Niko Huru! Baada ya Kutumia Miaka 20 Kizuizini
Kama Ilivyosimuliwa na Nancy Yuen
MLETA Habari za “Amkeni!” katika Hong Kong anaandika hivi:
Jamaa yetu katika makao ya tawi ya Sosaiti katika Hong Kong inaliona kuwa jambo la kawaida kutembelewa na wageni kutoka nchi za ng’ambo. Walakini Alhamisi, Februari 15, 1979, ulikuwa wakati wa pekee sana. Mgeni wetu alikuwa Nancy Yuen, shahidi wa Yehova mwaminifu, ambaye mara hiyo ndipo alikuwa ametoka China baada ya kutumia miaka 20 kifungoni. “Nina furaha tele kuwa pamoja nanyi. Nimeipata jamaa yangu,” akasema.
Sisi sote tulijua habari za Nancy Yuen pamoja na kumbukumbu la uaminifu wake, walakini sasa alikuwa pamoja nasi yeye mwenyewe nasi tungeweza kusikia hadithi yake kutoka kwake yeye mwenyewe. Akiturudisha nyuma katika mwaka 1949, alianza hadithi hiyo. Hivi ndivyo alivyotuambia:
ILIKUWA kama miaka 30 hivi iliyopita wakati Stanley Jones, mmisionari wa Sosaiti, alipotembelea nyumba yetu kwa mara ya kwanza katika Shanghai, China. Wakati huo nilikuwa nimeolewa nami nilikuwa na watoto wawili. Ujumbe aliotuletea juu ya Yehova Mungu pamoja na kusudi Lake kwa wanadamu ulinipendeza sana.
Nilibatizwa katika mwaka wa 1950 nami niliendelea kujifunza kwa bidii sana ili niongeze maarifa na ufahamu wangu. Nafurahi sana kwamba katika miaka hiyo ya mwanzo-mwanzo nilichukua madaraka yangu ya Kikristo kwa uzito sana, kwa kuwa kama sikufanya hivyo, singeweza kuvumilia majaribu yaliyokuwa mbele yangu.
Kufikia mwaka 1954 nilikuwa na watoto wachanga wanne na vilevile nilikuwa nikishiriki kwa bidii katika kutangaza habari njema za ufalme wa Yehova. Kufikia mwanzoni mwa mwaka 1956, Serikali ya Kikomunisti ilikuwa imechukua mamlaka kamili juu ya Shanghai. Tukaanza kuonywa tuache kuhubiri, tufanyie utendaji wetu kwenye Jumba la Ufalme peke yake. Walakini, mimi niliona kwamba ilinilazimu kuendelea kutimiza agizo letu tulilopewa na Mungu la kuhubiri, kwa hiyo mimi niliendelea kushiriki katika kazi ya nyumba kwa nyumba.
Nilikamatwa na kuzuiliwa mara nyingi ili nihojiwe, mara nyingine nikizuiliwa kwa muda wa saa tano na mara nyingine hata kwa muda wa siku tatu. Kwa wakati huu, kwa kuwa mume wangu alikuwa amehamia Hong Kong katika mwaka 1953, niliomba ruhusa nijiunge naye huko. Wenye mamlaka walisema kwamba wangenipa ruhusa ya kuondoka ikiwa tu ningeacha kuhubiri. Nilikataa kuacha na kwa sababu hiyo sikupata ruhusa hiyo.
Wakuu wa Kikomunisti walikasirishwa na azimio langu la kuendelea kuhubiri. Wakati wa pindi moja ya kuhojiwa, niliambiwa kwamba mimi ndimi mtu mwenye shingo ngumu zaidi katika China yote. Mwishowe, katika nusu ya pili ya mwaka 1956, baada ya kukamatwa mara sita kwa sababu ya kuhubiri, nilizuiliwa tena wakati mwenye nyumba mmoja aliporipoti kwa wenye mamlaka kwamba nilikuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba. Baada ya hapo sikuachiliwa tena.
KIZUIZI CHAANZA
Nilikuwa nimekulia katika jamaa yenye furaha nami mwenyewe nilikuwa na jamaa changa yangu mwenyewe. Sasa nilikuwa nimetenganishwa nao wote nami nilikuwa nimeketi chini katika chumba cha gereza chenye giza huku mikono yangu ikiwa imefungwa kwa pingu. Kwa ghafula machozi yakanitoka. Nilijisikia dhaifu sana na bila msaada! Ilielekea kama kwamba hakukuwa na njia ya kutokea. Upesi, mawazo ya Biblia yakaja akilini juu ya Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote,” ambaye huwapa watumishi wake nguvu. (2 Kor. 1:3, 4) Ndipo nilipomgeukia kwa sala ya bidii.
Tangu wakati huo nilizungumza na Yehova kwa sala mara nyingi nami nikajisikia nikiendelea kupata nguvu kila siku. Kwa kuwa askari wa gereza walipata kuona kwamba nilikuwa nikisali nikiwa nimeweka mikono mbele yangu, sana sana wakati wa chakula, mikono yangu ilifungwa nyuma yangu pingu zikifungwa juu ya sehemu iliyo katikati ya kiko cha mikono yangu na mabega yangu, nikalazimika kuvumilia mateso hayo kwa muda wa siku tatu mpaka mikono yangu ikavimba sana. Bila shaka, hili halikunizuia kuomba. Walakini, mpaka hivi leo waweza kuona alama hizo juu ya sehemu hiyo.
Nilitumia miaka minne kizuizini, nao wakati huo wote nilikuwa nikihojiwa. Walitaka niwasaliti wale ndugu wawili wamisionari tena niseme kwamba Sosaiti ni wakili wa ubeberu. Singeweza kufanya hivyo. Nilitumia wakati huo niwatolee wakuu ushuhuda na kuwaambia linavyosema Neno la Mungu. Mkuu mmoja alisema kwamba alikuwa ameshughulika na vikundi vya dini mbalimbali, navyo vyote vilikuwa vimekubali kushindwa. Walakini yeye alisifu sana ujasiri na bidii yangu. Alisema hivi: “Ni jambo la kusikitisha sana kwamba hukugeuzwa [kuwa mfuasi wa] Ukomunisti kabla ya kugeuzwa [uwe mfuasi wa] Ukristo, kwa sababu chama chetu kinahitaji watu wenye kusadikishwa kikweli kama wewe.” Mwaka 1960, nilihukumiwa kifungo cha miaka 10 gerezani, kifungo hicho kikianza tangu mwaka 1956 nilipozuiliwa.
Katika mwaka 1961 nilipelekwa kwenye kambi ya kufanyiziwa kazi ngumu huko mashambani, nako huko nilikuwa na nafasi ya kushiriki “habari njema” pamoja na wafungwa wenzangu. Sikuacha kamwe kazi yangu ya kuhubiri, na kama vile wakati ulivyoendelea, nilipata kuwa na ujasiri zaidi. Katika pindi moja, nilihubiri kikundi cha watu 12 waliosikiliza kwa makini sana. Jambo hilo likajulikana. Ndipo nilipotiwa gerezani ya mahali hapo kwa muda wa siku 19, nao wakaongeza miaka miwili zaidi katika kifungo changu cha kwanza cha miaka 10. Upesi, miaka hiyo 12 ikapita.
KUFUNGULIWA NA KURUDISHWA GEREZANI TENA
Katika mwaka 1968 nilifunguliwa nitoke katika kambi ya kufanyiziwa kazi ngumu, ijapokuwa mwendo wangu ulikuwa unazuiliwa. Sasa ningaliweza kufanya kazi na kupata mshahara wa shilingi 75 (Z25) kila mwezi. Wakati huu niliruhusiwa kuhama kutoka kikundi kimoja chenye kufanya kazi ngumu kwenda kingine naye mama yangu aliweza kuhamia wilaya hiyo ili awe karibu nami.
Kwa kupewa uhuru wa kutembea kutoka mahali pamoja kwenda mahali pengine, nilianza safari iliyonichukua kwenye miji kadha, kutia na Anching, Hangchow, Nanking na Shanghai. Niliwatembelea rafiki pamoja na jamaa nikashiriki nao pamoja na rafiki zao walionijulisha kwao kweli za Ufalme nilizokuwa nimejifunza. Karibu mwaka mmoja hivi ukapita nami nikaomba tena ruhusa ya kuondoka China nikajiunge na mume wangu huko Hong Kong. Ili nipate ruhusa, niliambiwa nirudi katika wilaya ya Chinsang mahali nilipokuwa nikifanya kazi na mahali mama yangu alipokuwa akiishi. Matokeo yalikuwa kwamba nilirudishwa Chinsang nikazuiliwa tena baada ya kuwa huru kwa muda wa miaka miwili.
HUKUMU YA HADHARANI
Nikawa tena nikihojiwa-hojiwa wakati wote. Mkuu wa polisi alinishtaki kuwa mwenye shingo ngumu, akaniambia kwamba afadhali niungame “matendo ya kuvunja sheria” yangu ama sivyo mambo yangeniwia magumu sana. Nilimwambia yote niliyokuwa nimesema wakati wa kuzungumza na wengine, nikifanya hivyo katika njia iliyoniwezesha kumtolea ushuhuda mzuri juu ya ufalme wa Mungu pamoja na taratibu Yake mpya ya mambo inayokuja. Nilimwambia mkuu wa polisi waziwazi kwamba lazima serikali zote ziuondokee ufalme wa Mungu. (Dan. 2:44) Haya yote yaliangaliwa kwa makini sana.
Ndipo, nikiwa pamoja na wafungwa wanaume wanne tukatembezwa kupitia barabara kuu za mji. Makosa yao yalikuwa ya namna mbalimbali kama vile wivi, uuaji pamoja na kushika wanawake kwa nguvu. Kila mmoja wetu alikuwa na tangazo la matendo ya uvunjaji wake wa sheria likiwa limefungwa nyuma yetu. Ndipo mkuu wa polisi akasoma kupitia kwa vikuza sauti “matendo ya kuvunja sheria” yangu mbele ya watu elfu moja waliokusanyika katika ua wa shule. Alisoma yote niliyokuwa nimesema. Nilifurahi sana kuona ilikuwa kama kwamba, alikuwa ametoa ushuhuda mzuri sana kwa watu wengi zaidi wa mji huo kuliko mimi.
Baadaye, nilijifunza kwamba uchunguzi juu ya utendaji wangu wa kuhubiri ulikuwa umehusu zaidi ya watu 100 katika mikoa tisa mbalimbali. Mkuu mmoja mwenye cheo kidogo alikuwa amesema kwamba mimi ni mtu mwenye shingo ngumu sana, nisingeweza kugeuzwa na kwa hiyo ilinipasa kuuawa. Walakini mkuu mwenye cheo cha juu zaidi hakukubaliana na hilo hivyo nilipaswa kuhukumiwa kifungo cha miaka 20 gerezani kwa mara ya pili.
Kwa muda wa miaka minne iliyofuata, kila siku ilikuwa kama nyingine. Niliruhusiwa nitoke ndani ya chumba changu cha gereza asubuhi na mapema nifue mavazi na kuoga mwili, na kurudishwa ndani ya chumba changu mpaka jioni, wakati ambapo niliruhusiwa kutoka nje tena kwa muda mfupi nichukue mavazi yangu. Kisha nikafungiwa ndani ya chumba changu cha gereza usiku kucha.
Novemba 1, 1978, nilipata habari kwamba ningeruhusiwa kuondoka China nikajiunge na mume wangu huko Hong Kong. Ndivyo ilivyokuwa kwamba mwishoni mwa Januari 1979, mume wangu nami pamoja na watoto wetu wanne, tuliungana tena kama jamaa moja kwa mara ya kwanza baada ya kupita muda wa miaka 26!
YEHOVA ALINITEGEMEZA
Maisha gerezani pamoja na kambi ya kufanyiziwa kazi ngumu yalikuwa magumu sana, ijapokuwa nyakati zote nilikuwa na vyakula pamoja na mavazi ya kunitosha. Sana sana chakula kilikuwa cha mchele pamoja na mboga, kukiwa na nyama mara nne hivi kwa mwaka. Kilikuwa chakula chenye afya, nami niliendelea kuwa na nguvu na mwenye afya. Niliendelea kufanyiza akili yangu kazi, nikijikumbusha mistari ya Biblia pamoja na kweli nilizokuwa nimejifunza katika miaka yangu ya mwanzoni. Sikuzote nilitafuta nafasi za kushiriki tumaini langu pamoja na wengine nalo jambo hili liliniwezesha kuendelea kuwa na shughuli nyingi na kuwa na furaha.
Katika majaribu yangu yote, sikujisikia nimeachwa hata kidogo. Sikuzote niliomba uongozi ili nipate kufanya linalofaa sikuzote. Niliomba nipate nguvu na ujasiri wa kuvumilia. Baada ya kusali, sikuzote nilijisikia kuhakikishwa kwamba sikuwa nimekosea na kwamba mwendo niliokuwa nikichukua ulikuwa unafaa. Naweza kusema kwa kweli kwamba sala ilinisaidia kumkaribia Yehova, nikajisikia kuwa karibu naye hivi kwamba nyakati nyingine nilijisikia kama kwamba nilikuwa nikimwona kwa macho. Mara nyingi nilikumbuka uhakikisho wa Isaya 66:2, kwamba Mungu anamwangalia “mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka.” Sikuzote hili lilinitia nguvu na kunifariji.
Alipoulizwa kama aliona kuhojiwa-hojiwa na wakuu pamoja na mapolisi kuwa jambo gumu kuvumilia, Nancy Yuen alijibu hivi:
Mwanzoni ilinipasa kulizoelea. Walakini nilipotengeneza upya kufikiri kwangu juu ya hali hiyo, halikuwa jambo baya sana. Ni jambo la maana kuwa na maoni yanayofaa juu ya mambo. Wakati wa mapema sana wa kuzuiliwa kwangu, nilikumbuka maneno haya ya Yesu kama yalivyoandikwa katika Luka 21:14, 15: “Kusudieni mioyoni mwenu, kutofikiri-fikiri kwanza mtakavyojibu; kwa sababu mimi nitawapa kinywa na hekima ambayo watesi wenu wote hawataweza kushindana nayo wala kuipinga.” Hivyo, nilijifunza kutokuwa na wasiwasi hata kidogo juu ya kuhojiwa. Nilikuona kama nafasi ya kuwatolea wakuu ushuhuda. Sikuzote nilikuwa na jambo la kuwaambia juu ya Yehova Mungu na kusudi lake kwa wanadamu, nami sikuzote nilielekea kupata akilini mwangu andiko linalofaa kwa wakati huo.
Anapotazama nyuma, anajisikiaje juu ya miaka 20 aliyotumia kizuizini? Yeye anasema hivi:
Ilifaa kabisa nami namshukuru sana Yehova, Mungu wangu, kwa sababu ya nafasi niliyokuwa nayo ya kuonyesha upendo na kujitoa kwangu kwake. Kama ilivyoandikwa katika Mathayo 13:45, 46, Yesu alifananisha Ufalme na mfanya biashara mwenye kusafiri akitafuta lulu nzuri. Alipoiona moja yenye thamani kubwa, aliuza vitu vyote alivyokuwa navyo akainunua. Nililazimika kuacha kila kitu, hata watoto wangu wadogo, ili niwe mshikamanifu kwa Yehova, Mungu wangu. Yehova hakunitahayarisha katika njia yo yote. Alinitegemeza na kuangalia jamaa yangu katika njia yake mwenyewe ya ajabu.
Alipoulizwa kama ana shauri lo lote zuri la kuwapa Wakristo wenzake, Nancy Yuen alijibu hivi kwa kufikiria:
Usiogope hata kidogo majaribu ambayo huenda yakakupata. Inatupasa sote kutazamia majaribu ya namna moja au nyingine. Ni yenye faida kwetu. Yanatuadibisha na kutusafisha na kuonyesha sisi ni Wakristo wa namna gani. Majaribu yanatuonyesha namna imani yetu ilivyo na nguvu na sehemu zinazohitaji kutiwa nguvu. Leo mimi ninajisikia kuwa na nguvu sana katika imani yangu kama matokeo ya majaribu yangu. Kwa hiyo usiogope hata kidogo. Mara nyingi nilifarijiwa sana na maneno ya mtume Petro ‘kumtwika Yehova masumbuko yako yote, kwa kuwa anakujali wewe.’ (1 Pet. 5:6, 7) Waweza kufanya vivyo hivyo.
Mfano wa uvumilivu pamoja na ushikamanifu wa dada huyu mwenye kujitoa unatia moyo na kutia imani nguvu. Katika sala zao kwa Yehova Mungu, kwa muda wa zaidi ya miaka 20 Mashahidi wa Yehova kuzunguka ulimwenguni pote wamekuwa wakikumbuka ndugu na dada zao wapendwa wa huko China. Sasa tunajifunza kutokana na mmoja wao namna amepata kuwaangalia na kuwategemeza kwa upendo mpaka hivi sasa.
Nancy Yuen alitembelea afisi ya tawi ya Sosaiti katika Hong Kong Februari 15, 1979, akahudhuria mkutano wake wa kwanza wa Kikristo katika muda wa miaka 22 Februari 16 na kushiriki tena pamoja na ndugu zake katika kutangaza ufalme wa Mungu nyumba kwa nyumba Februari 17. Mioyo yetu inatusukuma tumshukuru Yehova kwa sababu ya mifano ya kisasa ya uaminifu inayotutia moyo sisi Wakristo wote wa kweli tuendelee kuwa washikamanifu kwa Yehova, Mungu wetu.