Mtegemee Yehova Akupe Nguvu
1 Twahitaji kumtegemea Yehova katika hali nyingi. Kuhubiri habari njema “katika dunia yote inayokaliwa” ni kazi ngumu. (Mt. 24:14) Tunapambana na hali ya kutokamilika daima. (Rom. 7:21-23) Vilevile, “tuna kushindana mwereka . . . dhidi ya watawala [wasio wanadamu] wa ulimwengu wa giza hili.” (Efe. 6:11, 12) Ni wazi kwamba twahitaji msaada. Twawezaje kupata nguvu kutoka kwa Yehova?
2 Kupitia Sala: Yehova huwapa watumishi wake roho takatifu wanapoiomba. (Luka 11:13) Je, unashuku uwezo wako wa kuhubiri nyumba hadi nyumba, barabarani, au kwa simu? Je, wewe huogopa kuhubiri kivivi hivi? Je, ubaridi wa watu kwenye eneo umepunguza bidii yako? Vipi ukishawishiwa ukane imani yako au uaminifu wako? Mtegemee Yehova. Mwombe nguvu.—Flp. 4:13.
3 Kupitia Funzo la Kibinafsi: Kama vile tupatavyo nguvu kwa kula chakula cha kimwili, ndivyo tunavyoimarishwa pia kiroho kwa kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu na vichapo vinavyotoka kwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 4:4; 24:45) Wakati Stanley Jones alipoulizwa kile kilichompa nguvu za kuvumilia kifungo cha upweke kwa miaka mingi huko China bila kuwa na Biblia, yeye alisema hivi: “Twaweza kusimama imara katika imani. Bila shaka, ni lazima tujifunze kwanza. Pasipo kujifunza hatuwezi kuwa na nguvu.”
4 Kwa Kuhudhuria Mikutano: Kwenye mkutano wa Kikristo katika karne ya kwanza, Yudasi na Sila ‘waliwatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.’ (Mdo. 15:32) Vivyo hivyo leo, yale tunayosikia mikutanoni huongeza uthamini wetu kwa Yehova, hujenga imani yetu, na kutuchochea katika huduma. Kwenye mikutano, tunakutana kwa ukawaida na ‘wafanyakazi wenzetu kwa ajili ya ufalme wa Mungu,’ ambao ni “msaada wenye kutia nguvu” kwetu.—Kol. 4:11.
5 Twahitaji msaada katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Kuhusu wale wanaopata nguvu kutoka kwa Yehova, twahakikishiwa hivi: “Watapanda juu kwa mbawa kama tai; watapiga mbio, wala hawatachoka; watakwenda kwa miguu, wala hawatazimia.”—Isa. 40:31.