Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 10/15 kur. 16-20
  • Hatua Unayopaswa Kuchukua!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Hatua Unayopaswa Kuchukua!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Nipo Pamoja na Ninyi Siku Zote”
  • Maonyo ya Dhoruba
  • Kutekeleza Hukumu
  • Wenye Furaha ni Wale Wanaookoka
  • Kutoka Katika Taabu ya Ulimwengu Kuingia Katika “Nchi Mpya” Yenye Amani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Mamilioni ya Walio Hai Sasa Hawatakufa Kamwe Wamalizike Katika Dunia Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Shangwe ya Ushindi wa Ufalme!
    “Ufalme Wako Uje”
  • Matetemeko ya Dunia Katika Siku ya Bwana
    Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu!
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 10/15 kur. 16-20

Hatua Unayopaswa Kuchukua!

1. Mikutano ya kundi ya Mashahidi wa Yehova inafaidije jamaa nyingi?

LEO kuna makundi zaidi ya 43,000 ya Mashahidi wa Yehova duniani pote. Wao wanakutana pamoja kila juma katika Majumba ya Ufalme yao wajifunze Biblia, mikutano yao ikiwa inaweza kuhudhuriwa na mtu ye yote anayetaka kwa unyofu wa moyo kujiongezea maarifa ya Biblia. Jamaa nzima-nzima, zenye watoto mbalimbali wa umri wote, zinaihudhuria mikutano hiyo kwenye Jumba la Ufalme. Hakika ziko faida kubwa utakazopata licha ya kuyafahamu maulizo mengi ya Biblia ambayo hapo kwanza yamekuwa yakikusumbua. Jamaa yako yote ishirikipo katika mikutano hiyo kwa saa moja au zaidi kila juma, nao wote wayatwaapo maarifa ya kanuni za Biblia, mambo yaletayo ugomvi na kuzuia jamaa isipashane habari yatakwisha kidogo-kidogo. (Zaburi 119:165) Kutakuwa na upatano mkubwa zaidi na kutumainiana kwingi zaidi. Je! hayo siyo mambo yenyewe yanayohitajiwa na jamaa nyingi?

2. Kutumia kanuni za Biblia kutasaidia katika hali gani mbalimbali maishani, na katika njia gani?

2 Kujifunza kanuni za Biblia na kuzitumia katika maisha yako ya kila siku kutakuchochea kwa njia nzuri katika hali nyingi. Kutampa mwanafunzi wa shule kusudi la kwenda shuleni, kumpe maendeleo ya kuweza kujifunza mambo na kufaidika nayo. Kutamsaidia mke mwenye kukaa nyumbani authamini ubora wa daraka lake katika jamaa. Kutamfanya mfanya kazi awe na uhusiano bora na wafanya kazi wenzake, kumwonyeshe ubora wa mfanya kazi kutambuliwa na tajiri wake. Naye tajiri wa kazi atapata kuthamini kwamba jinsi anavyoshughulika na wale walio chini ya mamlaka yake, ndivyo Yehova naye atakavyoshughulika naye. Kwa njia hiyo kuwa na kiasi na ushirikiano wa mapatano kutaziondosha nia za kichoyo, za kujitegemea binafsi, ambazo zimeenea sana katika huu ulimwengu wa kale.​—Yakobo 3:17, 18.

“Nipo Pamoja na Ninyi Siku Zote”

3. Watumishi wa Mungu wanapaswa kupigania nini kwa bidii, hata hivyo wakiwa na uhakikisho gani?

3 Wakati kanuni na mazoea ya taratibu hii ziendeleapo kuharibika, wale wanaompenda Mungu na kumfuata Kristo hawatajishusha waingilie mambo mapotovu sana yatakayoistahili adhabu ya kimungu katika ile taabu ya taabu zote zilizopata kuonekana. Watumishi waaminifu walio mashahidi wa yule Mungu wa kweli watapiga kwa umoja vita yenye jasho kuipigania imani, adui za Mungu wajapofanya jitihada za kuwaingilia wawachafue na kuwaongoza vibaya. (Linganisha Yuda 3, 4.) Watumishi hawa wa Yehova wanaahidiwa hivi na Mfalme asiyeonekana aliyechaguliwa na Mungu, ambaye sasa anatawala: “Tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka umalizio wa taratibu ya mambo [iliyopo].”​—Mathayo 28:20, NW.

4. Ni hali gani zilizobadilishwa zinazoweza kutazamiwa baada ya “dhiki ile iliyo kuu”?

4 Kuwa pamoja nao mpaka wakati huo kunamaanisha, pia, kwamba Kristo Yesu atawaingiza upesi waokokaji wa ile dhiki kubwa katika hali itakayokuwa imebadilika kabisa duniani, hali ambayo utawala wa Kristo ukiwa mbinguni utahakikisha kwamba “hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima [ufalme] wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9; Ufunuo 7:14) Watakuwa wamepotelea mbali wenye kuiharibu dunia, pamoja na silaha zao za nyukilia zilizotengenezwa kwa ufundi usioeleweka kwa urahisi! Watakuwa wamepotelea mbali waonezi na waongo na wauaji! Wakati wa utawala wa Kristo Yesu wa miaka elfu moja, yeye atawaongoza kwa imara lakini kwa upole wanadamu watakaokaa duniani, akiwapitisha kwenye ile njia inayokwenda kwenye ukamilifu wa kibinadamu.​—Ufunuo 21:4.

5. Tunapata onyo gani la upole katika Luka 21:36 na 2 Petro 3:10?

5 Karibuni sana badiliko kubwa katika hali za ulimwengu litatufikilia mbio-mbio, katika wakati ambao watu wengi watakuwa hawalitazamii, kwa maana wao hawakulisikiliza onyo hili la Biblia: “Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama [kwa njia yenye kukubalika] mbele za Mwana wa Adamu.” (Luka 21:36) Kutakuwa na machafuko makubwa ajabu katikati ya tawala zionekanazo na zisizoonekana za hii taratibu mbovu ya mambo. Akiandika kwa uongozi wa Mungu, Petro alionya hivi: “Siku ya Yehova itakuja kama mwivi, ambayo katika hiyo mbingu hizo zitatokomea kwa kelele ya s-s-s-s, lakini kwa kuwa vitu vya asili vitapata moto mwingi sana vitafumuliwa, na dunia na kazi zilizomo vitavumbuliwa.” (2 Petro 3:10, NW) Naam, Yehova atazifunua wazi hila zote za wanadamu waovu na za mashetani waovu atakapokuwa akileta taratibu nzima ya ulimwengu kwenye kikomo kinachoistahili.​—Yeremia 25:31-33.

Maonyo ya Dhoruba

6. (a) Ishara za nyakati zinaonyesha nini kuhusu wakati ujao ulio karibu? (b) Tendo la Mungu litakuwa lenye kuharibu kadiri gani?

6 Kama vile, ishara zionekanazo katika anga halisi hutoa onyo la mapema juu ya dhoruba za mvua kali na uharibifu wenye kuenea sana, na kwa hiyo ishara za nyakati zinaonyesha kwamba ile dhoruba ya mwisho inakaribia na kwamba maangamizi yanazidi kujongea yaufikilie ulimwengu. (Luka 12:54-56) Maangamizi ya tendo hilo la kimungu yatakuwa ya kadiri gani juu ya taratibu hii yenye udhalimu mwingi wa utawala wa ulimwengu? Jiamulie mwenyewe kutokana na maneno haya ya nabii wa Mungu aliyeongozwa kwa roho: “Maana [Yehova] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. . . . Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu zitakunjwa kama karatasi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika.”​—Isaya 34:2, 4.

7. (a) Isaya 51:6 inasimuliaje mwisho wa taratibu ya ulimwengu? (b) Wokovu na haki ya Yehova zinahusianaje?

7 Akitabiri tena mwisho wa taratibu nzima ya ulimwengu, pamoja na watawala wayo wenye utukufu kama nyota, na wale wanaowafuata na kuwaunga mkono, nabii anatamka hivi kwenye Isaya 51:6: “Inueni macho yenu mbinguni, mkaitazame nchi chini; maana mbingu zitatoweka kama moshi, na nchi itachakaa kama vazi, nao wakaao ndani yake watakufa kadhalika [kama nzi mdogo aumaye]; bali wokovu wangu [asema Yehova] utakuwa wa milele, na haki yangu haitatanguka.”

Kutekeleza Hukumu

8. Ni zipi sehemu za ujumbe wenye kutia woga mwingi ulioandikwa katika Ufunuo 6:12-17?

8 Halafu, pia, Mfalme aliyetukuzwa, Kristo Yesu, kupitia malaika wake alimwagiza mtume Yohana aandike ujumbe huu wenye kutia woga mwingi: “Nami nikaona, alipoifungua muhuri ya sita, palikuwa na tetemeko kuu la nchi; jua likawa jeusi kama gunia la singa, mwezi wote ukawa kama damu, na nyota zikaanguka juu ya nchi kama vile mtini upukutishavyo mapooza yake, utikiswapo na upepo mwingi. Mbingu zikaondolewa kama ukurasa ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake. Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima, wakiiambia milima na miamba, Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi [Yehova], na hasira ya Mwana-Kondoo. Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama?” (Ufunuo 6:12-17) Hakuna adui ye yote wa Yehova na wa Kristo aliye Mfalme atakayeokoka!

9. (a) Ni vikundi gani mbalimbali vitakavyolazimika kukubali hukumu ya Yehova juu yavyo? (b) Zaburi 83:17, 18 na Ezekieli 39:6, 7 zinatuambia sababu ya hukumu hiyo ni nini?

9 Hapa Biblia inaonyesha kwamba walio hodari wa dunia—watawala wa mataifa, viongozi wa kijeshi, matajiri wa kibiashara—na wote wanaowaunga mkono, ama kwa kuajiriwa au kwa kujitolea, watalazimika kukabili hukumu ya Yehova. Hawatakuwa na njia ya kutorokea! Mipango yao ya choyo ya kuhifadhi taratibu hii mbovu ya kale itashindwa. Watalazimishwa kuona kwamba hawana kibali ya mbingu. Sala ya Zaburi 83:17, 18 (NW) itajibiwa, kwa maana maadui hao wa Mungu ‘wataaibishwa na kuangamia.’ Kwa sababu gani? “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiwe Uliye Juu Zaidi ya dunia yote.” Ndiyo, huo utakuwa wakati wa Yehova kutimiza tangazo lake linalorudiwa mara 60 hivi kupitia nabii wake Ezekieli, kwamba wao “watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.”​—Ezekieli 39:6, 7, NW.

Wenye Furaha ni Wale Wanaookoka

10. Watu watakosa kupata ulinzi chini ya nini wakati wa hiyo dhiki?

10 Wanadamu watakimbia wakatafute mahali pa kujificha ili waokoe maisha zao isije ikawapata dhiki kubwa zaidi isiyopata kuonekana katika historia yote ya kibinadamu. Lakini wajifiche wapi? Wao hawatakuwa wakati huo wakimtumainia Yehova, bali watayatumainia matengenezo yao wenyewe. Basi watayaendea matengenezo ya kibinadamu ya kibiashara na serikali za kisiasa, ambayo yanaitawala dunia kama milima mirefu, yakiwa ndiyo msingi unaoishikilia taratibu iliyopo ya mambo, na hivyo wajifiche, wakijaribu kuiepuka hasira kali ya Yehova. Pasipo shaka lo lote unabii wa kimungu utatimizwa. Kilichotabiriwa na zile ishara za nyakati kitawafikia kwa kuwakatilia mbali milele katika uharibifu wenye kuwashukia wote waupingao Ufalme wa Mungu.

11. Ni nini zitakazokuwa baadhi ya sababu za furaha kati ya waokokaji hao?

11 Lakini looo, hiyo itakuwa siku yenye utukufu kama nini kwa wanyenyekevu wote wa dunia! Itakuwa ni kama kuamka baada ya kuota ndoto mbaya. Furaha itakuwa yao waokokaji hao. Kupenda fedha, ambako ndiko “shina moja la mabaya ya kila namna” kama vile kupunja watu na mashindano ya kuangamizana, kutang’olewa pamoja na mizizi yote. (1 Timotheo 6:10) Wakaaji watafanya kazi wakiwa chini ya hali zenye furaha, nao watayafurahia matunda ya kazi yao, kwa maana nabii wa Mungu anatamka hivi: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha [Yehova] wa majeshi kimesema hivi.” (Mika 4:4) Ebu fikiri! Mambo yote yaletayo mahangaiko na wasiwasi yawe yameondolewa milele ati—ajabu gani! Je! sisi tunalifurahia tumaini hilo?

12. (a) Malaki 4:2 inaelekeza kwenye kuponya gani kwa wakati ujao? (b) Mungu mwenyewe ataondolea wanadamu kasoro gani?

12 Badala ya kuwapo jua lichomalo la utawala mbaya na uonezi wa Shetani yule mungu mdogo wa bandia, Yehova wa majeshi anaahidi kwamba “kwenu ninyi mnaolicha jina langu, jua la haki litawazukia, lenye kuponya katika mbawa zake (au, miale).” (Malaki 4:2) Na licha ya magonjwa ya kimwili kuponywa, magonjwa ya akilini na moyoni pia yataponywa, ambayo yameletwa na huzuni nyingi sana nyakati zilizopita. Yataponywaje? Yataponywa kwa kukiondosha kifo na maangamizi yacho kati ya jamaa ya kibinadamu. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba jambo hilo litatukia kwa sababu Mungu anatupa ujumbe huu wenye faraja: “Tazama! Mungu amefanya makao yake kati ya watu. Atakaa kati yao, nao watakuwa watu wake, naye atakuwa Mungu wao. Yeye atayafuta machozi yao yote; maana hakutakuwako tena na kifo, wala uchungu, wala kilio, wala maumivu; maana ile hali ya kale imepita!”​—Ufunuo 21:3, 4, HNWW.

13. (a) Biblia inaelezaje tumaini la ufufuo? (b) Halafu wengi watakuwa na nafasi gani za “kwanza”?

13 Lakini namna gani wale mabilioni ambao wamekufa wakawa ‘wakilala katika mavumbi ya nchi’? (Danieli 12:2) Je! kuna tumaini lo lote kwao? Ndivyo, kwa maana kulingana na fundisho la Kristo Yesu, Paulo mtumwa wake mwaminifu alisema: “Nina tumaini kwa Mungu, . . . ya kwamba kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Ule utawala wa Kristo wa miaka 1,000 utawapa wengi wa hao wenye kurudi kutoka makaburini nafasi yao ya kwanza ya kupata ufahamu mzuri wa makusudi ya Mungu, nafasi yao ya kwanza ya kupatanisha maisha yao kwa kupenda yalingane na mapenzi ya Mungu. Huo utakuwa wakati mtukufu kama nini wa kuungana tena kwa furaha mtu na rafikiye!

14. (a) Sasa tupo katika wakati gani wenye kufaa sana? (b) Ishara za nyakati zinapaswa kutuchochea jinsi gani?

14 Kwa uhakika sisi tumependelewa kuwapo leo kwenye wakati huu wenye kufaa sana! Sasa tunaziona kila mahali zile ishara zinazoonyesha kutatokea badiliko la upesi lililo kubwa ajabu. Sisi tunaweza kufahamu kwamba Yehova amejizuia asiukatize utawala wa mataifa unaoongozwa na wanadamu wachoyo na mashetani wenye tabia za upotovu kwa muda wa kiasi ili awaonyeshe hawawezi kamwe kamwe kuletea watu wote amani na ufanisi. Sasa zile ishara za nyakati zinayafunulia macho yetu ya ufahamu kwamba hakuna wakati wa kupoteza. Ni jambo la haraka tuchukue hatua zitakazotustahilisha kupata upendeleo wa Mungu. Inatupasa tuchochewe kuchukua hatua na maneno ambayo mtume Paulo aliliambia kundi la wasikilizaji katika mji Athene wa kale. Yeye alisema kwamba Mungu ‘anawaagiza watu wa kila mahali watubu.’ (Matendo 17:30) Tukifanya hivyo, kwa kuyategemea maarifa sahihi, kisha tujiweke wakf kwa Mungu, tunakuwa na nafasi ya kumwonyesha Mwamuzi wa waamuzi wote kwamba tunaupendelea Ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo. Lakini lazima tuzichukue hatua hizo sasa, bila kukawia, maadamu utawala wa Shetani ungali unaendelea kuitawala dunia. Kufanya hivyo kutatujaribu vikali sana ionekane wazi kama tunaipenda kweli ya Mungu na haki yake.​—1 Petro 1:6, 7.

15. (a) Sasa unaweza kujibu maulizo gani, kwa faida yako mwenyewe? (b) Kama inavyoonyeshwa katika Zaburi ya 146, ni tendo gani upande wako litakaloongoza kwenye furaha ya kweli?

15 Je! wewe utakuwa mmoja wa kundi hilo lenye furaha la wakaaji? Je! wewe utakuwa umekwisha kusimama umpinge Shetani na mambo yote yasiyo haki, na kusimama umtetee Mungu na ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo kwa kumwonyesha Mungu ushikamanifu kamili? Je! wewe utakuwa umekwisha kushiriki kuwaonya viumbe wenzako na kuwapa nafasi ya kujiokoa na maangamizi ya kizazi kiovu? Ee, hilo na liwe fungu lako lenye baraka, kisha sauti yako na iunganike milele katika ule wimbo wa kumsifu Yehova kwa shukrani, yeye Mfanyiza mbingu na dunia na bahari na vyote vilivyomo.​—Zaburi 146:1, 2, 5, 6.

​—Kutoka The Watchtower, May 15, 1982.

Je! Unakumbuka?

◻ Jinsi ushirika wa kawaida katika kundi la Kikristo la kweli unavyoleta faida

◻ Yale aliyoshauri Yesu alipokuwa akimalizia unabii wake juu ya ile ishara (Luka 21:36)

◻ Maandiko fulani yanayoonyesha kadiri na sababu za tendo la hukumu la Yehova

◻ Ni mataraja gani yenye furaha yaliyo mbele ya waokokaji na ya wafu waliomo sasa ndani ya kaburi

◻ Ni hatua gani inayofaa ambayo inatakwa kwa wale wanaotumaini kuokoka

[Picha katika ukurasa wa 17]

Katika Har–Magedoni waovu hawatakuwa na kimbilio

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki