Wasaidie Watoto Wanufaike Zaidi na Mikutano
1 Watoto wako wanapohudhuria mikutano, je! kweli wao wanasikiliza? Je! wao wanaweza kukusimulia mambo ambayo wamejifunza katika kila mkutano baadaye? Je! wewe umewatia moyo wakaze fikira na watumie maarifa yanayopatikana kwa kutazama kwa uangalifu? Je! wewe unawatolea kielelezo kilicho hai kwa maelezo yako mikutanoni, kielelezo ambacho wanaweza kuona, kusikia, na kuiga? Je! watoto wako wanaiga imani yako? Majibu chanya kwa maswali haya ni yenye umaana ikiwa watoto watakua wakiwa watumishi wa Yehova waliojitoa.
FUNDISHA UMAANA WA KUHUDHURIA MIKUTANO
2 Mtoto anahitaji agizo la Biblia ikiwa atapata uhai wa milele. (Yn. 17:3, NW) Ikiwa mtoto atajifunza kuthamini mambo ya kiroho, kuhudhuria mikutano kunahitajiwa. Nyakati nyingine, wazazi wanasita-sita kuwapeleka watoto kwenye mikutano kwa sababu wanaogopa kwamba watoto watasumbua wengine. Huenda wengine wakawaacha watoto wao nyumbani ili wafanye kazi yao ya shuleni. Hata hivyo, mzazi mwenye hekima anawaleta watoto wake mikutanoni.—Kum. 31:12.
3 Jambo la kwanza ambalo mtoto anapaswa kujifunza tangu utotoni ni kwamba anaenda kwenye Jumba la Ufalme akasikilize. Lakini ikiwa anapewa vitu vya kumshughulisha, kama vile vitu vya kuchezea au chakula, au ikiwa anaruhusiwa kucheza kwenye kiti chake, je! yeye atajifunza kusikiliza na kuthamini kwa nini tunahudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme? Inakubalika kwamba watoto wengine wanakaza fikira kuliko wengine. Hata hivyo, mtoto anapokosa adabu, mzazi mwenye hekima atamsahihisha na kumzoeza kwa upendo ili asikilize, si kwa kumhonga kwa kumpa peremende au vitu vya kuchezea, bali kwa kutumia nidhamu ya Neno la Mungu.—Mit. 13:24; Efe. 6:4.
KIELELEZO CHAKO UKIWA MZAZI
4 Mnara wa Mlinzi wa Julai 15, 1982, uku. 9 uliuliza maswali yafuatayo: “Je! watoto wako wanajua kwamba wewe unaichukua mikutano ya kujifunza Biblia kuwa ya maana sana? Je! wanaona kwamba wewe unaiona kuwa yenye ubora wa kukufanya ushiriki katika hiyo kwa kutoa maelezo yanapotakwa, badala ya kuhudhuria na kujinyamazia?” Ikiwa watoto wako wanakuona ukipiga domo nyakati zisizohitajiwa mikutanoni au ikiwa wewe au wengine wanacheza nao, hiyo itawapa maoni gani? Wao wataonaje nyakati za mikutano? Kwa kuwa watoto ni waigaji wazuri, kielelezo chako kinaweza kuwaathiri sana.
5 Wazazi fulani wameliona kuwa jambo lenye mafaa kuwaandalia hata watoto wadogo nakala zao wenyewe za vichapo vinavyotumiwa mikutanoni. Labda wakati wa funzo la jamaa, wanawasaidia watoto wao watayarishe maelezo yanayofaa. Pia, wazazi wanaweza kuwatia moyo watoto wao kwa kurudia mambo ambayo yalizungumziwa wakati wa mikutano na kwa kuchukua wakati kujibu maswali ambayo huenda wakawa nayo. Wazazi wanapaswa kuwa macho pia kuwapongeza watoto wao kwa ushirika wao mikutanoni.
6 Ni kweli kwamba kuzoeza huko kunatia ndani kazi ngumu kwa wazazi. Hata hivyo, kufanya mambo katika njia ya Mungu kunatokeza matokeo mazuri. Kama maandiko yasemavyo: “Mwenye uadilifu anatembea katika ukamilifu wake. Wenye furaha ni wana wake baada yake.”—Mit. 20:7, NW.