Uwezo Wenye Kutegemeza wa Neno la Mungu
UA LILILOKATWA linaweza kudumu kwa siku kadha tu kabla halijanyauka na kufa. Walakini mti uliopandwa mahali penye maji mengi waweza kukua na kuwa mkubwa na wenye nguvu na huenda ukaishi kwa muda wa mamia mengi au maelfu mengi ya miaka. Kwa kupendeza, Biblia inamfananisha mtu ambaye “kupendezwa kwake ku katika sheria ya Yehova” na “mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki.”—Zab. 1:1-3, NW.
Mti unaopata maji vizuri unaweza kukua na kuwa na nguvu na kuendelea kuzaa matunda. Vivyo hivyo mtu ambaye hunywa kwa kawaida kutokana na kweli yenye thamani na yenye kuendeleza uhai ya Neno la Mungu kupitia kwa funzo la uangalifu na kutafakari anaweza kukua na kuwa na nguvu kiroho na kuendelea kuzaa matunda.
Kama vile maji yalivyo ya lazima katika kuendeleza uhai wa wanyama na wa mimea, ndivyo na kweli inayopatikana katika Neno la Mungu ilivyo ya lazima ili kuendeleza uzima wa kiroho. Leo watumishi wa Yehova wamo kwenye vita ya kupigania uzima wao. Ni kama vile mtume Paulo alivyosema: “Tunako kushindana mweleka, si juu ya damu na nyama, bali juu ya . . . majeshi ya roho yenye uovu katika mahali pa kimbinguni.” (Efe. 6:12, NW) Hivyo, lazima Wakristo wapige vita ya kiroho juu ya viumbe wenye nguvu zipitazo za kibinadamu. Katika jitihada zao za kuharibu uhusiano walio nao watumishi wa Yehova pamoja na Mungu, roho hao wabaya wanatumia njia zenye jeuri za kushambulia moja kwa moja kama vile mateso na mikazo yenye hila, kama vile vishawishi vinavyohusu uasherati au kupenda mambo ya kimwili.
Kwa sababu ya nguvu zipitazo za kibinadamu pamoja na hila za adui zetu, hatuwezi kwa kweli kutumaini kuokoka mashambulio yao kwa nguvu zetu wenyewe. Walakini, tukiwa watumishi wa Mungu, twaweza kutegemea nguvu anazotoa Yehova. Maadamu tunamtumaini kabisa kabisa Mungu Mwenye Nguvu Zote, twaweza kuwa na uhakika kama ule aliouonyesha mtume Paulo, ambaye alisema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”—Flp. 4:13.
Maneno hayo ya Paulo hayakuwa tu maneno mazuri yasiyo na maana. Yeye aliandika akiwa na uhakika uliotokana na mambo aliyopata kuyaona yeye mwenyewe kwa muda wa miaka mingi. Kulingana na ushuhuda wake mwenyewe, mtume huyo alikuwa “katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi.” (2 Kor. 11:23-27) Lakini kwa uwezo aliopewa na Mungu aliweza kuvumilia kwa uaminifu katika utendaji wa kimungu, mpaka wakati wa kifo chake mikononi mwa adui.
Walakini, ili apate nguvu za kiroho na uwezo wa kuelekeana na wakati ujao akiwa mshika-ukamilifu, ni lazima Mkristo awe na ufahamu mzuri wa Neno la Mungu. Kupitia kwa Maandiko, Baba wetu wa kimbinguni mwenye upendo ametupatia uongozi wa lazima kwa maisha yenye furaha pamoja na chanzo kisicholinganika cha nguvu za kiroho. Bila shaka Mwana wa Mungu alithamini ubora wenye kudumisha uhai wa Neno la Babaye, kama vile inavyoweza kuonwa kwa namna alivyolitumia akisema katika kuvijibu vishawishi vya Shetani: “Imeandikwa, mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha [Yehova].”—Mt. 4:4.
Wakati na Jitihada Huhitajiwa
Hata hivyo, hatuwezi kutazamia Mungu atupe ufahamu wa Biblia kwa mwujiza. Ili tulishike vizuri Neno la Mungu, lazima tutumie wakati na jitihada katika kujifunza Biblia na kuyatafakari yale tunayojifunza.
Ni kweli, kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu, hakuna ye yote kati yetu anayeweza kukumbuka kila kitu anachojifunza. Lakini ikiwa tumejitahidi kujifunza Biblia kwa uangalifu, twaweza kuitegemea roho ya Yehova itukumbushe mawazo ya Kimaandiko ambayo yatatupatia uongozi pamoja na kitia-moyo kinachohitajiwa ili kuelekeana na majaribu mbalimbali pamoja na habari inayohitajiwa ili kuitetea imani yetu. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake hivi: “Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni [roho ya] Baba yenu [isemayo] ndani yenu.”—Mt. 10:19, 20.
Bila shaka, si kwamba sikuzote tunahitajiwa kutoa ushuhuda mbele ya watawala na wale wanaotuuliza tuwaeleze juu ya imani yetu pamoja na utendaji wetu wa Kikristo. Mara nyingi tunapatwa na magumu na mateso, hata kutiwa kifungoni kwa muda mrefu. Je! Neno la Mungu lina uwezo wenye kutegemeza katika hali kama hizo? Bila shaka ndiyo.
Mifano Iliyo Hai
Wengi wa watumishi wa Mungu wanaweza kushuhudia juu ya uwezo wa ajabu wenye kutegemeza wa Neno la Mungu. Kwa mfano, ebu wafikirie Wakristo wa kweli katika China, ambao baadhi yao walivumilia magumu mengi sana katika gereza na kambi za kufanyia kazi ngumu. Kwa muda wa miaka mingi hawakuwa na nakala za Biblia wala hawakuwa na nafasi ya kushirikiana na Wakristo wenzao. Hata hivyo, yale waliyokuwa wamejifunza katika Neno la Mungu kabla ya kutiwa gerezani yaliwategemeza muda wote huo wa miaka mingi yenye majaribu.
Mmoja wa watu hao alikuwa Stanley Jones, aliyekamatwa katika mwaka wa 1958 na kuhukumiwa kifungo cha miaka saba gerezani. Ijapokuwa yeye hakuwa na Biblia, yeye aliweza kukumbuka maandiko mengi naye alipata faraja na nguvu nyingi kwa kuyatafakari. Andiko moja lililomfariji sana ni Warumi 12:12, linalosomwa hivi: “Furahini katika tumaini. Vumilieni dhiki. Dumuni katika sala.” NW.
Mfano mwingine ni ule wa Harold King, ambaye alikamatwa akahukumiwa kufungwa miaka mitano katika China. Ndugu King alikuwa amejifunza Biblia kwa muda wa miaka 26. Kwa hakika, kwa muda wa miaka 22 alikuwa amekuwa akiitumia Biblia wakati wote alipokuwa akishiriki kazi ya kuhubiri wakati wote. Jambo hilo lilimsaidia awe na ufahamu mzuri wa Neno la Mungu. Alipojikuta akiwa gerezani huku akitenganishwa na ndugu zake za kiroho, yeye alimwomba Yehova kuhusiana na hali yake, akimwuliza ni wakati gani na ni kwa namna gani jaribu hilo lingemalizika. Maneno ya Yesu katika Mathayo 6:31-34 yakaja akilini mwake nao wasiwasi wake ukatoweka. Ilikuwa kama kwamba Yehova alikuwa akimwambia hivi: ‘Ishi maisha yako siku kwa siku wala usisumbukie ya kesho. Nitakuangalia vizuri, kama vile nimekuwa nikifanya sikuzote.’ Vilevile ndugu King alimfikiria Yeremia nabii wa Mungu, ambaye wakati mmoja alikuwa ametiwa kwenye shimo lenye matope, kwa wazi akiachwa afie humo. (Yer. 38:6) Hata hivyo, Yeremia aliokolewa kutoka katika hali hiyo iliyoelekea kutokuwa na matumaini. Kwa kufikiria mfano huo wa kale wa uaminifu, Harold King aliona kwamba mwishowe Yehova angemwokoa yeye, hivi kwamba angeweza kurudia ndugu zake na kuendelea na utumishi wake katika uhuru.
Akiendelea kutumia uwezo wenye kutegemeza wa Neno la Mungu, Harold King alijaribu kukumbuka maandiko mengi iwezekanavyo, kama vile alivyofanya Stanley Jones. Kama ndugu hao wawili walikuwa wameshindwa kujifunza Biblia kwa uangalifu na kwa juhudi hapo kwanza, je! wangeweza kukumbuka maandiko mengi ambayo yangewasaidia na kuwategemeza kiroho?
Tena kuna mfano wa Nancy Yuen, ambaye alitumia miaka 20 gerezani na katika kambi za kufanyia kazi ngumu huko China. Katika muda huo mrefu wa kuzuiwa kwake, yeye alikuwa ametenganishwa na jamaa yake licha ya kukazwa wakati wote aikane imani yake. Hata hivyo, aliweza kushinda hali hiyo yenye kujaribu na iliyo ya muda mrefu kwa kumtegemea Yehova ampe nguvu na kwa kutumia uwezo wenye kutegemeza wa Neno lake. Kwa msaada wa roho ya Mungu, yeye aliweza kukumbuka maandiko yaliyoelekea kufaa sana katika kutosheleza mahitaji yake chini ya hali mbalimbali. Kama alivyosema: “Sikuzote kulikuwako maandiko yafaayo niliyoyakumbuka ya kunipa uongozi na nguvu kukabiliana na kila hali.”
Kwa mfano, wakati Dada Yuen alipoelekeana na vitisho vya kutendewa kijeuri na kuumizwa mwili, yeye alikumbuka maneno ya Yehova yenye kufariji aliyoambiwa nabii Ezekieli: “Usiwaogope hao, wala usiyaogope maneno yao.” (Eze. 2:6) Alipohuzunika sana kwa kutokuwa pamoja na jamaa yake, maneno haya ya Yesu yakaja akilini mwake: “Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili. Wala mtu asiyechukua [mti wake wa mateso] akanifuata, hanistahili.” (Mt. 10:37, 38) Jambo hilo lilimsaidia kufanya upya azimio lake la kushikamana na ukamilifu wake, hata apate hasara gani.
Wakati Dada Yuen alipofanyiwa matendo ya aibu na kutendwa vibaya, alikumbuka namna walivyofanya mitume wa Yesu walipopigwa mijeledi kwa kuhubiri “habari njema.” Yeye alikumbuka kwamba “wakatoka mbele ya ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo [la Kristo].” (Matendo 5:40-42) Kwa hiyo, aliweza kuvumilia aibu hiyo kwa furaha. Alipopatwa na gumu la kunyimwa chakula, alikumbuka kwamba ‘mtu hataishi kwa mkate tu.’—Luka 4:4.
Dada Yuen alifikiri juu ya watumishi wengi waaminifu wa Yehova ambao waliendeleza ukamilifu wao kwa Mungu walipopatwa na magumu na majaribu. Yeye alipata faraja nyingi kutokana na mifano ya Ayubu na Danieli, kwa kuwa aliona kwamba yeye alikuwa akipatwa na mambo kama yale waliyoyavumilia wanaume hao waaminifu wa nyakati za kale. Bila shaka, mfano ulio mkubwa zaidi, ule wa Kristo Yesu, ulikuwa wakati wote chanzo cha kutia moyo.
Katika visa vingine vingi, watumishi wa Mungu wa nyakati hizi wakiwa wanaishi katika sehemu mbalimbali za ulimwengu, wamevumilia majaribu makali ya imani na yenye kuendelea kwa muda mrefu. Wakristo hao, ambao wameshinda majaribu, ni wanaume na wanawake wa kawaida tu kama sisi sote. Kwa hakika, ‘uwezo upitao ule wa kawaida ni wa Mungu wala si kutoka kwao wenyewe.’—2 Kor. 4:7, NW.
Neno la Mungu Li “Hai, Tena Lina Nguvu”
Ni kweli, si waabudu wote wa Yehova wanaolazimika kuvumilia majaribu yale yale magumu, kama vile kutiwa kifungoni kwa ajili ya imani yao. Walakini watumishi wote wa Mungu wanalazimika kupitia katika majaribu ya namna fulani ili kuijaribu imani yao kikamilifu. Huenda majaribu yakaja kwa namna ya upinzani kutoka kwa washiriki wa jamaa, vishawishi vya uasherati, mikazo kutoka kwa rafiki ili wafuate mwendo fulani usio wa kimaandiko, masumbufu ya maisha, afya, mbaya, magumu mbalimbali ya kibinafsi, na vivyo hivyo. Walakini, hata majaribu yawe magumu kadiri gani, twaweza kuwa na hakika kwamba faraja pamoja na nguvu tunayopata kutokana na Neno la Mungu itakuwa msaada usiolinganika kwetu katika wakati wetu wa uhitaji ikitusaidia tusimame imara na kudumisha imani yetu katika Mungu.—Rum. 15:4.
Maelfu mengi ya watu wa Yehova wanaweza kushuhudia juu ya uwezo wenye kutegemeza wa Neno lake. Wamewezeshwa kuvumilia upinzani kila siku kwa muda wa miaka mingi kutoka kwa washiriki wa jamaa. Wameweza kuendeleza mwenendo mwema wa Kikristo katika ulimwengu unaozidi kuwa mwasherati na usiotii sheria. Wameweza kuonyesha imani thabiti zijapokuwa dhihaka na madharau ya jamii ya wanadamu isiyo na imani. Mifano hii halisi, ya watu wanaoishi kweli kweli yaonyesha kwamba Neno la Mungu li “hai, tena lina nguvu.” (Ebr. 4:12) Laweza kufananishwa na upanga wa kutumiwa kwa makusudi yote mawili, kushambulia na kujikinga. Lakini, upanga hauwezi kusaidia sana ukiwa mkononi mwa mtu ambaye hajazoezwa kuutumia. Hivyo, Neno la Mungu halimfaidi sana mtu aliye na ujuzi kidogo tu wa Neno hilo na ambaye hajui namna ya kuutumia maishani.—Efe. 6:17.
Neno la Mungu lilitokezwa na roho takatifu ya Yehova, ambayo ndiyo nguvu yenye uwezo zaidi katika ulimwengu wote. Ili tuwe na ufahamu ufaao wa Neno hilo, tunahitaji kujifunza Neno hilo kwa njia ya sala kwa msaada wa roho ya Mungu na kwa kushirikiana na kundi la watu wake. (Mt. 24:45-47; Matendo 8:30-35; 1 Kor. 2:10) Ijapokuwa ulimwengu huu umo katika kipindi chenye msukosuko na taabu isiyo na mfano wake katika wakati uliotangulia, ikitokeza hali zenye kujaribu sana, sisi twaweza kupata faraja kutokana na Maandiko. Kwa hakika, sasa, ndio wakati wa kujifunza Neno la Mungu kwa juhudi ili tufaidike kikamilifu na uwezo wake wa ajabu wenye kutegemeza.