Pindi ya Kulishwa Kiroho na Kushangilia
1. Yehova anashughulikiaje mahitaji ya kiroho ya watumishi wake?
1 Yehova anashughulikia kwa upendo mahitaji ya kiroho ya watumishi wake. Ingawa watu wengi ulimwenguni wana njaa ya kiroho, tunalishwa vizuri sana. (Isa. 65:13) Njia moja ambayo Yehova anatulisha kiroho ni kupitia makusanyiko yetu ya wilaya ya kila mwaka. Je, unafanya matayarisho ili uhudhurie vipindi vyote vya Kusanyiko la Wilaya la “Kuongozwa na Roho ya Mungu”? Mipango imefanywa ili kuwe na karamu yenye vyakula vitamu na yenye kujenga kiroho.
2. Kufanya mipango mapema kwa ajili ya kusanyiko kunahusisha nini?
2 Fanya Mipango Mapema: “Mipango ya mwenye bidii bila shaka huleta faida.” (Met. 21:5) Hivyo, unapofanya mipango ya kuhudhuria siku zote tatu za kusanyiko, usikawie-kawie kumwomba mwajiri wako ruhusa. Ikiwa utahitaji mahali pa kulala, je, umekwisha kufanya mipango? Pia itafaa kufanya mipango ili ule chakula cha mchana pamoja na ndugu zako mahali pa kusanyiko. Panga kufika mapema vya kutosha kwenye kusanyiko kila siku ili upate mahali pa kuketi na kushiriki katika wimbo na sala ya kufungua.
3. Tunapaswa kupanga kuvalia mavazi ya aina gani?
3 Tunapaswa kuhakikisha kwamba mavazi tutakayovalia ni ya kiasi na yenye mpangilio mzuri. (1 Tim. 2:9, 10) Makusanyiko ya wilaya hutupa fursa nzuri ya kutoa ushahidi katika jumuiya. Tunapovalia kwa heshima tunapokuwa katika jiji la kusanyiko na kuvaa beji zetu za kusanyiko, tunaonekana kwamba tuko tofauti na wasio waamini na tunawavutia watu wanaotutazama.
4. Ni nini kitakachotusaidia kufaidika kabisa kutokana na programu pamoja na familia zetu?
4 Sikiliza kwa Makini: Hatutaki kukosa chakula chochote kile kitakachoandaliwa kwenye karamu hii ya kiroho! (Met. 22:17, 18) Kuandika mambo makuu machache na kufungua Biblia zetu na kufuatana na msemaji anaposoma maandiko kutatusaidia kukazia fikira programu na kuepuka kukengeushwa. Kisha, jioni, tunaweza kutumia mambo tuliyoandika ili kuzungumza pamoja na wengine kuhusu mambo makuu ya programu. Katika miaka ya karibuni, vijana fulani wameonekana wakiketi pamoja kwenye kusanyiko na kuzungumza programu inapoendelea au kutuma-tuma ujumbe kupitia simu zao za mkononi. Ikiwa tuna watoto, kutia ndani matineja, itafaa kuketi pamoja nao ili kusikiliza programu kama familia badala ya kuwaruhusu kuketi kwingineko pamoja na vijana wengine.
5. Ni nini kitakachotuwezesha kufurahia kusanyiko zaidi?
5 Furahia Ushirika: Chakula kitamu hufurahisha zaidi kinapoliwa pamoja na marafiki. (Met. 15:17) Vivyo hivyo, ushirika pamoja na ndugu na dada zetu hutuwezesha kufurahia zaidi kusanyiko. Hivyo, kabla na baada ya programu, inafurahisha kama nini kuchukua hatua ya kwanza kuzungumza na wahudhuriaji wengine ili kufurahia ushirika pamoja nao! (Zab. 133:1) Mwenyekiti anapotuomba kwa fadhili tuketi kabla muziki haujaanza, tunapaswa kukatiza mazungumzo yetu na kuketi kabla ya programu kuanza.
6. Simulia jambo fulani ulilojionea kuonyesha jinsi tunavyoweza kuwahubiria watu katika jiji la kusanyiko.
6 Tumia Kila Nafasi Kutoa Ushahidi: Kwa kawaida, makusanyiko huandaa fursa nzuri za kutoa ushahidi. Wahudhuriaji wengi ambao huenda kwenye mikahawa baada ya programu huulizwa na wahudumu wa hoteli na watu wengine kuhusu kichwa kilicho kwenye beji ya kusanyiko. Hilo limewawezesha kuanzisha mazungumzo na kutoa ushahidi mzuri kuhusu ile kweli. Baadhi ya wale waliouliza kuhusu kichwa cha kusanyiko walialikwa kwenye kusanyiko na wakahudhuria.
7. Kwa nini tuhudhurie kusanyiko la wilaya linalokuja?
7 Muda mwingi sana umetumiwa kutayarisha programu, kutayarisha mahali pa kusanyiko, kupanga idara za kusanyiko, na kutayarisha hotuba. Jitihada zote za upendo ambazo zimefanywa ili kutayarisha karamu hiyo ya kiroho zinaonyesha kwamba Yehova anawajali sana watu wake. Sote na tuazimie kuhudhuria na kujifunza mengi! Tukifanya hivyo, tofauti na ulimwengu, ‘tutapiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo.’—Isa. 65:14.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya
◼ Saa za Programu: Siku zote tatu programu itaanza saa 3:20 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Muziki wa utangulizi unapoanza, sisi sote tunapaswa kuwa tumeketi ili programu ianze kwa njia ya heshima. Programu itaisha saa 10:55 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 10:00 jioni siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana pasipo malipo. Wale watakaofika kwanza, ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Beji za kusanyiko zitatumiwa kama vitambulisho ili kupata mahali pa kuegesha. Walemavu ambao wanataka kuegesha magari yao karibu na mahali pa kuingilia wanaweza kuomba msaada kwa wakaribishaji.
◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu wanaosafiri pamoja nawe katika gari moja, au wanaoishi pamoja nawe katika nyumba moja.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali bebeni chakula cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kwenda kutafuta chakula. Sanduku dogo la kuhifadhia chakula, ambalo linaweza kutoshea chini ya kiti kimoja linaweza kutumiwa. Masanduku makubwa ya kuhifadhia chakula, vyombo vya glasi, na pombe haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote kwenye Jumba letu la Ufalme au kwenye kusanyiko. Hundi zozote zitakazotolewa kusanyikoni zinapaswa kuandikwa jina la shirika letu linalotambuliwa kisheria katika nchi yenu.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikizuka kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajiwa. Wafanyakazi wa huduma ya kwanza wataamua jinsi watakavyoshughulikia hali hiyo ya dharura.
◼ Wasio na Uwezo Mzuri wa Kusikia: Omba msaada ili uketi mahali ambapo ni karibu zaidi na msemaji.
◼ Marashi: Huenda makusanyiko mengine yakafanyiwa katika majumba. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Kufuatia Upendezi: Tukikutana na mtu yeyote anayependezwa tunapohubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko, tunapaswa kutumia fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) kutoa habari kuhusu mtu huyo. Wahubiri wanapaswa kuwa na fomu moja au mbili kusanyikoni. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu ili zishughulikiwe au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu unaporudi kutanikoni.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2005, uku. 6.
◼ Mikahawa: Fanya jina la Yehova liheshimiwe kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Katika sehemu nyingi, ni jambo la kawaida kutoa bakshishi, ikitegemea huduma iliyotolewa.
◼ Hoteli: (1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kimoja kisikaliwe na watu wanaozidi idadi inayoruhusiwa. (2) Ikiwa hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa kwa ajili yako, julisha hoteli mara moja. (3) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati tu unapokihitaji, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia. (4) Usipike ndani ya vyumba ikiwa hairuhusiwi kufanya hivyo. (5) Mwachie bakshishi yule anayetunza chumba. (6) Nyakati zote onyesha matunda ya roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli. (7) Kukiwa na shida katika chumba chako, hakikisha unaijulisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa kusanyikoni.