Zaburi
Uhakika Wakati wa Hatari
MFALME DAUDI alikuwa anakabili hali ngumu sana. Mwana wake mwenyewe Absalomu alijifanya atangazwe kuwa mfalme akafanya hila akitwae kiti cha enzi. Mwana huyo mwasi alikuwa na wafuasi wengi sana hata Daudi akalazimika kukimbia kutoka mji mkuu Yerusalemu. Hata hivyo, Daudi aliendelea kuweka tumaini lake hakika katika Yehova Mungu.
Hilo laonekana wazi kutokana na wimbo ambao Daudi alitunga alipokuwa akimkimbia Absalomu. (Zaburi ya 3, maandishi ya juu katika tafsiri ya New World) Mjumbe aliripoti hivi: “Mioyo ya watu wa Israeli inashikamana na Absalomu.” (2 Sam. 15:13) Uhakika wa kwamba jambo hilo lilikuwa limetokea ulimfadhaisha sana Daudi. Alitaka kujua sababu gani jambo hilo lilikuwa limetokea na iliwezekanaje Absalomu akawa na wafuasi wengi hivyo. Kwa hiyo, katika Zaburi ya 3, Daudi alipaza sauti hivi: “[Ee Yehova], ni kwa sababu gani adui zangu wamekuwa wengi? Ni kwa sababu gani wengi wanainuka juu yangu?”—Mst. 1, NW.
Hali ilikuwa yenye kutisha sana hivi kwamba Waisraeli wengi walikata maneno kwamba hata Aliye Juu Zaidi hangeweza kumwokoa Daudi asianguke mbele ya Absalomu na watu wake. Akitaja jambo hilo, Daudi alisema hivi: “Wengi wanasema juu ya nafsi yangu: ‘Hakuna wokovu kwake kutoka kwa Mungu.’ “(Zab. 3:2, NW) Lakini je! jambo hilo lilidhoofisha uhakika wa Daudi? Hapana, kwa kuwa aliendelea kusema hivi: “Hata hivyo wewe, Ee Yehova, ndiwe ngao yangu, utukufu wangu na Yeye anayeinua kichwa changu. Kwa sauti yangu nitamwita Yehova mwenyewe, naye atanijibu kutoka mlima wake mtakatifu.”—Zab. 3:3, 4, NW.
Daudi alimwona Yehova Kama Yeye ambaye angeweza kumlinda na msiba, akimkinga kama vile ngao inavyokinga askari. Alipokuwa akimtoroka Absalomu, Daudi alitembea kwa miguu bila viatu, huku akilia na kuinamisha kichwa chake. (2 Sam. 15:30) Bila shaka aliinamisha kichwa chake kwa kuaibika. Hata hivyo, Daudi hakutia shaka kwamba Aliye Juu Zaidi angebadili hali yake iwe ya utukufu na kukiinua kichwa chake, akimwezesha kuinua kichwa chake juu, wima. Ndiyo sababu akamwitisha Yehova msaada, akiwa na tumaini hakika kwamba yeye angemjibu. Kwa kuwa sanduku la agano, ishara ya kuwapo kwa Yehova, lilikuwa limeletwa kwenye Mlima Sayuni, Daudi alitaja kwa kufaa kwamba sala yake ingejibiwa kutoka mlima mtakatifu wa Mungu.—2 Sam. 15:24, 25.
Hivyo, hata wakati wa usiku, kulipokuwa na hatari kubwa sana ya kushambuliwa ghafula, Daudi hakushikwa na woga mwingi sana na kuogopa kulala. Twasoma maneno yake haya: “Kwa habari yangu mimi, nitalala nipate usingizi; nitaamka bila shaka, kwa kuwa Yehova mwenyewe aendelea kuniunga mkono.” (Zab. 3:5, NW) Akionyesha kwamba alisadiki kabisa uwezo wa Yehova wa kuokoa, Daudi aliandika hivi: “Sitaogopa watu elfu kumi waliojipanga kunipinga wakinizunguka. Inuka, Ee Yehova! Niokoe mimi, Ee Mungu wangu! Kwa kuwa utawapiga adui zangu zote kwenye taya. Utayavunja meno ya waovu. Wokovu una Yehova. Baraka yako i juu ya watu wako.”—Zab. 3:6-8, NW.
Kuvunjwa meno kwa adui za Daudi kungeonyesha kwamba uwezo wao wa kudhuru ulikuwa umevunjwa. Yehova peke yake ndiye angeweza kuleta wokovu kama huo. Ndiyo sababu mtunga zaburi huyo akakiri kwamba “wokovu una Yehova.” Kisha, alipokuwa akifikiria magumu yake mwenyewe, Daudi alisukumwa afikirie watu wote wa Mungu akaomba baraka ya kimungu iwe juu yao.
Kama vile Daudi, haitupasi kujiachilia tushindwe na kuwaogopa wanadamu. Bila kujali yale wanayoweza kufanya waovu, Yehova hatawaacha watu wake, na kuruhusu wamalizwe duniani. Kwa hiyo, sisi nasi, na tuendelee kumhesabia wokovu Aliye Juu Zaidi.