Uwe Msikilizaji Mzuri
1 Ili kusikiliza kwa makini mtu anahitaji kujidhibiti. Pia msikilizaji anahitaji kuwa na hamu ili ajifunze na kunufaika na yale anayosikia. Kwa sababu hiyo, Yesu alisisitiza uhitaji wa ‘kukazia uangalifu jinsi usikilizavyo.’—Luka 8:18.
2 Jambo hilo lafaa hasa tuhudhuriapo mikutano ya kutaniko, makusanyiko, na mikusanyiko. Hizo ndizo pindi ambazo lazima tusikilize kwa makini. (Ebr. 2:1) Yafuatayo ni baadhi ya mambo yatakayokusaidia uwe msikilizaji mzuri kwenye mikutano ya Kikristo.
◼ Thamini faida ya mikutano. Mikutano ni njia kuu ambayo katika hiyo ‘twafundishwa na Yehova’ kupitia “msimamizi-nyumba mwaminifu.”—Isa. 54:13; Luka 12:42.
◼ Tayarisha mapema. Chunguza habari itakayozungumziwa, na uhakikishe umebeba Biblia yako na nakala ya kibinafsi ya kichapo mtakachojifunza.
◼ Wakati wa mikutano, jitahidi sana kusikiliza kwa makini. Epuka kuzungumza na wale wanaoketi karibu nawe na pia kutazama kile ambacho wasikilizaji wengine wanafanya. Jaribu kutokengeushwa fikira kwa kuwazia yale utakayofanya baada ya mkutano au mambo mengine ya kibinafsi.
◼ Changanua yanayozungumziwa. Jiulize hivi: ‘Habari hii yanihusuje? Nitaitumia wakati gani?’
◼ Andika maandishi mafupi ya mambo makuu na maandiko. Hilo hukusaidia kukazia fikira yale yanayozungumziwa na hukusaidia kukumbuka mambo makuu ili uyatumie baadaye.
3 Fundisha Watoto Wako Kusikiliza: Watoto wanahitaji mafundisho ya kiroho. (Kum. 31:12) Katika nyakati za kale iliwabidi “wote walioweza kusikia na kufahamu” miongoni mwa watu wa Mungu wasikilize kwa makini walipokuwa wakisomewa Sheria. (Neh. 8:1-3) Wazazi wanaposhiriki katika mikutano na kusikiliza kwa makini, watoto wao vilevile watafanya hivyo. Si jambo la hekima kubeba vitu vya kuchezea au vitabu vya kuchorea picha ili kufurahisha watoto. Kwenda msalani isivyo lazima pia huwakengeusha wasisikilize. Kwa kuwa “ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto,” yapasa wazazi wajitahidi kuona kwamba watoto wao wanakaa kimya na kusikiliza mikutanoni.—Mit. 22:15.
4 Tunapokuwa wasikilizaji wazuri, twathibitisha kwamba sisi kwa kweli ni wenye hekima na twataka “kuongezewa elimu.”—Mit. 1:5.