Jinsi ya Kutumia Kitabu “Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko”
Njia ya kufuatwa tunapowasaidia wengine waifahamu Biblia ni ile ambayo Yesu Kristo na mitume wake waliitumia. Katika kujibu maswali, Yesu alinukuu maandiko na wakati mwingine alitumia mifano inayofaa ambayo ingewasaidia watu wenye mioyo minyoofu wapokee mambo ambayo Biblia inasema. (Mt. 12:1-12) Mtume Paulo alikuwa na zoea la ‘kujadiliana akitumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo’ mambo aliyofundisha. (Mdo. 17:2, 3) Habari zilizo katika kitabu hiki zinaweza kukusaidia ufanye vivyo hivyo.
Badala ya kuzungumzia kirefu na kwa ujumla kila kichwa, kitabu hiki Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kinaelekeza fikira hasa kwenye maswali ambayo watu wengi wanauliza leo.
Kitabu hiki hakikuandikwa kwa kusudi la kumsaidia mtu “ashinde mabishano” anapozungumza na watu ambao hawaiheshimu kweli. Badala yake, kinatoa habari yenye thamani ambayo imekusudiwa itumiwe katika kuwapa sababu watu ambao watakuruhusu ufanye hivyo. Huenda wengine kati yao wakauliza maswali ambayo wanataka sana kujibiwa kwa njia yenye kuridhisha. Wengine, wakati wa mazungumzo, huenda wakaeleza tu imani zao nao huenda wakafanya hivyo wakiwa na usadikisho kiasi fulani. Lakini je, wao ni watu wenye usawaziko ambao wako tayari kusikiliza maoni tofauti? Ikiwa ndivyo, unaweza kuzungumza pamoja nao mambo ambayo Biblia inasema, na ufanye hivyo ukisadiki kwamba habari hizo zitapokewa katika mioyo ya watu wanaopenda kweli.
Katika kitabu hiki, unaweza kupataje habari hususa unayohitaji? Mara nyingi utaipata kwa urahisi kwa kufungua moja kwa moja kichwa kilicho na habari zinazozungumziwa. Chini ya vichwa vyote vikuu, ni rahisi kuyapata maswali makuu; yameandikwa kwa maandishi manene yanayolingana na pambizo la kushoto. Usipopata haraka habari unayohitaji, angalia Fahirisi upande wa nyuma wa kitabu.
Ni vizuri sikuzote kufanya matayarisho mapema kwa ajili ya mazungumzo. Lakini kama hujazoelea sehemu fulani za kitabu hiki, bado unaweza kuzitumia vizuri. Jinsi gani? Unapopata swali linalolingana na jambo unalotaka kuzungumzia, tazama vichwa vidogo vyovyote vilivyo chini yake. Vichwa hivyo vidogo vimeandikwa kwa maandishi manene ya mlazo, navyo vimeingizwa ndani kidogo chini ya maswali yanayohusiana navyo. Ikiwa tayari unazijua habari zinazozungumziwa, huenda ukahitaji tu kuvirudia vichwa hivyo vidogo na kuyatupia jicho mawazo fulani yaliyo chini yake, kwa kuwa yana muhtasari wa sababu zinazoweza kutumiwa. Usisite kueleza habari hizo ukitumia maneno yako mwenyewe.
Je, unaona kwamba unahitaji habari zaidi—labda maandiko yenyewe, sababu za kutumia kuambatana na maandiko hayo, mifano fulani ya kukusaidia ufafanue wazi uzuri wa yale ambayo Biblia inasema, na kadhalika? Ikiwa ndivyo, labda unaweza kumwonyesha mtu unayezungumza naye mambo yaliyo katika kitabu hiki kisha msome pamoja sehemu inayoshughulika na swali ambalo ameuliza. Hata kama hujasoma habari hizo mapema, unaweza kuzitumia kutoa jibu linaloridhisha. Kila jambo limo ndani ya kitabu hiki, likiwa limeelezwa kwa urahisi na kwa ufupi.
Kumbuka kwamba kitabu hiki ni kifaa cha kukusaidia tu. Biblia ndiyo mamlaka. Hiyo ndiyo Neno la Mungu. Ikiwa manukuu yaliyo katika kitabu hiki yametoka katika Biblia, kazia jambo hilo katika akili za wale unaosema nao. Inapowezekana, waombe wachukue Biblia yao na wafungue maandiko hayo ili waone kwamba yale unayosema kwa hakika yamo ndani ya Biblia yao wenyewe. Ikiwa tafsiri fulani za Biblia zinazotumiwa na watu wengi zinatafsiri mistari fulani kwa njia tofauti, mara nyingi fikira huelekezwa kwenye jambo hilo, na tafsiri mbalimbali zimenukuliwa kwa kusudi la kulinganisha.
Kupatana na mfano ambao mtume Paulo aliweka katika kuitaja ile madhabahu yenye maandishi “Kwa Mungu Asiyejulikana” na katika kunukuu habari fulani za kilimwengu ambazo zilikubaliwa na watu wengi alipokuwa akiwahubiria Waathene (Mdo. 17:22-28), kitabu hiki kinatumia kwa kiasi habari zilizonukuliwa kutoka katika historia ya kilimwengu, ensaiklopidia, vitabu vya marejeo vya kidini, na kamusi za lugha ya Biblia. Basi, badala ya kusisitiza chanzo cha mazoea ya kidini ya uwongo, kusitawi kwa mafundisho fulani, na maana ya maneno ya Kiebrania na Kigiriki, kitabu hiki kinaonyesha sababu za maneno yaliyosemwa. Hata hivyo, kinaelekeza fikira kwenye Biblia kuwa ndiyo chanzo cha msingi cha kweli.
Ili kukusaidia zaidi kutayarisha njia ya kushiriki kweli ya Biblia pamoja na wengine, sehemu za mwanzo za kitabu hiki zina orodha ya “Matangulizi ya Kutumia Katika Huduma ya Shambani” na mkusanyo wa mapendekezo kuhusu “Jinsi Unavyoweza Kujibu Vizuia-Mazungumzo Vikitokea.” “Vizuia-mazungumzo” vingine vingi vinavyoweza kutokea vinahusiana na imani fulani, na hivyo vimezungumziwa mwishoni mwa kila moja ya sehemu kuu zinazoshughulika na imani hizo. Haikusudiwi kwamba ukariri moyoni majibu hayo, lakini bila shaka utaona inasaidia kuchanganua sababu gani wengine wameyaona kuwa yenye matokeo; kisha useme mawazo hayo kwa kutumia maneno yako mwenyewe.
Kutumia kitabu hiki kutakusaidia usitawishe uwezo wa kutoa sababu kwa kutumia Maandiko na kuyatumia kwa matokeo katika kuwasaidia wengine wajifunze “mambo makuu ya Mungu.”—Mdo. 2:11.