Zaburi
Mungu Humwokoa Mwenye Kuhurumia
JE! UMEONA kwamba mara nyingi watu wengi humiminika karibu na matajiri na wenye vyeo vikubwa katika matengenezo ya kijamii? Kwa upande mwingine, mara nyingi wanaepuka walio fukara (maskini), wagonjwa ama wengine wasio na mamlaka.
Jambo lililotokea la namna hiyo linasimuliwa katika Zaburi 41. Zaburi hii inaweza kugawanywa sehemu tatu. Kwanza kutajwa ni baraka ambazo Mungu anawapa watu mmoja mmoja wanaowahurumia “wanyonge.” (Mist. 1-3) Halafu mtunga zaburi anaeleza juu ya alivyokuwa mgonjwa mahututi na maadui wake walivyomsaliti. (Mist. 4-9) Hatimaye, pana sala ya kuomba usaidizi wa kimungu na onyesho la tumaini thabiti kwamba sala hiyo ingesikiwa ifaavyo. (Mist. 10-12) Mstari wa mwisho (13) unafahamika kuwa unakamilisha cha kwanza cha vile “vitabu” vidogo vitano ambavyo katika hivyo kitabu cha Zaburi kimegawanywa.
Kichwa cha Zaburi 41 kinasema kwamba ni “wimbo wa Daudi.” Hali zinazoelezwa katika zaburi hiyo zinapatana vizuri na miaka yenye kujaa shida ya maisha ya Daudi iliyofuata kutenda dhambi kwake na Bath-Sheba. (2Sam. Sura 11-18) Hata hivyo, inasimulia mambo kama yale ambayo yamewapata watumishi waliojitoa wa Mungu katika vipindi vyote vya historia.
Zaburi hiyo inaanza hivi: “Mwenye furaha ni ye yote anayemtendea mnyonge kwa huruma.” (Zab. 41:1a, NW) Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “mnyonge” kwa halisi linamaanisha “-konda”, “-embamba.” Lina maana ya mtu ambaye ni dhaifu kwa ajili ya umaskini, maradhi ama hali zenye kushusha moyo, na ambaye anahitaji msaada. Mtu ‘anayetenda kwa huruma’ anaona uhitaji wa mtu mnyonge. Badala ya kumpita tu bila kupendezwa naye, anajali na kusaidia mtu yule mwenye uhitaji, akionyesha kuhurumia mtu mwenzake. Mtu mwenye huruma hiyo kwa kweli ni “mwenye furaha,” kwa sababu ya kufurahia hali njema ya pekee inayopatikana na mtu mkarimu na kwa sababu ya kuwa na kibali ya Mungu Mwenye Nguvu Zote, yeye ambaye ukarimu wake anauiga.—Matendo 20:35; Yak. 1:17.
Mtunga zaburi anaendelea kusema hivi kuhusu mwenye kuhurumia: “Katika siku ya msiba Yehova atamtorosha. Yehova mwenyewe atamlinda na kumhifadhi hai. Atatangazwa kuwa mwenye furaha duniani; nawe huwezi kumpeleka kwenye nafsi ya adui zake.”—Zab. 41:1b, 2, NW.
“Siku ya msiba” inaweza kuwa inahusu wakati wo wote wa msiba ama hata kipindi chenye kuendelea cha magumu. Mstari wa 3 unaonyesha kwamba mtunga zaburi alikuwa akiwazia hasa ugonjwa uliokuwa umemdhoofisha sana yule mwenye kuhurumia wanyonge. Mtu huyo alionyesha uhakika kwamba Yehova angemlinda wakati wa ugonjwa wake na ahakikishe amepona akiwa hai. Wakati ambapo wengine wangeona ushuhuda wa Mungu akitoa wokovu kutoka katika hali hiyo isiyo na tumaini ‘wangemtangaza kuwa mwenye furaha duniani’ kwa kueneza mbali habari ya Mungu ya kumtendea mtu huyo kwa rehema.
Mtunga zaburi anaendelea kusema hivi: “Yehova mwenyewe atamtegemeza [mwenye kuhurumia] akiwa mgonjwa kitini. Kitanda chake chote utakibadili kwa hakika wakati wa ugonjwa wake. Kwa habari yangu nikasema: ‘Ee Yehova nionyeshe kibali. Iponye nafsi yangu, maana nimekutenda dhambi.’”—Zab. 41:3, 4,Aliyoona mtunga zaburi alipokuwa “mgonjwa kitini” yaweza kuwa yalitokea wakati mwana wake Absalomu alipokuwa akifanya hila anyakue kiti cha enzi. Biblia inaonyesha kwamba mambo ya serikali yalikuwa yenye mchafuko wakati wa kipindi hicho cha utawala wa Daudi. Hiyo yaweza kuwa kwa sababu ugonjwa wa mfalme huyo ulikuwa unamzuia asiendeshe mambo vizuri. (2 Sam. 15:1-6) Uasi wa Absalomu na matukio mengine yenye msiba katika nyumba ya Daudi yalitimiza hukumu ya Mungu juu ya mfalme huyo kwa ajili ya uzinzi wake na Bath-Sheba na kuendesha mambo kijanja ili mumewe auawe. (2 Sam. 11:1–12:12) Daudi alikuwa anajua kwamba Mungu alikuwa amemsamehe kwa ajili ya mwenendo wake wa aibu. (2 Sam. 12:13) Walakini, akiwa amedhoofika mwili, likiwa jambo la kawaida angekumbuka kwamba alikuwa amefanya dhambi nzito.
Hata hivyo, mtunga zaburi huyo aliona kwamba iwapo angekuwa akifuatia mwendo wa kuhurumia wanyonge, Mungu ‘angemtegemeza,’ akimwegemeza na kumpa nguvu akiwa amelala asijiweze ali mgonjwa kitandani. (Linganisha Zaburi 18:24-26.) Ingawa alikuwa mgonjwa mahututi, mwandikaji huyo wa Biblia alikuwa na uhakika kwamba Mungu ‘angebadili kitanda chake,’ si kwa kuondoa ugonjwa huo kwa mwujiza, bali kwa kumtia nguvu mwenye kuteseka kwa mawazo yenye kufariji ambayo yanaleta tumaini la kupona. Ingekuwa kana kwamba Mungu alikuwa akibadili kitanda chake cha ugonjwa kuwa cha kupata afya. Kukubali kwake kuwa alikuwa ‘amemtenda dhambi’ Mungu kulimweka katika hali ya kupata kibali kwa mara nyingine. Kwa hiyo, angeweza kumuuliza Mungu ‘aponye nafsi yake,’ au amsaidie apate nafuu kutoka kwa ugonjwa wake.—Linganisha Zaburi 32:1-5.
Mtunga zaburi huyo anaendelea kusema juu ya hila aliyofanyiwa na washiriki wake alipokuwa dhaifu: “Kwa habari ya adui zangu, wanasema mabaya kunihusu: ‘Atakufa wakati gani nalo jina lake litoweke kabisa?’ Na mmoja ajapo kuniona, moyo wake unasema yasiyo kweli; anajikusanyia jambo lenye kuumiza; anaondoka nje; huko nje anazungumza juu yake.”—Zab. 41:5, 6, NW.
Adui za Daudi hawakuwa na jambo lo lote zuri la kusema juu yake. Wakiwa na kijicho walimtaja kuwa mtu mwovu. Kwa kukosa subira walitamani sana afe asikumbukwe tena. Hata wakati ‘mmoja alipokuja kumwona’ akiwa mgonjwa kitandani, maneno yake ya kusikitikia yalikuwa “yasiyo ya kweli,” yakichochewa na moyo uliotaka mgonjwa huyo afe. Mahali pa kujaribu kutoa faraja, msikitikiaji huyo mnafiki alikuwa “anajikusanyia jambo lenye kuumiza,” akitafuta jambo katika maneno, maelekeo au hali ya mwili ya mwenye kuteseka ambalo angeweza kutumia juu yake katika njia yenye kuumiza. Mara tu mgeni huyo alipoondoka “nje” ya makao ya mfalme huyo mgonjwa, alikuwa “anazungumza juu yake,” yaani, kueneza mbali habari zo zote zisizomfaa mfalme alizokuwa amekusanya wakati wa ziara yake.
Akionyesha namna porojo hizo zenye kudhuru zingeenea, mtunga zaburi huyo anaendelea kusema hivi: “Kwa umoja wote wenye kunichukia wananong’onezeana; wananifanyia hila ya jambo baya: ‘Jambo lisilofaa kitu limemwagwa juu yake; kwa kuwa sasa amelala, hatainuka tena.’”—Zab. 41:7, 8, NW.
Wenye kufanya hila juu ya Daudi walikuwa wakikusanyika na ‘kunong’onezeana,’ au kuzungumza kwa sauti za chini, uvumi wao wa kila mara, hivyo kumletea mfalme madhara. Waliendelea ‘kufanya hila’ ya jambo baya juu ya mtunga zaburi huyo kwa kueneza mazungumzo mabaya kwamba “jambo lisilofaa kitu,” yaani, maradhi, yalikuwa yameambukia mfalme sana hata kwamba ilikuwa kama kwamba yalikuwa ‘yamemwagwa juu yake.’
Maradhi hayo yalikuwa kama jambo ambalo ‘hangeinuka tena’ au kuliokoka. Hiyo ingeongeza moto wa uasi juu ya ufalme wa Daudi.
Walakini Daudi alipatwa na usaliti mbaya zaidi. Yeye anaadika hivi: “Vilevile mwanamume mwenye amani nami, ambaye nilimtumaini, aliyekuwa akila mkate wangu, amekuza kisigino chake juu yangu.” —Zab. 41:9, NW.
Hata rafiki msiri, “aliyekuwa akila mkate” akiwa mpokeaji wa kawaida wa ukaribishaji wa Daudi, alimgeuka. Msaliti huyo ‘alikuza kisigino chake’ juu ya mfalme huyo kama vile farasi anavyoweza kugeuka na kupiga teke mwenye kumlisha. Hayo yanafahamika kuwa yanahusu mshauri wa kibinafsi wa Daudi, Ahithofeli, ambaye shauri lake liliheshimiwa kana kwamba lilikuwa neno la moja kwa moja kutoka kwa Yehova. (2 Sam. 15:12; 16:23) Ahithofeli aligeuka akawa msaliti akajiunga na Absalomu katika kumpindua mfalme. (2 Sam. 15:31; 16:15)a Kwa hiyo hakuna ye yote wa wanaume hao wenye kufanya hila juu ya Daudi aliyejionyesha kuwa mtu mwenye “furaha” “anayemtendea mnyonge kwa huruma,” anayetajwa katika mstari wa kwanza wa zaburi hiyo.
Mtunga zaburi huyo anaendelea hivi: “Kwa habari yako wewe, Ee Yehova, nionyeshe kibali na unifanye niinuke, ili niwalipize.” —Zab. 41:10, NW.
Sasa mfalme huyo aliyedhoofika anazungumza na Mungu. Kwa kuwa wenzi wa Daudi walikuwa wamedai “hatainuka tena” (mst. 8), mtunga zaburi huyo alimuuliza Mungu ‘amfanye ainuke,’ yaani, amsaidie apate afya na nguvu tena. Tamaa ya ‘kulipiza’ adui zake haikuwa roho ya kulipa kisasi cha kibinafsi. Mahali pake, mfalme huyo, akiwa hakimu mkuu zaidi wa taifa hilo, alikuwa anajua kwamba wafanya hila hao wasaliti walipaswa kuadhibiwa kwa kufuata sheria kwa wakati wake kwa ajili ya faida ya wote.—Tazama Kumbukumbu la Torati 19:15-21.
Kisha, Daudi anaonyesha uhakika kwamba Mungu angesikia sala yake, akisema hivi: “Kupitia kwa hilo najua kwamba umependezwa nami, kwa sababu adui yangu hapigi kelele ya kunishinda. Kwa habari yangu, kwa sababu ya ukamilifu wangu umenitegemeza, nawe utaniweka mbele ya uso wako kwa wakati usiojulikana.”—Zab. 41:11, 12, NW.
Ilikuwa wazi kwamba Mungu alikuwa amependezwa na mtunga zaburi “kupitia kwa hilo,” yaani, kupitia kwa uhakika wa kwamba Mungu alimpa uhakikisho wa ndani kwamba adui zake ‘hawangepiga kelele ya kumshinda’ kama vile wapiganaji wenye kushinda vitani. Wakati wa ugonjwa wa Daudi, Mungu aliongoza mawazo yake kwenye sadikisho thabiti kwamba angetegemezwa ‘kwa sababu ya ukamilifu wake.’ Hapo mtunga zaburi huyo hakani kutenda dhambi kwake na vitendo vyake visivyo vya haki bali anataja mwendo wote wa maisha ya kujitoa kwa moyo wote kwa Mungu. Mahali pa kuangukia kifo cha ghafula, mtunga zaburi huyo alitazamia kuendelea kwa wakati mrefu (“kwa wakati usiojulikana”) ‘mbele ya uso wa Mungu,’ yaani, akiwa katika uhusiano wa kirafiki pamoja na Muumba na akiwa mpokeaji wa ulinzi wake.
Mstari wa mwisho wa zaburi hiyo unasema hivi: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli toka wakati usiojulikana mpaka wakati usiojulikana. Amina na Amina.” (Zab. 41:13, NW) Baada ya hayo, cha kwanza cha vitabu vile vitano vya Zaburi kinamalizika, mstari wa 13 ukiwa ni wimbo wa kusifu au namna ya maneno yenye kutoa sifa kwa Yehova Mungu na unalingana na nyimbo za sifa ambazo zamalizia miisho ya kila kimoja cha vile vitabu vingine vinne, yaani, Zaburi 72, 89, 106, na 150.
[Maelezo ya Chini]
a Alipokuwa akizungumza na mitume wake 12 wakati wa Chakula cha Jioni cha mwisho, Yesu alitumia maneno haya ya Daudi. Akionyesha uhakika wa kwamba mmoja wa wale 12 angemsaliti, Yesu alisema hivi: “Nawajua wale niliochagua. Walakini kusudi ni kwamba Andiko litimizwe, ‘Yeye aliyekuwa akila mkate wangu ameinua kisigino chake juu yangu.’” (Yohana 13:18, NW) Mungu alikuwa anajua kwamba Yesu angetendewa vibaya na mshiriki wa karibu katika njia ambayo ilifanana na yale yaliyompata Daudi.