Zingatia Matamko Yaliyo Matakatifu
1 Si lazima kuzingatia kipekee kila kitu kinachosemwa na mwanadamu. Lakini Mungu anapozungumza, kuna sababu muhimu ya kusikiliza. (Kum. 28:1, 2) Tunashukuru kwamba wanaume waliopuliziwa walirekodi “matamko yaliyo matakatifu ya Mungu” kwa faida yetu. (Rom. 3:2) Mkusanyiko wa wilaya ujao utaandaa fursa zenye thamani za kusikiliza matamko hayo yanaposomwa na kuzungumziwa. Unaweza kusikilizaje kwa makini?
2 Fika Mapema Kila Asubuhi: Wazia msisimko ambao Waisraeli walikuwa nao walipoambiwa wakakutane na Yehova kwenye Mlima Sinai ili wasikilize Sheria yake! (Kut. 19:10, 11, 16-19) Ukiwa na mtazamo kama huo kuhusu kupokea maagizo ya Yehova kwenye mkusanyiko wa wilaya, utafanya mipango ya kufika mapema kila siku. Hatuwezi kusikiliza programu nzima tukichelewa kufika na kusumbua wengine tunapojaribu kutafuta viti. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi kwenye uwanja wa mkusanyiko, na programu itaanza saa 3:30 asubuhi kila siku.
3 Hata wengine wanaofika mapema hawawi wameketi kipindi kinapoanza. Kwa nini? Wao hungoja mpaka mwenyekiti anapoanza kutangaza wimbo wa kufungua ndipo waache kuzungumza na rafiki zao na kuanza kuelekea kwenye viti vyao. Twapaswa kutambua kwamba dakika kadhaa kabla ya wimbo wa kufungua kila kipindi, mwenyekiti atakuwa ameketi kwenye jukwaa wakati muziki wa pekee wa Ufalme unapochezwa. Hiyo ni ishara kwamba twapaswa kuwa tumeketi! Kisha, wimbo wa kufungua unapotajwa, tutakuwa tayari kujiunga katika kuimba wimbo huo ili kumsifu Yehova.
4 Sikilizeni Mkiwa Familia Iliyoungana: Matamko matakatifu yaliposomwa kwa familia za Waisraeli waliokutanika pamoja, kutia ndani “watoto,” walipaswa kusikiliza na kujifunza. (Kum. 31:12) Kwenye mikusanyiko yetu, watoto hawapaswi ‘kuachiliwa.’ (Mit. 29:15) Wazazi—pangeni familia yenu nzima iketi pamoja, kutia ndani matineja. Wazazi fulani hungoja hadi wimbo wa kufungua uanze ndipo wawapeleke watoto wao msalani. Hata hivyo, hilo halitawafunza watoto umuhimu wa nyimbo na sala katika ibada yetu. Ingekuwa afadhali kama nini kwenda msalani kabla ya kila kipindi kuanza ikiwa yawezekana kwa vyovyote vile!
5 Tutaweza kusikiliza tukipumzika vya kutosha kila jioni na kutokula chakula kingi mchana. Kazia fikira yale yanayosemwa na msemaji. Usiruhusu akili yako itangetange. Fungua Biblia na kufuata maandiko yanaposomwa. Andika mambo makuu machache. Kila hotuba inapotolewa, pitia akilini mwako mambo yaliyosemwa na msemaji na ufikirie jinsi utakavyotumia habari hiyo. Zungumzieni programu hiyo mkiwa familia jioni. Kila mmoja alifurahia mambo gani? Familia yako yaweza kutumiaje habari hiyo kwa njia ifaayo?
6 Stahi Neno la Mungu: Mikusanyiko hutupa fursa nzuri ya kuzungumza na marafiki na kufurahia ushirika unaojenga. Tukifika mapema, tutakuwa na wakati wa kuzungumza kabla programu haijaanza. Hata hivyo, wengine huzungumza wakati wa programu, wakifikiri kwa makosa kwamba jambo hilo halisababishi mvurugo mkubwa kwenye stediamu kubwa au majumba. Hata wakati mikutano inapofanywa mahali palipo na watu wengi, ni wakati wa kusikiliza kama tufanyavyo tunapohudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Programu haipasi kuvurugwa na simu za mikononi, pager, kamera za vidio, na kamera.
7 Musa alipokuwa akipokea Sheria kutoka kwa Yehova, “hakula chakula, wala hakunywa maji.” (Kut. 34:28) Vivyo hivyo, haingefaa kula wala kunywa vipindi vya mkusanyiko vinapoendelea. Isipokuwa uwe na tatizo kubwa la kiafya, subiri hadi “majira yake” ili kufanya hivyo.—Mhu. 3:1.
8 Katika mikusanyiko fulani, akina ndugu na dada wengi na hata watoto wachanga bado wana tatizo la kutembea katika vikundi kwenye vijia vipindi vinapoendelea. Wakaribishaji wataagizwa kuomba watu kama hao warudi kwenye viti vyao. Wafanyakazi wa kujitolea wanaofanya kazi katika idara mbalimbali wapaswa kuketi pamoja na wasikilizaji mara tu kazi yao imalizikapo. Isipokuwa wafanyakazi wapewe mgawo muhimu wa kufanya wakati wa programu, wapaswa kuketi na kusikiliza programu. Hawapaswi kukawia-kawia kwenye idara wakitembeleana programu inapoendelea.
9 Hatungependa kamwe kuwa ‘wazito katika kusikia kwetu’ tunaposikiliza Neno la Mungu. (Ebr. 5:11) Acheni basi tuazimie kuonyesha staha inayofaa kwa kusikiliza kwa makini matamko matakatifu kutoka kwa Yehova yazungumziwapo kwenye mkusanyiko wetu wa wilaya ujao.