Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 9/22 kur. 18-20
  • Naweza Kukazaje Fikira?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kukazaje Fikira?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uwe na Upendezi
  • Kuchoshwa na Walimu Wachoshi
  • Kukazia “Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”
  • Jinsi ya Kunufaika Zaidi na Mikutano
  • “Kazia Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kwa nini uhudhurie mikutano ya Kikristo?
    Amkeni!—2012
  • ‘Kazia Uangalifu Jinsi Unavyosikiliza’
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Jinsi Yehova Anavyotuongoza
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 9/22 kur. 18-20

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kukazaje Fikira?

“Nilitumia muda mrefu mikutanoni bila kufaidika nayo. Akili zangu zingetangatanga tu.”—Matthew.

JE, UMEWAHI kuketi darasani au kwenye mikutano ya Kikristo na kisha kwa ghafula ukatambua kwamba hukuwa na habari kuhusu mambo yaliyokuwa yakizungumziwa? Basi, ikiwa akili yako hutangatanga nyakati fulani, si wewe peke yako. Kama ilivyotaja makala moja iliyotangulia, kukaza fikira kwa muda mfupi ni jambo la kawaida miongoni mwa vijana.a Hata hivyo, waweza kukuza uwezo wako wa kukaza fikira kwa kufanya jitihada kidogo na marekebisho fulani katika mtazamo wako.

Uwe na Upendezi

Fikiria mwanariadha aliyezoezwa. “Kila mtu anayeshiriki katika shindano hutumia kujidhibiti katika mambo yote,” asema mtume Paulo. Mwanariadha akijiruhusu avutwe fikira hata kwa kitambo kidogo, atashindwa. Ili ashinde, apaswa kukaza fikira—akipuuza makelele ya umati, maumivu yake na uchovu, bila kufikiria uwezekano wa kushindwa. Lakini ni nini huchochea wanariadha kufanya jitihada kama hiyo isiyo ya kawaida? Kulingana na mtume Paulo, wao hufanya hivyo ili “waweze kupata taji lenye kuharibika”—vikombe na sifa wanayopewa washindi.—1 Wakorintho 9:25.

Vivyo hivyo, ili kukaza uangalifu lazima uchochewe! Kitabu Study Is Hard Work, cha William H. Armstrong, chasema: “Ni daraka la mwanafunzi kupendezwa na somo. Hakuna mtu awezaye kukufanya upendezwe, na hakuna mtu awezaye kuongeza upendezi wako isipokuwa watamani kufanya hivyo mwenyewe.” Ili kufahamu ulimwengu unaokuzunguka, wahitaji ujuzi. Kadiri ujuavyo mengi zaidi, ndivyo uwezavyo kujifunza mengi zaidi. “Maarifa huwa mepesi kwa mwenye ufahamu,” yasema Mithali 14:6. Huenda usikumbuke mambo yote unayojifunza shuleni, lakini angalau, shule hukusaidia kusitawisha uwezo wa kufikiri. (Linganisha Mithali 1:4.) Kujitia nidhamu ya akili na kuwa na uwezo wa kufikiri kutakunufaisha katika maisha yako yote.

Kuchoshwa na Walimu Wachoshi

Hata hivyo, vijana fulani hulalamika kwamba hata walimu wao hawapendezwi. Kijana mmoja anayeitwa Jesse asema hivi: “Walimu wanasimama mbele yako, wanasema kitu fulani, wanakupa mgawo, na kisha kukuambia uende nyumbani. Nafikiri ni wazembe. Hatuoni haja ya kukaza uangalifu kwa sababu walimu hawatendi kama habari hiyo ni ya maana.”

Basi, je, ufikie mkataa kwamba kukaza fikira ni kupoteza wakati? Si lazima iwe hivyo. Walimu wengi waweza kukwama katika hali hiyo. Kijana mmoja anayeitwa Collin aeleza hivi: “Hakuna mtu anayekazia fikira walimu, kwa hiyo walimu wanafikiri kwamba hakuna anayetaka kujifunza. Kisha hawafundishi kwa nguvu na shauku.”

Amini usiamini, waweza kuacha tabia hii. Jinsi gani? Kwa kukaza uangalifu tu. Mwalimu aliye mchoshi aweza kuamsha tena upendezi katika kazi yake akiwa na mwanafunzi mmoja tu anayependezwa. Ni kweli kwamba walimu fulani hawawezi kudumisha upendezi wa wanafunzi. Lakini, kabla hujajiingiza katika ndoto za mchana, jiulize mwenyewe, ‘Je, anafahamu anachoongea?’ Ikiwa ndivyo, amua kujifunza kitu fulani kutoka kwake. Sikiliza kwa makini—kaza fikira! Shiriki mazungumzo ya darasani. Uliza maswali yenye kulenga shabaha. Kitabu How to Study in High School chasema: “Wanafunzi wengi huliona kuwa jambo lenye kusaidia kuchora michoro, kuandika maneno, chati, fasili, na mawazo makuu ambayo mwalimu huandika kwenye ubao au kuyakazia.”

Kukazia “Uangalifu Zaidi Kuliko Ilivyo Kawaida”

Hata hivyo, waweza kufaidika au kupata hasara zaidi unaposikiliza mikutano ya Kikristo. Jesse akiri hivi: “Nyakati fulani vijana hawakazii uangalifu mikutano kwa sababu hawatambui umaana wa mikutano.” Kwenye Waebrania 2:1, twaamriwa “kukazia uangalifu zaidi kuliko ilivyo kawaida mambo yaliyosikiwa nasi, ili tusipate kamwe kupeperushwa mbali.” Je, waweza kukumbuka jambo fulani katika kila hotuba baada ya kuhudhuria mkutano wa kutaniko? Au je, nyakati fulani hupata kwamba hata huwezi kukumbuka waliokuwa na sehemu katika programu?

Mara nyingine tena, kutambua umaana wa yale unayojifunza kwahusika. Kwani, uhai wako hasa wahusika! (Yohana 17:3) Jambo jingine la kutafakari ni: Unapojifunza juu ya Biblia, unajifunza kufikiri kama Mungu! (Isaya 55:8, 9) Na utumiapo mambo unayojifunza, unakuwa ukivaa ule unaoitwa na Biblia “utu mpya.” (Wakolosai 3:9, 10) Kwa upande mwingine, ukikosa kukaza fikira, huenda usifanye maendeleo yanayohitajika katika maisha yako; utaduwaza ukuzi wako wa kiroho. Yehova anajua kwamba sote tuna mwelekeo wa kuacha akili zetu zivutwe kwingineko. Hivyo, anatusihi: “Nisikilizeni kwa bidii . . . Tegeni masikio yenu na kunijia. Sikieni, na nafsi zenu zitaishi.”—Isaya 55:2, 3.

Jinsi ya Kunufaika Zaidi na Mikutano

Ijapokuwa hivyo, huenda likawa jambo gumu kukaza uangalifu kwa mikutano mara ya kwanza. Lakini watafiti wanadai kwamba kadiri tujizoezavyo kukaza fikira, ndivyo akili zetu huwa stadi katika kazi hii. Matthew, aliyetajwa katika utangulizi, alishinda mwelekeo wa kutangatanga kwa akili zake wakati wa mikutano. Asema hivi: “Nilipata kwamba napaswa kujitia nidhamu ili kukaza uangalifu. Baada ya muda hali huwa bora, na unaweza kukaza uangalifu kwa vipindi virefu.” Pia Matthew ataja jambo moja kubwa linalofanya mikutano impendeze. Asema hivi: “Mimi hujifunza mapema.” Vivyo hivyo, kijana aitwaye Charese asema: “Ninapokuwa nimejitayarisha, mimi huhisi kuwa nahusika na mikutano. Hotuba huvutia zaidi na huwa zenye umaana zaidi kwangu.”

Ni muhimu pia kuzuia mawazo yenye kukengeusha. Kweli, waweza kuwa na mahangaiko kadhaa ya halali akilini: mtihani utakaofanya juma lijalo, kutopatana kunakokusababishia mkazo, gharama fulani utakayohitaji kulipia. Lakini Yesu alitoa shauri hili: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika aweza kuongeza dhiraa moja kwenye muda wake wa uhai? Kwa hiyo, msihangaike kamwe juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe. Waitosha kila siku ubaya wayo yenyewe.” (Mathayo 6:27, 34) Kukaza fikira kwenye mikutano ya kutaniko hakutaondoa matatizo yako, lakini kutakuimarisha kiroho, ili uweze kukabiliana vema na matatizo.—Linganisha 2 Wakorintho 4:16.

Kusikiliza kwa makini kwaweza kukusaidia pia ukaze fikira. Matthew asema hivi: “Mimi hutazamia mambo atakayotaja msemaji katika hotuba yake na kisha kuona namna anavyofanya.” Jiulize mwenyewe hivi, ‘Ni yapi mambo makuu yanayojadiliwa? Naweza kutumiaje mambo yanayofundishwa?’ Kutazamia mambo yatakayosemwa na msemaji kwaweza pia kukusaidia kukaza fikira. Jaribu kuelewa hoja zake. Ona hoja za Kimaandiko anazotumia. Fikiria na kufanya muhtasari wa mambo makuu aliyotaja. Andika mambo machache yenye maana. Shiriki katika sehemu inayohusisha wasikilizaji! Kufanya hivyo kwaweza kusaidia kufanya akili yako ikaziwe na kuzuia mawazo yako yasitangetange.

Ni kweli kwamba kusikiliza kwaweza kuwa jambo gumu hasa ikiwa msemaji hana shauku au utoaji wake unachosha. Kumbuka yale ambayo Wakristo fulani wa karne ya kwanza walisema kuhusu namna walivyoona uwezo wa mtume Paulo wa kusema: “Kuwapo kwake mwenyewe binafsi ni dhaifu na usemi wake wa kudharaulika.” (2 Wakorintho 10:10) Lakini Paulo alijibu uchambuzi huo kwa kusema: “Lakini hata ikiwa sina ustadi katika usemi, hakika sivyo nilivyo katika ujuzi.” (2 Wakorintho 11:6) Ndiyo, ikiwa wasikilizaji wake wangepuuza udhaifu wa Paulo wa kusema na kukazia mambo aliyokuwa akisema, wangejifunza mengi ya “mambo yenye kina kirefu ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Kwa njia hiyohiyo, unaweza kujifunza hata kutoka kwa msemaji “mchoshi,” ukikaza fikira na kusikiliza. Labda. Huenda hata akataja maana yenye tofauti kidogo au akatumia andiko katika njia ambayo hujapata kufahamu kamwe.

Maneno ya Yesu kwenye Luka 8:18 yatoa muhtasari huu mzuri: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo.” Kwa kweli, kujifunza kukazia uangalifu na si kuacha fikira zitangetange kwahitaji jitihada na mazoezi. Lakini baada ya muda utanufaika. Kujifunza kukaza fikira kwaweza kumaanisha kupata maksi bora—na la maana zaidi, ukuzi wa kiroho!

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Siwezi Kukaza Fikira?,” katika toleo letu la Julai 22, 1998.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ili kukazia uangalifu ni muhimu kukuza upendezi katika mambo unayosikiay

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki