Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 6/13 kur. 2-5
  • Sikiliza na Ujifunze

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sikiliza na Ujifunze
  • Huduma ya Ufalme—2013
  • Habari Zinazolingana
  • “Haki ya Kimungu” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1988
    Huduma Yetu ya Ufalme—1988
  • Je, Uko Tayari kwa Ajili ya Karamu ya Kiroho?
    Huduma ya Ufalme—2009
  • ‘Sikiliza Uongezewe Elimu’
    Huduma Yetu ya Ufalme—2001
  • Pindi ya Kulishwa Kiroho na Kushangilia
    Huduma Yetu ya Ufalme—2008
Pata Habari Zaidi
Huduma ya Ufalme—2013
km 6/13 kur. 2-5

Sikiliza na Ujifunze

1. Kwa nini huenda jitihada za pekee zikahitajika ili tusikilize na kujifunza kwenye kusanyiko la wilaya?

1 Hivi karibuni makusanyiko ya wilaya ya mwaka wa 2013 yataanza. Kazi kubwa imefanywa ili kutayarisha programu inayozungumzia mahitaji ya sasa ya watu ulimwenguni pote. Je, umefanya mipango ili uhudhurie siku zote tatu za kusanyiko? Makusanyiko makubwa yanaweza kuwa na vikengeusha fikira vingi, hivyo huenda jitihada nyingi sana zikahitajika ili kukazia fikira programu. Kwa kuwa vipindi vya kusanyiko huchukua muda mrefu zaidi kuliko mikutano ya kutaniko, tunahitaji kukaza fikira kwa muda mrefu zaidi. Kwa kuongezea, kusafiri na mambo mengine huenda yakatufanya tuchoke kwa kiasi fulani. Ni nini kitakachotusaidia tuendelee kuwa makini ili tusikilize na kujifunza?​—Kum. 31:12.

2. Tunawezaje kutayarisha moyo wetu kwa ajili ya kusanyiko?

2 Kabla ya Kusanyiko: Tovuti yetu rasmi ya www.jw.org/sw, huonyesha programu ya kusanyiko la wilaya ambayo inatia ndani vichwa vya hotuba zote na andiko moja au mawili ya msingi ya kila hotuba. Ikiwa tunatumia Intaneti, tunaweza kupitia habari hiyo kabla ya kusanyiko ili tutayarishe moyo wetu. (Ezra 7:10) Je, mnaweza kuzungumzia programu ya kusanyiko linalokuja wakati wa jioni ya Ibada ya Familia ili mtazamie kwa hamu mambo mtakayojifunza kusanyikoni?

3. Ni nini kitakachotusaidia kusikiliza kwa makini?

3 Wakati wa Kusanyiko: Ikiwezekana, ingefaa uende msalani kabla ya kipindi cha kusanyiko kuanza. Zima simu yako ili usikengeushwe fikira na watu wanaokupigia au wanaokutumia ujumbe mfupi au usishawishike kutuma ujumbe mfupi programu inapoendelea. Ikiwa ni lazima utumie simu yako, fanya hivyo kwa njia ambayo haitawasumbua wengine iwapo utapigiwa simu programu inapoendelea. Ikiwa unatumia kompyuta ndogo (tablet) wakati wa programu, itumie kwa njia ambayo haiwasumbui wengine. Epuka kula au kunywa programu inapoendelea. (Mhu. 3:1) Mtazame msemaji. Andiko linaposomwa fungua Biblia yako na ufuatane na msemaji. Andika mambo makuu.

4. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao kusikiliza na kujifunza?

4 Pia, tungependa watoto wetu wasikilize na wajifunze. Andiko la Methali 29:15 linasema hivi: “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” Kwa hiyo, ni vizuri familia zikae pamoja ili wazazi wahakikishe kuwa watoto wao wanakazia fikira programu badala ya kuongea, kutuma ujumbe mfupi, au kutembea huku na kule. Hata ikiwa watoto hao ni wachanga sana hivi kwamba hawawezi kuelewa mambo yote yanayozungumziwa, wanaweza kuzoezwa kukaa macho na kuketi wakiwa kimya.

5. Kwa nini ni jambo lenye manufaa kupitia mambo tuliyojifunza kusanyikoni, na tunawezaje kufanya hivyo?

5 Kila Siku Baada ya Programu: Usichelewe kulala. Lala mapema ili upumzike vya kutosha. Ni vizuri kupitia mambo uliyosikiliza ili uyakumbuke kwa muda mrefu zaidi. Kwa hiyo, itafaa mtumie dakika chache kila jioni kuzungumzia programu mkiwa familia. Ikiwa unaenda kwenye mkahawa na marafiki, kwa nini usibebe mambo uliyoandika na kisha uzungumzie jambo moja au mawili yaliyokupendeza zaidi? Baada ya kusanyiko, mnaweza kutumia muda fulani wakati wa jioni ya Ibada ya Familia kuzungumzia jinsi mnavyoweza kutumia mambo mliyojifunza mkiwa familia. Pia mnaweza kutenga wakati kila juma ili kupitia sehemu za machapisho yoyote mapya mliyopokea kusanyikoni.

6. Je, inatosha tu kuwepo kwenye kusanyiko? Eleza.

6 Kunapokuwa na karamu, chakula hutimiza kusudi lake kinapoliwa na kumeng’enywa. Tunaweza kusema vivyo hivyo kuhusiana na karamu ya kiroho itakayoandaliwa kwenye kusanyiko la wilaya. Acheni tufaidike kikamili kwa kuhudhuria kila kipindi cha kusanyiko, kwa kusikiliza kwa makini, na kwa kutumia mambo tunayojifunza.

[Sanduku katika ukurasa wa 2]

Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya—2013

◼ Saa za Programu: Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Kipindi cha muziki kitaanza saa 3:20 asubuhi siku zote tatu. Wakati huo, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Wimbo na sala ya kumalizia itatolewa saa 10:50 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:35 alasiri siku ya Jumapili.

◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo, lakini wale watakaofika kwanza ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Kwa kawaida sehemu za kuegesha ni chache, hivyo ingefaa sana watu wasafiri pamoja kwa gari moja, badala ya kila mmoja kuja na gari lake.

◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili tu ya wale unaoishi nao, au unaosafiri nao katika gari moja au wanafunzi wako wa Biblia. Kuna viti vichache kwa ajili ya wale waliozeeka na walio dhaifu, kwa hiyo huenda wasiweze kuketi pamoja na watu wao wa familia. Tafadhali waachieni viti hivyo wale waliozeeka na walio dhaifu na wale wanaowatunza.—1 Kor. 13:5.

◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula chepesi cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kwenda kutafuta chakula. Mfuko au sanduku dogo la kuhifadhia vyakula vikiwa baridi linaweza kuwekwa chini ya kiti. Mifuko au masanduku makubwa ya kuhifadhia vyakula vikiwa baridi na vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.

◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kusanyikoni kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Cheki au hundi zozote zinazotolewa zinapaswa kuandikwa zilipwe kwa IBSA au jina la shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu.

◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikitokea kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajika. Ikihitajika, ndugu katika idara hii watatafuta gari la kubebea wagonjwa. Jambo hili litapunguza idadi ya simu zinazopokewa na kitengo cha huduma za dharura.

◼ Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha, kwa kuwa hazitapatikana kusanyikoni. Mabomba ya sindano au sirinji na sindano zinazotumiwa na wagonjwa wa kisukari hazipaswi kutupwa ovyoovyo kwani ni takataka hatari, wala zisitupwe pamoja na takataka zilizo katika eneo la kusanyiko au hotelini.

◼ Viatu: Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu, hasa viatu vyenye kisigino kirefu. Itafaa sana kuvaa viatu vinavyofaa, vinavyokutoshea vizuri na vinavyokuwezesha kutembea vizuri kwenye sehemu zilizoinuka, ngazi, vifuniko vyenye matundu vinavyofunika mashimo ya maji machafu na sehemu nyinginezo.

◼ Marashi: Makusanyiko mengine hufanyiwa ndani ya majumba. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.

◼ Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi inapaswa kutumiwa kutoa habari kuhusu mtu yeyote mwenye kupendezwa ambaye ulimpata ulipokuwa ukihubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu utakaporudi nyumbani.

◼ Mikahawa: Liheshimu jina la Yehova kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Mavazi yetu yaonyeshe kwamba sisi ni wahudumu Wakristo. Toa bakshishi ikiwa kufanya hivyo ni desturi katika eneo lenu.

◼ Hoteli:

(1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi ya watu inayoruhusiwa.

(2) Usivunje mipango uliyofanya mapema ya kuwa na chumba isipokuwa hali ya dharura itokee, na unapaswa kuwajulisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa ili wengine wenye uhitaji huo waweze kukitumia. (Mt. 5:37) Ikiwa utahitaji kuvunja mipango ya kuwa na chumba, hakikisha umepata nambari inayoonyesha kwamba umevunja mipango hiyo. Ikiwa utavunja mipango ya kuwa na chumba chini ya saa 48 kabla ya kutumia chumba hicho, hutarudishiwa pesa ulizotoa ili kuhifadhi chumba hicho.

(3) Tafadhali zingatia kwamba ikiwa utatumia kadi ya mkopo kulipia gharama unapojiandikisha kwenye hoteli, ni zoea la kawaida kwa wasimamizi wa hoteli “kuweka kando” kiasi fulani cha pesa zako ambazo zitatoshea kulipia gharama zako zote za chumba, kutia ndani uharibifu au matukio yasiyotazamiwa ambayo huenda yakatukia unapokuwa hotelini. Baada ya kuondoka hotelini, hutaweza kutumia pesa hizo zilizowekwa kando mpaka siku kadhaa za kushughulikia akaunti yako zipite.

(4) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.

(5) Ikiwa ni desturi katika eneo lenu, wape bakshishi kila siku wafanyakazi wa hoteli wanapokubebea mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.

(6) Pika tu katika vyumba ambavyo upishi umeruhusiwa.

(7) Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.

(8) Nyakati zote onyesha tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi hotelini. Wanawahudumia watu wengi, nao wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.

(9) Wazazi wanapaswa kuwasimamia watoto wao nyakati zote wanapokuwa kwenye hoteli, kutia ndani wanapopanda lifti, wanapotumia kidimbwi cha kuogelea, wanapokuwa sebuleni, katika chumba cha mazoezi, na kadhalika.

(10) Kukiwa na shida kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.

◼ Kazi ya Kujitolea: Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa mchango mkubwa kwa kufanya kazi chini ya usimamizi wa mzazi, mtunzaji wao, au mtu mzima mwingine ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki