“Fulizeni Kufanya Hili Katika Ukumbuko Wangu”
1 Wanadamu huelekea kuacha umaana wa mambo ufifie kwa kipindi fulani cha muda. Hii ndiyo sababu moja ambayo, alipokuwa akianzisha “mlo wa jioni wa Bwana,” Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” Tangu wakati huo, katika siku ya ukumbusho wa kifo cha Yesu, Wakristo kwa kutii wamefuliza “kutangaza kifo cha Bwana, mpaka awasilipo.”—1 Kor. 11:20, 23-26.
2 Sasa hivi karibuni sana, Yesu atapokea katika makao yake ya kimbingu wale wa mwisho kati ya mabaki ya “kundi dogo” wanaopungua. (Luka 12:32; Yn. 14:2, 3) Mwaka huu mabaki ya watiwa-mafuta pamoja na umati mkubwa wenye kuongezeka wa “kondoo wengine” watakuwa tena na pendeleo la kuadhimisha ule Mlo wa Jioni wa Bwana, Aprili 11. (Yn. 10:16; Ufu. 7:9, 10) Uthamini wa upendo mkubwa wa Yehova wa kumtuma Mwana mzaliwa-pekee kwa niaba ya wanadamu utaimarishwa. Mambo yatakayokaziwa yatakuwa kielelezo cha Yesu, upendo wake, uaminifu wake hadi kifo katika kuandaa fidia, na kutawala kwake sasa akiwa Mfalme wa Ufalme uliosimamishwa wa Mungu, na vilevile baraka ambazo Ufalme huo utaletea wanadamu. Kwa kweli litakuwa tukio la kukumbukwa!
3 Jitayarishe Sasa: Acheni sote tujitahidi kufanya majira haya ya Ukumbusho yawe shangwe kubwa na furaha kwetu na kwa wote watakaoshirikiana nasi. Twaweza kutayarisha mioyo yetu kwa kusoma tena masimulizi ya Biblia kuhusu siku chache za mwisho za huduma ya Yesu na matukio yaliyoongoza kwenye kifo chake. Funzo letu la familia majuma kadhaa kabla ya Ukumbusho laweza kuwa kupitia sura ya 112-116 ya kitabu Mtu Mkuu Zaidi.
4 Ni wangapi ujuao ambao huenda wakaja kwenye Ukumbusho ikiwa ungechukua hatua ya kwanza kujenga uthamini wao kuelekea pindi hii, kuwaalika, na kuwafanya wahisi wanahitajiwa? Andika orodha sasa, na ufanye uwezalo kuwasaidia waje. Baadaye, wasaidie wafulize kukua kiroho kwa kuwatia moyo wahudhurie mikutano kwa ukawaida.
5 Wakati wa majira ya Ukumbusho, mipango ya pekee itafanywa ya kuongeza fursa za kila mmoja za kuhubiri. Ukiratibu vizuri, je, waweza kufanya upainia-msaidizi Aprili? Mei? Mojawapo ya njia bora zaidi kuonyesha kwamba twakumbuka kwa kuthamini yote ambayo dhabihu ya Yesu yamaanisha kwetu, ni kuongea kuhusu Mungu wetu, Yehova, na baraka ambazo utawala wa Ufalme huo kupitia Mwana wake utaleta.—Zab. 79:13; 147:1.