‘Kazia Uangalifu Jinsi Unavyosikiliza’
KUSIKILIZA ni muhimu ili kujifunza mambo. Pia kusikiliza kunaweza kuokoa uhai. Yehova alipokuwa akitayarisha kuwakomboa watu wake watoke utumwani Misri, alimpa Musa maagizo. Musa akawapa wazee wa Israeli masharti ya kufuata ili malaika wasiwaue wazaliwa wao wa kwanza. (Kut. 12:21-23) Wazee hao wakajulisha kila familia habari hiyo kwa mdomo. Watu walipaswa kusikiliza kwa makini. Walitendaje? Biblia inaripoti hivi: “Ndivyo walivyofanya wana wa Israeli wote; kama BWANA alivyowaagiza Musa na Haruni, ndivyo walivyofanya.” (Kut. 12:28, 50, 51) Matokeo yakawa kwamba Waisraeli walikombolewa kwa njia ya kustaajabisha sana.
Leo, Yehova anatutayarisha tupate ukombozi mkubwa hata zaidi. Na tuchukulie kwa uzito maagizo anayoandaa. Maagizo hayo huandaliwa katika mikutano ya kutaniko. Je, unafaidika kabisa na mikutano hiyo? Hiyo inategemea sana jinsi unavyosikiliza.
Je, wewe hukumbuka mambo makuu ya maagizo tunayopata kwenye mikutano? Je, una mazoea ya kujaribu kuona jinsi unavyoweza kutumia katika maisha yako maagizo yanayotolewa, au kuwaeleza wengine mambo hayo, juma baada ya juma?
Tayarisha Moyo Wako
Tunahitaji kutayarisha mioyo yetu ili tufaidike kabisa na maagizo yanayoandaliwa kwenye mikutano ya Kikristo. Kisa fulani kilichotokea wakati wa utawala wa Mfalme Yehoshafati wa Yuda kinakazia kwamba ni muhimu kutayarisha mioyo yetu. Yehoshafati aliunga mkono ibada ya kweli kwa ujasiri. ‘Alipaondoa mahali mahali pa juu na maashera katika Yuda.’ Pia aliwaamuru wakuu, Walawi, na makuhani wawafundishe watu Sheria ya Yehova katika majiji yote ya Yuda. Lakini, “mahali pa juu hapakutoweka kabisa.” (2 Nya. 17:6-9; 20:33, NW) Ibada ya miungu ya uongo na ibada mbaya iliyotumiwa kumwabudu Yehova katika mahali mahali pa juu pa kipagani ilikuwa imesitawi sana hivi kwamba haikuweza kuondolewa kabisa.
Kwa nini agizo lililotolewa na Yehoshafati halikufaulu baadaye? Maandiko yanaendelea kusema: “Mioyo ya watu bado haijakazwa [“haikuwa imetayarishwa,” NW] kwa Mungu wa baba zao.” Walisikia lakini hawakutenda waliyosikia. Labda waliona wanajisumbua tu kusafiri kwenda hekaluni Yerusalemu kutoa dhabihu. Kwa vyovyote vile, imani haikuchochea mioyo yao.
Ni lazima tutayarishe mioyo yetu kupokea maagizo ambayo Yehova anaandaa leo ili tusije tukazirudia polepole njia za ulimwengu wa Shetani. Tutayarisheje mioyo yetu? Njia moja muhimu ni sala. Tunapaswa kusali ili tupokee maagizo ya Mungu kwa shukrani. (Zab. 27:4; 95:2) Sala itatusaidia tuthamini jitihada za ndugu zetu ambao, ingawa si wakamilifu, wanakubali kutumiwa na Yehova kuwafundisha watu wake. Itatuchochea kumshukuru Yehova kwa ajili ya mambo mapya tunayojifunza na vilevile nafasi tunazopata za kuthamini hata zaidi mambo ambayo tayari tumejifunza. Kwa sababu tunataka kufanya mapenzi ya Mungu kikamilifu, tunasali hivi: “Unifundishe, Ee Yehova, njia yako. . . . Ungamanisha moyo wangu kuhofu jina lako.”—Zab. 86:11, NW.
Kaza Fikira
Kuna mambo mengi yanayofanya tusisikilize kwa makini. Huenda akili zetu zikajaa mahangaiko mengi. Tunaweza kukengeushwa na kelele na pia watu wanaopita-pita miongoni mwa wasikilizaji au nje. Huenda ikawa vigumu kukaza fikira kama kuna kitu kinachoharibu starehe yetu. Mara nyingi wale wenye watoto wachanga husikiliza nusu-nusu. Basi tunaweza kufanya nini ili tukaze fikira kwenye programu?
Macho huongoza sana fikira zetu. Uyatumie kukaza fikira kwa kumtazama msemaji wakati wote. Anapotaja andiko la Biblia, lifungue na ufuatane naye anapolisoma hata kama unalifahamu andiko hilo. Epuka kutazama sehemu ambayo kelele zinatokea au kumtazama mtu anayepita. Ikiwa macho yako yanajaza akili yako habari zenye kukengeusha, utakosa sehemu kubwa ya mambo yanayozungumzwa jukwaani.
Ikiwa “mawazo ya moyoni” yanafanya iwe vigumu ukaze fikira kwenye programu, omba Yehova upate utulivu wa akili na moyo ili usikilize kwa makini. (Zab. 94:19; Flp. 4:6, 7) Ikihitajika, sali tena na tena. (Mt. 7:7, 8) Mikutano ya kutaniko ni uandalizi wa Yehova. Uwe na hakika ya kwamba anataka ufaidike nayo.—1 Yoh. 5:14, 15.
Kusikiliza Hotuba
Inaelekea kwamba kuna mambo ya kupendeza sana ambayo umewahi kusikia katika hotuba mbalimbali. Lakini kusikiliza hotuba hakumaanishi kukumbuka tu mambo yenye kutokeza. Hotuba ni kama safari. Ingawa huenda kukawa na vitu vingi vyenye kuvutia njiani, jambo kuu ni kusudi au mwisho. Huenda ikawa msemaji anajaribu kuongoza wasikilizaji wafikie uamuzi fulani au kuwachochea wachukue hatua fulani.
Ebu fikiria hotuba ambayo Yoshua alitolea taifa la Israeli. Hotuba hiyo iko katika Yoshua 24:1-15. Kusudi lake lilikuwa kuwachochea watu wawe thabiti katika ibada ya kweli kwa kujitenga kabisa na ibada ya sanamu ya mataifa jirani. Kwa nini hiyo ilikuwa muhimu sana? Ibada ya uongo ilikuwa imeenea na ilihatarisha sana uhusiano mzuri uliokuwapo kati ya taifa hilo na Yehova. Watu waliitikia ombi la Yoshua wakasema: ‘Hasha! tusimwache BWANA, ili kuitumikia miungu mingine. Sisi tutamtumikia BWANA.’ Na ndivyo walivyofanya!—Yos. 24:16, 18, 31.
Unaposikiliza hotuba, jaribu kutambua kusudi lake. Fikiria jinsi ambavyo maneno ya msemaji yanaingiana na kusudi hilo. Jiulize habari hiyo inataka ufanye nini.
Kuwa Msikivu Wakati wa Mazungumzo
Funzo la Mnara wa Mlinzi, Funzo la Kitabu la Kutaniko, na sehemu fulani za Mkutano wa Utumishi ni mazungumzo ya maswali kwa majibu ya habari ambazo zimechapwa zinazotegemea Biblia.
Kwa njia fulani, kusikiliza mazungumzo ni kama kushiriki katika mazungumzo. Ili ufaidike kabisa, sikiliza kwa makini. Angalia mazungumzo yanaelekea wapi. Ona jinsi kiongozi anavyokazia kichwa kikuu na mambo makuu. Uyajibu maswali yake kimoyomoyo. Sikiliza wengine wanapotoa maelezo na kuonyesha jinsi habari hiyo inavyotumika. Kwa kufikiria habari hiyo kulingana na maoni ya wengine, unaweza kuelewa hata zaidi jambo ambalo tayari unalifahamu. Changia mazungumzo hayo kwa kutoa maelezo yako mwenyewe ya imani.—Rom. 1:12.
Ukijifunza mapema habari itakayoshughulikiwa, utaweza kushiriki katika mazungumzo na kufuatana na maelezo ya wengine. Ikiwa hali zako zinafanya iwe vigumu kujifunza vizuri habari hiyo, chukua angalau dakika chache kuipitia kabla ya mkutano. Ukifanya hivyo, utafaidika zaidi na mazungumzo.
Kusikiliza Kwenye Makusanyiko
Inaelekea kwamba kuna mambo mengi yenye kukengeusha fikira kwenye makusanyiko kuliko kwenye mikutano ya kutaniko. Na mambo hayo yanaweza kufanya iwe vigumu zaidi kusikiliza. Ni nini kinachoweza kutusaidia?
Ni muhimu kulala vizuri usiku. Kila siku kabla ya programu kuanza, kazia akilini kichwa cha siku hiyo. Tazama kichwa cha kila hotuba na ujaribu kuwazia mambo ambayo yatazungumziwa. Tumia Biblia yako vizuri. Watu wengi wamegundua kwamba wanapoandika maandishi mafupi ya mambo makuu wao hukaza akili kwenye programu. Andika mambo ambayo unapanga kutumia katika maisha yako na huduma yako. Zungumzieni mambo machache kila siku mnaposafiri kwenda kwenye mkusanyiko na mnaporudi kutoka huko. Hiyo itakusaidia kukumbuka mambo unayosikia.
Kuwazoeza Watoto Kuwa Wasikivu
Wazazi Wakristo wanaweza kuwasaidia watoto wao—hata wale wachanga—wawe na “hekima kwa ajili ya wokovu.” Wanaweza kufanya hivyo wakija nao kwenye mikutano ya kutaniko na makusanyiko. (2 Tim. 3:15) Kwa kuwa watoto wanatofautiana na wana uwezo tofauti wa kukaza fikira, ufahamu unahitajika ili kuwasaidia wajifunze kusikiliza kwa makini. Labda madokezo yanayofuata yanaweza kusaidia.
Mkiwa nyumbani, panga kuwe na nyakati ambazo watoto wako wachanga wanaketi kimya na kusoma au kutazama picha za vichapo vyetu vya Kikristo. Usiwape watoto vitu vya kuchezea kwenye mikutano eti wasisumbue. Kama ilivyokuwa katika Israeli la kale, leo pia watoto huhudhuria mikutano ili “wapate kusikia na kujifunza.” (Kum. 31:12) Mahali inapowezekana, wazazi wengine huwapa hata watoto wachanga sana vichapo vinavyotumiwa mikutanoni. Watoto wanapozidi kukua, uwasaidie kutayarisha ili washiriki katika programu zinazohusu maswali na majibu.
Maandiko yanafunua kwamba kumsikiliza Yehova kunahusiana sana na kumtii. Maneno haya ambayo Musa aliambia taifa la Israeli yanathibitisha jambo hilo: ‘Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima; kwa kumpenda BWANA, Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye.’ (Kum. 30:19, 20) Kusikiliza maagizo ambayo Yehova anaandaa na kuyatii maishani mwetu ni muhimu ili kupata kibali cha Mungu na baraka ya uhai wa milele. Basi ni muhimu kama nini kutii himizo hili la Yesu: “Kazieni uangalifu jinsi msikilizavyo”!—Luka 8:18.