-
Maswali Kutoka kwa WasomajiMnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
-
-
Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Baadhi ya Mashahidi wa Yehova wameombwa wafanye kazi inayohusisha majengo au mali za kidini. Maandiko yana maoni gani kuhusu kazi kama hiyo?
Swali hilo laweza kuwakabili Wakristo ambao kwa moyo mweupe wanataka kutumia andiko la 1 Timotheo 5:8, linalokazia umuhimu wa mtu kuwaandalia kimwili watu wa nyumbani mwake. Ingawa bila shaka Wakristo wapaswa kutii shauri hilo, hilo halifanyi iwe halali kwao kukubali kazi za kimwili za aina zote, bila kujali wanahitajika kufanya nini. Wakristo huthamini uhitaji wa kuwa wepesi kuelewa madokezo mengine kuhusu mapenzi ya Mungu. Kwa kielelezo, tamaa ya mtu ya kutegemeza familia yake haingefanya iwe halali kwake kukiuka yale ambayo Biblia husema kuhusu ukosefu wa adili na kuua kimakusudi. (Linganisha Mwanzo 39:4-9; Isaya 2:4; Yohana 17:14, 16.) Ni muhimu pia kwamba Wakristo watende kupatana na amri ya kutoka katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli.—Ufunuo 18:4, 5.
Watumishi wa Mungu tufeni pote hukabili hali mbalimbali zinazohusu kazi ya kuajiriwa. Haingekuwa na maana yoyote wala hatuna mamlaka ya kujaribu kuorodhesha hali hizo zote na kutoa sheria za kijumla. (2 Wakorintho 1:24) Ingawa hivyo, acheni tutaje mambo fulani ambayo Wakristo wapaswa kufikiria wanapofanya maamuzi ya kibinafsi juu ya kazi ya kuajiriwa. Mambo hayo yaliorodheshwa kwa ufupi katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1982, katika makala kuhusu kufaidika na dhamiri uliyopewa na Mungu. Sanduku lilizusha maswali mawili muhimu, kisha likaorodhesha mambo mengine yenye kusaidia.
Swali la kwanza muhimu ni hili: Je, kazi hiyo ya kimwili inalaumiwa katika Biblia? Likielezea jambo hilo, gazeti Mnara wa Mlinzi lilisema kwamba Biblia hulaumu mambo kama kuiba, matumizi mabaya ya damu, na kuabudu sanamu. Mkristo apaswa kuepuka kazi ya kimwili ambayo huendeleza moja kwa moja shughuli ambazo Mungu hakubali, kama zile ambazo zimetoka tu kutajwa.
Swali la pili ni: Je, kufanya kazi hiyo kungemfanya mtu ashiriki katika zoea lenye kulaumiwa? Ni wazi kwamba mtu ambaye ameajiriwa katika chumba cha siri cha kuchezea kamari, kliniki ya utoaji-mimba, au nyumba ya kufanyia umalaya angekuwa akishiriki katika zoea lisilo la Kimaandiko. Hata ikiwa kazi yake ya kila siku hapo ingekuwa tu kufagia sakafu au kupokea simu, angekuwa akisaidia zoea ambalo Neno la Mungu hulaumu.
Wakristo wengi wanaokabiliwa na maamuzi kuhusu kazi ya kuajiriwa wamepata kwamba kuchanganua maswali hayo tu huwasaidia kufikia uamuzi wa kibinafsi.
Kwa mfano, kutokana na maswali hayo mawili, mtu aweza kuona ni kwa nini mwabudu wa kweli hangeweza kuajiriwa moja kwa moja na shirika la dini ya uwongo, akifanya kazi kwa ajili ya kanisa na katika kanisa. Andiko la Ufunuo 18:4 linatoa amri hii: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake.” Mtu aweza kuwa anashiriki kazi na dhambi za Babiloni Mkubwa ikiwa yeye ni mwajiriwa wa kawaida wa dini inayofundisha ibada ya uwongo. Hata mwajiriwa huyo awe ni mtunza-bustani, bawabu, mtengenezaji, au mhasibu, kazi yake ingeendeleza ibada ambayo huhitilafiana na dini ya kweli. Isitoshe, watu ambao wangemwona mwajiriwa huyu akifanya kazi ya kupamba kanisa, kulifanyia marekebisho, au kutekeleza shughuli zake za kidini, kwa kufaa wangemhusisha na dini hiyo.
Ingawa hivyo, namna gani mtu ambaye si mwajiriwa wa kawaida wa kanisa au shirika la kidini? Labda anaitwa kufanya kazi ya dharura ya kurekebisha bomba la maji katika sehemu ya kanisa iliyo chini ya ardhi. Je, kazi hiyo haingekuwa tofauti na kutafuta kupata kandarasi, kama vile ya kuezeka kwa mbao au kuziba paa la kanisa?
Tena, hali za namna mbalimbali zaweza kufikiriwa. Kwa hiyo, acheni tupitie mambo matano zaidi yaliyotajwa na gazeti hilo la Mnara wa Mlinzi:
1. Je, kazi hiyo ni utumishi wa kibinadamu tu ambao haukataliwi Kimaandiko? Ebu ona kielelezo cha tarishi. Kupeleka barua hakungemaanisha kwamba yeye anaendeleza kazi yenye kulaumiwa ikiwa jengo moja katika eneo analohudumia ni kanisa au kliniki ya utoaji-mimba. Mungu hutoa nuru ya jua ambayo huangaza kupitia madirisha ya majengo yote, kutia ndani kanisa au kliniki ya aina hiyo. (Matendo 14:16, 17) Huenda Mkristo ambaye ni tarishi akakata kauli kwamba anatoa utumishi wa kibinadamu kwa wote, siku baada ya siku. Hali yaweza kuwa vivyo hivyo kwa Mkristo ambaye ameitikia kazi ya dharura—fundibomba ambaye ameitwa kutengeneza bomba ambalo limesababisha mfuriko kanisani au mhudumu wa ambulansi ambaye ameitwa kusaidia mtu ambaye amezirai wakati wa ibada ya kanisa. Huenda akaona kazi hiyo kuwa ni utoaji wa dharura tu wa msaada wa kibinadamu.
2. Mtu ana mamlaka kadiri gani juu ya kazi inayofanywa? Mkristo mwenye duka hangekubali kuagiza na kuuza sanamu, hirizi za uwasiliani-roho, sigareti, au soseji zilizotengenezwa kwa damu. Akiwa mmilikaji yeye ndiye mwenye mamlaka. Huenda watu wakamsihi auze sigareti au sanamu na kupata faida, lakini yeye angetenda kupatana na itikadi zake za Kimaandiko. Kwa upande mwingine, huenda mwajiriwa Mkristo kwenye duka kubwa la chakula akapewa mgawo wa kuhesabu pesa akitumia mashine, kung’arisha sakafu, au kutunza hesabu. Yeye hana mamlaka ya kuamuru bidhaa zitakazoagizwa na kuuzwa, hata ikiwa chache kati ya bidhaa hizo zimekataliwa, kama vile sigareti au bidhaa zinazotumiwa kwa ajili ya sikukuu za kidini.a (Linganisha Luka 7:8; 17:7, 8.) Hilo linahusiana na jambo linalofuata.
3. Mtu anahusika kwa kiwango gani? Acheni turudie kile kielelezo cha duka. Labda mwajiriwa aliyepewa mgawo wa kuhesabu pesa akitumia mashine au kujaza bidhaa katika rafu, hushughulika na sigareti au bidhaa za kidini mara chache tu; hiyo ni sehemu ndogo tu ya kazi yake kwa ujumla. Hiyo ni tofauti jinsi gani na kazi ya mwajiriwa mwingine katika duka hilo ambaye hufanya kazi kwenye kaunta ya kuuzia tumbaku! Kazi yake yote, siku nenda siku rudi, yahusisha jambo lililo kinyume cha itikadi za Kikristo. (2 Wakorintho 7:1) Hilo latoa kielezi juu ya ni kwa nini kiwango cha uhusikaji au mara ambazo mtu anashughulika na bidhaa fulani, ni mambo yapaswayo kuchanganuliwa wakati wa kuamua juu ya masuala yanayohusu kazi ya kuajiriwa.
4. Malipo yanatoka wapi au kazi hiyo inafanyiwa wapi? Fikiria hali mbili. Kliniki ya utoaji-mimba yaamua kuajiri mtu wa kutunza usafi wa barabara za eneo lililoko karibu ili kuweza kuvutia umma zaidi. Malipo yake yatoka kwa kliniki hiyo ya utoaji-mimba, lakini hafanyi kazi huko, na hakuna anayemwona katika kliniki hiyo mchana kutwa. Badala yake, watu wanamwona akifanya kazi ya umma ambayo yenyewe haipingani na Maandiko, bila kujali analipwa na nani. Sasa tufikirie hali tofauti. Katika nchi ambako umalaya ni halali, shirika la huduma ya afya ya umma lamlipa muuguzi kufanya kazi kwenye madanguro, akifanya uchunguzi unaonuiwa kupunguza kuenea kwa maradhi ya kuambukiza kingono. Ingawa analipwa na shirika la huduma ya afya ya umma, yeye anafanya kazi yake yote kwenye nyumba za umalaya, akifanya ukosefu wa adili uwe salama zaidi, wenye kukubalika zaidi. Vielelezo hivyo vyatoa kielezi juu ya ni kwa nini mahali malipo ya mtu yanapotoka na mahali anapofanyia kazi, ni mambo ya kufikiriwa.
5. Matokeo ya kufanya kazi hiyo ni nini; je, itaumiza dhamiri ya mtu binafsi au kukwaza wengine? Dhamiri yetu wenyewe na ya wale wengine yapasa kufikiriwa. Hata ikiwa kazi fulani (kutia ndani mahali inapofanyiwa na mahali malipo yanapotoka) yaonekana kuwa yakubalika kwa Wakristo wengi, huenda mtu akaona kwamba hiyo ingesumbua dhamiri yake binafsi. Mtume Paulo, aliyeweka kielelezo chema, alisema hivi: “Sisi twaitibari tuna dhamiri yenye kufuata haki, kwa kuwa twataka kujiendesha wenyewe kwa kufuata haki katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Twapaswa kuepuka kufanya kazi ambayo ingetuacha katika hali ya kusumbuka; na wakati huohuo, hatupaswi kuchambua wengine ambao dhamiri zao ni tofauti. Kwa upande mwingine, huenda Mkristo asione kufanya kazi fulani kuwa kwahitilafiana na Biblia, lakini ang’amua kwamba kazi hiyo ingesumbua sana wengi katika kutaniko na katika jumuiya. Paulo alionyesha mtazamo ufaao katika maneno yake: “Katika njia yoyote sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza, ili huduma yetu isitafutiwe kosa; bali katika kila njia twajipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu.”—2 Wakorintho 6:3, 4.
Sasa acheni turudie lile swali kuu kuhusu kufanya kazi kwenye jengo la kanisa, kama vile kuweka madirisha mapya, kusafisha mazulia, au kutengeneza tanuri. Mambo yaliyo juu yaweza kuhusikaje?
Kumbuka ile hali ya kuwa na mamlaka. Je, Mkristo ndiye mmilikaji au msimamizi ambaye aweza kuamua kama atafanya kazi hiyo kwenye kanisa? Je, Mkristo mwenye mamlaka hiyo angetaka kushirikiana na Babiloni Mkubwa kwa kutafuta kupata kazi au kandarasi ya kusaidia dini fulani iendeleze ibada isiyo ya kweli? Je, jambo hilo halingekuwa sawa na kuamua kuuza sigareti au sanamu katika duka la mtu binafsi?—2 Wakorintho 6:14-16.
Ikiwa Mkristo ni mwajiriwa asiye na mamlaka ya kuamua ni kazi gani zinazokubaliwa, mambo mengine yapasa kufikiriwa, kama vile mahali kazi inapofanyiwa na kadiri anavyohusika. Je, mwajiriwa anaombwa tu mara kwa mara kupeleka au kuweka viti vipya au kutoa utumishi wa kibinadamu, kama vile kuzima moto kanisani kabla haujaenea? Wengi wangeona hiyo kuwa tofauti na kazi ya mwajiriwa kwenye biashara fulani ambaye hutumia wakati mrefu akilipaka kanisa rangi au akifanya kazi kwa ukawaida katika bustani ili kulifanya livutie. Kazi hiyo ya ukawaida au ya muda mrefu ingezidisha uwezekano kwamba wengi wangemhusianisha Mkristo huyo na dini anayodai kutounga mkono, kukiwa na uwezekano wa kuwakwaza.—Mathayo 13:41; 18:6, 7.
Tumetaja mambo kadhaa muhimu ya kufikiriwa kuhusiana na kazi ya kuajiriwa. Mambo hayo yamewasilishwa kupatana na swali hususa linalohusu dini isiyo ya kweli. Hata hivyo, mambo hayo yanaweza kufikiriwa kupatana na aina nyinginezo za kazi ya kuajiriwa. Katika kila kisa, mambo yapasa kuchanganuliwa kwa sala, kwa kuzingatia mambo hususa—na labda ya kipekee—ya hali ya wakati huo. Mambo yaliyowakilishwa juu tayari yamewasaidia Wakristo wengi wenye mioyo myeupe wafanye maamuzi ya kidhamiri ambayo yanaonyesha tamaa yao ya kutembea kwa unyofu na kwa uadilifu mbele za Yehova.—Mithali 3:5, 6; Isaya 2:3; Waebrania 12:12-14.
[Maelezo ya Chini]
a Wakristo fulani wanaofanya kazi hospitalini wamelazimika kufikiria jambo hili la mamlaka. Tabibu aweza kuwa na mamlaka ya kutoa agizo mgonjwa apewe dawa fulani au atibiwe kwa kufuata utaratibu fulani. Hata ikiwa mgonjwa hakatai, daktari Mkristo mwenye mamlaka anawezaje kuagiza utiaji-damu mishipani au utoaji-mimba, akijua vile Biblia isemavyo kuhusu mambo hayo? Kinyume cha hilo, huenda muuguzi aliyeajiriwa hospitalini asiwe na mamlaka hiyo. Anapofanya utumishi wake mbalimbali wa kawaida, huenda daktari akamwagiza apime damu kwa kusudi fulani au atunze mgonjwa aliyekuja ili kutoa mimba. Kwa kupatana na kielelezo kilichorekodiwa kwenye 2 Wafalme 5:17-19, huenda akakata kauli kwamba kwa kuwa si yeye mwenye mamlaka ya kuagiza utiaji-damu mishipani au utoaji-mimba ufanywe, basi anaweza kutoa utumishi wa kibinadamu kwa mgonjwa. Bila shaka, bado atalazimika kuifikiria dhamiri yake, ili ‘ajiendeshe mbele ya Mungu kwa dhamiri iliyo safi.’—Matendo 23:1.
-
-
Je, Wakumbuka?Mnara wa Mlinzi—1999 | Aprili 15
-
-
Je, Wakumbuka?
Je, umethamini kusoma matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Basi, ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:
◻ Kwa nini usemi wa Paulo “mabalozi walio badala ya Kristo” unafaa hasa kwa Wakristo watiwa-mafuta? (2 Wakorintho 5:20)
Nyakati za kale, mabalozi walitumwa hasa nyakati za uhasama ili kuona ikiwa vita vingeweza kuepushwa. (Luka 14:31, 32) Kwa kuwa ulimwengu wenye dhambi wa wanadamu umetengwa na Mungu, yeye amewatuma mabalozi wake watiwa-mafuta ili kuarifu watu juu ya matakwa yake ya upatanisho, akiwasihi watafute amani pamoja na Mungu.—12/15, ukurasa wa 18.
◻ Ni mambo gani manne yaliyoimarisha imani ya Abrahamu?
Kwanza, yeye alionyesha imani yake katika Yehova kwa kusikiza Mungu aliposema (Waebrania 11:8); pili, imani yake ilihusiana sana na tumaini lake (Waroma 4:18); tatu, Abrahamu alizungumza na Yehova mara nyingi; na nne, Yehova alimpa Abrahamu utegemezo alipofuata mwongozo wa Mungu. Mambo hayohayo yaweza kuimarisha imani yetu leo.—1/1, ukurasa wa 17, 18.
◻ Usemi “usituingize katika kishawishi” wamaanisha nini? (Mathayo 6:13)
Tunamwomba Mungu asituache tushindwe tunaposhawishiwa kutomtii. Yehova aweza kutuongoza tusishawishike na tusishindwe na “yule mwovu,” Shetani. (1 Wakorintho 10:13)—1/15, ukurasa wa 14.
◻ Ni lazima mtu afanye nini ili Mungu amsamehe kosa?
Ni lazima tuungame kwa Mungu tukiwa na majuto na “matunda yafaayo toba.” (Luka 3:8) Mtazamo wa toba na tamaa ya kusahihisha kosa ungechochea mtu pia atafute msaada wa kiroho wa wazee Wakristo. (Yakobo 5:13-15)—1/15 ukurasa wa 19.
◻ Kwa nini twapaswa kujitahidi kuwa wanyenyekevu?
Mtu mnyenyekevu ni mwenye subira na ustahimilivu, na hajioni kuwa wa maana sana. Unyenyekevu huvuta marafiki wa kweli wanaokupenda. Zaidi ya hayo, unyenyekevu huleta baraka za Yehova. (Mithali 22:4)—2/1, ukurasa wa 7.
◻ Ni tofauti gani muhimu iliyopo kati ya kifo cha Yesu na kile cha Adamu?
Adamu alistahili kufa, kwa kuwa alikosa kumtii Muumba wake kimakusudi. (Mwanzo 2:16, 17) Tofauti naye, Yesu hakustahili kabisa kufa, kwa kuwa “hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:22) Kwa hiyo, Yesu alipokufa, alikuwa na kitu chenye thamani kubwa sana ambacho Adamu mtenda-dhambi hakuwa nacho alipokufa, yaani, haki ya kuwa na uhai mkamilifu wa kibinadamu. Hivyo, kifo cha Yesu kilikuwa na thamani ya kidhabihu yenye kukomboa wanadamu.—2/15, ukurasa wa 15, 16.
◻ Katika ono la kiunabii la Ezekieli, jiji lilifananisha nini?
Ni lazima jiji liwe la kidunia kwa kuwa limo katikati mwa sehemu ya nchi “chafu” (isiyo takatifu). Hivyo, yaonekana jiji hilo hufananisha usimamizi wa kidunia unaowafaidi wote watakaofanyiza jamii yenye uadilifu ya kidunia.—3/1, ukurasa wa 18.
◻ Kwa nini Yesu aliosha miguu ya wanafunzi wake walipokuwa wakisherehekea Sikukuu ya Kupitwa mwaka wa 33 W.K.?
Yesu hakuwa akianzisha desturi ya kuosha miguu. Badala yake, alikuwa akiwasaidia mitume wake wawe na mtazamo mpya—mtazamo wa unyenyekevu na utayari wa kufanya kazi zilizo za chini zaidi kwa niaba ya ndugu zao.—3/1, ukurasa wa 30.
◻ Tunapofundisha wengine, ni jambo gani lililo muhimu zaidi kuliko uwezo wetu mbalimbali wa asili?
Ni sifa tulizo nazo na aina ya mazoea ambayo tumesitawisha yanayoweza kuigwa na wanafunzi. (Luka 6:40; 2 Petro 3:11)—3/15, ukurasa wa 11, 12.
◻ Wasemaji wa watu wote wanaweza kuboreshaje usomaji wao wa Maandiko?
Kwa kujizoeza. Naam, kwa kusoma kwa sauti kubwa tena na tena mpaka waweze kufanya hivyo kwa ufasaha. Ikiwa kaseti za usomaji wa Biblia zapatikana katika lugha yako, ni jambo la hekima kusikiliza namna msomaji anavyokazia maana na kubadilisha sauti na kusikiliza jinsi majina na maneno yasiyo ya kawaida yanavyotamkwa.—3/15, ukurasa wa 20.
◻ ‘Roho humrudiaje Mungu’ mtu anapokufa? (Mhubiri 12:7)
Kwa kuwa roho ndiyo kani ya uhai, hiyo ‘humrudia Mungu’ katika maana ya kwamba tumaini lolote la uhai wa wakati ujao wa mtu huyo humtegemea Mungu peke yake. Ni Mungu pekee awezaye kuirudisha roho, au kani ya uhai, akimrudisha mtu kwenye uhai. (Zaburi 104:30)—4/1, ukurasa wa 17.
-