Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 6/1 kur. 6-7
  • Je! Wewe Unathamini Kuwa Pamoja na Watumishi wa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unathamini Kuwa Pamoja na Watumishi wa Mungu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Habari Zinazolingana
  • Wewe Unachagua Kuwa Wapi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Nguzo Juu ya Bahari
    Amkeni!—2009
  • Mngojee Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Mungu Humwokoa Mwenye Kuhurumia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 6/1 kur. 6-7

Zaburi

Je! Wewe Unathamini Kuwa Pamoja na Watumishi wa Mungu?

IKIWA wewe ungezuiwa kuwa pamoja na ndugu zako za kiroho, ungeonaje? Je! ungekuwa na tamaa kubwa sana ya kushiriki pamoja nao katika ibada?

Zaburi ya 42 inatuonyesha hali ya Mlawi, aliyekuwa mzao wa Kora, ambaye alijikuta akiwa uhamishoni. Maneno yake yaliyoongozwa na Mungu yanaweza kutusaidia sana katika kudumisha hali ya kuthamini sana ushirika wetu pamoja na waamini wenzetu na kuvumilia chini ya hali zisizofaa.

Mtunga zaburi huyo alisema hivi: “Kama vile ayala atamanivyo vijito vya maji, ndivyo nafsi yangu yenyewe inavyokutamani, Ee Mungu. Hakika nafsi yangu yaona kiu ya Mungu, ya Mungu aliye hai. Nitakuja wakati gani nionekane mbele za Mungu?” (Zab. 42:1, 2, NW) Ayala, au paa jike, hawezi kuendelea kuishi kwa muda mrefu bila maji. Kiumbe huyu hutafuta-tafuta umajimaji huo wenye kuendeleza uhai na kunywa, ijapokuwa kufanya hivyo kwaweza kumfanya ashambuliwe na wanyama wala-nyama. Kama vile ayala anavyotamani maji kwa sababu ni ya lazima, mtunga zaburi huyo alimtamani Yehova.

Katika nchi kavu, ambako majani hukauka upesi wakati wa majira yasiyo na mvua, maji ni yenye thamani sana nayo hayapatikani kwa urahisi. Ndiyo sababu mtunga zaburi huyo anajisema kuwa ‘akiona kiu ya Mwenye Nguvu Zote.’ Kwa sababu ya kunyimwa nafasi ya kwenda kwenye patakatifu, yeye anauliza ni wakati gani atakapoweza ‘kuonekana mbele za Mungu’ tena.

Wakati kuwekwa kizuizini kwa sababu ya mateso kunapomzuia asiwe pamoja na waamini wenzake, hilo laweza kuwa jambo lenye kushusha moyo sana. Mstari wa 3 wa Zaburi 42 huonyesha kwamba kupelekwa uhamishoni kwa mtunga zaburi huyo kulikuwa na matokeo katika maono yake ya moyoni. Tunasoma hivi: “Kwangu mimi machozi yangu yamekuwa chakula mchana na usiku, huku wakiniambia mchana kutwa: ‘Yuko wapi Mungu wako?’” Kwa sababu ya hali isiyofaa ambayo katika hiyo mtunga zaburi alijikuta, alikuwa na huzuni nyingi sana hata kwamba alipoteza hamu ya chakula. Hivyo machozi yake yakawa kama chakula kwake. Mchana na usiku machozi yalikuwa yakitiririka mashavuni pake na kuingia kinywani mwake. Wenye kudhihaki walikuwa wakisema: “Yuko wapi Mungu wako?” Ni kana kwamba walikuwa wakiuliza: ‘Ni kwa sababu gani Mungu unayemtumaini hakusaidii?’ Dhihaka hiyo ilizidisha mateso ya mtunga zaburi.

Yeye alijaribu kujitia moyo namna gani ili asishindwe na huzuni yake? Anaendelea kusema hivi: “Mambo haya nitayakumbuka, nami nitamwaga nafsi yangu ndani yangu. Kwa kuwa nilikuwa nikipita pamoja na makutano, nilikuwa nikitembea polepole mbele yao nikienda kwenye nyumba ya Mungu, kwa sauti ya kilio cha furaha na kushukuru, ya kundi linalosherehekea sikukuu. Kwa sababu gani unakata tamaa, Ee nafsi yangu, na ni kwa nini unapiga kelele ndani yangu? Mngojee Mungu, kwa kuwa bado nitamsifu akiwa wokovu wangu mkuu. Ee Mungu wangu, moyo wangu unakata tamaa ndani yangu. Ndiyo sababu nakukumbuka wewe, toka nchi ya Yordani na vilele vya Hermoni, toka kilima.”​—Zab. 42:4-6, NW.

Angalia kwamba mtunga zaburi aliukumbuka wakati uliopita, wakati ambapo hakuwa uhamishoni. Yeye anamwaga nafsi, yake, mwili wake wenyewe, kwa maono ya nguvu sana, na kusema yale aliyofurahia wakati mmoja. Mlawi huyu anakumbuka namna ilivyokuwa katika nchi ya kwao, namna yeye akishirikiana na Waisraeli wenzake, walivyokuwa wakienda kwenye patakatifu pa Yehova ili washerehekee sikukuu. Loo! Alifurahi na kushukuru kama nini wakati huo!

Mwanzoni, kukumbuka huku kwa wakati uliopita hakukumfariji mtunga zaburi huyu, bali kulizidisha maumivu yake, kwa kuwa alifahamu mengi aliyokuwa akiyakosa. Alijiuliza ni kwa nini alikuwa akifadhaika sana ndani yake jinsi hiyo, na kuhuzunika jinsi hiyo? Hata hivyo, kufikiria wakati uliopita kulimkumbusha Mungu wake. Ndiye aliyekuwa faraja yake. Kwa hiyo alijitia moyo amngojee Yehova achukue hatua. Mtunga zaburi huyo hakuruhusu hali hiyo isiyofaa idhoofishe tumaini lake la kwamba, katika wakati wake, Yehova angekuja kumsaidia, na kumwezesha amsifu Aliye Juu Zaidi kwa kumfanyia wokovu mkuu au ukombozi. Ajapokuwa mbali sana na patakatifu, kwa wazi akiwa karibu na Mlima Hermoni na vilele vyake, mtunga zaburi huyo alimkumbuka Yehova.

Ikiwa unajikuta umevunjika moyo kwa sababu ya hali zisizofaa fanya kama mtunga zaburi. Ukumbuke kwamba Yehova hatawaacha watumishi wake. Yeye atakusaidia. Hata hivyo, huenda ukaona sana matokeo mabaya ya majaribu yako. Hiyo haina maana kwamba umepoteza imani yako. Ijapokuwa mtunga zaburi huyo alikuwa na tumaini hakika kwamba Yehova angekuja kumwokoa, bado yeye alihuzunika. Kwani, mazingira yenyewe ya mahali pake pa uhamisho, yajapokuwa mazuri yenyewe, yalimkumbusha hali yake yenye kuhuzunisha! Twasoma hivi: “Kilindi chapigia kilele kilindi kwa sauti ya maboromoko ya maji yako, gharika zako zote na mawimbi yako yote yamepita juu yangu.”​—Zab. 42:7.

Maneno hayo yaweza kueleza yanayotokea wakati theluji juu ya Mlima Hermoni inapoyeyuka. Maboromoko mengi ya maji hutokea nayo humwagika na kuingia kwenye Mto Yordani, na kuufanya ufurike. Ilikuwa kama kwamba wimbi moja linasemezana na wimbi jingine. Wonyesho huo wenye kuvutia wa nguvu ulimkumbusha mtunga zaburi huyo namna alivyokuwa amelemewa na mateso kana kwamba alikuwa amezungukwa na gharika.

Baada ya hapo, anaonyesha tumaini lake hakika katika yeye Aliye Juu Zaidi, akisema: “Mchana Yehova ataamuru fadhili zake za upendo, na usiku wimbo wake utakuwa nami; kutakuwa na sala kwa Mungu wa uhai wangu.” (Zab. 42:8, NW) Mlawi huyo wa jamaa ya Kora hana shaka kwamba Yehova atamwonyesha fadhili zake za upendo, au kumhangaikia kwa huruma, na kumpelekea msaada. Hilo litamwezesha kumsifu Yehova kwa wimbo na kumtolea sala ya shukrani.

Hata hivyo, mtunga zaburi huyo hawezi kujizuia asifikirie hali iliyopo yenye kutaabisha. Yeye anaendelea kusema hivi: “Nitamwambia Mungu mwamba wangu; ‘Kwa sababu gani umenisahau? Kwa sababu gani ninatembea nimehuzunika kwa sababu ya uonevu wa adui yangu?’ Wale wanaonionyesha uadui wananishutumu kwa [maneno yenye] kuua mifupa yangu, huku wakiniambia mchana kutwa: ‘Yuko wapi Mungu wako?’ Kwa sababu gani unakata tamaa, Ee nafsi yangu, na ni kwa nini unapiga kelele ndani yangu?”​—Zab. 42:9-11a, NW.

Ijapokuwa mtunga zaburi huyo alimwona Yehova akiwa kama mwamba wenye nguvu mahali ambapo mtu angeweza kupata usalama anapokimbizwa na adui, alitaka kujua kwa sababu gani ilionekana kama kwamba alikuwa ameachwa. Ndiyo, aliye Juu Zaidi alikuwa amemwacha aendelee kuhuzunika huku adui wakishangilia kwa kushinda. Mtunga zaburi huyo anasema kwamba alishutumiwa katika njia yenye chuki. Dhihaka hizo zilikuwa za ukatili hivi kwamba zingeweza kufananishwa na ‘uuaji juu ya mifupa yake’ au mwili wake wenyewe. Kwa hiyo, kwa mara nyingine aliuliza sababu alitaabika hivyo. Walakini yeye hakuyumbayumba katika imani yake, kwa kuwa alimalizia hivi: “Mngojee Mungu, kwa kuwa bado nitamsifu akiwa wokovu wangu mkuu na Mungu wangu.”—Zab. 42:11b, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki