Endeleeni Kumtarajia Yehova
1 “Yehova ni Mungu wa hukumu,” akaandika Isaya. “Wenye furaha ni wale wote wanaoendelea kumtarajia.” (Isa. 30:18b) Kuna masimulizi mengi ya Biblia kuhusu kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu dhidi ya maadui wake na ya kukombolewa kwa watumishi wake waaminifu. Ni mambo gani ambayo waabudu wa Yehova leo wanaweza kujifunza kutokana na masimulizi kama hayo? Tunaweza kufanya nini sasa ili kujitayarisha kwa ajili ya “ile siku ya Yehova iliyo kuu na yenye kuogopesha”? (Yoe. 2:31, 32) Kusanyiko letu la Wilaya linalokuja lenye kichwa “Ukombozi Unakaribia!” litatuchochea kufikiria maswali hayo na kujichunguza. Litatusaidia kuendelea kumtarajia Yehova.
2 Je, umefanya mipango ili uwepo na kunufaika na siku zote tatu za kusanyiko? Kwa mfano, je, umemwomba mwajiri wako ruhusa ya kuhudhuria? Usitazamie kwamba itawezekana tu kupata ruhusa bila kujitahidi. Sali kuhusu jambo hilo. Kisha omba ruhusa. (Neh. 2:4, 5) Vilevile, hatupaswi kuahirisha kufanya mipango ya usafiri, mahali pa kulala, na mambo mengine muhimu. Kufanya mipango mizuri jinsi hiyo kunaonyesha tunathamini sana meza ya kiroho ya Yehova. Wazee wanapaswa kuwa chonjo kuwasaidia wale watakaohitaji msaada wa kufanya mipango kwa ajili ya kusanyiko, hasa wale wenye umri mkubwa katika kutaniko.—Gal. 6:10.
3 Mwenendo Mzuri Humletea Mungu Heshima: Tunapokusanyika katika makusanyiko, mwenendo wetu mzuri hutoa ushahidi mzuri kwa jamii. Basi tunapaswa kufanya nini? Tunapokuwa hotelini, mikahawani, na katika sehemu nyingine za biashara katika eneo la kusanyiko, wale tunaoshughulika nao wanapaswa kuvutiwa na sifa zetu za Kikristo kama vile ustahimilivu, upole, kujizuia, na usawaziko. (Gal. 5:22, 23; Flp. 4:5) Sote tunapaswa kuonyesha upendo ambao “haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki.” Hata matatizo au mambo ya kuudhi yanapotokea, tutajitahidi kufanya “mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Kor. 10:31; 13:5.
4 Baada ya kusanyiko moja, meneja wa hoteli alivutiwa sana na mwenendo na mavazi ya vijana wetu hivi kwamba akasema angependa “sikuzote Mashahidi wa Yehova wawe wageni katika hoteli yake.” Hilo ni jambo lenye kufurahisha kama nini! Linaonyesha kwamba wazazi huwazoeza na kuwasimamia watoto wao kwa njia nzuri. Si jambo la hekima kuwaruhusu watoto kukaa katika hoteli au mahali pa kulala bila usimamizi. Sikuzote watoto wanapaswa kusimamiwa vizuri. (Met. 29:15) Mwenendo wao mzuri na umletee Yehova sifa na kufanya moyo wake ushangilie!—Met. 27:11.
5 Kuvaa na Kujipamba kwa Kiasi: Kila mmoja wetu anaweza kufanya watu wawe na maoni mazuri kuhusu kusanyiko kwa kuepuka kuvaa au kujipamba kwa kufuata mitindo yenye kushtua, isiyo ya kiasi, au ya kizembe. Hilo linahusu pia wakati tunaposafiri kwenda na kutoka jiji la kusanyiko, tunaposaidia kutayarisha mahali pa kusanyiko, na tunapokuwa kwenye kusanyiko. Tukiwa watumishi wa Mungu, jambo kuu kwetu ni jina la Yehova na sifa yake, si mapendezi au starehe yetu ya kibinafsi. Vichwa vya familia wana daraka la kuhakikisha kwamba washiriki wa familia yao wanavaa na kujipamba kwa kiasi na kwa utimamu wa akili nyakati zote.—1 Tim. 2:9.
6 Vilevile ni muhimu kuvaa kwa heshima tunapostarehe hotelini, madukani, na mikahawani. Inafaa kuvaa mavazi tuliyokuwa nayo kusanyikoni tunapokula mikahawani baada ya programu. Kuvaa beji zetu za kusanyiko hutokeza nafasi za kuhubiri isivyo rasmi.—2 Kor. 6:3, 4.
7 Isaya alitabiri: “Yehova ataendelea kutarajia kuwaonyesha ninyi kibali, na kwa hiyo atasimama ili kuwaonyesha ninyi rehema.” (Isa. 30:18a) Shukrani kwa rehema na fadhili zisizostahiliwa za Yehova, inapaswa kutuchochea tumletee sifa kwa mwenendo na sura yetu tunapokusanyika pamoja katika makusanyiko yetu. Kusanyiko letu la Wilaya la “Ukombozi Unakaribia!” na limletee Mungu wetu sifa na kutusaidia tuendelee kumtarajia!
[Maswali ya Funzo]
1. Kusanyiko la wilaya lina kichwa gani, na kwa nini kichwa hicho kinafaa?
2. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini kusanyiko letu la wilaya?
3. Ni sifa gani ambazo zinapaswa kuonekana wazi kati ya watu wa Yehova katika jiji la kusanyiko?
4. Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kujiendesha katika njia inayomletea Yehova sifa?
5. Tunaweza kumheshimuje Yehova kwa mavazi na mapambo yetu?
6. Kwa nini inafaa tuvae kwa heshima tunapostarehe sawa tu na vile sisi huvaa wakati wa programu ya kusanyiko?
7. Tunaweza kuchangiaje kufanya makusanyiko yetu ya wilaya yawe yenye utaratibu na shangwe? (Ona “Vikumbusha vya Kusanyiko la Wilaya.”)
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Vikumbusha vya Kusanyiko la Wilaya
◼ Saa za Programu: Siku zote tatu programu itaanza saa 3:30 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Dakika chache kabla ya programu kuanza, mwenyekiti atakuwa ameketi jukwaani huku muziki wa Ufalme ukichezwa. Kila mmoja wetu anapaswa kuketi wakati huo ili programu ianze kwa njia ya heshima. Siku ya Ijumaa, programu itakwisha saa 11:15 jioni, siku ya Jumamosi saa 11:05 jioni, na saa 10:10 jioni siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko zenye maegesho yanayolindwa, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo. Wale watakaofika kwanza, ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Beji za kusanyiko zitatumiwa kama kitambulisho ili kupata mahali pa kuegesha gari.
◼ Kuhifadhi Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu unaosafiri nao katika gari moja au mnaoishi pamoja katika nyumba moja.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula chako cha mchana badala ya kuondoka eneo la kusanyiko ili kutafuta chakula wakati wa pumziko la mchana. Sanduku dogo la kuhifadhi chakula kikiwa baridi (cooler) ambalo linaweza kutoshea chini ya kiti linaweza kutumiwa. Masanduku makubwa ya kuhifadhi chakula kikiwa baridi, vyombo vya glasi, na pombe haviruhusiwi kwenye eneo la kusanyiko.
◼ Michango: Pesa nyingi sana hutumiwa kugharimia mahitaji ya kusanyiko la wilaya. Tunaweza kuonyesha uthamini wetu kwa kutoa michango ya hiari kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote kwenye Jumba la Ufalme au kwenye kusanyiko.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Kunapotokea hali ya dharura, tafadhali mjulishe mkaribishaji aliye karibu, naye atajulisha Idara ya Huduma ya Kwanza mara moja ili wachunguze hali hiyo na kutoa msaada. Ikihitajika, mtu anaweza kupelekwa hospitali iliyo karibu.
◼ Kurekodi: Vifaa vyovyote vya kurekodi havipaswi kuunganishwa kwa mfumo wa umeme au wa sauti wa kusanyiko, navyo vinaweza kutumiwa tu kwa njia ambayo haitawasumbua wengine.
◼ Kupiga Picha: Ikiwa utapiga picha programu ikiendelea, tafadhali usitumie flashi.
◼ Peja na Simu za Mkononi: Hazipaswi kutoa sauti itakayowakengeusha wasikilizaji.
◼ Marashi: Huenda makusanyiko fulani yakafanyiwa katika majumba ambako hakuna mfumo wa kusafisha hewa. Ikiwa ndivyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Kufuatia Upendezi: Tukikutana na mtu yeyote anayependezwa tunapohubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko, tunapaswa kutumia fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) kutoa habari kuhusu mtu huyo. Wahubiri wanapaswa kuwa na fomu moja au mbili kusanyikoni. Fomu hizo zitapatikana pia kwenye Idara ya Vitabu ya kusanyiko. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu ili zishughulikiwe au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lako.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2005, uku. 6.
◼ Mikahawa: Katika sehemu nyingi, ni jambo la kawaida kutoa bakshishi ya asilimia 15 au 20, ikitegemea huduma iliyotolewa.
◼ Hoteli au Mabweni: (1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kimoja kisikaliwe na watu wanaozidi idadi inayoruhusiwa. (2) Ikiwa hutatumia chumba ulichokuwa umehifadhiwa, julisha hoteli mara moja. (3) Usipike ndani ya chumba ikiwa hairuhusiwi kufanya hivyo. (4) Mwachie atakayesafisha chumba bakshishi. (5) Onyesha matunda ya roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli, hasa wakati ambapo kuna wateja wengi wanaoingia na kutoka.