Sali Upate Msaada wa Yehova
1 Yesu alikazia wanafunzi wake uhitaji wa baraka za Yehova katika huduma yao. (Mt. 9:37, 38) Sala zetu za kutoka moyoni za sifa na shukrani pamoja na maombi na dua ya bidii zaonyesha kumtegemea kwetu Yehova kabisa tupate msaada wake. (Flp. 4:6, 7) Maandiko hutuhimiza twendelee kusali “kwa kila namna ya sala na dua,” na hilo lahusu sala zetu kuhusu huduma.—Efe. 6:18.
2 Twamsifu Yehova katika sala kwa sababu ya sifa zake na matimizo yake yasiyo na kifani. Twamsifu pia akiwa Mpaji wa habari njema tunazohubiri. Yeye anastahili sifa yetu kwa sababu ni yeye pekee afanikishaye huduma yetu.—Zab. 127:1.
3 Sala zetu za shukrani hueleza uthamini kwa uelewevu ambao Yehova ametupatia kuhusu mapenzi yake na kusudi lake. Je, si pendeleo kushiriki kweli za Ufalme na wengine? Twamshukuru Yehova kwa yote tunayotimiza katika huduma.—Zab. 107:8; Efe. 5:20.
4 Kwa kufaa twamwomba Yehova atupe msaada wa kupata watu ambao watakubali funzo la Biblia, na twamwomba msaada wa kufikia mioyo yao na ile kweli. Kwa kuomba dua hizo, twatambua kwamba Mungu peke yake ndiye anayeweza kufanya kazi yetu katika huduma iwe na matokeo.—1 Kor. 3:5-7.
5 Dada mmoja alihisi kwamba mwanamke mmoja aliyekuwa akimpelekea magazeti kwa ukawaida hakuwa akisoma Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa kuwa hakutaka magazeti hayo yapotee bure, alimwomba Yehova kwa bidii kwamba kama mwanamke huyo hakuwa akiyasoma, basi ayakatae. Dada aliporudi wakati uliofuata, mume wa mwanamke huyo alisema: “Asante kwa kuleta magazeti haya kwa ukawaida. Ninayasoma nami nayapenda sana.”
6 Kwa kuomba kwa unyenyekevu na kwa bidii, twaweza kuomba Yehova dua atusaidie tushughulikie ubaridi wa watu, maeneo magumu na dhihaka na tuishinde hali yoyote ya kumhofu mwanadamu ili twendelee kutolea wengine ushahidi kwa ujasiri. (Mdo. 4:31) Tukiendelea kusali “kwa kila namna ya sala na dua” tukifuatia kwa utii utumishi wetu mtakatifu, twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia.—1 Yoh. 3:22.