Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w93 6/1 kur. 8-13
  • Kumtumikia Yehova kwa Roho ya Kujidhabihu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kumtumikia Yehova kwa Roho ya Kujidhabihu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Mtu Ye Yote Akitaka Kunifuata”
  • Kuza na Kudumisha Ile Roho ya Kujidhabihu ya Yesu
  • Kujidhabihu Kunaleta Baraka Nyingi
  • Kuishi Si Kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Mfuate Yesu kwa Kuendelea
    Huduma Yetu ya Ufalme—1997
  • Je! Wewe Unajifurahisha Ana Nyingi Mno—Ama Unajinyima?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
  • Kwa Nini Uwe Mwenye Kujitolea?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
w93 6/1 kur. 8-13

Kumtumikia Yehova kwa Roho ya Kujidhabihu

“Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake [mti wake wa mateso, NW], anifuate.”—MATHAYO 16:24.

1. Yesu aliwaarifuje wanafunzi wake kuhusu kifo chake kilichokuwa kikikaribia?

KARIBU na Mlima Hermoni wenye theluji, Yesu Kristo afikia hatua kuu maishani mwake. Yeye ana muda unaopungua mwaka mmoja wa kuishi. Anajua hilo; wanafunzi wake hawajui hilo. Wakati wao wa kujua hilo umefika. Ni kweli kwamba, kabla ya hapo Yesu ametaja kifo chake kinachokaribia, lakini hii ni mara yake ya kwanza kusema waziwazi juu yacho. (Mathayo 9:15; 12:40) Usimulizi wa Mathayo wasomwa hivi: “Tangu wakati huo Yesu alianza kuwaonya wanafunzi wake ya kwamba imempasa kwenda Yerusalemu, na kupata mateso mengi kwa wazee na wakuu wa makuhani, na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu kufufuka.”—Mathayo 16:21; Marko 8:31, 32.

2. Itikio la Petro lilikuwa nini kwa maneno ya Yesu kuhusu kuteseka Kwake kwa wakati ujao, na Yesu aliitikiaje?

2 Ni muda mfupi ambao umebaki kabla ya Yesu kufa. Lakini Petro, akasirishwa na wazo hilo lionekanalo kuwa lenye kuhofisha sana. Hawezi kukubali kwamba kwa kweli Mesiya atauawa. Kwa hiyo, Petro athubutu kumkemea Bwana-Mkubwa wake. Akichochewa na nia njema kabisa, yeye asihi hivi bila kufikiri: “Hasha, [ujihurumie, NW] Bwana, hayo hayatakupata.” Lakini mara hiyo Yesu alikatalia mbali fadhili ya Petro isiyofaa, kwa hakika kama vile mtu angeponda kichwa cha nyoka mwenye sumu. “Nenda nyuma yangu, Shetani; u kikwazo kwangu; maana huyawazi yaliyo ya Mungu, bali ya wanadamu.”—Mathayo 16:22, 23.

3. (a) Petro alijifanyaje mwakilishi wa Shetani bila kukusudia? (b) Petro alikuwaje kikwazo kwa mwendo wa kujidhabihu?

3 Bila kukusudia Petro amejifanya mwenyewe mwakilishi wa Shetani. Jibu kali la Yesu ni lenye kukata maneno kama vile alivyomjibu Shetani jangwani. Huko Ibilisi alijaribu kumshawishi Yesu awe na maisha ya starehe, awe na ufalme bila kuteseka. (Mathayo 4:1-10) Sasa Petro amtia moyo ajihurumie. Yesu ajua kwamba hayo si mapenzi ya Baba yake. Ni lazima maisha yake yawe ya kujidhabihu, si ya kujitosheleza. (Mathayo 20:28) Petro anakuwa kikwazo kwa mwendo huo; huruma yake yenye nia njema inakuwa mtego.a Lakini, Yesu aona kwa wazi kwamba ikiwa angekuwa na wazo lolote la maisha bila kujidhabihu, angepoteza upendeleo wa Mungu kwa kunaswa katika mtego wa kishetani wa kuleta kifo.

4. Kwa nini Yesu hakujitakia wala kuwatakia wafuasi wake maisha ya starehe ya kula raha?

4 Kwa hiyo, fikira za Petro zilihitaji kurekebishwa. Maneno yake kwa Yesu yaliwakilisha wazo la mwanadamu, si la Mungu. Maisha ya starehe ya kula raha, njia rahisi ya kuepuka kuteseka, hayakuwa ya Yesu; wala wafuasi wa Yesu hawangekuwa na maisha kama hayo, kwani Yesu aendelea kumwambia Petro na wale wanafunzi wengine hivi: “Mtu ye yote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake [mti wake wa mateso, NW], anifuate [daima, NW].”—Mathayo 16:24.

5. (a) Ni nini ugumu wa kuishi maisha ya Kikristo? (b) Mkristo apaswa kuwa tayari kwa ajili ya mambo gani matatu?

5 Tena na tena, Yesu arudia kichwa hiki kikuu cha habari: ugumu wa kuishi maisha ya Kikristo. Ili kuwa wafuasi wa Yesu, ni lazima Wakristo, kama vile Kiongozi wao, wamtumikie Yehova kwa roho ya kujidhabihu. (Mathayo 10:37-39) Hivyo, yeye atoa orodha ya mambo matatu ya lazima ambayo Mkristo apaswa kuwa tayari kufanya: (1) kujikana mwenyewe, (2) kujitwika mti wake wa mateso, na (3) kumfuata Yeye daima.

“Mtu Ye Yote Akitaka Kunifuata”

6. (a) Mtu anajikanaje? (b) Tunapaswa kumpendeza zaidi nani kuliko kujipendeza wenyewe?

6 Kujikana mwenyewe kunamaanisha nini? Kunamaanisha kwamba mtu anapaswa ajikane mwenyewe kabisa, aina fulani ya kifo kwa binafsi. Maana ya msingi ya neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ajikane” ni “kusema la”; linamaanisha “kukana kabisa.” Kwa hiyo ukikubali ugumu wa maisha ya Kikristo, utakuwa na nia ya kusalimisha mapendezi, starehe, tamaa, furaha, anasa zako mwenyewe. Kwa kweli, unamtolea Yehova Mungu maisha yako yote na yote yanayohusiana nayo kwa wakati wote. Kujikana kunamaanisha zaidi ya kujinyima anasa fulani-fulani mara kwa mara. Bali, kunamaanisha kwamba ni lazima mtu ajitoe kwa Yehova kuwa mali Yake. (1 Wakorintho 6:19, 20) Mtu ambaye amejikana huishi ili kumpendeza Mungu, wala si kujipendeza mwenyewe. (Warumi 14:8; 15:3) Kunamaanisha kwamba kila wakati maishani mwake, yeye husema la kwa tamaa zenye ubinafsi, na kusema ndiyo kwa Yehova.

7. Mti wa mateso wa Mkristo ni nini, na yeye huuchukuaje?

7 Kwa hiyo, kujitwika mti wako wa mateso, kuna maana yenye uzito. Kuchukua mti ni mzigo wenye kulemea na ni ufananisho wa kifo. Mkristo ana nia ya kuteseka inapohitajiwa, au kuaibishwa, au kuteswa au hata kuuawa kwa sababu ya kuwa mfuasi wa Yesu Kristo. Yesu alisema hivi: “Mtu asiyechukua msalaba wake [mti wake wa mateso, NW] akanifuata, hanistahili.” (Mathayo 10:38) Si wote wenye kuteseka wanaouchukua mti wa mateso. Waovu wana “mapigo” mengi lakini hawana mti wa mateso. (Zaburi 32:10) Hata hivyo, maisha ya Mkristo ni ya kuchukua mti wa mateso wa utumishi wa kujidhabihu kwa Yehova.

8. Yesu aliwawekea wafuasi wake kigezo kipi cha maisha?

8 Takwa la mwisho lililotajwa na Yesu ni kwamba tumfuate daima. Yesu hataki tu tukubali na kuamini yale aliyofundisha bali pia, kwa maisha yetu yote, tufuate daima kile kigezo alichoweka. Na ni zipi zile sehemu kuu zinazoonwa katika kigezo chake cha maisha? Alipowapa wafuasi wake utume wao wa mwisho, alisema hivi: “Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi . . . , na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Yesu alihubiri na kufundisha habari njema za Ufalme. Ndivyo wanafunzi wake wa karibu walivyofanya pia na hata, lile kundi zima la Kikristo la mapema. Utendaji huo wenye bidii pamoja na kutokuwa kwao sehemu ya ulimwengu kulileta juu yao chuki na upinzani wa ulimwengu, uliosababisha mti wao wa mateso uwe mzito hata zaidi kuchukua.—Yohana 15:19, 20; Matendo 8:4.

9. Yesu aliwatendeaje watu wengine?

9 Kigezo kingine mashuhuri kinachoonwa katika maisha ya Yesu ni njia ambayo aliwatendea watu wengine. Alikuwa mwenye fadhili na “mpole na mnyenyekevu wa moyo.” Hivyo, wasikilizaji wake walihisi wakifanywa wapya katika roho na walitiwa moyo na kuwapo kwake. (Mathayo 11:29) Hakuwakandamiza wamfuate au kuwapa amri moja baada ya nyingine kuhusu jinsi ambavyo wangefanya hivyo; wala hakuchochea hisi za kuwa na hatia ili kuwalazimisha kuwa wanafunzi wake. Yajapokuwa maisha yao ya kujidhabihu, walionyesha shangwe ya kweli. Hiyo ni tofauti kama nini na wale wenye roho ya kilimwengu ya kula raha inayotia alama “siku za mwisho”!—2 Timotheo 3:1-4.

Kuza na Kudumisha Ile Roho ya Kujidhabihu ya Yesu

10. (a) Kulingana na Wafilipi 2:5-8, Kristo alijikanaje? (b) Ikiwa sisi ni wafuasi wa Kristo, tunapaswa kuonyesha nia gani ya akilini?

10 Yesu aliweka mfano katika kujikana. Alijitwika mti wake wa mateso akauchukua daima kwa kufanya mapenzi ya Baba yake. Paulo aliwaandikia Wakristo katika Filipi hivi: “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba [mti wa mateso, NW].” (Wafilipi 2:5-8) Ni nani angeweza kujikana kikamili zaidi ya hivyo? Ikiwa wewe ni mali ya Kristo Yesu nawe ni mmoja wa wafuasi wake, ni lazima uwe na nia iyo hiyo.

11. Kuishi maisha ya kujidhabihu kunamaanisha kuishi kwa ajili ya mapenzi ya nani?

11 Mtume mwingine, Petro, atuambia kwamba kwa kuwa Yesu aliteseka na kufa kwa ajili yetu, Wakristo wanapaswa kujivika silaha, kama vile wanajeshi ambao wamejitayarisha vizuri, wakiwa na roho ileile ambayo Kristo alikuwa nayo. Yeye aandika hivi: “Basi kwa kuwa Kristo aliteswa katika mwili wake, ninyi nanyi jivikeni silaha ya nia ile ile; kwa maana yeye aliyeteswa katika mwili ameachana na dhambi. Tangu sasa msiendelee kuishi katika tamaa za wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wenu uliobaki wa kukaa hapa duniani.” (1 Petro 3:18; 4:1, 2) Mwendo wa Yesu wa kujidhabihu ulionyesha kwa wazi jinsi alivyohisi juu ya mapenzi ya Mungu. Alikaza akili zake zote katika ujitoaji, akiweka sikuzote mapenzi ya Baba yake juu ya mapenzi yake mwenyewe, hata kufikia hatua ya kifo cha aibu.—Mathayo 6:10; Luka 22:42.

12. Je! maisha ya kujidhabihu yalimchukiza Yesu? Eleza.

12 Ingawa maisha ya Yesu ya kujidhabihu yalikuwa mwendo wenye kuchosha na ulio mgumu kwake kufuata, hakuyaona kuwa yenye kuchukiza. Bali, Yesu alifurahia kujitiisha mwenyewe kwa mapenzi ya kimungu. Kwake, kufanya kazi ya Baba yake kulikuwa kama chakula. Alitosheka kikweli kutokana nayo, jinsi ambavyo mtu angetoshelezwa na mlo mzuri. (Mathayo 4:4; Yohana 4:34) Hivyo, ikiwa wataka kuhisi umetosheka maishani mwako, jambo bora zaidi la kufanya ni kufuata kielelezo cha Yesu kwa kukuza nia yake ya akilini.

13. Upendo ni kani inayochochea roho ya kujidhabihu jinsi gani?

13 Kwa kweli, ni kani gani inayochochea roho ya kujidhabihu? Kwa neno moja, upendo. Yesu alisema: “Mpende Bwana [Yehova, NW] Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako.” (Mathayo 22:37-39) Mkristo hawezi kuwa akijitafutia mambo yake mwenyewe na, wakati uo huo, akiyatii maneno hayo. Furaha na mapendezi yake mwenyewe yanapasa kuongozwa kwanza kabisa na upendo wake kwa Yehova na kisha na upendo wake kwa jirani. Ndivyo Yesu alivyoishi maisha yake, na ndivyo anavyowatazamia wafuasi wake waishi.

14. (a) Ni madaraka gani yanayoelezwa kwenye Waebrania 13:15, 16? (b) Ni nini kinachotusukuma tuhubiri habari njema kwa bidii?

14 Mtume Paulo alielewa sheria hiyo ya upendo. Aliandika hivi: “Kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake. Lakini msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizo ndizo zimpendezazo Mungu.” (Waebrania 13:15, 16) Wakristo hawamtolei Yehova dhabihu za wanyama au dhabihu za jinsi hiyo; kwa hiyo, hawahitaji makuhani wa kibinadamu kwenye hekalu halisi kuisimamia ibada yao. Dhabihu yetu ya sifa hutolewa kupitia Kristo Yesu. Na hasa ni kupitia dhabihu hiyo ya sifa, lile julisho la wazi la jina lake, kwamba tunaonyesha kumpenda kwetu Mungu. Hasa roho yetu isiyo na ubinafsi yenye msingi wa upendo ndiyo ambayo hutuchochea kuhubiri habari njema kwa bidii, sikuzote tukijitahidi kuwa wenye hamu ya kumtolea Mungu tunda la midomo yetu. Katika njia hiyo tunaonyesha upendo kwa jirani pia.

Kujidhabihu Kunaleta Baraka Nyingi

15. Tunaweza kujiuliza maswali gani ya kujichunguza kuhusu kujidhabihu?

15 Tua kidogo ukafikirie maswali yafuatayo: Je! kigezo cha sasa cha maisha yangu kinaonyesha mwendo wa kujidhabihu? Je! miradi yangu huonyesha maisha ya jinsi hiyo? Je! washiriki wa familia yangu wanavuna faida za kiroho kutokana na kielelezo changu? (Linganisha 1 Timotheo 5:8.) Namna gani yatima na wajane? Je! wao pia hufaidika kutokana na roho yangu ya kujidhabihu? (Yakobo 1:27) Je! ninaweza kupanua wakati ninaotumia katika dhabihu yangu ya sifa ya hadharani? Je! ninaweza kufikia lile pendeleo la utumishi wa painia, Betheli, au mishonari, au naweza kuhama ili kutumikia katika eneo ambamo uhitaji ni mkubwa zaidi wa wapiga mbiu ya Ufalme?

16. Kutumia akili zaidi kunaweza kutusaidiaje kuishi maisha ya kujidhabihu?

16 Nyakati nyingine tunahitaji tu kutumia akili yetu zaidi ili kufikia uwezo wetu kamili katika kumtumikia Yehova kwa roho ya kujidhabihu. Kwa kielelezo, Janet, painia mmoja wa kawaida katika Ekwedori, alifanya kazi ya kimwili ya wakati wote. Upesi, ratiba yake ilifanya iwe vigumu kwake kutimiza matakwa ya saa za upainia wa kawaida kwa roho yenye uchangamfu. Aliamua kueleza tatizo hilo kwa mwajiri wake akaomba apunguziwe saa za kufanya kazi. Kwa kuwa mwajiri wake hakuwa na nia ya kupunguza wakati wake wa kazi, baadaye aliandamana na Maria aliyekuwa akitafuta kazi ya muda-muda ili aweze kufanya upainia. Kila mmoja wao alijitolea kufanya kazi ya nusu siku, wakishiriki kazi ya siku nzima. Mwajiri huyo alikubali pendekezo hilo. Sasa akina dada hao wawili ni mapainia wa kawaida. Alipoona tokeo hilo zuri ajabu, Kaffa, ambaye pia alikuwa amechoka na kufanyia kampuni iyo hiyo kazi ya wakat na kung’anga’na ili aendelee kutimiza wakati wa upainia wake, aliandamana na Magali akatoa pendekezo ilo hilo. Hilo lilikubaliwa pia. Hivyo, akina dada wanne wanaweza kufanya upainia, badala ya wawili ambao walikuwa wamefikia hatua ya kuacha utumishi wa wakati wote. Kutumia akili na kuchukua hatua ya kwanza kulikuwa na matokeo yenye mafaa.

17-21. Wenzi wawili wa ndoa walikadiriaje upya kusudi lao maishani, kukiwa na tokeo gani?

17 Zaidi ya hayo, fikiria mwendo wa kujidhabihu uliofuatwa na Evonne kwa muda wa miaka kumi iliyopita. Aliandika yafuatayo kwa Watch Tower Society katika Mei 1991:

18 “Katika Oktoba 1982, familia yangu na mimi tulitalii Betheli ya Brooklyn. Kuiona kulinifanya nitake kujitolea kufanya kazi huko. Nilisoma ombi moja, na kulikuwako swali moja lenye kutokeza, ‘Ni nini saa zako za wastani katika utumishi wa shambani kwa miezi sita iliyopita? Ikiwa saa za wastani ni chini ya kumi, eleza ni kwa nini.’ Sikuweza kufikiria sababu yoyote halali [kwa saa zangu za chini], kwa hiyo niliweka mradi nikaufikia kwa miezi mitano.

19 “Ingawa ningeweza kufikiria udhuru fulani-fulani mchache wa kutofanya upaina, niliposoma 1983 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, nilikuwa nimesadikishwa kwamba wengine walikuwa wameshinda vizuizi vikubwa zaidi kuliko vyangu ili kufanya upainia. Kwa hiyo, katika Aprili 1, 1983, niliacha kazi yangu yenye kuleta faida nyingi nikawa painia msaidizi, na kujiunga na mapainia wa kawaida katika Septemba 1, 1983.

20 “Nilifurahia kuolewa na mtumishi wa huduma mwema katika Aprili 1985. Miaka mitatu baadaye, hotuba moja ya mkusanyiko wa wilaya kuhusu kufanya upainia ilimsukuma mume wangu anisemee sikioni na kuniuliza, ‘Je! waona sababu sipaswi kuanza kufanya upainia kufikia Septemba 1?’ Alijiunga na mimi katika kazi hiyo kwa miaka miwili iliyofuata.

21 “Mume wangu alijitolea pia kufanya kazi ya ujenzi kwenye Betheli ya Brooklyn kwa majuma mawili na akatoa ombi la kushiriki katika Programu ya Ujenzi ya Kimataifa. Kwa hiyo katika Mei 1989 tulikwenda Naijeria kwa mwezi mmoja kusaidia katika ujenzi wa tawi. Kesho tutasafiri kwenda Ujerumani, ambako viza vitapangwa ili tuweze kuingia Polandi. Tunasisimuka kushiriki katika mradi wa ujenzi wa maana na wenye kukumbukwa kama huo na kuwa sehemu ya aina hiyo mpya ya utumishi wa wakati wote.”

22. (a) Tungewezaje, kama vile Petro, kuwa kikwazo bila kukusudia? (b) Kumtumikia Yehova kwa roho ya kujidhabihu hakutegemei nini?

22 Ikiwa wewe mwenyewe huwezi kufanya upainia, je, waweza kuwatia moyo wale waliomo katika utumishi wa wakati wote washikilie pendeleo lao na labda hata kuwasaidia wafanye hivyo? Au, je, utakuwa kama washiriki wa familia au marafiki wengine wenye nia njema, ambao kama vile Petro, huenda wakamwambia mtumishi wa wakati wote apumzike na kuishi kwa starehe, ajihurumie, bila kutambua jinsi hicho kiwezavyo kuwa kikwazo? Ni kweli, ikiwa afya ya painia imo hatarini sana au kama anapuuza wajibu wake mbalimbali wa Kikristo, huenda akalazimika kuacha utumishi wa wakati wote kwa muda fulani. Kumtumikia Yehova kwa roho ya kujidhabihu hakutegemei jina fulani, kama vile painia, Mwanabetheli, au jingine. Bali, kunategemea jinsi tulivyo tukiwa watu—jinsi tunavyofikiri, yale tunayofanya, na jinsi tunavyowatendea wengine, jinsi tunavyoishi maisha yetu.

23. (a) Tunaweza kuendeleaje kuwa na shangwe ya kuwa wafanyakazi pamoja na Mungu? (b) Tunapata uhakikishio gani kwenye Waebrania 6:10-12?

23 Ikiwa kwa kweli tuna roho ya kujidhabihu, tutakuwa na shangwe ya kuwa wafanyakazi pamoja na Mungu. (1 Wakorintho 3:9) Tutakuwa na uradhi wa kujua kwamba tunafanya moyo wa Yehova ushangilie. (Mithali 27:11) Na tuna uhakikishio wa kwamba Yehova hatatusahau kamwe wala kutuacha maadamu twaendelea kuwa waaminifu kwake.—Waebrania 6:10-12.

[Maelezo ya Chini]

a Katika Kigiriki, mwanzoni “kikwazo” (σκάνδαλον, skanʹda·lon) lilikuwa “jina la sehemu ya mtego ambapo chambo kinashikanishwa, kwa hiyo, mtego au tanzi yenyewe.”—Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words.

Maoni Yako ni Nini?

◻ Petro alikujaje kuwa kikwazo kwa mwendo wa kujidhabihu bila kukusudia?

◻ Kujikana kunamaanisha nini?

◻ Mkristo huchukuaje mti wake wa mateso?

◻ Sisi hukuzaje na kudumisha roho ya kujidhabihu?

◻ Ni kani gani inayochochea roho ya kujidhabihu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je! una nia ya kujikana, kujitwika mti wako wa mateso, na kumfuata Yesu daima?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki