Je, Hatujapata Kuyasikia Hapo Awali?
1 Bila shaka tumepata kuyasikia! Yehova hurudia mambo mara nyingi katika Neno lake kwa manufaa ya watu wake. Mara nyingi Yesu alirudia mafundisho yake kuhusu habari mbalimbali za Ufalme. Mitume wake walirudia mambo ya kiroho kwa kuendelea na wale ambao walikuwa wameimarishwa katika kweli.—Rom. 15:15; 2 Pet. 1:12, 13; 3:1, 2.
2 Wakati wetu, tengenezo la Yehova limepanga habari za maana zirudiwe mara nyingi katika mikutano ya kutaniko. Vichapo fulani vimesomwa mara nyingi. Naam, ni muhimu kusikia mambo ambayo tumepata kuyasikia!
3 Urudiaji Hutimiza Uhitaji Muhimu: Vikumbusha vya Yehova huongeza kwa kina uelewevu wetu, hupanua maoni yetu, na kuimarisha azimio letu la kudumu kwenye mwendo wa kiroho. (Zab. 119:129) Kuchunguza viwango vya Mungu na kanuni zake ni kama kujiangalia kwenye kioo. Hutusaidia tujichanganue wenyewe na huzuia mwelekeo wa kuwa “msikiaji msahaulifu.”—Yak. 1:22-25.
4 Tusipoendelea kujikumbusha juu ya kweli, mambo mengine yataathiri mioyo yetu. Vikumbusha vya Mungu hutuimarisha tukinze uvutano wenye kufisidi wa ulimwengu wa Shetani. (Zab. 119:2, 3, 99, 133; Flp. 3:1) Vikumbusha vya kawaida tunavyopokea kuhusu kutimizwa kwa makusudi ya Mungu hutuchochea ‘kufuliza kuwa macho.’ (Mr. 13:32-37) Kurudiwa kwa kweli za Kimaandiko hutusaidia tudumu katika barabara ya uhai wa milele.—Zab. 119:144.
5 Jinsi ya Kunufaika Kibinafsi: Lazima ‘tuelekeze mioyo yetu na vikumbusha vya Mungu.’ (Zab. 119:36) Somo lenye kufahamika linapopangiwa kuchunguzwa kwenye mkutano wa kutaniko, twapaswa kutayarisha mapema, kusoma maandiko yaliyotajwa bila kunukuliwa, na kutafakari jinsi tunavyoweza kutumia habari hiyo. Na tusikose kutayarisha pitio la kuandika la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, tukifikiria halihitajiwi. (Luka 8:18) Hatutataka kamwe kukosa kuwa makini kwa sababu kweli za msingi mara nyingi hurudiwa kwenye mikutano yetu.—Ebr. 5:11.
6 Na tuwe na mtazamo ambao mtunga-zaburi alikuwa nao: “Nimeifurahia njia ya shuhuda zako kana kwamba ni mali mengi.” (Zab. 119:14) Naam, tumesikia mambo haya yenye thamani hapo awali, na yaelekea tutayasikia tena. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anajua twahitaji kuyasikia tena!