Mtegemee Yehova Akuze Vitu
1 “Kwa mara ya kwanza nilipata shangwe ya pekee ya kusaidia kuanzisha kutaniko jipya. Hilo lilichukua zaidi ya miaka miwili ya kazi yenye juhudi, sala za daima na utegemeo kwa Yehova ‘akuzaye vitu.’” Ndivyo alivyoandika painia mmoja mwenye kudhamiria ambaye alijifunza uhitaji wa kumtegemea Yehova kwa ajili ya ukuzi. (1 Kor. 3:5-9) Katika kutafuta kwetu watu wenye mwelekeo wa kiroho, sisi pia twahitaji tegemezo la Mungu ili huduma yetu izae matunda.—Mit. 3:5, 6.
2 Ukuzi Wahitaji Kupalilia: Mbegu ya kweli yahitaji kupaliliwa ili ikue. Kurudi tena siku moja au mbili baada ya ziara ya kwanza hutokeza matokeo mazuri. Uwe mchangamfu na mwenye urafiki. Mfanye yule mtu mwingine astarehe. Usiongee wewe pekee tu. Mruhusu akujue, na umwonyeshe kwamba unapendezwa naye akiwa mtu.
3 Mwezi wa Julai na kuendelea hadi Agosti, tutakazia fikira kutolea watu tunaokutana nao broshua mbalimbali. Hata hivyo, twahitaji pia kufuatia kupendezwa kunakopatikana na maangusho yanayofanywa. Twafanya hivyo kwa kufanya ziara za kurudia na kutoa mafunzo ya Biblia. (Mt. 28:19, 20) Tukiwa na lengo hilo, broshua Anataka yaweza kutumiwa kuanzisha mafunzo. Huenda ukaona madokezo manne yafuatayo kuwa yenye msaada.
4 Ikiwa uliongea na mtu ambaye anahangaikia unakoelekea ulimwengu, unaweza kufanya upya mazungumzo kwa kusema:
◼ “Naamini kwamba unahangaika kama mimi kuhusu mvunjiko wa maadili katika jamii ya binadamu. Twasikia ripoti zenye kutaabisha za jeuri ya nyumbani, inayosababisha kutendwa vibaya kwa watoto, wazazi, na wenzi wa ndoa. Na yaonekana kwamba watu wengi hawaoni ubaya katika kudanganya au kuiba ili kutimiza tamaa zao tu. Je, wafikiri Mungu anajali vile watu huishi maisha zao? [Ruhusu itikio.] Mungu aliwekea mwanadamu viwango kadhaa ili aishi kupatana navyo, navyo kwa kweli si mzigo wenye kutulemea.” Soma 1 Yohana 5:3. Kisha toa broshua Anataka, na uifungue kwenye somo la 10. Soma fungu la kwanza. Onyesha maneno na vifungu vya maneno yaliyochapwa kwa herufi za mlazo mwanzoni mwa fungu la 2-6, na umwulize mwenye nyumba zoea ambalo yeye anahisi ni lenye madhara sana kwa jamii. Soma fungu linalohusiana nalo na mchunguze andiko moja au mawili fursa ikiruhusu. Malizia kwa kusoma fungu la 7, kisha ufanye mipango ya kurudi tena kwa mazungumzo zaidi.
5 Kwa wale uliokuta ambao wanahangaikia mambo ya familia, unaweza kusema hivi:
◼ “Je, wafikiri ni jambo la kiakili kutazamia kwamba Muumba angetupatia sisi vyombo tunavyohitaji kujengea maisha ya familia yenye mafanikio?” Ruhusu itikio. Toa broshua Anataka, fungua somo la 8, na ueleze kwamba ina kanuni za Biblia kwa kila mshiriki wa familia. Jitolee kuonyesha jinsi ya kutumia broshua hiyo pamoja na Biblia ili kupata manufaa nyingi zaidi kutokana nayo. Fuata maagizo ambayo yanapatikana kwenye ukurasa wa 2 wa broshua hiyo. Fanya mipango ya kurudi tena ili mwendelee na funzo la somo hilo, au mkilimaliza, mjifunze somo jingine ambalo mwenye nyumba anachagua katika broshua hiyo.
6 Huu ni mfikio wa moja kwa moja unaoweza kutumia ili kutoa programu ya funzo la Biblia. Onyesha broshua “Anataka,” na useme hivi:
◼ “Broshua hii ina mtaala wa funzo wenye kuhusisha mambo mengi, unaoshughulikia mafundisho ya msingi ya Biblia. Katika kila ukurasa, utapata majibu kwa maswali ambayo yametaabisha watu wengi kwa karne kadhaa. Kwa mfano, Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia?” Fungua somo la 5, na usome maswali yaliyo mwanzoni mwa somo hilo. Mwulize mwenye nyumba ni somo gani linalompendeza zaidi, kisha usome fungu au mafungu yanayolingana, mkichunguza maandiko yanayolihusu. Eleza kwamba majibu yenye kuridhisha kwa maswali mengine yanaweza kupatikana kwa urahisi tu kama hili. Dokeza urudi tena ili mzungumzie swali na jibu jingine.
7 Au huenda ukapendelea kujaribu mfikio sahili wa kuanzisha funzo la Biblia kwa kusema hivi:
◼ “Je, ulipata kujua kwamba kwa kuchukua dakika chache tu, unaweza kupata jibu kwa swali la maana la Biblia? Kwa mfano, . . . ” Kisha taja swali ambalo lapatikana mwanzoni mwa mojawapo ya masomo yaliyo katika broshua, lile ambalo unafikiri lingempendeza mtu huyo. Ili kupata mawazo fulani ya maswali ambayo huenda ukawa nayo, ona fungu la 15 na 16 katika nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Machi 1997, yenye kichwa: “Jipe Ujasiri wa Kufanya Ziara za Kurudia.”
8 Kukubali kwa shangwe ugumu wa kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Bibilia ni sehemu ya kuwa “wafanyakazi wenzi” wa Mungu. (1 Kor. 3:9) Tujitahidipo kusitawisha kupendezwa tunakopata kisha kumtegemea Yehova akuze vitu, tutaona uradhi halisi ambao hakuna kazi nyingine iwezayo kutokeza.