Je, Wewe Hutamani Kutumikia Kikamili Zaidi?
“NILIMKASIRIKIA Yehova,” asema Laura. “Nilisali na kusali atusaidie kusuluhisha matatizo yetu ya kifedha ili niweze kuendelea na upainia—lakini bila mafanikio. Hatimaye nililazimika kuacha utumishi wangu wa painia. Lazima pia nikubali kwamba niliwaonea wivu wale ambao wangeweza kuendelea.”
Fikiria pia, kisa cha Michael, mtumishi wa huduma katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Alikuwa akijitahidi kufikia wadhifa wa kuwa mwangalizi. (1 Timotheo 3:1) Miaka kadhaa ilipopita bila tamaa yake kutimizwa, alihisi uchungu mwingi wa moyo hivi kwamba hakutaka tena kufikiriwa kwa ajili ya pendeleo hilo. “Singeweza kustahimili maumivu ya mtamauko tena,” yeye asema.
Je, wewe umepatwa na jambo kama hilo? Je, umelazimika kuacha pendeleo la kitheokrasi ulilopenda? Mathalani, je umewahi kulazimika kuacha kutumikia ukiwa painia, mpiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote? Au unatamani madaraka fulani ya kutaniko waliyokabidhiwa wengine? Hata waweza kuwa unatamani sana kutumikia kwenye Betheli au ukiwa mishonari, lakini hali zako hazikuruhusu.
“Kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua,” chakubali kitabu cha Mithali. (Mithali 13:12) Hilo lawezekana hasa wengine wanapopata mapendeleo yaleyale unayotazamia. Je, Neno la Mungu huandaa ufahamu wenye kina, faraja, na tumaini kwa wowote ambao wamepatwa na mitamauko kama hiyo? Ndiyo, huandaa. Kwa hakika, Zaburi ya 84 yaonyesha hisia za mtumishi wa Yehova aliyekuwa na tamaa kama hizo kuhusu utumishi wa Yehova ambazo hazikuwa zimetimizwa.
Uthamini wa Mlawi
Watungaji wa Zaburi ya 84 walikuwa wana wa Kora, Walawi waliotumikia kwenye hekalu la Yehova na waliostahi sana mapendeleo yao ya utumishi. “Maskani zako zapendeza kama nini, Ee BWANA wa majeshi!” apaaza sauti mmoja wao. “Nafsi yangu imezionea shauku nyua za BWANA, naam, na kuzikondea. Moyo wangu na mwili wangu vinamlilia Mungu aliye hai.”—Zaburi 84:1, 2.
Mlawi huyo alikuwa na tamaa kubwa ya kutumikia kwenye hekalu la Yehova hivi kwamba hata mandhari ya kawaida njiani kuelekea Yerusalemu ilionekana kuwa yenye kuvutia kwake. “Wakipita katika bonde la Vilio,” asema, “hulifanya kuwa chemchemi.” (Zaburi 84:6) Ndiyo, eneo la kawaida lililo kame lilikuwa kama mkoa uliotiwa maji vizuri.
Kwa kuwa mtunga-zaburi alikuwa Mlawi asiye wa kikuhani, angeweza kutumika hekaluni juma moja tu kwa miezi sita. (1 Mambo ya Nyakati 24:1-19; 2 Mambo ya Nyakati 23:8; Luka 1:5, 8, 9) Wakati wake uliosalia ulitumiwa nyumbani katika mojawapo ya majiji ya Walawi. Kwa hiyo aliimba hivi: “Shomoro naye ameona nyumba, na mbayuwayu amejipatia kioto, alipoweka makinda yake, kwenye madhabahu zako, Ee BWANA wa majeshi, mfalme wangu na Mungu wangu.” (Zaburi 84:3) Huyo Mlawi angalifurahi kama nini ikiwa angalikuwa kama ndege ambao walikuwa na mahali pa kudumu zaidi hekaluni!
Ingalikuwa rahisi kwa huyo Mlawi kuwa na uchungu wa moyo kwa sababu hangeweza kutumikia hekaluni mara nyingi zaidi. Hata hivyo, alifurahia kutumikia kadiri angeweza, na bila shaka alitambua kwamba ujitoaji wa moyo wote kwa Yehova ulistahili jitihada hiyo. Ni nini lililomsaidia Mlawi huyo mwaminifu abaki akiwa ameridhika na mapendeleo yake ya utumishi?
Jifunze Kuridhika
“Siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu,” asema huyo Mlawi. “Ningependa kuwa bawabu nyumbani mwa Mungu wangu, kuliko kukaa katika hema za uovu.” (Zaburi 84:10) Aling’amua kwamba kutumia hata siku moja nyumbani mwa Yehova ni pendeleo lisilo na kifani. Na huyo Mlawi alikuwa na zaidi ya siku moja ya kutumikia hekaluni. Kuridhishwa kwake na mapendeleo yake kulimfanya aimbe kwa shangwe.
Namna gani sisi? Je, twahesabu baraka zetu, au twaelekea kusahau yale ambayo tayari tunayo katika utumishi wa Yehova? Kwa sababu ya ujitoaji wao kwake, Yehova amewakabidhi watu wake wajibu na mapendeleo mengi. Hayo hutia ndani yale madaraka mazito zaidi ya usimamizi, uchungaji, ufundishaji, na nyanja mbalimbali za utumishi wa wakati wote. Lakini pia yahusisha mambo mengine yenye thamani yanayohusiana na ibada ya Yehova.
Kwa kielelezo, fikiria huduma ya Kikristo. Mtume Paulo analinganisha pendeleo letu la kuhubiri habari njema na kuwa na ‘hazina katika vyombo vya udongo.’ (2 Wakorintho 4:7) Je, wewe wauona utumishi huo kuwa hazina yenye thamani isiyo na kifani? Yesu Kristo, aliyeanzisha utendaji wa kuhubiri Ufalme, aliuona hivyo, akiacha kigezo. (Mathayo 4:17) “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii . . . , hatufi moyo,” akasema Paulo.—2 Wakorintho 4:1.
Mikutano ya Kikristo ni utumishi mtakatifu pia usiopasa kuchukuliwa vivi hivi. Kwenye mikutano yetu, twapokea maagizo ya maana na kufurahia ushirika unaohitajiwa. Mikutanoni twaweza pia kudhihirisha imani na tumaini letu kwa kutoa maelezo kwa ukawaida na kwa kushiriki katika programu kwa njia nyinginezo. (Waebrania 10:23-25) Mikutano yetu ni uandalizi unaostahili kuthaminiwa kikweli!
Michael, aliyetajwa mapema, aliziona baraka hizo kuwa zenye thamani sana, akazithamini sana. Lakini mtamauko wake wa kutoweza kutumikia akiwa mzee ulisukuma nyuma uthamini wake kwa ajili yazo kwa kipindi fulani. Kwa kuzifikiria, aliweza kupata tena usawaziko na kumngojea Yehova kwa subira.
Badala ya kuhisi kutoridhika kwa sababu ya kutokuwa na pendeleo fulani, inafaa tuchunguze tena njia ambazo Yehova anatubariki, kama alivyofanya mtunga-zaburi.a Tukishindwa kuona mengi, twahitaji kuangalia tena, tukimuuliza Yehova afumbue macho yetu tuone mapendeleo yetu na njia ambazo anatubariki na kututumia tumsifu.—Mithali 10:22.
Pia ni jambo la maana kutambua kwamba mapendeleo ya pekee, kama vile wadhifa wa mwangalizi, hutaka sifa mahususi za ustahili. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9) Kwa hiyo twahitaji kujichunguza wenyewe, tukitafuta maeneo yoyote ambayo maendeleo yanahitajiwa na kisha kufanya jitihada zenye bidii ili kufanya maendeleo.—1 Timotheo 4:12-15.
Usivunjike Moyo
Tusipopokea pendeleo fulani la utumishi, hatuhitaji kukata maneno kwamba Yehova anawapenda zaidi wale wanaolifurahia au kwamba anatunyima mema. Kwa kweli, hatupaswi kudhania tukiwa wenye wivu kwamba hao wengine wamepokea bila kustahili mapendeleo yao kupitia upendeleo wa kibinadamu badala ya kuwekwa rasmi kitheokrasi. Kuwazia mawazo kama hayo kwaweza kuongoza kwenye wivu, ugomvi, na hata kufa moyo kwetu wenyewe.—1 Wakorintho 3:3; Yakobo 3:14-16.
Laura, aliyetajwa mwanzoni, hakufa moyo. Hatimaye aliazimia kushinda hisia zake za hasira na wivu. Laura alisali kwa Mungu tena na tena ili apate msaada kushinda itikio lake lisilofaa kuelekea kutoweza kupainia kwake. Pia alitafuta msaada kutoka kwa wanaume wenye sifa za ustahili kutanikoni, akahisi akiwa amehakikishiwa upendo wa Mungu tena. “Yehova alinipa amani ya akili,” alisema. “Ingawa mume wangu nami hatuwezi kupainia sasa, twauthamini kikweli wakati tuliopainia na kupata nguvu kutokana na mambo yaliyoonwa tuliyopata. Pia tunamsaidia mwana wetu mkubwa katika upainia wake.” Akiwa ameridhika, Laura sasa anaweza ‘kushangilia pamoja na watu washangiliao’ katika utumishi wa painia.—Waroma 12:15.
Weka Miradi Iwezayo Kufikiwa
Kuridhika kwetu na mapendeleo ya sasa ya utumishi hakumaanishi kwamba tukome kuweka miradi zaidi ya kitheokrasi. Akizungumza juu ya ufufuo wa kimbingu, Paulo alisema juu ya “kujinyoosha mbele kwenye mambo ya mbele.” Pia alisema hivi: “Kwa kadiri ambayo tumefanya maendeleo, acheni tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.” (Wafilipi 3:13-16) Miradi ya kitheokrasi yaweza kutusaidia kujinyoosha mbele. Hata hivyo, jambo lililo gumu ni kudumisha miradi hiyo ikiwa halisi.
Miradi halisi ni yenye kufaa na iwezayo kufikiwa. (Wafilipi 4:5) Hilo halimaanishi kwamba mradi unaohitaji miaka mingi ya kazi ngumu si halisi. Mradi huo wa muda mrefu waweza kufikiwa hatua kwa hatua kwa kuweka mfululizo wa miradi ya katikati, au hatua. Hatua hizo zaweza kutumika zikiwa vitia alama maendeleo ya kiroho. Kumaliza kila hatua kwa mafanikio kutaandaa kwa wakati uliopo hali ya uradhi badala ya mtamauko.
Usawaziko Mzuri
Hata hivyo, ni jambo la maana kutambua kwamba kwa sababu ya hali zetu na mipaka yetu, mapendeleo fulani huenda yasipokewe. Kuyaweka kuwa miradi huongoza tu kwenye mtamauko na kuvunjika moyo. Miradi kama hiyo yapasa kuahirishwa, angalau kwa wakati uliopo. Haitakuwa vigumu kufanya hivyo, tukisali kupata uradhi wa kimungu na kufanya hangaiko letu kuu kuwa kufanya mapenzi ya Yehova. Tujaribupo kufikia mapendeleo, utukufu wa Yehova—wala si kutambuliwa kwa matimizo yetu ya kibinafsi—ndilo jambo la maana. (Zaburi 16:5, 6; Mathayo 6:33) Kwa kufaa Biblia hutuambia hivi: “Mkabidhi BWANA kazi zako, na mawazo yako yatathibitika.”—Mithali 16:3.
Katika kuichunguza Zaburi ya 84, twaweza kuona kwamba mtunga-zaburi alidhihirisha mtazamo huo kuelekea mapendeleo ya utumishi, na Yehova alimbariki sana. Isitoshe, zaburi hiyo yaendelea kuwanufaisha watu wa Yehova hata leo.
Kwa kumtegemea Yehova kwa sala, waweza kusawazisha kutamani kwako mapendeleo zaidi na kuridhika na yale unayofurahia sasa. Usiruhusu kamwe tamaa ya kufanya mengi zaidi ikunyang’anye uthamini kwa ajili ya uliyo nayo sasa na shangwe ya kumtumikia Yehova milele. Mtumaini Yehova, kwa kuwa kufanya hivyo hutokeza furaha, kama ionyeshwavyo katika maneno ya Mlawi: “Ee BWANA wa majeshi, heri mwanadamu anayekutumaini Wewe.”—Zaburi 84:12.
[Maelezo ya Chini]
a Tafadhali ona makala “Je! Wewe Unathamini Mambo Matakatifu?” katika toleo la Juni 15, 1988, la Mnara wa Mlinzi.
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Miradi Tuwezayo Kuweka
Kusoma Biblia kila siku.—Yoshua 1:8; Mathayo 4:4
Kuboresha nguvu zetu za ufahamu kupitia kujizoeza Kimaandiko.—Waebrania 5:14
Kukuza uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Mungu.—Zaburi 73:28
Kusitawisha kila moja la matunda ya roho.—Wagalatia 5:22, 23
Kuboresha sala zetu.—Wafilipi 4:6, 7
Kuwa wenye matokeo zaidi katika kuhubiri na kufundisha.—1 Timotheo 4:15, 16
Kusoma na kutafakari kila toleo la magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!—Zaburi 49:3
[Picha katika ukurasa wa 9]
Katika kuweka miradi ya kibinafsi, tanguliza kufanya mapenzi ya Mungu