Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 10/15 kur. 21-22
  • Wewe Unachagua Kuwa Wapi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wewe Unachagua Kuwa Wapi?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Habari Zinazolingana
  • Je, Wewe Hutamani Kutumikia Kikamili Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Je! Wewe Unathamini Kuwa Pamoja na Watumishi wa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Mahali pa Ibada Penye Kupendeza pa Yehova
    Mwimbieni Yehova Sifa
  • Mahali Pafaapo pa Ibada ya Yehova Maishani Mwetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 10/15 kur. 21-22

Zaburi

Wewe Unachagua Kuwa Wapi?

WATUMISHI wa Yehova Mungu wanaomtumikia kwa bidii nyingi sana wanathamini sana kuweza kufurahia ushirika pamoja na watu walio na imani bora sana kama yao. Kati ya Waisraeli, hali hiyo ya kuthamini ilionekana wazi walipotamani kwa unyofu wa moyo kwenda patakatifu. Je! hata wewe unafurahia sana kushiriki pamoja na wengine katika ibada?

Mwandikaji wa Zaburi 84, ambaye ni Mlawi aliyekuwa katika ukoo wa Kora, aliweka mfano mwema wa kutaka kuwa kati ya watumishi waaminifu wa Mungu. Yeye alisema hivi: “Maskani zako zapendeza kama nini, Ee [Yehova] wa majeshi! Nafsi yangu imezionea shauku nyua za [Yehova], naam, na kuzikondea. Moyo wangu na mwili wangu vinamlilia Mungu aliye hai. Shomoro naye ameona nyumba, na mbayuwayu amejipatia kioto, alipoweka makinda yake, kwenye madhabahu zako, Ee [Yehova] wa majeshi, Mfalme wangu na Mungu wangu.”​—Zaburi 84:1-3.

Patakatifu ‘palimpendeza sana’ mtunga zaburi, pakawa kwake kama mahali malidadi sana, ndiyo, mahali pa kuvutia sana kwa sababu palikuwa ndipo mahali pa Yehova pa ibada. Shauku nyingi sana ambayo Mlawi huyu alitumia kueleza maoni yake ya kutamani sana kuwa katika nyua za hema takatifu ya Yehova inatukumbusha kwamba wale Walawi makumi ya maelfu waliokuwako wakati wa ule ufalme walikaa katika yale majiji 48 waliyogawiwa Walawi katika nchi yote ya Israeli. Ni mara moja tu kila nusu-mwaka zamu moja kati ya zile zilizopangwa au kikundi kimoja kati ya vilivyopangwa cha Walawi wasio wa kikuhani kilipotumikia juma zima hekaluni. Kwa hiyo, sehemu kubwa ya mwaka waliitumia kwenye nyumba zao binafsi wakiwa pamoja na jamaa zao katika majiji ya Walawi. Kwa upande mwingine, kwa sababu ya Walawi hao kutokuwapo huenda ikawa ndege wadogo walipata makao ya muda mrefu zaidi kwenye hekalu.

Mlawi wa ukoo wa Kora alikuwa akiwaza sana juu ya furaha nyingi waliyoipata wale waliokwenda patakatifu kwa ukawaida nyakati zilizopangwa. Anaendelea kusema: “Heri wakaao nyumbani mwako, wanakuhimidi daima. Heri ambaye nguvu zake zatoka kwako, na njia ziendazo Sayuni zimo moyoni mwake. Wakipita kati ya bonde la Vilio [la vichaka vya baka, NW], hulifanya kuwa chemchemi, naam, mvua ya vuli hulivika baraka [hata yule mwalimu anajifungilia baraka nyingi, NW]. Huendelea toka nguvu hata nguvu, huonekana Sayuni kila mmoja mbele za Mungu.”​—Zaburi 84:4-7.

Kwa sababu ya kazi zao mbalimbali, makuhani na Walawi walikaa kwa muda kwenye nyumba ya Yehova wakaweza kumhimidi (kumsifu) yule Aliye Juu Zaidi kwa njia ya moja kwa moja. Acha wafurahi nyakati hizo, wee! Waisraeli wale wengine waliojipa nguvu kutokana na Mungu walifurahi pia, nguvu hizo zikiwa ni za wakati walipohitaji faraja na msaada. Waisraeli hao waliweka mawazo ya mioyo yao juu ya zile “njia” kuu, yaani, juu ya njia zilizoelekea kwenye patakatifu. Kwa sababu ya kupendezwa kwao na ibada ya kweli, hata eneo kavu la vichaka vya baka (miti yenye kutona-tona utomvu ulio kama maziwa, kama kwamba inalia), ambalo walipitia katika safari ya kwenda Yerusalemu, lilionekana lenye kupendeza kama jimbo lenye maji mengi ambako chemchemi inatiririsha maji. Waisraeli waaminifu walimchukua Yehova kuwa ndiye “Mwalimu” wao. (Isaya 30:20, NW) Kwa kuwa wangemhimidi au wamsifu, inaweza kusemwa kwamba ‘mwalimu alijifungilia’ baraka (sifa) hizo kama kwamba ni kwa kutumia vazi. Hata kama safari iliyofungwa ilikuwa ndefu, waabudu wenye kujitoa kwa bidii nyingi hawakujichosha kipimo cha kuwa hoi. Wao walizidi kupata nguvu mpya kwa sababu ya tazamio lao la kupafikia patakatifu.

Sasa, mtunga zaburi anafikia hatua nyingine ya kumsihi Yehova, akisema: “[Yehova], Mungu wa majeshi, uyasikie maombi yangu, Ee Mungu wa Yakobo, usikilize, Ee Mungu, ngao yetu, uangalie, umtazame uso masihi wako.” (Zaburi 84:8, 9) Hivyo, Mlawi huyu hajitafutii peke yake tu upendeleo wa Yehova bali anamtafutia pia mtiwa mafuta (masihi), ambaye inaelekea kuwa ni mfalme wa Yudea. Mlawi huyu anafahamu kwamba yule Aliye Juu Zaidi ni ngao yenye kulinda Israeli, kwa hiyo anampelekea sala ya kuomba msaada.

Kwa sababu mtunga zaburi ana tamaa kubwa ya kuwa kwenye patakatifu, yeye anasema: “Hakika siku moja katika nyua zako ni bora kuliko siku elfu [kwingineko]. Ningependa kuwa bawabu nyumbani mwa Mungu wangu, kuliko kukaa katika hema za uovu.” (Zaburi 84:10) Lo, anathamini mambo kama nini! Kwa mtunga zaburi, siku moja tu ya kuwa katika nyua za patakatifu pa Yehova ilikuwa bora zaidi ya siku elfu moja zenye kutumiwa kwingineko. Yeye alipendelea kusimama akitumikia kwenye kiingilio, ndiyo, kwenye mlango wa kuiingia nyumba ya Yehova badala ya kuwa katika hema za watu waovu, hata kama zilikuwa na mambo ya raha nyingi sana.

Kwa sababu gani aliithamini sana nyumba ya Mungu? Angalia maneno yake: “Kwa kuwa [Yehova], Mungu, ni jua na ngao, [Yehova] atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema hao waendao kwa ukamilifu. Ee [Yehova] wa majeshi, heri mwanadamu anayekutumaini Wewe.” (Zaburi 84:11, 12) Ndiyo, mtunga zaburi alifahamu Yehova ni Mungu wa namna gani. Yule Aliye Juu Zaidi ni jua kwa watu wake, mwenye kuwapa nuru. Anawapa pia ulinzi akiwa kama ngao. Mawonyesho ya upendeleo na baraka yanamiminika kutoka kwake, naye anawapa utukufu na heshima wale anaowakubali. Yehova hatawanyima mema wale wanaojaribu kutembea kwa unyofu. Atawabariki sana, na wale wanaomtumaini Mwenye Nguvu Zote hawatakatishwa tumaini bali wataendelea kuwa na furaha halisi.

Je! wewe unajisikia ukichochewa na ufahamu wako wa kujua kwamba Yehova ni Mlinzi na Chemchemi ya zawadi zote zilizo nzuri kiasi cha kukufanya uwe ukikusanyika kwa ukawaida pamoja na watu wake? Je! kuwa na msimamo mzuri ndilo jambo linalokufurahisha zaidi ya yote? Kwa uhakika tunapaswa tupatanishe matendo yetu na mawazo yaliyotajwa na mtunga zaburi na kwa njia hiyo tuendelee kuiona furaha inayokuja Yehova anapokuwa Mungu wetu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki