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo?
6 Viongozi wa dini wa Jumuiya (jamii) ya Wakristo wanadai kwamba wao ni Wakristo. Lakini je! mafundisho na matendo yao yanahakikisha dai lao? Au, wanaonekana kuwa sawa na viongozi wa kidini wa siku za Yeremia? Kwa habari yao, Yeremia alisema hivi:
“Hutega mtego, na kunasa watu. Kama tundu lijaavyo ndege, kadhalika nyumba zao zimejaa hila; kwa hiyo wamekuwa wakuu, wamepata mali.” (Yer. 5:26, 27)
Wamewatamani watu, wakawavuta kwa kujionyesha kijuujuu kwamba wao ni watawa au wakatumia upanga kuwalazimisha wageuke wafuate dini yao, kama ilivyokuwa katika siku zile ambazo mataifa yalikuwa yakihamia nchi mpya na kuanza kuitawala. Lakini msingi wa dini yao ni mafumbo ya kale ya Babeli, wala si Neno la Mungu. (Ufu. 17:5) Mungu wao ni “utatu” wenye kuvuruga akili za watu. Wameingiza katika watu wengi woga wa kuchomwa na “moto wa milele” kwa kuwafundisha uongo kwamba nafsi haifi, kisha wakajipatia pesa nyingi kwa kuombea wale wanaosemekana wanateseka katika ile purgatori ya hadithi tu. Wanauabudu msalaba, kama walivyofanya Wamisri muda mrefu kabla ya Kristo kutokea. Wanazipamba sanamu za watakatifu wao kwa kuzungusha duara ya mwanga wa jua katika vichwa vyazo na kuziwekea tasbihi (ushanga), kama zinavyofanya dini za Mashariki (upande wa Bara Hindi).
“Wamewanda [wamenenepa] sana, wang’aa; naam, wamepita kiasi kwa matendo maovu.”—Yer. 5:28.
7. Ni kwa njia gani watu wengi katika Jumuiya Wakristo wanafanana na waliokuwa katika Yerusalemu wa siku za Yeremia?
7 Wakati wa Yeremia, wingi wa watu walichagua kuendelea kuiunga mkono taratibu iliyokuwa imehukumiwa maangamizi. Waliupenda udanganyifu, upotovu na uasherati wake. Je! hivyo sivyo walivyo watu wengi leo katika Jumuiya ya Wakristo? Yehova anaonyesha hukumu yake:
“Je! nisiwapatilize kwa mambo hayo? asema [Yehova]; na nafsi yangu, je! nisijilipize kisasi juu ya taifa la namna hii? Jambo la ajabu, la kuchukiza, limetokea katika nchi hii! Manabii wanatabiri uongo, na makuhani wanatawala kwa msaada wa hao; na watu wangu wanapenda mambo yawe hivyo.” (Yer. 5:29-31)
Waache viongozi wa dini waendelee kuyahubiri mambo ya uongo ya Kibabeli. Waache wawaunge sana mkono wanasiasa wapotovu. Waache wawaachilie watu wafanye uasherati ovyo ovyo tu, wawaachilie wanaume na wanawake walalane na wenzao, wacheze kamari na kufanya mazoea mengine yanayokatazwa na Neno la Mungu. Huenda wingi wa watu wakapendezwa sana na mambo hayo. Huenda watu wengi ‘wakapenda mambo yawe hivyo.’ Lakini Mungu anasema kwamba karibuni sana atawahukumu kwa sababu ya unafiki wote huo wa kidini.
8. Maangamizi ya Shilo ni unabii wa kitu gani? (ye 7:12)
8 Wakati wa waamuzi wa kwanza wa Israeli, hema na sanduku la Yehova lilikuwako Shilo. Lakini makuhani waliachilia sana mambo mabaya na uasherati mpaka Yehova ‘akawapatiliza’ kwa mambo hayo. Israeli walishindwa kabisa na Wafilisti, sanduku likachukuliwa halafu Eli kuhani mkuu akafa pamoja na wana wake waasherati. (1 Sam. 2:12-29; 4:2-18; 3:10-14)
-