Makusanyiko ya Wilaya—Kipindi cha Ibada Chenye Shangwe
1. Ni katika njia gani sherehe za Waisraeli zinafanana na makusanyiko ya wilaya ya siku hizi?
1 Yosefu, Maria, watoto wao, na watu wengine walienda Yerusalemu kwa ukawaida kuhudhuria sherehe za kila mwaka. Wakati wa sherehe hizo, wao na waabudu wengine walijitahidi kutofikiria matatizo yao na badala yake kuzingatia mambo ya kiroho yaliyokuwa muhimu zaidi maishani mwao. Sherehe hizo ziliwapa fursa ya kutafakari na kuzungumza kuhusu wema wa Yehova na Sheria yake. Makusanyiko ya wilaya yanayokuja yatatupa fursa kama hizo za kumwabudu Yehova kwa shangwe.
2. Tunapaswa kufanya nini ili tujitayarishe kwa ajili ya kusanyiko la wilaya linalokuja?
2 Uhitaji wa Kujitayarisha: Familia ya Yesu iliyoishi Nazareti ilihitaji kutembea umbali wa kilomita 200 hivi kwenda na kurudi kutoka Yerusalemu. Ingawa hatujui Yesu alikuwa na ndugu na dada wangapi, tunaweza kuwazia jitihada ambazo Yosefu na Maria walifanya ili kujitayarisha kwa ajili ya safari hiyo. Je, umefanya matayarisho yanayohitajiwa ili kuhudhuria siku zote tatu za kusanyiko la wilaya linalokuja? Huenda ukahitaji kuchukua likizo kazini au kumwomba mwajiri wako ruhusa kwa ajili ya siku hizo tatu. Pia, huenda ukahitaji kumweleza mwalimu wa mtoto wako kwamba hatakuwa shuleni kwa kipindi hicho. Je, umehifadhi chumba cha hoteli iwapo utakihitaji? Je, unaweza kumsaidia ndugu au dada kutanikoni ambaye ana mahitaji ya pekee ahudhurie kusanyiko?—1 Yoh. 3:17, 18.
3. Ni katika njia gani sherehe za Waisraeli ziliandaa fursa za kuwa na ushirika wenye kujenga?
3 Ushirika Wenye Kujenga: Kwenye sherehe za Wayahudi, waabudu walipata fursa ya kufurahia ushirika wenye kujenga. Bila shaka, familia ya Yesu ilitazamia kwa hamu kukutana tena na marafiki zao wa muda mrefu. Pia walifurahia fursa ya kuanzisha urafiki na baadhi ya Wayahudi na wageuzwa-imani wengi ambao walihudhuria sherehe hizo au ambao walikuwa wakisafiri kwenda au kutoka Yerusalemu.
4. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini udugu wetu wa Kikristo wenye umoja?
4 Mtumwa mwaminifu na mwenye busara anataka tutiane moyo na hiyo ndiyo sababu anafanya mipango ili tukusanyike pamoja kusikiliza hotuba kwenye makusanyiko badala ya kuchapa hotuba hizo ili watu wajisomee wenyewe. (Ebr. 10:24, 25) Kwa hiyo, fanya mipango ili ufike kusanyikoni mapema kila siku na kufurahia ushirika pamoja na wengine kabla ya mwenyekiti wa kipindi kutangaza kuanza kwa muziki ambao huashiria kwamba ni wakati wa kuketi. Badala ya kuondoka kwenda kutafuta chakula cha mchana, tunatiwa moyo tubebe chakula chepesi na kubaki mahali pa kusanyiko ili tuweze kufahamiana na kuzungumza na ndugu na dada kusanyikoni. Udugu wetu wa Kikristo wenye umoja ni zawadi kutoka kwa Yehova ambayo tunapaswa kuithamini.—Mika 2:12.
5. Ni nini kitakachotusaidia kunufaika kikamili na programu?
5 Wakati wa Kujifunza: Tangu alipokuwa mtoto, Yesu alitumia vipindi vya sherehe kujifunza kumhusu Baba yake wa mbinguni. (Luka 2:41-49) Ni nini kitakachotusaidia sisi na familia zetu kunufaika kikamili na sehemu zote za programu? Wakati programu inapoendelea, usiondoke kwenye kiti chako wala kuzungumza isivyo lazima. Usiruhusu simu yako, peja, au vifaa vingine vya aina hiyo vikukengeushe wala kuwakengeusha wengine. Mtazame msemaji, na uandike mambo makuu. Ketini pamoja mkiwa familia ili kuhakikisha kwamba watoto wanasikiliza pia. Wakati wa jioni, mnaweza kutumia muda fulani kuzungumzia mambo mliyofurahia kusanyikoni.
6. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu mavazi na mapambo yetu?
6 Mavazi na Mapambo: Wafanyabiashara wasio Wayahudi wangeweza kuitambua kwa urahisi familia ya Yesu na waabudu wengine Wayahudi waliokuwa wakisafiri kwenda na kurudi kutoka kwenye sherehe, kwa sababu miisho ya nguo zao ilikuwa na upindo wenye nyuzinyuzi, ambao ulikuwa na uzi wa bluu juu yake. (Hes. 15:37-41) Ingawa Wakristo hawavai mavazi fulani rasmi, tunajulikana kwa kuvaa mavazi yenye kiasi, nadhifu, na safi. Tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na mapambo yetu tunaposafiri kwenda na kutoka kusanyikoni, na tunapokuwa kwenye jiji la kusanyiko. Hata tukibadili mavazi baada ya programu, tunapaswa kuvalia kwa njia inayomletea Yehova heshima na kuvaa beji yetu ya kusanyiko. Kwa njia hiyo, tutaonekana tofauti na watu wasio Mashahidi na sura yetu itakuwa yenye kuvutia.
7. Kwa nini tunapaswa kufikiria kujitolea kufanya kazi kwenye kusanyiko la wilaya?
7 Wafanyakazi wa Kujitolea Wahitajika: Wafanyakazi wengi wanahitajiwa kusanyikoni ili mambo yawe shwari. Je, unaweza kujitolea kusaidia? (Zab. 110:3) Kazi inayofanywa makusanyikoni ni sehemu ya utumishi wetu mtakatifu na hutoa ushuhuda mzuri. Msimamizi wa jengo fulani lililotumiwa kwa ajili ya kusanyiko alivutiwa sana na kazi ya wajitoleaji waliosafisha jengo hilo hivi kwamba aliandika hivi: “Ningependa kuwashukuru kwa kazi yenu kuhusiana na kusanyiko lenu ambalo ni tofauti sana na makusanyiko ya watu wengine ambayo yamewahi kufanywa hapa. Nimekuwa nikisikia kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu wa pekee ambao kwa muda mrefu wamedumisha sifa nzuri ya kuacha mahali pa kusanyiko pakiwa safi zaidi kuliko palivyokuwa kabla ya kusanyiko. Ninyi na shirika lenu mlifanya mahali hapa pafae zaidi kwa ajili ya jamii na mlifanya hivyo mkisaidiwa na kikundi cha watu wazuri sana ambao tulifurahia kuwajua.”
8. Kutakuwa na fursa gani za kuhubiri kwenye jiji la kusanyiko?
8 Fursa za Kuhubiri: Watu wengi kwenye jiji la kusanyiko wataona wajumbe waliovalia na kujipamba vizuri wakiwa na beji zao za kusanyiko. Jambo hilo linaweza kuwasukuma watu hao waulize maswali, na hivyo kutokeza fursa za kuwaeleza kuhusu kusanyiko letu. Baada ya programu, mtoto fulani wa miaka minne alibeba hotelini kitabu kilichokuwa kimetolewa kusanyikoni na kumwonyesha mhudumu fulani wa hoteli. Kitendo hicho kiliwapa fursa wazazi wa mvulana huyo kumwalika mhudumu huyo kwenye kusanyiko.
9. Tunaweza kuigaje uthamini wa familia ya Yesu kwa maandalizi ya kiroho ya Yehova?
9 Sherehe za kale zilikuwa vipindi vya shangwe ambavyo Wayahudi waliotaka kujifunza mengi kumhusu Yehova walitazamia kwa hamu. (Kum. 16:15) Familia ya Yesu ilifurahi kujidhabihu ili kuhudhuria sherehe hizo na kunufaika kikamili. Tunayathamini vivyo hivyo makusanyiko yetu ya wilaya, na kuyaona kuwa zawadi kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. (Yak. 1:17) Sasa ndio wakati wa kujitayarisha kwa ajili ya tukio hili la kila mwaka la kumwabudu Yehova kwa shangwe!
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya
◼ Saa za Programu: Siku zote tatu, programu itaanza saa 3:20 asubuhi. Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Muziki wa kuanza programu unapotangazwa, sote tunapaswa kuwa tumeketi ili programu ianze kwa utaratibu unaomletea Yehova heshima. Programu itaisha saa 10:55 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:40 jioni siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo. Wale watakaofika kwanza, ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza.
◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili ya wale tu wanaosafiri pamoja nawe katika gari moja, au wanaoishi pamoja nawe katika nyumba moja, na pia watu unaojifunza nao Biblia.—1 Kor. 13:5.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kwenda kutafuta chakula. Kifaa kidogo cha kubebea chakula ambacho kinaweza kutoshea chini ya kiti kinaweza kutumiwa. Vifaa vikubwa vya kubebea chakula na vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote kwenye Jumba letu la Ufalme au kwenye kusanyiko. Cheki zozote za benki zinazotolewa kusanyikoni zinapaswa kuandikwa jina la shirika letu la kisheria.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikitokea kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajiwa. Ikihitajika, ndugu katika idara hii wataitisha gari la kubebea wagonjwa. Jambo hili litapunguza idadi ya simu kwa kitengo cha huduma za dharura kwa sababu ya matatizo madogo-mdogo.
◼ Viatu: Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu. Kwa hiyo, ni vizuri kuvaa viatu vya kawaida, vinavyokutoshea vizuri na vinavyokuwezesha kutembea kwenye ngazi, viunzi vya chuma, na maeneo mengine, bila kujikwaa.
◼ Kurekodi: Vifaa vya kurekodia havipaswi kuunganishwa kwenye mfumo wa umeme au wa sauti. Vinaweza kutumiwa tu kwa njia ambayo haitawasumbua wengine.
◼ Marashi: Makusanyiko mengine hufanywa ndani ya majumba. Basi, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Kufuatia Upendezi: Ukikutana na mtu yeyote anayependezwa unapohubiri wakati wa kusanyiko, unapaswa kutumia fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) kutoa habari kumhusu mtu huyo. Wahubiri wanapaswa kubeba fomu moja au mbili kusanyikoni. Unaweza kuacha fomu ulizojaza kwenye Idara ya Vitabu ili zishughulikiwe au kumpa mwandishi wa kutaniko lenu unaporudi nyumbani.—Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 2009, uku. 4.
◼ Mikahawa: Fanya jina la Yehova liheshimiwe kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Katika sehemu nyingi, ni jambo la kawaida kutoa bakshishi.
◼ Hoteli: (1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kimoja kisikaliwe na watu wanaozidi idadi inayoruhusiwa. (2) Ikiwa hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa kwa ajili yako, julisha wasimamizi wa hoteli mara moja. (3) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati ule tu unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia. (4) Usipike ndani ya vyumba ikiwa hairuhusiwi kufanya hivyo. (5) Kila siku, mwachie bakshishi yule anayetunza chumba. (6) Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni. (7) Nyakati zote, onyesha matunda ya roho unaposhughulika na wafanyakazi wa hoteli. Wanawahudumia watu wengi sana na wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi. (8) Kukiwa na shida katika chumba chako hotelini, ijulishe Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili waweze kukusaidia.
◼ Kazi ya Kujitolea: Tutafurahia kusanyiko hata zaidi iwapo tutajitolea kusaidia kazi inayohusika. (Mdo. 20:35) Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kujitolea kufanya kazi, lakini wafanye hivyo chini ya usimamizi wa mzazi au mtunzaji wao. Pia, wanaweza kufanya kazi chini ya usimamizi wa mtu mzima ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.