SOMO LA 1
Kusoma kwa Usahihi
MAANDIKO yanasema kwamba Mungu anataka watu wa hali zote ‘waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli.’ (1 Tim. 2:4) Kwa hiyo, tunaposoma Biblia kwa sauti, tamaa yetu ya kujulisha wengine ujuzi sahihi inapasa kutuchochea kusoma vizuri.
Uwezo wa kusoma Biblia kwa sauti pamoja na vichapo vingine vinavyoifafanua ni muhimu sana kwa vijana na wazee. Sisi Mashahidi wa Yehova tuna daraka la kuwajulisha wengine ujuzi juu ya Yehova na njia zake. Mara nyingi sisi husomea mtu mmoja au watu kadhaa. Sisi husoma pia katika familia. Shule ya Huduma ya Kitheokrasi huwapa akina ndugu na dada, vijana kwa wazee, fursa nzuri ya kupokea mashauri yanayowasaidia kusoma vizuri kwa sauti.
Ni jambo zito kusoma Biblia mbele ya watu au mbele ya kutaniko. Biblia imepuliziwa na Mungu. Na pia ‘neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu na linaweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.’ (Ebr. 4:12) Neno la Mungu lina ujuzi wenye thamani sana ambao haupatikani mahali pengine popote. Pia linaweza kumsaidia mtu amjue Mungu wa pekee wa kweli na kujenga uhusiano mzuri naye. Hali kadhalika linaweza kumsaidia kukabiliana na matatizo ya maisha kwa mafanikio. Linaeleza jinsi ya kupata uhai wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Tunapaswa kuweka mradi wa kusoma Biblia kwa kadiri iwezekanavyo.—Zab. 119:140; Yer. 26:2.
Jinsi ya Kusoma kwa Usahihi. Kusoma vizuri kunahusisha mambo mengi, lakini hatua ya kwanza ni kusoma kwa usahihi. Hiyo inamaanisha kujaribu kusoma maneno yaliyochapwa jinsi yalivyo hasa. Jihadhari usiruke-ruke maneno, usikose kutamka sehemu fulani za maneno, wala usisome maneno vibaya kwa sababu ya kuchanganyikiwa na maneno mengine yanayofanana nayo.
Ili uweze kusoma maneno kwa usahihi, inatakikana uelewe muktadha. Hiyo inahitaji matayarisho mazuri. Baada ya muda utaweza kusoma kwa usahihi zaidi unapokuza uwezo wa kutazama maneno yanayofuata na kufahamu jinsi ambavyo mawazo yamefuatana.
Vituo na alama za matamshi ni sehemu muhimu za maandishi. Vituo vinaweza kuonyesha mahali pa kutua, muda wa kutua, na labda mahali pa kubadili sauti. Katika lugha nyinginezo, swali linaweza kubadilika kuwa taarifa au maana ya sentensi inaweza kubadilika kabisa mtu asipobadili sauti anapofikia kituo. Nyakati nyingine vituo hutumiwa hasa kwa minajili ya sarufi. Katika lugha nyingi, huwezi kusoma kwa usahihi bila kufikiria kwa makini alama za matamshi zinazoonyeshwa na pia zile ambazo zinaeleweka tu kutokana na muktadha. Alama hizo hubadili sauti za herufi zinazohusika. Hakikisha unajua kutumia vituo katika lugha yenu. Hiyo ndiyo njia ya kusoma vizuri. Kumbuka kwamba kusudi lako ni kuwasilisha mawazo, si kusema tu maneno.
Ili uweze kukuza uwezo wa kusoma kwa usahihi, unahitaji kufanya mazoezi sana. Soma fungu moja tu, kisha urudie kulisoma tena na tena mpaka uweze kulisoma bila kufanya kosa lolote. Kisha usome fungu linalofuata. Hatimaye, jaribu kusoma kurasa kadhaa bila kuruka-ruka maneno, bila kujirudia-rudia, au bila kusoma maneno vibaya. Baada ya kufanya hivyo, omba mtu mwingine akusikilize unaposoma ili akukosoe unapokosea.
Katika sehemu nyingine za ulimwengu, matatizo ya macho na kukosa mwangaza wa kutosha kunaweza kutokeza matatizo ya kusoma. Hali hizo zikiboreshwa, bila shaka wengi wanaweza kusoma vizuri.
Baada ya muda, ndugu wanaojua kusoma vizuri wanaweza kupewa mgawo wa kusoma kwenye Funzo la Kitabu la Kutaniko na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Lakini ili uweze kusoma vizuri ukipewa migawo hiyo, kuna mengi yanayotakikana kufanywa kuliko kutamka tu maneno kwa usahihi. Ili uweze kuwa msomaji mzuri mbele ya watu kutanikoni, kuza mazoea mazuri ya usomaji wa kibinafsi. Hiyo inatia ndani kutambua kwamba kila neno katika sentensi linatimiza fungu fulani. Huwezi kupuuza maneno mengine na bado uelewe vizuri mambo yanayosemwa. Ukisoma maneno vibaya, hata kama unajisomea mwenyewe, maana ya sentensi hupotea. Unaweza kusoma maneno vibaya ukipuuza alama za matamshi au muktadha wa maneno unayosoma. Jaribu kuelewa maana ya kila neno kama lilivyotumiwa katika muktadha. Fikiria pia jinsi kituo kinavyobadili maana ya sentensi. Kumbuka kwamba mara nyingi mafungu ya maneno ndiyo yanayotokeza maana. Fikiria jambo hilo ili unaposoma kwa sauti, usome mafungu-mafungu ya maneno badala ya kusoma neno moja moja tu. Ukielewa vizuri jambo unalosoma, utakuwa umepiga hatua kubwa ya kuweza kuwapa wengine ujuzi sahihi unaposoma mbele ya watu.
Mtume Paulo alimwandikia hivi mzee Mkristo mwenye ujuzi: “Endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote.” (1 Tim. 4:13) Bila shaka sisi sote tunaweza kufanya maendeleo kuhusu jambo hili.