‘Sikiliza Uongezewe Elimu’
1 Kitabu cha Mithali huonyesha hekima inaita ikisema: “Sikieni, maana nitasema yaliyo mazuri, na kufumbua midomo yangu kutakuwa maadili. Shauri ni langu na maarifa yaliyo sahihi. . . . Nisikilizeni sasa; maana heri hao wazishikao amri zangu. Maana yeye anionaye mimi aona uzima, naye atapata kibali kwa BWANA.” (Mit. 8:6, 14, 32, 35) Maneno hayo yanafafanua vizuri mafundisho tutakayopata sote kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Walimu wa Neno la Mungu.”
2 Mahitaji ya akina ndugu ulimwenguni pote yamechunguzwa, na programu ya mkusanyiko imetayarishwa kuyashughulikia mahitaji hayo. Mafundisho ya kiroho na madokezo yenye kutumika yatakayotolewa, yatatusaidia tuwe wenye furaha, tudumishe uhusiano mzuri na Yehova, na kudumu katika njia ya uhai wa milele endapo tutayatumia. Kwa hakika, tuna sababu nzuri ya ‘kusikiliza tuongezewe elimu.’—Mit. 1:5.
3 Kabla ya Programu Kuanza: Ili kunufaika kabisa na yale yanayotolewa, twahitaji kuwa tumeketi kwenye viti vyetu na kutayarisha akili zetu programu inapoanza. Hilo lahitaji mpango mzuri wa kibinafsi. Siri ya kufanya hivyo ni kujitayarisha mapema. Lala mapema usiku. Amka mapema vya kutosha ili wengine wajitayarishe na kupata kiamsha kinywa. Fika mapema mkusanyikoni ili uweze kupata mahali pa kuketi na kushughulikia mambo mengine ya muhimu kabla ya programu kuanza. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi, na programu itaanza saa 3:30 asubuhi kila siku.
4 Kwa kuwa kusudi hasa la kukusanyika kwetu ni kumsifu Yehova “katika makusanyiko,” kila kipindi chapasa kufunguliwa kwa njia itakayomtukuza Mungu. (Zab. 26:12) Hivyo, wote wanatiwa moyo kuketi kabla ya wimbo wa kufungua kutangazwa. Hilo lapatana na shauri la Kimaandiko: “Acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Hiyo yamaanisha nini kwa kila mmoja wetu? Unapoona mwenyekiti ameketi jukwaani wakati wa muziki, nenda uketi bila kukawia. Hiyo itakuwezesha kushiriki kwa moyo wote wimbo unaofungua kila kipindi, ukimwimbia Yehova sifa.—Zab. 149:1.
5 Wakati wa Programu: Ezra “alikuwa ameuelekeza moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda.” (Ezra 7:10) Twaweza kutayarishaje mioyo yetu ipokee mafundisho kutoka kwa Yehova? Unapopitia vichwa vya sehemu mbalimbali vilivyoorodheshwa kwenye programu, jiulize, ‘Yehova ananiambia nini kupitia programu hii? Naweza kutumiaje habari hiyo nijinufaishe mimi binafsi na familia yangu?’ (Isa. 30:21; Efe. 5:17) Endelea kujiuliza maswali hayo muda wote wa mkusanyiko. Andika mambo makuu unayopanga kutumia. Tumia wakati kuyazungumzia mwishoni mwa kila siku. Hiyo itakusaidia ukumbuke na kutumia habari hiyo.
6 Kukaza fikira kwa muda wa saa kadhaa si jambo rahisi. Ni nini kinachoweza kutusaidia tukinze mwelekeo wa kukengeuka fikira? Tumia vizuri uwezo wa jicho. Kwa kiwango kikubwa, yale tunayokazia macho yetu ndiyo huvutia fikira zetu. (Mt. 6:22) Kwa hiyo, kinza mwelekeo wa kugeuza kichwa chako usikiapo kelele yoyote au mtu anapotembea. Kazia macho msemaji. Fuatana na Biblia yako andiko linaposomwa, na uache Biblia yako wazi andiko lizungumziwapo.
7 Upendo wa Kikristo utatuchochea tuepuke kusumbua wengine programu inapoendelea. (1 Kor. 13:5) Huo ni “wakati wa kunyamaza” na kusikiliza. (Mhu. 3:7) Kwa hiyo, epuka kuzungumza na kutembeatembea isivyo lazima. Punguza kwenda msalani kwa kupanga mapema. Usile au kunywa hadi wakati unaofaa, isipokuwa iwe una matatizo makubwa ya afya. Wale wanaobeba simu za mkononi, peja, videokamera, na kamera za kawaida wasizitumie kwa njia inayokengeusha wengine. Wazazi wanapaswa kupanga ili familia yote, kutia ndani matineja, waketi pamoja ili waweze kuwasimamia vizuri watoto wao.—Mit. 29:15.
8 Mwaka uliopita, mzee mmoja ambaye amekuwa akihudhuria mikusanyiko kwa miaka mingi alisema hivi: “Niliona mkusanyiko huu kuwa wenye kutokeza kwa sababu fulani. Karibu kila mtu aliyehudhuria alikuwa akiandika mambo makuu, kutia ndani watoto. Jambo hilo lilinifurahisha sana. Biblia zilitumiwa vizuri wakati msemaji alipoomba maandiko fulani yafunguliwe.” Kusikiliza kwa makini jinsi hiyo kwastahili pongezi. Hakutuletei manufaa sisi na pia wenzetu wanaohudhuria mkusanyiko tu, bali zaidi ya yote kwamtukuza Mfunzi wetu Mkuu Yehova Mungu.—Isa. 30:20.