Rekebisho la Matakwa ya Saa kwa Mapainia
1 Sisi sote huthamini kuwa na mapainia wa kawaida na wasaidizi wenye bidii katika kutaniko. Hata mahali ambapo eneo halitoshi na limehubiriwa kikamili kwa ukawaida, mapainia wameweka kielelezo kizuri kwa utumishi wao wa Ufalme wenye bidii. Wametia moyo wahubiri wote waendelee kutafuta wale “walio na mwelekeo ufaao.”—Mdo. 13:48.
2 Sosaiti imeona magumu yenye kuongezeka wanayokabili mapainia, hasa kuhusu kupata kazi ya kuajiriwa isiyo ya wakati wote itakayowaruhusu kutunza mahitaji yao ya kibinafsi vya kutosha ili kudumu katika utumishi wa wakati wote. Hali ya sasa ya kiuchumi katika nchi nyingi inazidi kufanya iwe vigumu kwa wengine kujiunga na kazi ya upainia, hata ingawa hiyo ni tamaa yao ya moyoni. Wakati wa miezi ya karibuni, mambo haya pamoja na mengineyo yamefikiriwa kwa uangalifu.
3 Kwa hiyo, kwa kufikiria mambo yaliyotajwa juu, Sosaiti imepunguza takwa la saa kwa mapainia wa kawaida na wasaidizi. Kuanzia mwaka wa kalenda wa 1999, takwa la saa kwa mapainia wa kawaida litakuwa saa 70 kila mwezi, au jumla ya saa 840 kwa mwaka. Takwa la saa la kila mwezi kwa mapainia-wasaidizi litakuwa saa 50. Takwa la saa kwa mapainia wa pekee na wamishonari labaki vilevile, kwa kuwa Sosaiti hufanya maandalizi ya kuwasaidia kushughulikia mahitaji yao ya kimwili ya msingi. Hivyo, wanaweza kukazia uangalifu kikamili kazi yao ya kuhubiri na kufanya wanafunzi.
4 Yatumainiwa kwamba rekebisho hilo la matakwa ya saa litasaidia mapainia wengi wadumu katika pendeleo hili la utumishi lenye thamani. Pia rekebisho hilo lapaswa kufungua njia kwa wahubiri wengi zaidi kuchukua kazi ya upainia wa kawaida na msaidizi. Lapaswa kuthibitika kuwa baraka kama nini kwa kila mmoja katika kutaniko!