Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 5/22 kur. 12-14
  • Ni Nani Apaswaye Kuwa Kiolezo Changu cha Kuigwa?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ni Nani Apaswaye Kuwa Kiolezo Changu cha Kuigwa?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Violezo vya Kuigwa —Vyenye Mafaa na Vinavyodhuru
  • Jinsi Kiolezo Chema cha Kuigwa Kiwezavyo Kukusaidia
  • Wazazi Wakiwa Violezo vya Kuigwa
  • Kiolezo cha Kuigwa Kilicho Bora Zaidi
  • Ninaweza Kuchagua Jinsi Gani Mtu Mzuri wa Kumwiga?
    Vijana Huuliza
  • Nichague nani kuwa mfano wa kuiga?
    Amkeni!—2012
  • Vijana Mtafanya Nini na Maisha Zenu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Je, Dini Yangu Ni Chaguo Langu au la Wazazi Wangu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 5/22 kur. 12-14

Vijana Huuliza . . .

Ni Nani Apaswaye Kuwa Kiolezo Changu cha Kuigwa?

“Kipawa chake akiwa mchezaji wa mpira wa kikapu kilikuwa kisicho cha kawaida. Marafiki wangu wote walimpenda. Alikuwa kiolezo changu cha kuigwa, na nilitaka kuwa kama yeye na kupata alichokuwa nacho.”—Ping, kijana Mwasia.

WATU ambao husifiwa na kuigwa mara nyingi huitwa violezo vya kuigwa. Mwandishi Linda Nielsen alionelea hivi: “Vijana huiga watu ambao wanaweza kushiriki hisia na mawazo yao na ambao hupokea uangalifu au thawabu watamanizo.” Kwa hiyo, vijana huelekea kuvutiwa na marika ambao hupendwa au huvutia. Lakini vijana wengi hasa huvutiwa na mabingwa wa sinema, wanamuziki, na wanariadha kuwa violezo vya kuigwa.

Bila shaka, dhana ya umma kuhusu watu wengi walio maarufu mara nyingi huwa ni ubuni uliochanganuliwa, mpango uliobuniwa kwa uangalifu ili kuficha dosari, kutia moyo usifaji wa kupita kiasi, na zaidi ya yote, kuuza! Ping, aliyenukuliwa mapema, akiri: “Nilinunua vidio zote za shujaa wangu mchezaji wa mpira wa vikapu na kuvalia aina yake ya mavazi na viatu.” Vijana wengine huvalia kama sanamu zao za televisheni au za michezo, huwa na mtindo wa nywele unaofanana na sanamu zao, na hata hutembea na kuzungumza kama sanamu zao.

Violezo vya Kuigwa —Vyenye Mafaa na Vinavyodhuru

‘Lakini kuna dhara gani katika kuvutiwa na mtu fulani?’ wauliza. Hilo lategemea unayevutiwa naye. Biblia husema: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Biblia haitutii moyo tuwe wafuasi wa binadamu. (Mathayo 23:10) Lakini hutuambia tuwe “waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Waebrania 6:12) Mwandishi wa maneno hayo, mtume Paulo, aliweka kielelezo bora kwa Wakristo wa mapema. Hivyo, angeweza kusema: “Iweni waigaji wangu, kama vile mimi nilivyo mwigaji wa Kristo.”—1 Wakorintho 11:1.

Mwanamume kijana aliyeitwa Timotheo alifanya hivyo kabisa. Alisitawisha urafiki wa karibu pamoja na Paulo kwenye safari yao ya umishonari wakiwa pamoja. (Matendo 16:1-4) Paulo akaja kumwona Timotheo kuwa ‘mtoto wake mpendwa na mwaminifu katika Bwana.’ (1 Wakorintho 4:17) Kwa msaada wa Paulo, Timotheo akawa mwanamume Mkristo mwenye kutokeza.—Wafilipi 2:19-23.

Ingawa hivyo, ni nini kinachoweza kutukia, ikiwa wachagua kiolezo cha kuigwa kisichofaa? Mwanamume kijana aliyeitwa Richard asimulia: “Nilipokuwa na umri wa miaka 15, mwanashule aliyeitwa Mario akawa rafiki yangu bora zaidi. Wazazi wangu walikuwa Wakristo, na walijaribu kunisaidia kiroho. Lakini Mario alifurahia kila kitu—disko, sherehe, pikipiki na vitu kama hivyo. Angefanya alilotaka, alipotaka. Sikuruhusiwa kufanya nililotaka. Hivyo nilipofika umri wa miaka 16, niliwaambia wazazi wangu kwamba sikutaka kuendelea kuwa Mkristo, na nikafanya hivyo.”

Je, kuna hatari zinazofanana na hizo katika kuwaona watu mashuhuri na mashujaa wa michezo kuwa violezo vya kuigwa? Ndiyo, kunazo. Basi, hakuna ubaya wowote kuvutiwa na ufundi wa mwanariadha, mwigizaji, au mwanamuziki. Lakini jiulize, ‘Watu hawa huweka kielelezo cha aina gani katika maisha yao ya kibinafsi?’ Je, wengi wa mashujaa wa michezo, wanamuziki, na wachezaji wengine hawajulikani kwa sababu ya kujiingiza kwao katika ukosefu wa adili katika ngono, dawa za kulevya, na alkoholi? Je, pia si kweli kwamba wengi huishi maisha yasiyo na furaha, maisha yasiyoridhisha, licha ya pesa zao na fahari? Utazamapo mambo kwa maoni haya, ni manufaa gani iwezayo kupatikana kutokana na kuwaiga watu kama hawa?

Kweli, kuiga mtindo wa nywele wa mtu maarufu, mavazi yake, au usemi wake huenda kukaonekana kuwa jambo dogo. Lakini hiyo yaweza kuwa hatua ya kwanza kuuruhusu ulimwengu “ukufinyange kulingana na mtindo wake.” (Waroma 12:2, Phillips) Kufinyangwa huko kwaweza kuonekana kuwa kwenye kupendeza mara ya kwanza. Lakini ikiwa utashindwa kabisa na uvutano wake, utafinyangwa katika njia ambazo kwa hakika zitakufanya utofautiane na Mungu. “Urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu,” yasema Biblia katika Yakobo 4:4.

Jinsi Kiolezo Chema cha Kuigwa Kiwezavyo Kukusaidia

Hata hivyo, kumwiga mtu fulani ambaye anaweka kielelezo chema, kwaweza kuathiri maisha yako kwa njia inayofaa! Miongoni mwa Wakristo wenzako, waweza kuwapata wengi ambao ni “kielelezo . . . katika kusema, katika mwenendo, katika upendo, katika imani, katika usafi wa kiadili.” (1 Timotheo 4:12) Kweli, lazima uwe mwenye tahadhari uchaguapo washiriki, hata katika kutaniko la Kikristo. (2 Timotheo 2:20, 21) Lakini kwa kawaida huwa si vigumu kutambua wale ambao katika kutaniko kwa kweli “wanatembea katika kweli.” (2 Yohana 4) Kanuni iliyo katika Waebrania 13:7 hutaarifu: “Nanyi mfikiriapo jinsi mwisho wa mwenendo wao upatavyo kuwa, igeni imani yao.” Kwa wengi wa marika wako, namna mwenendo wao utakavyokuwa ni jambo lisilojulikana bado. Lakini kunao wenye umri mkubwa zaidi katika kutaniko ambao wamethibitisha imani yao, na ni jambo la hekima kufahamiana nao.

‘Nifahamiane na wenye umri mkubwa zaidi?’ huenda ukauliza. Kweli, huenda hili lisisikike kuwa jambo lenye kuvutia sana mara ya kwanza. Lakini kumbuka uhusiano aliokuwa nao Timotheo pamoja na rafiki yake mwenye umri mkubwa zaidi mtume Paulo. Paulo aliona uwezo wa Timotheo na kumtia moyo ‘achochee kama moto zawadi ya Mungu’ iliyo katika yeye. (2 Timotheo 1:6) Je, halingekuwa jambo lenye mafaa kuwa na mtu wa kukusaidia na kukutia moyo, mtu ambaye atakuhimiza kusitawisha zawadi zako za kupewa na Mungu?

Kijana aitwaye Bryan alipata jambo hili kuwa kweli. Alikuwa akipigana na hisia za kujihisi duni alipofahamiana na mtumishi wa huduma mseja, mwenye umri mkubwa zaidi katika kutaniko. Bryan asema: “Navutiwa na hangaiko lake lenye upendo kwa wengine, kutia ndani mimi; bidii yake kwa ajili ya huduma; na hotuba zake nzuri.” Tayari Bryan ananufaika kutokana na uangalifu wa kibinafsi ambao amepokea kutoka kwa Mkristo huyu mwenye umri mkubwa zaidi. Yeye akiri hivi waziwazi: “Jambo hili limenisaidia kubadilika—kutoka kuwa mtu mwenye haya na mwenye utu usio na uchangamfu.”

Wazazi Wakiwa Violezo vya Kuigwa

Kitabu Adolescence—Generation Under Pressure husema kwamba wazazi ndio “uvutano wa nje wa pekee zaidi katika kusaidia au kuzuia mbalehe wa kawaida kuwa na utu unaofaa.” Bila mwongozo huo dhahiri na utambulisho, kitabu hicho chaongezea, vijana “watakuwa kama meli isiyo na mtambo wa usukani, inayobadili mwendo wakati kila wimbi lipitapo.”

Shauri hili ladhihirisha kile alichoandika mwanafunzi Yakobo zaidi ya miaka 1,900 iliyopita, kama ilivyorekodiwa katika Yakobo 1:6: “Acheni afulize kuomba katika imani, bila kutia shaka hata kidogo, kwa maana yeye atiaye shaka ni kama wimbi la bahari liendeshwalo na upepo na kupeperushwa huku na huku.” Labda unawajua vijana fulani wa rika lako walio hivyo. Wao huelekea kuishi kwa misisimuko ya leo, bila kufikiria ya kesho.

Je, umebarikiwa kuwa na wazazi wenye kumhofu Mungu ambao huweka kielelezo chema katika kutaniko? Ikiwa ndivyo, je, unakubali uvutano wao? Au je, unapigana nao wakati wote? Kweli, wazazi wako si wakamilifu. Lakini usifunge macho kuona sifa zao nzuri—sifa utakazofanya vizuri kuiga. “Navutiwa sana na wazazi wangu,” aandika kijana mmoja Mkristo anayeitwa Jarrod. “Bidii yao yenye kuendelea katika huduma, namna walivyokabili magumu ya kiuchumi, na kitia-moyo walichonipa kushiriki katika huduma ya wakati wote, yote hayo yaliniathiri ifaavyo. Wazazi wangu wamekuwa violezo vyangu vya kuigwa sikuzote.”

Kiolezo cha Kuigwa Kilicho Bora Zaidi

Wakati shirika la ukaguzi la Gallup lilipowauliza vijana nchini Marekani ni nani waliyemfikiria kuwa mtu mkuu zaidi katika historia, wengi zaidi walichagua wanasiasa Wamarekani walio mashuhuri. Ni asilimia 6 tu waliochagua Yesu Kristo. Hata hivyo, Biblia hutuambia kwamba Yesu Kristo alituachia ‘kigezo ili sisi tufuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21; Waebrania 12:3) Anawatia moyo wanafunzi wake wajifunze kutoka kwake. (Mathayo 11:28, 29) Ungeweza kujifunza namna gani kutoka kwa Yesu?

Fahamu kikamili maisha ya Yesu. Jaribu kusoma masimulizi yote ya Gospeli, pamoja na kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi.a Chunguza namna ambavyo Yesu alifundisha, njia ya fadhili aliyotumia kushughulika na watu, na moyo mkuu alioonyesha alipokuwa chini ya mkazo. Utapata kwamba Yesu ndiye kiolezo cha kuigwa kilicho bora zaidi ambacho ungeweza kufuata.

Kadiri utakavyofahamu zaidi kiolezo cha kuigwa kilicho kikamilifu, ndivyo utakavyovutwa kwa kadiri ndogo kwa marika wasiofaa au watu mashuhuri. Je, wamkumbuka Ping na kuvutiwa kwake na shujaa wa michezo? Ping hufurahia mchezo wa mpira wa vikapu pindi kwa pindi, lakini amekuja kuona kwamba ni jambo la upumbavu kuiga watu mashuhuri.

Namna gani Richard? Uchaguzi wake wa violezo vya kuigwa ulimwongoza kuacha imani ya Kikristo. Hata hivyo, Richard alikuja kumfahamu mwanamume mchanga aliyekuwa katika umri wake wa miaka ya 20, aliyeitwa Simon, ambaye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Simon alinifanya kuwa rafiki,” asema Richard, “na kunisaidia nione kwamba mtu aweza kufurahia maisha bila kuridhiana kanuni za Biblia. Upesi nikaanza kumstahi Simon, na kielelezo chake kilichangia sana kurudi kwangu kwenye kutaniko na kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova. Sasa nina furaha zaidi, na maisha yangu yana kusudi halisi.”

Ndiyo, uchaguzi wako wa violezo vya kuigwa ni wa maana sana!

[Maelezo ya Chini]

a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kushirikiana na watu wenye umri mkubwa zaidi walio na sifa njema kwaweza kukusaidia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki