Uthamini kwa Ndugu Zetu
“Kwa shauku ya kidugu isiyo ya kinafiki . . . , pendaneni mmoja na mwenzake kwa juhudi nyingi kutoka moyoni.”—1 PETRO 1:22, NW.
1. Ni nini kilichosadikisha watu wengi kwamba Mashahidi wa Yehova wanazoea Ukristo wa kweli?
UPENDO ndiyo chapa bora ya kutambulisha Ukristo wa kweli. Wakati wa mlo wa mwisho ambao Yesu alishiriki pamoja na mitume wake, yeye alikazia jambo hilo, akitaarifu hivi: “Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.” (Yohana 13:34, 35) Watu wengi walikuja kusadiki mara ya kwanza kwamba Mashahidi wa Yehova ndio wanaozoea Ukristo wa kweli wakati walipohudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme au walipoenda kwenye kusanyiko kubwa zaidi. Wao waliona upendo ukionyeshwa kwa kitendo, na kupitia jambo hilo wakajua kwamba wao walikuwa miongoni mwa wanafunzi wa kweli wa Kristo.
2. Mtume Paulo alisema nini kwa habari ya upendo, ile ishara yenye kupambanua Ukristo?
2 Sisi sote tunashangilia kwamba ishara hiyo yenye kupambanua Ukristo halisi inaonekana miongoni mwa watu wa Yehova leo. Hata hivyo, kama Wakristo wa mapema, sisi tunang’amua kwamba inatupasa tutafute daima njia za kudhihirisha uthamini kwa ndugu zetu. Paulo aliandika hivi kwa kundi katika Thesalonike: “Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi.” (1 Wathesalonike 3:12) Ni jinsi gani sisi tunaweza kuongezeka katika upendo wetu kwa mmoja na mwenzake?
Upendo na Shauku ya Kidugu
3. Kuongezea kuendesha maisha safi, mtume Petro alisema ni nini linalohitajiwa kabisa kwa Wakristo?
3 Katika barua moja ya ujumla iliyoelekezwa kwa makundi ya Kikristo katika Esia Ndogo, mtume Petro aliandika hivi: “Kwa kuwa sasa ninyi mmetakatisha nafsi [au, maisha] zenu kwa kutii kwenu ukweli mkiwa na shauku ya kidugu [phi·la·del·phiʹa] kama tokeo la kufanya hivyo, pendaneni [namna moja ya a·ga·paʹo] mmoja na mwenzake kwa juhudi nyingi sana kutoka moyoni.” (1 Petro 1:22, W) Petro anaonyesha kwamba haitoshi kutakatisha maisha zetu. Utii wetu kwa ule ukweli, kutia ndani ile amri mpya, unapasa kutokeza shauku ya kidugu isiyo ya kinafiki na upendo wa juhudi nyingi sana kwa mmoja na mwenzake.
4. Ni maswali gani tunayopaswa kuuliza, na Yesu alisema nini kuhusiana na jambo hilo?
4 Je! upendo na uthamini wetu kwa ndugu zetu una mbetuko wa kuonyeshwa kwa wale tu ambao sisi tunafurahishwa nao? Je! sisi tuna elekeo la kuwa wakarimu kuelekea hao, huku tukifunga macho yetu yasione makosa ya kupungukiwa kwao, hali tukifanya haraka kuona dosari na mapungukiwa ya wengine ambao sisi hatuhisi tukiwa na upendezo wa kiasili kwao? Yesu alisema hivi: “Mkiwapenda [namna moja ya a·ga·paʹo] wanaowapenda ninyi, mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! nao hawafanyi yayo hayo?”—Mathayo 5:46.
5. Ni upambanuzi gani ambao mwanachuo mmoja wa Biblia anafanya kati ya neno la Kigiriki linalomaanisha “upendo” na lile linalomaanisha “shauku”?
5 Katika kitabu chake New Testament Words, Profesa William Barclay anatoa maelezo yanayofuata juu ya neno la Kigiriki lililotafsiriwa “shauku” na lile lililofasiriwa “upendo”: “Kuna uchangamfu wa kuvutia kuhusiana na maneno haya [phi-li’a, linalomaanisha “shauku,” na kile kitenzi phi-le’o kinachohusiana nalo]. Yanamaanisha kufikiria mtu fulani kwa staha yenye shauku. Maneno ya kusema upendo ambayo yanapatikana kwa wingi sana kuliko mengineyo katika A[gano] J[ipya] ni ile nomino agape na kitenzi agapan. . . . Philia lilikuwa neno la kuvutia sana, lakini kwa uhakika lilikuwa neno la uchangamfu na ukaribiano na shauku. . . . Agape linahusiana na akili: si hisia inayotokeza katika mioyo yetu bila kuamshwa humo; ni kanuni ambayo sisi tunaishi kwayo kimakusudi. Agape linahusiana zaidi sana na nia. Ni ushindi wa kuzidia nguvu kitu chenye ukinzani, ushindi wa mafanikio, na utimizo wa mradi. Hakuna mmoja ambaye amepata kupenda adui zake kiasili. Kupenda adui za mmoja ni ushindi wa kuizidi nguvu mielekeo na mibetuko yetu ya kiasili na hisia-moyo zetu. Hiyo agape . . . kwa uhakika ni uwezo wa kupenda kisichopendeka, kupenda watu ambao sisi hatufurahii.”
6. (a) Ni maswali gani ya upekuzi tunayopaswa kujiuliza wenyewe? (b) Kulingana na Petro, kwa nini sisi hatuwezi kuweka hadi ya shauku yetu ya kidugu iwe kwa wale tu tunaovutiwa nao kiasili?
6 Je! sisi tuna mbetuko wa kutetea ukosefu wetu wa hisia kwa kuegemea kisingizio cha kwamba Maandiko yanaruhusu tuwe na hisia changamfu kwa akina ndugu fulani zaidi ya tulizo nazo kwa wengine? (Yohana 19:26; 20:2) Je! sisi tunafikiri tunaweza kuonyesha baadhi yao “upendo” baridi, wenye kutoka akilini tu kwa sababu ni sharti tufanye hivyo, huku tukiwahifadhia shauku changamfu ya kidugu wale ambao sisi tunavutiwa nao? Ikiwa ndivyo, tumeikosa maana ya himizo la Petro. Hatujatakatisha nafsi zetu vya kutosha kwa kutii ule ukweli, kwa maana Petro anasema: “Kwa kuwa sasa kupitia kutii ukweli ninyi mmetakatisha nafsi zenu mpaka mnahisi shauku ya moyo mweupe kuelekea Wakristo walio ndugu zenu, pendaneni mmoja na mwenzake kwa moyo wote kwa imara yenu yote.”—1 Petro 1:22, The New English Bible.
“Shauku ya Kidugu Isiyo ya Kinafiki”
7, 8. Ni nini asili ya neno lililotafsiriwa ‘usio wa kinafiki,’ kwa hiyo ni kwa nini Petro akatumia neno hilo?
7 Mtume Petro anasonga mbele zaidi ya hapo. Yeye anasema kwamba shauku yetu ya kidugu lazima iwe isiyo ya kinafiki. Neno lililotafsiriwa “isiyo ya kinafiki” linatokana na ile namna ya mwelekeo hasi ya neno la Kigiriki lililotumiwa kwa waigizaji wa jukwaani walionena wakiwa wamefunika nyuso zao kwa vibandiko vya usoni. Hiyo iliwawezesha kuchukua sehemu mbalimbali za wahusika wakati wa mchezo mmoja. Ndipo neno hilo likachukua ile maana ya unafiki, kusingizia hisia zilizo tofauti na zile za moyoni, au kujifanya.
8 Sisi tunahisi jinsi gani ndani kabisa katika kina cha mioyo yetu kuelekea baadhi ya ndugu na dada zetu katika kundi? Je! sisi huwasalimu mikutanoni kwa tabasamu ya kulazimishwa, halafu tunatazama mbali haraka au kupita moja kwa moja? Kwa ubaya zaidi, je! sisi tunajaribu kuepuka hata kuwapa salamu yenyewe? Ikiwa ndivyo, inaweza kusemwa nini juu ya ‘utii wetu kwa ule ukweli’ ambao ungalipaswa kutakatisha nafsi zetu kufikia hatua ya kuhisi shauku ya moyo mweupe kuelekea Wakristo wenzetu? Kwa kutumia neno “isiyo ya kinafiki,” Petro anasema kwamba shauku yetu kwa ndugu zetu lazima ionyeshwe kwa njia isiyo ya kujionyesha tu. Lazima iwe halisi, yenye kuhisiwa moyoni.
“Kwa Juhudi Nyingi Sana Kutoka Moyoni”
9, 10. Petro alimaanisha nini wakati aliposema kwmba inatupasa tupendane “kwa juhudi nyingi sana,” au ‘kwa kunyooka kirefurefu’?
9 Petro anaongezea hivi: “Pendaneni mmoja na mwenzake kwa juhudi nyingi sana [kwa uhalisi, “kwa kunyooshwa kirefurefu”] kutoka moyoni.” Inakuwa haihitajiwi kunyoosha moyo ili kuwaonyesha upendo wale ambao tunawafurahia kiasili na ambao wanarudisha ufurahio huo. Lakini Petro anatuambia tupendane mmoja na mwenzake ‘kwa kujinyoosha kirefu-refu.’ Wakati unapoonyeshwa miongoni mwa Wakristo, upendo wa a·gaʹpe hauwi wa akilini tu, wa kuhisiwa akilini tu, kama ule tunaopaswa kuwa nao kwa adui zetu. (Mathayo 5:44) Huo ni upendo wenye juhudi nyingi sana na unataka jitihada. Unahusisha ndani kunyoosha mioyo yetu, kuipanua ili iweze kuhusisha ndani watu ambao kwa kawaida hatungevutiwa nao.
10 Katika Linguistic Key to the Greek New Testament, Fritz Rienecker anatoa maelezo juu ya neno lililotafsiriwa “kwa juhudi nyingi sana,” au ‘kwa kunyooka kirefurefu,’ katika 1 Petro 1:22. Yeye anaandika hivi: “Wazo la kimsingi ni lile la bidii ya moyoni, ujitahidi (kufanya jambo si kijuujuu . . . bali [kwa] kujikakamua) (Hort).” Miongoni mwa maana nyinginezo, kujikakamua kunamaanisha “kujinyoosha kufikia kiwango cha mwisho.” Kwa hiyo kupendana mmoja na mwenzake kutoka moyoni kunamaanisha kujikaza wenyewe kufikia upeo katika jitihada zetu za kuwa na shauku ya kidugu kwa waandamani wetu wote wa Kikristo. Je! baadhi ya ndugu na dada zetu wamefinyika kwa kukosa kupewa nafasi katika shauku zetu nyororo? Ikiwa ndivyo, inatupasa sisi tupanuke.
‘Panukeni’
11, 12. (a) Ni shauri gani ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo katika Korintho? (b) Ni jinsi gani Paulo alivyoweka kielelezo kizuri katika habari hiyo?
11 Inaonekana mtume Paulo alihisi uhitaji wa jambo hilo katika kundi la Korintho. Yeye aliwaandikia hivi Wakristo wa huko: “Kinywa chetu kimefunguliwa kwa ninyi, Wakorintho, moyo yetu umepanuka. Ninyi hamfinyiki kwa kukosa kupewa nafasi ndani yetu, bali ninyi mnafinyika kwa kukosa kupewa nafasi katika shauku nyororo zenu wenyewe. Kwa hiyo, kama kwamba mnafanya malipo ya kurudisha—mimi nanena kama kwa watoto—ninyi, pia, panukeni.”—2 Wakorintho 6:11-13, NW.
12 Ni jinsi gani sisi tunaweza kupanua mioyo yetu ili itie ndani ndugu na dada zetu wote? Paulo aliweka kielelezo kizuri katika jambo hilo. Kwa uwazi yeye alitafuta kilicho bora zaidi katika ndugu zake, na hakuwakumbuka kwa ajili ya makosa ya kupungukiwa kwao bali kwa ajili ya sifa zao njema. Sura ya kufungia barua yake kwa Wakristo katika Roma inatoa kielezi cha jambo hilo. Acheni tuchunguze Waroma sura ya 16 na kuona jinsi inavyoonyesha mwelekeo chanya wa Paulo kuhusu ndugu na dada zake.
Uthamini Mchangamfu
13. Ni jinsi gani Paulo alivyoonyesha uthamini wake kwa Fibi, na kwa nini?
13 Paulo aliandika barua yake kwa Waroma akiwa Korintho karibu mwaka wa 56 W.K., wakati wa safari yake ya tatu ya umisionari. Inaonekana yeye alikabidhi hiyo hati ya mkononi kwa mwanamke mmoja Mkristo jina lake Fibi, mshiriki wa kundi la Kenkreae la hapo karibu, aliyekuwa akisafiri kwenda Roma. (Soma mistari 1, 2.) Angalia jinsi yeye anavyompendekeza huyo kwa uchangamfu kwa akina ndugu katika Roma. Kwa njia fulani, mwanamke huyo alikuwa amekinga Wakristo wengi, kutia na Paulo, labda wakati wa safari zao za kupitia bandari hiyo yenye shughuli nyingi ya Kenkreae. Kwa kuwa alikuwa mtenda dhambi asiyekamilika, kama wanadamu wengine wote, bila shaka Fibi alikuwa na udhaifu mbalimbali. Lakini badala ya kuonya kundi la Kiroma dhidi ya mapungukiwa ya Fibi, Paulo aliwaagiza ‘wampokee katika Bwana kama iwapasavyo watakatifu.’ Huo ni mwelekeo chanya ulio mzuri kama nini!
14. Ni mambo gani yenye fadhili ambayo Paulo alisema juu ya Priska na Akila?
14 Kuanzia mstari 3 mpaka mstari 15, Paulo anapeleka salamu kwa Wakristo zaidi ya 20 wenye kutajwa kwa jina na kwa wengine wengi wenye kutajwa mmoja mmoja au kwa ujumla. (Soma mistari 3, 4.) Je! wewe unaweza kuhisi shauku ya kidugu ambayo Paulo alihisi kwa Priska (au Prisila; linganisha Matendo 18:2) na Akila? Mume na mke hao walikuwa wamejitia katika hatari kadhaa kwa ajili ya Paulo. Sasa yeye alisalimu hawa wafanya kazi wenzi kwa shukrani na akawapelekea wonyesho wa shukrani kwa niaba ya makundi ya wasio Wayahudi. Lazima iwe Akila na Prisila walitiwa moyo sana na salamu hizo zenye kuhisiwa moyoni!
15. Ni jinsi gani Paulo alivyoonyesha ukarimu na unyenyekevu wake alipokuwa akisalimu Androniko na Yunia?
15 Paulo alikuja kuwa Mkristo aliyejitoa sana katika muda wa mwaka mmoja au miwili baada ya kifo cha Kristo. Kufikia wakati alipoandika barua yake kwa Waroma, alikuwa ametumiwa na Kristo kwa umashuhuri akiwa mtume kwa mataifa kwa miaka mingi. (Matendo 9:15; Warumi 1:1; 11:13) Hata hivyo, angalia ukarimu na unyenyekevu wake. (Soma mstari 7.) Yeye alisalimu Androniko na Yunia kuwa “maarufu miongoni mwa mitume” na akakiri kwamba wao walikuwa wamekuwa wakitumikia Kristo kwa muda mrefu kuliko yeye. Hapo hapaonekani kidalili chochote cha kiwivu kisichofaa!
16. (a) Paulo alinena juu ya Wakristo wengine katika Roma kwa maneno gani yenye upendo? (b) Kwa nini sisi tunaweza kuwa na uhakika kwamba salamu hizo zilikuwa vielelezo vya “shauku ya kidugu isiyo ya kinafiki”?
16 Yale tunayojua juu ya Wakristo wa mapema kama Epaineto, Ampliato, na Stakisi ni machache sana au hata hatujui lo lote juu yao. (Soma mistari 5, 8, 9.) Lakini kutokana tu na jinsi Paulo alivyowasalimu wote watatu, sisi tunaweza kuwa na uhakika kwamba wao walikuwa wanaume waaminifu. Wao walikuwa wamejifanya wapenzi wenye kuthaminika sana kwa Paulo hata yeye akaita kila mmoja wao “mpenzi wangu.” Paulo alikuwa na maneno yenye fadhili kwa Apele na Rufo pia, akirejeza kwao kwa kuita mmoja “mwenye kukubaliwa katika Kristo,” na yule mwingine “mteule katika Bwana.” (Soma mistari 10, 13.) Hizo zilikuwa pongezi nzuri kama nini kwa Wakristo hao wawili! Na kwa kuwa tunajua kwamba Paulo alikuwa mtu wa kutoboa mambo waziwazi, tunaweza kuwa na uhakika kwamba pongezi hizo hazikutolewa kama kawaida ya kidesturi tu. (Linganisha 2 Wakorintho 10:18.) Na kwa kupitia, Paulo hakusahau kusalimu mama ya Rufo.
17. Ni jinsi gani Paulo alivyoonyesha uthamini wenye kina kirefu kwa dada zake?
17 Hiyo inatuleta kwenye uthamini wa Paulo kwa dada zake. Zaidi ya mama ya Rufo, Paulo alitaja wanawake wengine wa Kikristo wasiopungua sita. Tayari sisi tumeona jinsi alivyonena kwa fadhili juu ya Fibi na Priska. Lakini angalia ni kwa shauku gani ya kidugu aliwasalimu Mariamu, Trifaina, Trifosa, na Persisi. (Soma mistari 6, 12.) Mmoja anaweza kuhisi kwamba moyo wa Paulo ulihisi shauku kwa dada hawa wenye bidii waliokuwa ‘wamejitaabisha sana’ kwa ajili ya ndugu zao. Ni jambo lenye kujenga kama nini kuona uthamini wa Paulo wenye kuhisiwa moyoni kwa ajili ya ndugu na dada zake, zijapokuwako hali zao za kutokamilika!
Kutoshuku Makusudio ya Ndugu Zetu
18. Ni jinsi gani sisi tunaweza kujitahidi kuiga Paulo, lakini ni jambo gani huenda likahitajiwa kabisa?
18 Kwa nini usiige Paulo na kujaribu kupata jambo fulani zuri la kusema juu ya kila ndugu na dada katika kundi? Kwa baadhi yao, hutaona ni tatizo hata kidogo. Kwa wengine, huenda ukahitaji kupekua-pekua kidogo ndipo uone uzuri huo. Kwa nini usijaribu kutumia wakati fulani ukiwa pamoja nao ili kuwajua vizuri zaidi? Kwa uhakika utagundua sifa zenye kupendeka ndani yao, na, nani ajuaye, huenda wao wakapata kukuthamini wewe zaidi ya wakati uliopita.
19. Kwa nini haitupasi kushuku makusudio ya ndugu zetu, na ni jinsi gani Yehova ametuwekea sisi kielelezo kizuri cha upendo?
19 Haitupasi kushuku makusudio ya ndugu zetu. Wote wanapenda Yehova, ama sivyo wasingalikuwa wameweka maisha zao ziwe wakfu kwake. Nacho ni kitu gani kinachowahami wasirudi ndani ya ulimwengu, kufuata njia zao za kutojali sana mambo? Ni upendo wao kwa Yehova, uadilifu wake, na Ufalme wake chini ya Kristo. (Mathayo 6:33) Lakini wote, kwa njia mbalimbali, wanalazimika kufanya pigano gumu ili wabaki wakiwa waaminifu. Yehova anawapenda wao kwa ajili ya jambo hilo. (Mithali 27:11) Yeye anawakubali kuwa watumishi wake wajapokuwa na dosari na mapungukiwa. Kwa kuwa ndivyo ilivyo, sisi ni akina nani hata tukatae kuwapokea katika shauku nyororo zetu?—Warumi 12:9, 10; 14:4.
20. (a) Kulingana na barua ya Paulo kwa Waroma, ni nani peke yao tunaopaswa kuwashuku, na ni uongozi wa nani tunaoweza kufuata kwa usalama katika habari hiyo? (b) Ama sivyo, inatupasa tuwaone ndugu zetu wote jinsi gani?
20 Watu wa peke yake ambao Paulo anatuonya tuwashuku ni “wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza,” na wale ambao wanatenda “kinyume cha mafundisho mliyojifunza.” Paulo anatuambia tuweke macho yetu juu ya watu kama hao na kuwaepuka. (Warumi 16:17) Wazee wa kundi watakuwa wamejaribu kusaidia watu hao. (Yuda 22, 23) Kwa hiyo sisi tunaweza kutegemea wazee watupashe habari ikiwa watu fulani wanahitaji kuepukwa. Ama sivyo, sisi tunapaswa kuwaona ndugu zetu wote kuwa wanastahili shauku ya kidugu isiyo ya kinafiki, na inatupasa tujifunze kuwapenda kwa juhudi nyingi sana kutoka moyoni.
21, 22. (a) Ni nini kilichoko mbele yetu? (b) Ni hali gani ambazo huenda zikatokea, kwa hiyo sasa ndio wakati wa kufanya nini? (c) Ni nini litakalofikiriwa katika makala inayofuata?
21 Shetani, roho wake walio wabaya, na mfumo wake mzima wa mambo uko dhidi yetu. Har–Magedoni iko mbele yetu. Itafyatushwa na shambulio la Gogu wa Magogu. (Ezekieli, sura 38, 39) Wakati huo, sisi tutahitaji ndugu zetu zaidi ya wakati mwinginewo wote. Huenda tukajikuta wenyewe tukiwa katika uhitaji wa kusaidiwa na wale wale ambao sisi hatuwathamini kihususa. Au huenda hao hao wakawa katika uhitaji mkubwa sana wa msaada wetu. Sasa ndio wakati wa kupanuka na kuongeza uthamini wetu kwa ndugu zetu wote.
22 Bila shaka, uthamini kwa ndugu zetu unatia ndani staha inayofaa kwa wazee wa kundi. Katika habari hiyo, wazee wenyewe wanapaswa kuwa vielelezo vizuri, si kwa kuonyesha uthamini unaofaa kwa ndugu wote tu bali kwa wazee wenzao pia. Upande huo wa habari hii utafikiriwa katika makala inayofuata.
Mambo ya Kupitia
◻ Ni nini ishara yenye kupambanua Ukristo wa kweli?
◻ Kwa nini upendo na shauku ya kidugu pia unahitajiwa kabisa?
◻ Ni jinsi gani sisi tunavyoweza kupendana mmoja na mwenzake “kwa juhudi nyingi sana,” au ‘kwa kunyooka kirefurefu’?
◻ Katika Waroma sura ya 16, ni jinsi gani Paulo alivyoonyesha uthamini kwa ndugu na dada zake?
◻ Kwa nini haitupasi kushuku makusudio ya ndugu zetu?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Jaribu kugundua sifa zenye kupendeka ndani ya wale ambao huvutiwi nao kiasili