“Acheni Mambo Yenu Yote Yatendeke kwa Upendo”
1 “Washiriki wenu wanapendeza kwelikweli, nao hujiendesha kwa adabu na staha nyingi sana.” Maoni hayo yanatoka kwenye dawati la mkusanyiko na la wageni katika jiji moja la Marekani ambapo mojawapo ya mikusanyiko yetu ya wilaya ulifanyiwa. Tunatiwa moyo kupokea pongezi ya namna hiyo kuhusu jinsi tunavyojiendesha mbele za umma. Hilo laonyesha kwamba kwa ujumla ‘tunaacha mambo yetu yote yatendeke kwa upendo.’ (1 Kor. 16:14) Wakati huohuo, kuna mambo fulani yapasayo kuhangaikiwa ambayo yasiposhughulikiwa yataharibu sifa njema ya watu wa Mungu.
2 Matatizo ya Idara ya Mahali pa Kulala: Katika kila jiji au mji wa mkusanyiko, kunakuwa na Idara ya Mahali pa Kulala ili kutusaidia tupate mahali pa kulala. Ndugu zetu hutumia wakati mwingi na hujitahidi sana kwa niaba yetu.
3 Tunapovunja mipango ya mahali pa kulala kwenye hoteli dakika ya mwisho tunasababisha matatizo makubwa sana kwa hoteli hizo na kwa wale wanaopanga mkusanyiko. Wasimamizi wa hoteli huhifadhi vyumba kadhaa kwa ajili ya wajumbe wetu nao huamini kwamba vyumba vyote vimejazwa, na kuja kugundua tu wakati wa mkusanyiko kwamba vyumba ni vitupu. Kwa kuongezea, lazima kulipa mapema kiasi fulani cha fedha kwa ajili ya usiku mmoja ili kuhakikisha kila chumba kimehifadhiwa. Kufanya hivyo pia kutazuia mtu mwingine asipatiwe chumba hicho hata kama utachelewa.
4 Ikiwa unalala kwenye mabweni au madarasani, tafadhali zingatia katazo la kupika katika majengo hayo. Kuna hatari ya kuanzisha moto na hilo lingesababisha matatizo mengi.
5 Kufanya Lililo Jema Kuelekea Wote: Tabia njema na mwenendo wa kuigwa huchochewa na kumpenda Yehova na jirani zetu. (Mt. 22:37-39; Yak. 3:13) Biblia hutusihi tuwe wenye upendo na kufikiria watu wote. (Gal. 6:10) Bila shaka kanuni hiyo hutumika tunapokuwa kwenye hoteli, mabweni, au madarasani. Tunapokosa kushirikiana tunaharibu sifa yetu, tunahatarisha mpango wa kupunguziwa bei, na kuwaudhi akina ndugu. Ikiwa shirika fulani lakataa kutupa mahali pa kulala tena, wengine wanaohudhuria mkusanyiko katika jiji au mji huo waweza kuathiriwa sana, hasa ikiwa hawawezi kugharimia malipo ya hoteli.
6 Mipango ya kulala inapovunjwa dakika ya mwisho, inamaanisha kwamba ndugu fulani alinyimwa nafasi hiyo ya mahali pa kulala. Huenda hilo likataka asafiri mbali zaidi au akubali mahali pa kulala pasipofaa sana. Je, huo ni upendo au kuwafikiria wengine? Ni afadhali kama nini kuonyesha upendo na kufanya lililo jema kuelekea wengine kwa kutanguliza masilahi yao badala ya masilahi yetu!—Mt. 7:12; Yn. 13:34, 35.
7 Tunatazamia kwa hamu kuhudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Je, umefanya mipango yako yote kutia ndani mahali pa kulala na usafiri? Mwenendo wetu tunapokuwa kwenye hoteli, mabweni, na madarasani katika mji au jiji la mkusanyiko sikuzote na udhihirishe kweli iliyo mioyoni mwetu na upendo kwa Muumba wetu.